The Chant of Savant

Sunday 28 August 2016

Makonda kujengea Bakwata hapana


Image result for makonda na bakwata
            Mkuu wa mkoa wa Dar es Salaam, Paul Makonda alikaririwa hivi karibuni akiahidi kulijengea Baraka Kuu la Waislam Tanzania (BAKWATA) makao makuu yenye hadhi. Makonda alisema makao makuu hayo yatakuwa jengo la ghorofa tatu lenye thamani ya shilingi 5, 080, 155, 600. hii si pesa kichele. Wapo waliotaka kujua fedha hii Makonda inatoka wapi; na ni nani wako nyuma ya hisani hii ya aina yake katika historia ya taifa. Makonda anatoa jibu akisema “Leo nimefika hapa ikiwa ni mwanzo wa safari mpya ya serikali ya mkoa wa Dar kujenga makao makuu mpya ya kisasa ya ndugu zangu.” Hivyo wasiojua nani atajenga jengo hili wajue; ni utawala wa mkoa wa Dar es Salaam. Je kuna wanaomtuma na kumtumia kwa faida yao? Hili swali wanapaswa wajibu wananchi wa mkoa wa Dar es Salaam. Sijui kama wamempa kibali cha kujenga makao makuu ya taasisi ya kidini wakati shule nyingi za serikali ni hoi kimajengo ukiachia mbali wafanyakazi wengi wa serikali kutokuwa na nyumba za uhakika. Je nini mantiki ya kufikia kipaumbele hiki na mchakato gani wa kidemokrasia umepitisha mradi huu? Je watanzania watanufaikaje na mradi huu?
Makonda aliongeza “viongozi wangu wa BAKWATA, najua watu wote wana viongozi kama baba ni kiongozi wa familia, watu wana vyama vyao vya siasa wana viongozi, watu wana makampuni yao wana viongozi lakini viongozi hawa wanatofautiana na viongozi wa dini kwa jambo moja, viongozi wa dini wanatuongoza kutupeleka kwa mola alietuumba sote.”
Kuna maswali ambayo Makonda na waliomtuma walipaswa kujiuliza.
Mosi, je makao makuu ya Bakwata ni muhimu kuliko watoto wetu wengi wanaosomea kwenye majengo mabovu au walimu wao wasio na maslahi na mishahara ya kutosha ukiachia mbali kutokuwa na vitendea kazi vya kutosha na vya kisasa?
Pili, je kweli Bakwata inastahili kupewa kipaumbele hivi? Pamoja na kuwa mpokea zawadi hachagui zawadi ya kupewa, hivi kweli Bakwata ilihitaji hata msaada mchoro kweli? Wapo waliodhani; Makonda alikuwa amekurupuka kutafuta ima umaarufu au kutaka kuwatumia waislamu aonekane anachapa kazi na mtatuzi wa matatizo ya jamii.
Wapo wanaoona kama Makonda ameshauriwa vibaya kwa kuhangaika na kuwajengea watu makao ya kifahari kwa vile hayakukumfurahisha wakati anawaacha wasio na hata mlo mmoja. Wapo wanaohofia Makonda hatafanikiwa katika kupata hicho unachokitafuta. Hali inakuwa ngumu hasa mtumishi wa umma unapojiingiza kwenye mambo ya dini wakati serikali haina na haipaswi kupendelea dini yoyote.  Wapo wanaodhani kuwa bilioni tano na ushei ni pesa ambayo si rahisi kuipata. Hata hivyo, inavyoonekana, Makonda anazo fedha. Maana alikaririwa akisema; anataka jengo lake likamilike ndani ya miezi 14. Huyu atakuwa na fedha. Kinachogomba ni alivyoipata na namna anavyotaka kuitumia kwenye nchi yenye matatizo mia kidogo.
Wapo wanaoona kama serikali ina fedha ya hata kujenga makao makuu ya asasi za kiraia wakati makao makuu yanaishinda, basi imekosa kipaumbele. Je serikali itapata faida gani kujiingiza kwenye biashara ya dini au kuchanganya siasa na dini? Sijui inatoa somo gani kwa watanzania wenye shida za msingi kama vile ukosefu wa maji, umeme na huduma nyingine? Je huku si kuwatumia waumini kisiasa jambo ambalo ni hatari huko tuendako? Wakati mwingine mtu anaweza kutaka kufanya jambo jema kwa njia mbaya. Hapa ndipo utata unapoanza. Huwezi kutumia fedha au nafasi ya umma kupigania haki ya kundi moja wakati ukiyaacha mengine.
Je Makonda na wanaomtuma walijua kuwa:
Mosi, Bakwata wana mali zao kama vile majengo na mali za wakfu ambazo zimetumiwa vibaya kiasi cha kuwaweka matatani baadhi ya waislam wakereketwa kama Shehe Ponda Juma Ponda. Heri Makonda angewapa Bakwata wakaguzi wa mahesabu na mali.
Pili, popote anapopata hiyo fedha, anaigawa kama nani wakati kuna matatizo kibao ya maana yanayolikabili taifa? Kama ni ya serikali ni kwa sheria gani au ni yale yale kuwa kuna watu sasa wana uwezo wa kujifanyia lolote bila kujali sheria kwa vile wako karibu na wakubwa zaidi? Je huu mradi umeridhiwa na mkoa; kwa faida gani na utajiri gani?
Tatu, kwanini hiyo pesa isielekezwe kwenye ujenzi wa madarasa, nyumba za walimu, maabara au kuboresha maslahi ya walimu badala ya kuwajengea wetu wenye uwezo na wajibu wa kujijengea makao yao makuu?
Nne, je Makonda na wenzake wanafahamu; serikali wanayoiongoza inaombaomba kwa wafadhili kutunisha bajeti ukiachia mbali michango kwenye madawati?
Tano, Kwanini serikali hata iwe ya mkoa tu ipate fedha ya kujenga makao makuu ya Bakwata wakati vijijini fedha inaenda kiduchu?
Sita, je lisingekuwa jambo la busara kwa fedha hiyo kuelekezwa kwa vijana wengi wanaohenyeshwa na mikopo ya elimu ya juu au zahanati nyingi zisizo na madawa au majengo stahiki? Hakika maswali ni mengi kuliko majibu.
Tumalizie kwa kuuliza maswali. Je Makonda na wenzake wanafahamu kuwa wanachotaka kufanya–pamoja na uzuri wake–kinaweza kutafsiriwa kama hongo au kishawishi kwa wahusika kwa malengo ya kisiasa hata kama si hivyo?
Saba, je Makonda na wenzake wamepata mchango wa wapinzani ambao nao wanaunda serikali ya mkoa wa Dar es Salaam hasa kwa kuzingatia mileage Makonda na wenzake wataipata kisiasa? Maana, wangefanya wao wangeambiwa wanachanganya dini na siasa.
Mwisho, je utajengea wangapi?
Chanzo: Tanzania Daima Jumapili leo.

