The Curse for Salvation

The Curse for Salvation

Monday, 7 April 2025

Umuhimi wa Wanandoa Kutunza Siri

Kuna busara wakati wa kuwafunda wanawali katika jamii moja nchini Uganda isemayo kuwa wanapoolewa lazima wajifunze kufunga miguu na kufungua macho badala ya kufungua miguu na kufunga macho. Hii hufanyika wakati mwali akijiandaa kwenda kwa mumewe. Wazazi hufanya hivyo kwa kujua kuwa nyumbani kwa mwali huacha kuwa kwao na huko aendako ndiko hugeuka kwake. Hamjasikia kwa Waswahili wakimwimbia bi harusi kuwa ‘sasa wenda kwako, utarudi huku kutembea?’

 Busara hii, licha ya kuzuia vishawishi vya  uasherati, inalenga kuwaambia wanandoa kuwa makini na waliowazunguka kuhusiana na maisha na ndoa zao. Inawahimiza kuchambua mambo na kujua ya kusema na ya kutosema. Siyo kila jambo lazima lisemwe au kuwekwa wazi kwa wasiohusika. Tumeshagusia kwenye kitabu cha kwanza namna mashoga wanavyoweza kuvunja ndoa. Pia, tuligusia juu ya imani au ushauri visivyofanyiwa utafiti vinaweza kuvunja ndoa. Ndoa nyingi zimevunjika na nyingine zitavunjika kwa sababu hizo. Hivyo, kama njia ya kuwafunda vijana, tumeamua kuchagua kisa hiki kufikisha ujumbe na ujuzi kadhalika.

            Kuna kisa cha mama tulichosoma kwenye gazeti moja la nchini Zimbabwe. Kisa hiki ni juu ya mwanandoa mwenye majivuno na asiyetunza siri za ndoa yake. Akiwa amekwenda kusuka nywele kwenye saluni, alizoea kumlaumu mumewe kwa wenzake kuwa alikuwa akimwachia pesa kidogo. Maskini, kayaya huyu hakujua kuwa alichoona kidogo, kilikuwa kikubwa kwa wenzake. Hivyo, baada ya kuwa akijisifu kwa kumsimanga mumewe kwa ‘kutomwachia’ pesa nyingi, walitokea waliotamani wangeolewa naye wakaanza kumuandama hadi ndoa ikavunjika na  mhusika akashangaa kujikuta aliyechukua nafasi yake alikuwa ni  mmojawapo wa mashoga yake aliyezoea kumlalamikia juu ya tabia za mumewe. Kimsingi, huyu mama hakufunga miguu na kufungua macho. Alipaswa afunge mdomo na kufungua masikio. Je ni wangapi wameishashuhudia au kukutwa na haya? Je hapa utamlaumu nani kama siyo wewe mwenyewe? Huwa tunawashauri na kuwahimiza wanandoa kutofanya maisha yao au ndoa zao magazeti au matangazo.

            Je ni wangapi hufunga miguu na kufungua macho au kufanya kinyume? Je hili halina faida kubwa kwao kama watalishika, kulikumbuka na kulitekeleza?   Unaweza kujisikia raha kuwasimulia wenzako juu ya maisha yako bila kujua madhara yake. Hata hivyom si wasikilizaji wako wote hujisikia kama unavyojisikia. Hivyo, si vibaya kushauri na kusisitiza kwa wanandoa kuchambua na kujua ya kusema na kutosema. Tunajua kuwa si wote wanapata bahati au kuwa na desturi, mila, na tamaduni za kufanya hivi hasa wakati huu wa utandawazi ambapo vijana wanaweza kukulia mbali na jamii zao hadi kuoa au kuolewa. Hivyo, kwa kuliibua na kulikumbushia hili, tunalenga kuwasaidia wasio na fursa au walio nayo lakini wasizingatie.    

