The Chant of Savant

Friday 28 September 2012

Hatimaye majeshi ya Kenya yaikamata Kismayo

Satellite map of KismayoHow KDF took KismayuMPs seek buffer zone after Kismayu take over
Habari zilizotufikia ni kwamba ngome kuu ya Al Shabab-Kismayo sasa iko chini ya majeshi ya Kenya pamoja na yale ya kulinda amani ya Umoja wa Afrika. Kuanguka kwa Kismayo laweza kuwa pigo la mwisho kwa kundi la Al Shabab kama siyo mwisho wake. Rais Mwai Kibaki wa Kenya amekaririwa akisema kuwa ushindi wa Kismayo ni game changer au tuseme karata ya mwisho. Je majeshi ya Kenya yataendelea kuikalia Kismayo na hatimaye kuikomboa Somalia? Ni suala la muda.

Thursday 27 September 2012

Kikwete apewa kitabu atakisoma?


Katibu mkuu wa zamani wa umoja wa mataifa (UN) Kofi Annan akisalimiana na rais Jakaya Kikwete baada ya kumkabidhi kitabu chake. Kwa wanaojua jinsi Kikwete anavyozidi kuua elimu na maadili nchini wanashangaa kama hii ni zawadi au suto. Je Kikwete asiye na muda wa kutulia hata kufanya kazi zake atapata muda wa kusoma hicho kitabu? Kikwete asiye na utamaduni wa kujisomea atakisoma au kukiweka kwenye shelves na huo kuwa mwisho wake? Kikwete rais atokanaye na kizazi kisichosoma wala kutunga na kuandika na kitabu wapi na wapi?

Wednesday 26 September 2012

Nani kiwanda cha uongo kati ya wapinzani na Kikwete?

 
Hivi karibuni, akizindua mradi wa ujenziw a daraja la Kigamboni jijini Dar es Salaam, rais Jakaya Kikwete alikaririwa akisema kuwa wapinzani wana viwanda vya uongo. Aliwanasihi bila kujinajisi, waache kusema uongo; wamsifie hata kama hawaoni sababu ya kufanya hivyo. Kwa wengi, maneno ya Kikwete yalikuwa kama harakati za mfa maji baada ya kuona mambo hayaendi. Hii ni kutokana na ukweli kuwa Kikwete hajakidhi matarajio ya watanzania.   Nikiri; ilikuwa ni mara ya kwanza kwangu kusikia kuwa kumbe kuna viwanda vya uongo.  Mwanzoni nilidhani nilikuwa nimesoma vibaya. Nilidhani alimaanisha viwanda vya gongo. Kumbe rais alimaanisha viwanda vya uongo!  Kwa hadhi na nafasi ya rais, kwanza, lugha aliyotumia ni ya matusi ukiachia mbali kusahau kuwa aliyeanzisha “viwanda” hiyo vya uongo hata kabla ya wapinzani ni yeye na chama chake.
 
Alikaririwa akisema, “Watu wana uongo mwingi eti nimeuza eneo kwa Bush, huo ni upotoshaji mwingi. Maana kuna watu kila kukicha wana viwanda vya kutengeneza uongo. Wako ambao hawapendi maendeleo,” 
Kuuza nchi si lazima auziwe George Bush. Je ni wawekezaji wangapi wanafanya mambo kama vile wamenunua Tanzania wakiwamo Dowans waliotokana na kampuni iliyoingizwa nchini kinyemela na Kikwete na Lowassa ya Richmond? Je ni matapeli wangapi wanaitwa wawekezaji wakati ni waganga njaa na makuadi wa wakubwa wenye madaraka wasio na uzalendo wala udhu wa kuwa hapo walipo? Hapa rais anataka kumdanganya na kumfanya nani mpumbavu asiyeona yanayoendelea?
 
Tofauti na wapinzani ni kwamba huyu mwanzilishi wa “viwanda” vya uongo ni mwepesi wa kusahau ukiachia mbali kupenda kujisahaulisha na kujifanya hajui kinachoendelea. Hivi kweli Tanzania kuna kiwanda cha uongo chenye ukubwa na hatari kuliko kile kiitwacho Jakaya Mrisho Kikwete aka Kipenzi cha watu? Kuna kiwanda cha uongo kama “Tumaini lililopotea?”
 