Saturday 27 August 2016

Mlevi kuwa bilionea kupitia bwimbwi

Baada ya kugundua kuwa nyavu za kupambana na uhalifu haziwagusi wauza bwimbwi na mafwisadi wakubwakubwa hasa waliokuwa marahis Mlevi nimeamua kuingia kwenye biashara ya bwimbwi tena bila kificho. Kwa vile mapapa wa bwimbwi ni untouchable, mlevi niogope nini kutia timu kwenye genge hili ili lau nami nichange njuluku ikiwezekana niwe bilionea kama Mo Jewji ambaye nilisikia akisema kuwa amejiunga na club ya mabilionea watakaogawa utajiri wao? Hakuna kilichonishangaza kusikia kuwa Jewji atagawa utajiri wake dunia nzima wakati aliuchuma kayani. Ama kweli, gabacholi wakati mwingine si wa kuamini. Sitashangaa kusikia kuwa Ugabacholini watapewa dau kubwa huku wadanganyika wakiishia kuusoma ukwasi huu magazetini.
Hakuna kitu kingine kilinkata kama kusikia kuwa na yule jambazi wa Kagoda ni bilionea wakati aliiba njuluku za walevi kupitia EPA na ujambazi mwingine. Kesho sitashangaa majambazi kama Ni Zero Kadamage yule jambazi wa Buzwagi aliyekwenda kuingia mkataba hotelini kule Uingerezani akitajwa kuwa bilionea wa Danganyika aka Bongolalaland.
Kama haitoshi, sitashangaa kusikia jambazi mwingine wa UdA ambaye hivi karibuni alibainika kuuziwa kiwanda cha mabilioni ya madafu kwa madafu milioni thelathini juu ya kugawiwa Dart naye akiingia kwenye club ya mabilionea. Hapa usisahau kuwa na mshitiri wake Riz naye siku moja ataitwa bilionea. Kwa wachumi kama mimi, natabiri kuwa Danganyika itazalisha mabilionea wengi kiasi cha kuchanganya dunia. Hapa rafiki yangu Jose Gwaijimmy, Kartortoise, Rwakatarehe, Gamanyue, Mwakasenge na wengine wanaotumia neno la Bwana kuwaibia wachovu nao bila shaka watatia timu kwenye club hii ya wakwasi.
Kwa vile nami nauzimia na kuukamia ukwasi, lazima niuze bwimbwi bila kujali kuwa vijana wetu wanaumizwa nalo. Mwanzoni nilikamia kuuza mibwimbwi baada ya kugundulika kuwa pale uwanja wa ndege wa mzee Mchonga wa Burito madude yalikuwa yanajipitia baada ya wanahizaya kuua mitambo ili kupitisha mizigo yao na wenzao. Baada ya mambo kuchenji, ilibidi nitulize boli na kusaka fursa nyingine ambayo nimeideku baada ya kuangalia historia ya trejecktori ya mapambano dhidi ya utengenezaji ukwasi wa haraka. Bandarini, kwenye mita za mafuta, mipakani, TRA, Banki kubwa na kwingineko ameziba. Kwa vile ameamua kuachia mibwimbwi iendelee kutawala, kwanini bingwa nisiiuze na kuwa bilionea?
Najua wengi wanaona kama ndoto za mchana na matokeo ya ile kitu ambayo huwa navuta. They are dead wrong. Seriously lazima nifanye biashara ya hii kitu hasa baada ya kuona wengi wakiifanya na kuibuka kwa wakwasi wa kutisha na kuogopewa kayani. Hamuoni watu wanavyoangusha mahekalu na migari ya bei mbaya kama Lungumingumi? Nani hataki kuwa bilionea kama kina Jewji na Roast Tamu?
Nina uhakika; hapa nitasepa na kupeta na kutokezea kuwa bilionea ghafla bin vu. Jiulize; tangu itangazwe vita dhidi ya ufisadi na uovu mwingine, mzungu gani wa bwimbwi ameishanyakwa na kunyea debe? Hakuna. Sasa kama hali ni hivyo, kuna haja gani kudharau mitikasi yangu ya kuuza mibwimbwi na kuukata hadi nikaitwa mtukufu, mheshimiwa, mpendwa, bilionea Mlevi mwana wa Mvuta ile kitu? Kwanini wewe unayekandia na kudharau mipango yangu hutaki kuelewa kuwa nikishazinyaka njuluku nitakuwa mwekezaji kama Kisenena ima kwa kununua makampuni kama UdA au ginneries za kuchambulia pamba tena kwa bei ya mchekea kama jamaa alivyofanya hadi kumuudhi dokta Kanywaji aliyetoa amri hivi karibuni kuwa jamaa arejeshe kiwanda lakini akagoma kumwambia arejeshe UdA na Udart aliyogawiwa hivi karibuni? Kwanini Mlevi nilaze damu wakati najua lisirikali linajichanganyasometimes  kama lilivyofanya kwenye kuigawa Udart kwa walioiba UdA badala ya kuwasweka lupango?
Kitu kingine kinachonipa imani ni ile ya kuwa kayani kwetu, ukilala apeche alolo na ukaamka bilionea, hakuna anayekuuliza ulivyochanganya njuluku haraka hivyo. Kwanini hiki kisiwe kishawishi kizuri cha wanjanja kama mimi kutgengeneza njuluk kwa njia yoyote? Danganyika aka Bongolalaland kaya nzuri sana. Angalia baadhi ya wachunaji wanavyomilki hata michopa huku wakipigapiga mikelele utadhani viongozi wa upingaji na wasifanywe kitu hata kuwauliza waeleze walivyochuma ukwasi. Kwanini mimi nilaze damu wakati milango ya kutengeneza ukwasi na kuwa bilionea chapchap kwa njia yoyote iwa halali au haramu iko wazi? My foot! Hii kitu lazima niifanye bila kujali watakaoumizwa nayo.  Mbona viwanda vya fegi vinanyonga wengi na hakuna anayejali wala kuadhibiwa? Mbona uchafuzi wa mazingira utokanao na utapishaji wa vimiminika vyenye sumu unaua wengi na hakuna anayejali? Nani hakuona mafwisadi wa Nida walivyotengeneza njuluku kwa kulangua vitambulisho ukiachia mbali kuwapa hata wasio raia? Nani anajali usawa huu kama wauza bwimbwi na waovu wengine wanaendelea kuwa mabilionea? Lazima niiuze bwimbwi ili kuwa bilionea au ikiwezekana kuazisha Kagoda namba mbili au siyo? Kwanini nisiiunde kama Kagoda one imezalisha bilionea ambaye alipaswa kuwa lupango akingojea kunyongwa?
Leo sitachonga sana. Badala yake nakwenda kusuka misheni ya kufanikisha dili la kuwa bilionea chapchap na kugeuka mwekezaji wa ndani hata kama ni mchuguaji actually.
Chanzo: Nipashe Jumapili Leo.