            Wewe na mwenzi wako ni sawa na kata na mtungi. Siri ya mtungi apaswaye kuijua ni kata tu. Hivyo, unapofungua mdomo ukaziba masikio, utaumia tu taka usitake. Kama hujaumia, ni suala la muda na si kama bali lini utaumia. Pia, ni vizuri kubainisha kuwa unapaswa kujua mambo ambayo ni siri na siyo siri. Kama hujui, acha kuongea kabisa ili usijikute ukivujisha siri ukidhani siyo siri wakati ni siri. Kwani usiposimulia juu ya maisha yako utakosa nini ikilinganishwa na kuyasimulia ukaishia kujuta? Hata habari huwa hatuzipati bure. Ima utanunua chombo cha habari kama gazeti, runinga, au redio ndio uzipate au ulipie kwa wanaozitoa. Mbali na majanga na misiba, hakuna habari za bure duniani hasa wakati huu ambapo kila kitu ni bidhaa inayoweza kutumiwa na baadhi ya watu kutengeneza faida hata kama ni kwa hasara ya au kuwaumiza wengine.

            Turejee tulikoanzia. Mbali na kushauriwa ufunge miguu na kufungua masikio, tuseme wazi. Je unakosa nini usipofichua siri zako? Je unapata nini unapozisambaza? Kwani, lazima kila unachofanya wakijue watu wakati hujui wafanyayo? Hata ukiyajua wafanyayo, kwani lazima uyafahamu kwa kuhatarisha maisha, ndoa, na siri zako? Hivyo, usikubali kuwa habari kwani si kila habari ni nzuri. Waandishi wa habari husema heri upate habari kuliko wewe kugeuka habari.

Chanzo: Mwananchi J'pili.


Saturday, 5 April 2025

Wamefyatuka wanafyatuana mbele ya mafyatu!


Juzi tilishangaa sana. Mwe! Nani angeamini kuwa mafyatu wanene na wanono wangefyatukiana na kufyatuana hadharani? Unene kweli taabu japo una raha ya kula bila kutoa jasho! Si fyatu mmoja aliyekaribu na mwenyewe kapwakia ulaji kiasi cha kuanza kuwapayukia walaji wa chini yake wasio na nasaba na mwenyewe! Fyatu huyu mwenye kutia shaka, inaonekana, hagusiki. Nani anaweza kumgusa Keinerugaby Mwana wa Mu7 pale jirani? Nasikia shemela zake nao wanafyatua ulaji simply because wanashea bedrooms na vitegemezi vya Mu7. Haka kaugonjwa kanaanza kuenea. Ukiachia mbali Mu7, Jake Zoomer wa Bondeni aliwahi kuruhusu kitegemezi chake kiitwacho Insectzane kutumia maulaji yake utadhani ufalme. Pale kwa Nyayo ya zamani, Billy Rootor na vitegemezi vyake ndo usiseme. Vinafyatua kama havina akili nzuri. Hali ilikuwa chafu hadi ikawapo ofisi ya first daughter. Mafyatu wa k ule walishupaa ikafyatuliwa mbali.
                Nchini Equatorial Guinea, kitegemezi cha mdingi ndiye makamu wa dingi yake. Wakati kaya ya jirani karibu na Diarasee, kitegemezi cha mdingi kinafyatua njuluku kama za dingi wake. Kule Gabon, kitegemezi cha king’ang’anizi aliyefyatua na kuibia kaya ile kwa zaidi ya miaka 40 kilifyatua maulaji baada ya dingi kufyatuliwa na Sir God mwenyewe. Hata hivyo, nacho kilifyatuliwa na geshi kikaishia kuuona unene runingani. Kule Tchad na Togo, bado vitegemezi vinatesa baada ya midingi yao kufyatuka na kurejesha namba.

Nirejee kayani. Japo si kwa sana ikizingatiwa kuwa Stone hakuendekeza ujinga huu sawa na Nchonga na Brother Ben Nkapa. Kamchezo ka kupeana ulaji kiukoo kanaanza kugeuka donda ndugu. Ajabu, mafyatu wanachekelea badala ya kufyatuka wakafyatyua hawa wanaowafyatua! Leo sifyatui majina ya mafyatu fyatuzi wanaofyatuana baada ya kuwafyatua mafyatu nikaishia kuchengetwa kama siyo kufyatuliwa au kuzuiwa ili nifyate. Natamani niorodheshe vitegemezi vya wanene vinavyofyatua mafyatu just because of their surnames. Wengine hata hawana surnames nene bali za madingi wa washirika wao wa bedroom kama aliyefyatuka juzi akamfyatukia fyatu mwenzake mbele ya mafyatu jamaa anayesifika kwa kufyatuka na kupayuka bila kichwa kuwasiliana na midomo.