Hebu tumpe ushahidi ili angalau imsaidie mheshimiwa huu kuamua nani mwenye kiwanda au viwanda vya uongo. Mwaka 2005 akiwa mgombea wa CCM aliwaahidi watanzania maisha bora chini ya kauli mbiu ya Maisha bora kwa wote. Je Kama rais hakuongopa, anaweza kuonyesha nini zaidi ya kulalamika kuhusiana na maisha bora kwa watanzania? Tofauti na alivyoahidi, rais ameletea maisha balaa kwa watanzania kutokana na kudaiwa kuwa alipata ushindi na kuwa rais kupitia pesa chafu ya iliyotokana na ufisadi wa EPA ambayo hajawahi kukanusha wala kutolea maelezo.
 
Kikwete aliahidi kutaja mali zake na mkewe. Hili huwa hapendi kulisikia achia mbali kutoa maelezo au kuzitaja hizo mali. Je anaogopa nini? Je kwa kutotaja mali wakati alipaswa kufanya hivyo na akaahidi kufanya hivyo si uongo? Nilishaliandikia zaidi ya mara saba lakini rais hajawahi kutaka hata kuligusia. Hata watu wake wa usalama huwa wanahofia hata kupiga mkwara kwa gazeti kwa kuhofia mengi yataibuka kuhusiana na usafi wake binafsi.
 
Turejee kwenye “viwanda” vya uongo. Kikwete aliongeza na kusema, “Hili daraja na barabara ambazo nasimamia vitabeba watu wa vyama vyote CCM, CUF, CHADEMA, TLP na wasio na vyama na wasiposhukuru au wakishukuru shauri yao lakini maendeleo yanafanyika na watu wanaona hata kama wanajifanya hawaoni,.”
 
Hii ni kauli ya ajabu inayoonyesha uwezo ima uwezo mdogo wa msemaji kuelewa mambo au kuamua kuongopa kusudi. Kwani ni wapinzani gani waliwahi kudai kuwa daraja na barabara vitatumiwa na wana CCM tu? Je kusema kuwa wapinzani wanaangalia miradi ya kitaifa kama mali ya chama si kuzua hata kuongopa? Wapinzani hawana ugomvi na kuanzishwa kwa miradi ilmradi wapate maelezo ya kina jinsi pesa ya walipa kodi inavyotumika.  Na isitoshe, Kikwete na chama chake hawajengi hivyo vitu kama hisani au msaada kwa watanzania. Wala hawajengi kwa pesa yao. Ni kazi ya serikali kufanya vitu hivyo kutokana na ukweli kuwa wananchi wanalipa kodi. Kinachogomba kwanza ni umadhubuti au uwezo wa kufikia viwango vinavyokubalika na gharama za miradi hiyo. ni ajabu kwa Kikwete kudhani kuwa watanzania wengi walio makini wanajiuliza swali moja kuu: Kama daraja la Kigamboni litajengwa hovyo hovyo kama barabara zetu kutokana na tenda kupatikana kwa kutumia ten percent, siku moja litaua wangapi? Huu ndiyo wasi wasi wa watu wenye kufikiri sawa sawa wanaojua jinsi serikali ya Kikwete inavyoendeshwa.
 
Muulize Kikwete kama anakumbuka alivyowahi kutamba tena hadharani kuwa ana orodha za wezi bandarini, majambazi na wauza mihadarati. Kama anakumbuka muulize tena, aliwafanya nini kama kweli alikuwa ana orodha yao zaidi ya kunogesha stori. je kama kweli anazo orodha za wahusika na vyombo vya dola vya kuwashughulikia, ana maslahi gani au ameshindwa nini kuwashughulikia? Je kuendelea kutowashughulikia wakati aliahidi kuwashughulikia si uongo tosha?   Ukimuuliza hili naamini hatakuwa na la kukwambia zaidi ya kukuweka kwenye kundi la watu wasiopenda maendeleo yake. amini maneno yangu. Hata baada ya watu wake kusoma makala hii, hawatajibu kwa kujua fika watakuwa wanamvua nguo mtu wao anayewatuhumu wapinzani kufanya kile ambacho kimemweka madarakani.  Ni mtu wa namna hiyo na kwa kiasi fulani watanzania wameishamzoea wakiomba Mungu muda wake uishe ajiondokee.
 