Wednesday 24 August 2016

Kijiwe chastukia ushauri wa kufyatua vitegemezi


Baada ya rahis kutoa amri kuwa wachovu wafyatue vinyemelezi, Kijiwe kimeamua kutoa angalizo juu ya ushauri na ushawishi huu ambao unaweza kukwamisha maendeleo na harakati za kaya za kujikomboa na umaskini na uombaomba.
Leo anayelianzisha ni Mbwamwitu. Baada ya kuamkua anakula mic, “Wazee mmesikia amri ya rais dokta Joni Kanywaji Makufuli kuwa lazima wachovu wafyatue vitegemezi kama hawana akili nzuri? Je nyie mmepanga kulitekeleza vipi?” anamalizia maswali yake huku akimdeku da Sofia Lion aka Kaunungaembe.
Mgosi Machungi hajivungi; anakula mic, “Mwenzenu sihitaji hivyo vitegemezi kwani ninavyo vingi kwei kwei. Laiti munene angejua adha za kuwa na vitegemezi ukuki waa asingetoa tamko hii ambao wengi wataichukuia siiyasii kiasi cha kuzaisha tatizo jingine. Tisiunge mkono ushaui huu hasa usawa huu wa kaya maskini na ombaomba.”
Msomi Mkatatamaa anakula mic, “Nadhani daktari wa tujipu alikuwa anatania watani zake wazaramizi vinginevyo–kama alimaanisha–basi akubali kuwa anatengeneza majipu mengine.  Sioni motisha ya watu wenye kuelewa mambo kuongeza vitegemezi hasa usawa huu wa kutumbuana na kubana matumizi. Kama ni elimu ya bure, hivyo vitegemezi si kabichi kuwa vitakuwa ndani ya miezi mitatu ndiyo vifaidi hiyo elimu ya bure. Vingi vya vitakavyofyatuliwa vitaingia kwenye shule za bure wakati jamaa akimalizia ngwe ya pili kama wachovu watampa. Hivyo, ushauri huu uchukuliwe kama utani na si ukweli.”
Mpemba anapoka mic na kudema, “yake mie siamini kama rahis alikuwa atania. Maana alirudia kauli yake ya kutaka watu wafyatue vitegemezi kwa kuwataka hata akina mama wasitumie madawa ya kuzuia kuzalisha vitegemezi. Nimjuavyo mimi dokta Kanywaji huwa si mtu wa utani. Nadhani alishauriwa vibaya au aliangalia vibaya mambo kiasi cha kutoa amri ya kuunda bomu ambalo wakati likifyatuka atakuwa mstaafu.”
Kapende anamuunga mkono Mgosi kwa kusema, “hata mimi nilishangaa kusikia kauli hii ambayo asipotafuta namna ya kuiweka sawa, inaweza kukamisha mipango yake mizuri. Nadhani hao vitegemezi anaotaka tufyatue hawahitaji elimu ya bure tu. Wanahitaji matunzo na mahitaji mengine muhimu kama vile ajira kwa wazazi wao, malazi na makandokando mengine.”
Mzee Maneno anaamua kumpinga Kapende, “kusema ukweli mimi namuunga mkono mtani wangu. Kama kaya inaweza kupokea wakimbizi na kuwapa uraia kila siku ukiachia mbali kujaa magabacholi na machina kibao, kwanini tusipunguze kutoa uraia wetu kama njugu na kujifyatulia wanakaya wenyewe? Nadhani hasara wanayosababisha wakimbizi wa kiuchumi toka Uhindi na Uchinani hata Unigeriani na Kenya ni makubwa kuliko vitegemezi tutakavyotengeneza wenyewe.”
Mijjinga anamuunga mkono Mzee Maneno, “nyie mnashangaa la kujaza wakimbizi wa kiuchumi! Hamuoni hili la kuunda umoja na vijikaya visivyo na ardhi huku vikitushupalia kuwa turuhu free movement vimuvu na kuchukua ardhi yetu? Hamjaona vijikaya uchwara vilivyotuzunguka vinavyotia kila mchakato wa kutaka kuja kufaidi ardhi yetu au hamuoni?”
Mpemba anakamua mic, “yakhe naamini kuwa hapa wasomi tuna tena wengi kweli kweli. Hata mie naona hili laingia akilini sana. Heri huyu bwana azuie uingiaji wa wakimbizi uchwara wa kiuchumi na miungano na vijikaya vingine wakati ule wa Zenj bado wantoa jasho. Heri angefyatua ajira na viwanda kwanza, haya ya vitegemezi yakaja baadaye baada ya kuona matunda ya majaribio yake wallahi.”
Kanji anakula mic, “veve Pemba sema kitu ya maana sasa. Kana Kufuli nafyatua jobs naveza leta endeleo kuba sana. Sana kama chovu nazaa kama kuku hapana ona kaya takosa riziki ya kulisha yeye? Kwanini hapana soma toka India. Kule hindi nazaa kama kuku na kila siku vatu naongezeka na nateseka sana.”
Da Sofia anampoka Kanji mic, “kwa vile mipango ya Kiswahili–mara nyingi ni ya muda mfupi–huenda mhishimiwa ametumia kigezo hicho bila kuangalia mambo mengine muhimu yanayoyitajika kama vile hospitali na zahanati za kutosha, huduma safi, madaktari na wakunga wa kutosha na mambo mengine nyeti.”
Mipawa ambaye muda wote alikuwa akiangalia huku akitabasamu, anawaacha wana kijiwe hoi. Anakula mic, “beng’we, sasa mie acha nitume fedha ya kununulia ng’ombe tayari kuongeza ngoma ya pili ili nitekeleze agizo la rahis bila kughairi wala kuuliza. Nyinyi mmeambiwaga mfyatuage vitegemezi mnaanza kuumiza vichwa wakati sirikali lipo litabeba mzigo wake. Nawashaurini tutekeleze wito wa rahis wa kufyatua vitegemezi huku tukimtaka naye afyatue huduma kama wajibu wake au vipi?”
Msomi aliyekuwa akinong’ona jambo na Mpemba anaamua kutia guu tena, “japo sina wasi wasi na uchapakazi na mipango ya bwana Kanywaji, hili sitaliunga mkono hasa kama mchumi. Huwezi kuongeza idadi ya wana kaya wakati iliyopo inakuelemea. Huwezi. Kufanya hivyo ni kujipiga mtama. Hivyo, nisiseme mengi, kuna haja ya kupanga kwenda kuonana na rahis kumshauri akanushe kauli hii kabla hajatengeneza balaa jingine. Nadhani kwa sasa kaya aihitaji vitegemezi badala kujitegemea.”
Kijiwe kikiwa kinanoga si Mipawa akaaga anaelekea zake usukumani kutafuta ngoma ya pili ili afyatue vitegemezi! Wote tulibaki hoi tusijue la kumshauri. Ama kweli usilojua sawa na usiku wa kiza!
Chanzo: Tanzania Daima leo.