Brother Al Chakumila upo hapo? Nilijisikia vibaya dogo fyatu wa mwenyewe alivyokufyatua mbele ya mafyatu asijue anaweza kuwafyatua wakafyatuka na kufyatua. Je kipindi hiki utapona kweli? Ilikuwajekuwaje ukamgusa pabaya fyatu wa mwenyewe? Umesahau ulivyopayuka ukafyatuliwa na kukaa pembeni hadi mwenye alipokuhurumia akakurejeshea ulaji unaoanza kudodesha? Inaonekana ufyatu umeanza kukuzidi hadi unajifyatua na kuishia kufyatuliwa. Kwanini hujifunzi au huna kumbukumbu? Ungejua namba unazocheza nazo, wala usingejifyatua ukaishia kufyatuliwa ukafyata. Umewapayukia wengine usijue duniani malipo ni hapa hapa. Sasa ona umefyatuliwa tena hadharani na unafyata. Ingekuwa mie, kwa ufyatu na ufyatuzi wangu, mbona nshajifyatua na kuachia ngazi zamani gani.

Kuna kamsemo kuwa madaraka hulevya chakari. Yakishakulevya, unapoteza uwezo wa kufikiri, kujifunza, kukumbuka, hata kuona na kukubali ukweli. Sijui kwanini mafyatu hawataki kujifunza toka kwa mafyatu waliotesa kama akina Nebukanezza, Mchonga, Jiwe, na wengine! Kufyatukiana na kufyatuana hadharani si uongozi bora bali bora uongo na uongozi. Inaboa na kukera my friends. Japo mafyatu waligoma kufyatua, angalieni msifyatuane mkaishia kuwafyatua wakawafyatua bila kutarajia.

Japo brother Moody alipomfyatua na kumfyatukia brother Al, alikuwa na pwenti, kwanini wasikutane faragha wakayamaliza au ni yale ya kutafuta ujiko wasijue wanavifua na kufuana nguo hadharani bila sababu za msingi. Huwezi kuruhusu ndinga zipitie kwenye uwanja wa mapipa hata kama una power. Huu siyo uzembe bali ni hatarishi kwa madebe na ndinga mbali na abiria. Inakuwaje kayani kila fyatu anajifanyia atakavyo kana kwamba hakuna sharia na miongozo? Huwa nashangaa kusikia eti mkuru wa uilaya anazuia say mikutano ya hadhara kwa vile wanaoiitisha ni wapingaji. Kwani wapingaji si wanakaya na wapo kinyume cha katiba? Mnamfyatua nani kwa kujifyatulisha? Mkifyatuliwa, mnaanza kulalama kama vichanga wanapofyatuliwa kutokana na ufyatu wao uchwara.

Sasa ufanye nini? Nakupa ushauri wa dezo. Achana na kufyatukafyatuka na kupayukapayuka hovyo. Utafyatuliwa. Shauri yako. Usijesema sikukuonya. Unene wa kupewa si unene kitu. Wapo wanaoulinda wakilala na kuamka wakiota ni jinsi gani waanzishe kwaya za sifa ili ulaji usiwatoke. Wapo ambao wako hata tayari kukufuru ilmradi waendelee na ulaji.

Hakuna fyatu anayenifurahisha hata kama sifurahi kama yule aliyefulia. Jamaa likifungua domo kufyatuka ni makufuru na sifa. Mara mwenyewe katenda miujiza, mara kavunja rekodi, mara hivi, mara vile ilmradi siku ziende na ulaji na ukamuaji viendelee. Kwa tunaojua haya mambo na dynamics zake usawa huu, unatumia busara ya Kijamaika isemayo play fool to catch wise. Ukijitia kujuajua na kufyatukafyatuka ukapayukapayuka, unafyatuliwa na wengine wanatesa. Nakushauri utafute the 48 laws of power upone. Hivi nshaamka usingizini?

Chanzo: Mwananchi J'tano iliyopita.