Kikwete kama rais aliapa kulinda wananchi na raslimali zao. Muulize hili amelifanyaje iwapo wanyama wetu wanatoroshwa huku serikali yake ikiwa inasema eti haina habari. Wananchi wanauawa na polisi kwa maagizo ya Kikwete kupitia wateule wake na usalama nchini umekuwa tatizo. Je wapinzani wakisema kuwa Kikwete aliwaongopea watanzania kuwa atawalinda wakati hafanyi hivyo ni kuchukia maendeleo au kuunda viwanda vya uongo? kama hivi ndivyo viwanda anavyoongelea Kikwete, tofauti na chake, ni viwanda vizuri maana hii ndiyo kazi ya upinzani-kumkosoa na kumshauri wanapohisi anakwenda ndivyo sivyo.  Kikwete aliahidi angefuata sheria za nchi na kuzitekeleza bila ubaguzi. Katika hili amenoa karibu kila eneo. Kuna watu kama rafiki zake na washirika zake kama Edward Lowassa na Andrew Chenge wako juu ya sheria.  Pamoja na wengine kukiri na wengine kuletewa ushahidi wa kutosha wa kushiriki wizi na ufisadi, bado Kikwete anasema ni wachapa kazi bora hakuna mfano. Hivi kuna kiwanda cha uongo kama hiki. Leo nimeongelea uchache tu juu ya products za kiwanda cha uongo cha Jakaya Kikwete. Kwa ufupi ni kwamba kama wapinzani wana viwanda vya uongo basi ni jua kali. Kile kiwanda mama yao na kikubwa kuliko yote cha uongo nchini si kingine bali JMK.
Chanzo; Tanzania Daima Sept. 26, 2012.