Sunday 21 August 2016

Magufuli ataibadili CCM au itambadili?

            Rais na mkiti wa CCM, Dk. John Magufuli amekaririwa mara nyingi akilaumu serikali iliyopita kwa kulegalega na kuruhusu uhujumu wa taifa. Amekuwa akisikika mara nyingi akisema; Tanzania ilikuwa imegeuzwa shamba la bibi na genge la watu wachache tokana na ufisadi na uzembe wa wale waliomtangulia. Hata hivyo, jambo moja linawashangaza wachambuzi wengi.  Pamoja na Magufuli kufichua na kulaumu uoza wa watangulizi wake, ameahidi kuwalinda wananchi walipomtaka awafikishe mahakamani. Tokana na hili, Magufuli anawapa taabu walio wengi kuamini kama anasema atakachotenda na kutenda atakachosema bila upendeleo, huba wala ubaguzi wakati ameishaonyesha upendeleo wa wazi kwa watangulizi wake wenye madhambi lukuki.
 Tujiulize; je hiyo serikali iliyolegalega ikaruhusu hujuma kwa taifa iliundwa na chama gani kama siyo Chama Cha Mapinduzi (CCM) alichopewa kuiongoza? Je kuna namna Magufuli anaweza kufanikiwa kuibadili Tanzania bila kuibadili CCM? Je Magufuli ataweza kuibadili CCM au itambidili?
Kwa wanaochunguza mwenendo wa Magufuli na timu aliyo nayo, kuna uwezekano CCM kumbadili.  Kwa mfano, wapo wanaoshangaa mantiki ya kubakisha sekretarieti ya CCM iliyosimamia madudu haya yote. Pia, wapo wanaoshangaa mantiki ya kumuacha mtendaji mkuu wa CCM, yaani Katibu Mkuu, Abdrahaman Kinana ambaye aliwahi kutuhumiwa kuhujumu taifa ukiachia mbali kusimamia chama dhaifu na fisadi hadi kilipokabidhiwa mikononi mwa Magufuli. Kampuni ya Kinana imewahi kutuhumiwa kusafirisha nyara za umma.   Nadhani hii ilitoshe kumwashia Magufuli taa nyekundu na kutombakiza kwenye nafasi nyeti chamani.
 Hata hivyo, wapo wanaotabiri kuwa Magufuli ametafuta fursa ya kukifumua chama kwa kumbakisha Kinana akitafuta fursa ya kupata mtu anayefaa. Wengine wanakwenda mbali na kutabiri kuwa Kinana ataondoka kama aliyekuwa Katibu Kiongozi, Ombeni Sefue baada ya Magufuli kumbakisha na akamtumbua baadaye baada ya kupata mtu wa kufaa kwenye nafasi yake. Tunaweza kusema bila wasi wasi kuwa dirisha la kuibadili CCM kabla ya kumbadilisha Magufuli unaweza kuliona kupitia kuendelea kuwepo kwa Kinana ambaye–pamoja na kusifiwa kukiendesha chama–ukilinganisha matarajio ya watanzania kwa chama tawala, huoni cha mno kwa Kinana kuendelea kuwa mtendaji mkuu wa CCM ile ile aliyoiacha ikatekwa na kutwaliwa na mafisadi na magenge ya wahalifu.
Kadhia nyingine inayoonyesha kuwa hadi sasa CCM imembadili Magufuli kabla hajaibadili inahusisha makada wa CCM wenye tuhuma mbali mbali za kifisadi kama vile uuzaji mihadarati, wizi wa mali za chama na umma, uzembe, kujuana, matumizi mabaya ya fedha za umma, ubinafsi, na kadhia nyingine nyingi tena wanaojulika.