Daraja la Kigamboni: Barua kwa Joni Bia Makufuri

 
Bwana Joni Kanywaji Makufuri,
Kwa heshima na taadhima napenda nikusalimie na kukutakia afya njema wakati nikiandika yafuatayo kama nilivyoelezwa.
Kwa ufupi hii ni injili kama ilivyoandikwa na Mtakatifu Mpayukaji Msemahovyo, mtume kwa walevi wote.
Hii mhishimiwa ni fursa ambayo hutaisahau maishani mwako kupata kuandikiwa waraka na mtume kama mimi.
Mimi ni tofauti na matapeli wanaojiita mitume na wachungaji wakati ni matapeli wa kawaida wanaowachuna watu kwa kutumia majoho na jina la Mungu.
Mimi ni tofauti na akina Ka-Tortoise, Rwakatarehe, Gamanyua, Mwakasenge, Lushekelo au Muzee wa Upakazio na matepeli wengine wengi waliojivika majoho wakati ni wezi wa kawaida.
Kijiwe kimeniagiza nikuandikie waraka huu kuelezea msimamo wao baada ya kuona walevi na Wadanganyika wakikenua njino walipomuona mkuu akizindua ujenzi wa daraja la kisasa na kisasi la Kigamboni. Wanakijiwe hawakuwa na furaha. Mwanzoni niliwashangaa nisijue nao walikuwa wakinishangaa!
Baada ya Dk. Msomi Mkatatamaa kunielimisha niligundua ni kwanini. Kuna madai kuwa kuna wahuni wanataka kutoza nauli ya kuvuka daraja hilo kwa vile wamelijenga. Kijiwe kinasema nasi tuwatoze kodi kwa kujenga kwenye ardhi na bahari yetu.
Wanakijiwe wana wasiwasi kuwa kama daraja litajengwa na makampuni yaliyopata tenda kupitia sayansi ya Ten percent basi litabomoka na kuangamiza maisha ya walevi wengi. Mie na bi mkubwa tunaogopa sana samaki. Kwani kwa mamia ya miaka, kama mkuu, tumekuwa na mapenzi makubwa ya kuwala.
Hivyo, tunahofia kuwa ufisadi wa ten percent unaweza kuwapa fish nafasi ya kutupenda kwa kutugeuza kitoweo kama ambayo maisha yetu yote tumewageuza.
Baada ya kutumia madaraka yangu kijiweni kumwezesha bi mkubwa kufungua NGO ambayo ilimuingiza pesa, tulifanikiwa kununua uwanja kule Kigamboni hasa baada ya kusikia kuwa kuna mpango wa kujenga daraja.
Hatukuwa tumeona mbali kama walevi. Pia tuna bahati kuwa uwanja wetu haukukumbwa na sekeseke la kupisha daraja na wajanja fulani kuutumia kujilipa fidia badala ya sisi.
Mwanzoni wasiwasi huu ulipoonyeshwa kwangu niliwaona walevi kama manazi wasiopenda hata kukubali kuwa haya ni maendeleo. Walinipa mifano ya barabara nyingi zilizojengwa ndani ya wiki na kuharibika ndani ya masaa kaya nzima.
Pia walikuwa na shaka na hili la kutozwa nauli. Walisema kuwa mbona kwenye daraja la Jangwani na mengine mengi hawatozwi ushuru wala nauli. Kwani daraja ni treni au basi au ndege? Je, daraja linatuma mafuta au umeme? Je, ni lini walevi watalitumia free wakati kaya na ardhi vyao vinatumika free?
Ingawa walevi ni walevi, wana hoja. Walisema kuwa wakikumbuka jinsi EPA ilivyoleta uchakachuaji wanakosa imani na binadamu ngurumbili.
Pia walitoa mfano wa Richmond ambapo mkuu na Ewassa waliahidi kuwa mgawo wa umeme ungekuwa historia na badala yake ikawa kinyume. Sana sana faida ya mgawo ni kutengeneza na kutotoa vitegemezi vingi ambavyo walevi hawawezi kuvimudu na mstakabali wao unazidi kubomolewa.
Mie nashukuru Mungu bi mkubwa alikubali ushauri wangu wa kuweka kakomeo ili asivitotoe vikatunyotoa roho maana ukiona hizo shule za kata na matuisheni ya wezi wanaoitwa walimu utaogopa. Jamani mtoto asipokwenda tuisheni siku mbili maksi zinashuka kama ndege ilizomika! Mwe! Tunakwenda wapi?
Sasa daraja likijengwa na watu wenye akili na roho za kituisheni si litaua hata kabla ya mwaka? Lazima tuseme kuwa daraja lisijengwe kivoda fasta ili kunusuru maisha ya walevi wetu wapenda amani na mshikamano hata kama havipo kivitendo bali kinadharia.
Wana Kijiwe siku zote ni mabingwa wa hoja kutokana na wote kuwa madaktari tena wa kusomea na si heshima kughushi wala kugawiwa kishikaji.
Walitoa pia mfano wa maisha bora kwa walevi wote ambayo yameishia kuwa maisha balaa kwao huku yakiwa bora kwa nyumba ntobhu. Hivyo siandiki kwa hiari yangu wala ushabiki bali kuwasilisha kilio cha walevi ili kikufikie nawe ukifikishe kunakohusika.
Kitu kingine walichoniambia walevi tena chenye kusikitisha ni wasiwasi wao kuhusiana na Eniesiesiefu (ENSSF) inayojenga hilo daraja. Tulikusikia ukisema kuwa mkurugenzi wake Juma Kidau apewe nishani badala ya wanagesi. Hayo ni yenu mtajuana. Mnaweza kupeana nishani hata za ufisadi na usanii. Walitaka kujua ni kwanini haina huruma na wachangiaji na inawekeza njuluku yao kwenye biashara wakati watoa michango wakiendelea kusota na hakuna anayejali?
Kusema ukweli nilishindwa kuwajibu kwa vile mie si mwajiriwa wa lisirikali na Eniesiesiefu wenye maulaji yao.
Kwanza, walevi walitaka wapewe hakikisho kuwa hakutakuwa na rushwa ya kuweza kusababisha daraja lijengwe chini ya kiwango na kuua walevi wasio na hatia kama ambavyo imewahi kutokea kwenye kashfa ya MV Bukoba na lile jahazi lililoua watu hivi karibuni kule Zenji.
Tukizingatia matukio hayo hapo juu ambayo yaliacha misiba mikubwa kwa walevi, kama thinkers of our own light and time, we need assurance from you by getting it from the mounth of the horse. Mark my words; I am not saying you are a horse neither are we. Again, we need convincing explanations befitting thinkers not horses like your cheerleaders and major domos.
Samahani mhishimiwa, huwa nina ka-ugonjwa ka kupandisha mwenembago ambapo hujikuta nikibwabwaja kikameruni ambacho naamini unakijua kutokana na kuwa daktari kama mimi. Najua udaktari wako siyo wa kupewa wala kughushi. Hivyo nisamehe. Naamini umenielewa bwana Kanywaji.
Tena kabla ya kusahau, napenda nichukue fursa hii kukwambia kuwa Kijiwe kimenituma nikwambie umwambie bosi wako aache matusi ya rejareja kama alilotoa juzi kuwa wapingaji wana viwanda vya kuunda uongo wakati mwanzilishi ni yeye.
Kusema ukweli mimi na wana Kijiwe hatukupenda haya matusi ya nguoni ikizingatiwa kuwa nasi ni wapinzani wanaopinga ulegelege na uholela wa lisirikali la jamaa yako.
Acha niwahi Brela kuona orodha ya makampuni yaliyopata tenda ya kujenga daraja na mbinu waliyotumia kupata ulaji huu.
Bwana Kanywaji, mfikishie salamu zake ndugu yetu, mpendwa wetu, kipenzi cha wengi na chaguo la God, Dk. Njaa Kaya.
Chanzo: Tanzania Daima Sept. 26,2012.