Bado Magufuli hatajatangaza kifo cha mitandao ya kifisadi iliyokidhoofisha chama kiasi cha kugeuka kama club ya matajiri kutumia kuliibia taifa.
Kimsingi, bila kukifumua na kukisuka upya chama–jambo ambalo, hakuna shaka, Magufuli anaonekana kukamia kutenda–ataishia kubadilishwa na CCM na kuwa kama wale ambao sasa anawalaumu kwa kukwamisha taifa letu chini ya siasa chafu na za kichoyo za kujuana na kujihudumia kama ilivyokuwa kwa miongi mingi tangu aondoke baba wa taifa Mwl Julius Kambarage Nyerere mwaka 1985.
Tuseme wazi; ni mapema mno kupitisha hukumu kwa Magufuli japo si vibaya kuanza kuiandaa kulingana na kutokana na namna anavyopambana na matatizo sugu ndani ya chama na nchi.  Kwanza, ni kutokan ana ufupi wa muda. Magufuli hajatimiza hata mwaka tangu aingie madarakani kama rais wa Tanzania ukiachia mbali kuwa kwenye uenyekiti wa CCM kwa mwezi mmoja tu.
  Pili ni ile staili yake ya kutotabirika kirahisi. Wapo wanaoona kuwa Magufuli amejipa nafasi ya kuisoma mifumo ya ndani ya CCM ili kuweza kujua namna ya kukibadili chama kabla hakijambadili; hasa ikizingatiwa kuwa CCM ni taasisi kubwa ambayo imechafuka kwa muda mrefu. Hivyo, si busara kukurupuka na kuanza kufyeka kila kitu bila kujua undani na mbadala wake. Muhimu ni kumbukumbusha Magufuli–ambaye watanzani wengi bado wana imani naye–kuwa timming na muda katika uongozi ni jambo muhimu sana. Kama Magufuli atachelewa kuchukua hatua za kukibadili chama, uwezekano wa kubadilishwa ni mkubwa kuliko kukibadili chama.
Tatu, kutokana na uoza wa muda mrefu wa kimfumo, uwezekano wa Magufuli kuchukua muda mrefu kutimiza anayotaka kutimiza ni mkubwa hata ikiwezekana kumaliza muda wake bila kukamilisha kazi anayoanza kwa chama na taifa.
Nne, kitakachoamua kama Magufuli ameibadili CCM au imembadili ni matunda ya kazi yake. Hapa lazima tuwe wazi. Magufuli anaweza kufanikiwa kutekeleza anayoamini yatabadili mfumo mfu na fisadi uliojengeka kwa zaidi ya miongo mitatu. Ingawa, anaweza asikidhi matarajio ya watanzania kutokana na kuchoswa na kuumizwa na mfumo huu.
Tano na mwisho, vyovyote itakavyokuwa, Magufuli ataacha CCM mpya kulinganisha na ile aliyokabidhiwa ikichungulia kaburi. Rejea kutetemeshwa na kada wake, waziri mkuu wa zamani Edward Lowassa aliyepambana na Magufuli kwenye uchaguzi mkuu akiibuka mshindi wa pili kwa kura 6,072,848 sawa na aslimia 39.97 ya kura zote dhidi ya kura 8,882,935 ikiwa ni aslimia 58.46 ya kura zote (BBC, Oktoba 30, 2015). Unaweza kuona kuwa hapa hapakuwa na ushindi wa kishindo wala wa ki-Tsunami kama ilivyozoeleka.
Kwani mwaka 1995 Jakaya Kikwete alipata jumla ya kura 5,276,827 ambazo ni sawa na asilimia 61.17 ya kura zote zilizopigwa (BBC, 5 Novemba, 2010).
Chanzo: Tanzania Daima Jumapili leo.

Wednesday 17 August 2016

Kijiwe chataka CCM irejeshe mali za umma


          Baada ya mwenyekiti mpya wa Chama Cha Makabaila (CCM) dokta Joni Kanywaji Makufuli kufichua kuwa kumbe CCM inamilki vitega uchumi zaidi ya 500 kayani, kijiwe kimeamua kumkabili kumwambia aitumbue CCM kwa kurejesha mali hizo ambazo nyingi ni viwanja  sirikalini.
Msomi Mkatatamaa ndiye analianzisha, “Jamani mmesikia hii mpya kuwa Chama Cha Makabaila kinamilki viwanja na vitega uchumi kayani kote?”
Kabla ya kuendelea, Mpemba anachomekea, “Japo nilikuwa najua kuwa ufisadi huu wa kunyakua umekuwapo kwa muda nrefu chini ya chama kimoja, sikujua kuwa kumbe walokuwa wakifaidi ni mafisadi na si chama hata kama nacho kina hatia ya kukwapua ardhi.”
Msomi anaendelea, “Nakubaliana nawe. Hili si jipya. Jipya ni kwamba huu ni mtihani kwa dokta Kanywaji anayesema anataka kuwaondolea wachovu kero. Nadhani kero mojawapo ni kutwaliwa kwa viwanja na ardhi yao na kutumiwa na chama kimoja wakati ni mali ya wote bila kujali vyama vyao.”
Kapende anapoka mic, “Kisheria, alichosema mkiti ni ushahidi tosha kukishughulikia chama chake. Hapa nashauri tushupae kuhakikisha vile viwanja vinarejeshwa sirikalini kama alivyofanya kwenye kota za Migomigo baada ya mafisadi kutaka kuwadhulumu wachovu.”
Mipawa anakatua mic, “Nakubaliana na ushauri wako. Ila nitaongeza kidogo. Lazima tumbane jamaa si kurudisha tu viwanja vilivyokuwa vikifisadiwa  na kumilkiwa kinyume cha sheria na CCM bali arejeshe na nyumba za wachovu alizouza Nkapa.”
Mijjinga naye anaamua kutia guu, “Ukisikia ujipu ni huu. Kwanza, ilikuwaje kaya ya kijamaa kuruhusu chama tena twawala kujiingiza kwenye uporaji viwanja na ukabaila? Je chama kinachotawala na kufanya biashara kitaacha kuichuuza kaya?”
Kabla ya kuendelea Mgosi Machungi anamchomekea, “Mgosi unataka kaya iuzwe maa ngapi wakati iishauzwa? Huoni jamaa anavyohangaika na ufisadi uioanzishwa na chama hiki hiki kinachotusanifu kuwa kipo kwa ajii ya wachomu? Hapa azima tiseme ukwei kuwa dokta wa majipu azima aitumbue CCM kwanza ndipo aendee na majipu mengine.”
Msomi anarejea, “Nadhani jamaa alipofichua siri hii hakujua madhara yake. Kwa vile tuna ushahidi wa kukiri kwake, kama atafanya vinginevyo, tunaweza kwenda hata kwenye mahakama za kimataifa kudai ardhi ya wachovu au siyo? Hakuna kilichoniacha hoi kama alivyoshangiliwa na wachovu huku vigogo wakishikwa na bumbuwazi kwa kumpitisha kwa kura zote wasijue atawatumbua.”
            dada Sofia Lion Kanungaembe anakula mic, “Hakuna aliponikuna dokta Kanywaji kama kuzifichua asasi za wizi kama vile umoja wa vijana na akina mama na wazazi ambazo ni taasisi za kiulaji zisizo na faida kwa chama wala umma. Nangoja kuona atakavyotumbua wakubwa wa asasi hizi ambazo zimetumika kwa muda mrefu kama mirija. Halo halo!”
Kanji anakula mic, “Veve sangaa hii jumuiya! Iko witu wingi kama vile SUKITA nakula juluku ya chovu. Mimi ona ajabu sana kweli. Kama chama namilki mali nyingi hiwi, kwanini kila chaguzi nenda kwa gabacholi ombaomba kama sikini?”
Mheshimiwa Bwege anatia buti, “Nyie mnashangaa samaki kufa kiu wakati amezungukwa na maji! Kwa kaya yetu ilivyojaliwa–kama chama twawala kisingekuwa kinafanya kazi ya kuwala wachovu–kina uwezo wa kuifanya kaya hii kuwa Ulaya nayo ikatoa misaada kwa kaya chovu duniani. Hata hivyo, unategemea nini unapokuwa na hamnazo wakisimamia shamba la bibi wakati bibi mwenyewe ni kipofu? Hapa kweli mtakoswa kuliwa hata kama neno lenyewe najua linaudhi? Ukisikia ubwege ndiyo huu na siyo wa jina kama langu.”
Mgosi anarejea, “ tate nane tate nane.Waahi maneno yenu yanamiumiza kwei kwei. Yaani tinatenzwa kama hatina akii jamani? Sasa nasema wazi kuwa azima tiende kwa huyo dokta Kanywaji na timwambie atiudishie mai zetu haaka kabla hatijatia mtu zongo.”
Kabla ya Mgosi kumaliza, Kapende anamchomekea, “Kaka ngoja nikuchomekee hata kama sina tabia hii.”
Kabla ya kuendelea, Mgosi anajibu, “Kapende angai maneno yako. Tiheshimiane. Yaani wewe ni wa kunichomekea mimi?”
Kapende anajibu huku akicheka, “Sina maana mbaya Mgosi. Ninachotaka kusema ni kwamba  habari kuwa chama tena kinachojidai kutetea wanyonge kinamilki viwanja zaidi ya 500 ni kufuru ya kupaswa kuwatia chuki wahanga wakafanya kitu cha maana. Hapa lazima ikiwezekana tuanzie hapa kwenda kumuona dokta Kanywaji kumtaka arejeshe mali zetu na kulipa fidia kwa miaka ambazo mali za umma zimetumiwa kinyume cha sheria.”
Kabla ya kuendelea Mipawa anakula mic, “Kwanini tusiondoke hapa tukaanzia pake SUKITA na kutaka kujua walioifilisi huku tukitaka watupe hati zake ili tumpe dokta Kanywaji kama kianzio?”
Kabla ya Mipawa kuendelea, Msomi anamchomekea, “Sidhani kama kuna haja ya kuamini kuwa dokta Kanywaji anaweza kutatua kila tatizo wakati sisi wahanga tukiangalia kama hayatuhusu. Kwanza, yeye ni mwana chama hicho hicho. Pili, hawezi kufanya kila kitu. Hivyo, nashauri tumsaidie kwa kwenda na kukamata mali zote za umma tunazojua bila kungoja CCM iorodheshe na kuficha baadhi. Ni rahisi kujua viwanja vya umma vinavyomilkiwa na CCM kinyume cha sheria. Si huwa wengi wanapaki mikangafu yao pale?”
Kijiwe kikiwa kinanoga si lakipita shangingi la kigogo wa CCM aliyeua SUKITA. Acha tumtoe mkuku!
Chanzo: Tanzania Daima Jumatano leo.

Sunday 14 August 2016

Kufungiwa Mseto ni vitisho na uonevu


            Kufungiwa kwa gazeti la kila wiki la Mseto tokana na kile kinachodaiwa kuandika habari za uchochezi, kuna kila sababu na ushahidi kuwa hatua hii–licha ya kulihujumu  gazeti na kutishia uhuru wa vyombo vya habari–imelenga kulikomoa na kulinyamazisha gazeti kama onyo kwa magazeti mengine yasiyolalia upande wa watawala.
Kwanza, inashangaza kuona Tanzania bado inatumia sheria ya kikale ya mwaka 1976 iliyotungwa wakati wa mfumo wa utawala wa chama kimoja
Pili, kuna mambo kadhaa yanayothibitisha kuwa uamuzi huu umefikiwa kwa hasira, visa au kutojua na kuheshimu haki za kikatiba. Kinachogomba sana ni suala lenyewe lililosababisha kufungiwa gazeti. Mbona magazeti mengine yameandika makubwa kuliko hili na hayakufungiwa bali kuamriwa yakanushe na kuomba msamaha? Rejea gazeti moja la kila wiki kuandika habari za ufisadi wa waziri mmoja mwanadamizi na kupotea kwa zana muhimu ya kivita kwenye taasisi moja nyeti bila kufungiwa? Je kuna sacred cows na black sheep hapa?
Tatu, tokana na ukandamizaji wa haki hizi za kikatiba za raia, kuna maswali kadhaa yanakosa majibu yaani:
Nne, kwanini kampuni moja kufungiwa magazeti mawili ndani ya kipindi kifupi kama hakuna namna? Kukosea kwenye taaluma yoyote ni jambo la kawaida. Linapotokea hili, mhusika hupewa fursa ya kujitetea au onyo; ndipo hatua zaidi hufuata. Kitendo cha kulifungia gazeti la Mseto tena bila kupewa haki ya kisheria ya kueleza upande wake ni dalili za watawala kutoa vitisho na kufanya udhalilishaji hasa kwa vyombo vya habari visivyolala kitanda kimoja nao.
Tano, kwanini waziri mhusika hakujua kuwa kufungia magazeti mawili tena ya kampuni moja ni kuwanyima fursa ya kufanya kazi waajiriwa wa magazeti husika, ukiachia mbali kuwanyima wananchi haki ya kupata na kutoa habari? wakati rais anahangaika kutengeneza ajira, waziri wake anaua hata zile ambazo zimeishatengenezwa na sekta binafsi! Rais wa kwanza wa Marekani George Washington aliwahi kusema, “Iwapo uhuru wa kujieleza utaondolewa, kwa ububu na kimya, tutapelekwa machinjioni kama kondoo.” Je nani takubali udhalilishaji huu?
Kimsingi, msingi mojawapo wa utawala bora na wa sheria, ni kuruhusu, kuvumilia na kuishi sambamba na uhuru wa kujieleza, kutoa na kupata habari. Sitaki niamini kuwa serikali yetu imefikia hapa. 
Sita, kwanini waziri hakuweka maanani kuwa mwandishi aliyeandika habari husika alipewa tip–hata kama baadaye ilibainika kuwa feki, kama inavyodaiwa–akiwa na lengo safi la kufichua uovu?       Saba, je hapa kosa ni nini iwapo mwandishi alitumia taarifa alizopata akiamini ni sahihi? Kisheria, huwa inaadhibiwa nia na si kitendo. Chini ya dhana ya mistake of fact, mtuhumiwa anapotenda kosa akiamini kuwa alichokuwa akifanya si kosa, hupunguziwa makali ya adhabu. Mfano, kama nikimpiga mtu risasi akiwa shambani mwangu nikiamini kuwa niliyempiga risasi ni nguruwe anayeshambulia mazao yangu, siwezi kushitakiwa na kupatikana na hatia ya kuua kwa kukusudia. Sambamba na nayaraka husika, serikali inajua fika kuwa habari za uchunguzi hutegemea tips na nyaraka. Hivyo, basi, kama mwandishi alijiridhisha kuwa nyaraka husika zilikuwa sahihi, waziri hakupaswa kufungia gazeti kwa miaka mitatu.
Isitoshe, hata serikali yenyewe imekuwa na waajiliwa wengi wenye vyeti feki iliowaajili ikiamini ni sahihi; na serikali yenyewe haijatimliwa madarakani kwa kuanjiri watu ilioamini wana sifa hata kama ikibainika kuwa hawakuwa na sifa. Hapa tunaangalia nia (spirit) ya kutenda kosa husika na si kosa. Kwenye makosa ya jinai kuna vitu viwili muhimu viitwavyo mens rea (nia ovu) na actus reus (tendo lililokatwaza kisheria). Katika kushughulikia kesi vitu hivi huangaliwa sana ili kuamua kama mhusika alitenda kosa analokabiliwa nalo kwa makusudi au bahati mbaya.
Nane, kitu kingine, makosa ya kiuhabarishaji yanapotokea, mhusika–licha ya kupewa fursa ya kujitetea, mara nyingi, huambiwa akanushe habari husika na kumuomba msamaha mhanga.
Tisa, kwanini waziri alikurupuka na kuchukua uamuzi mzito hivi ndani ya muda mfupi? Haiwezekani kosa litendeke tarehe 4 Agosti na hukumu ifuatie tarehe 11 Agosti yaani siku tatu baada ya kosa kutendeka–kama kweli lilitendeka.  Waziri alikuwa na haraka ya nini au alifanya maamuzi yake ima kwa chuki au kushinikizwa? Maana haiingii akilini kwa waziri –ambaye tunaamini amesoma barabara–kuchukua uamuzi kwa pupa na haraka hivi na haki ikatendeka. Hapa–kwa ushahidi wa mazingira (circumstantial evidence) ni kwamba waziri alishaamua kuadhibu gazeti bila kutoa muda wa kutosha kusikiliza upande wa pili. Waziri hakuvaa viatu vya mwandishi ndipo akaamua–angekuwa yeye angefanya nini–katika mazingira kama haya ambapo kupambana na ufisadi ni sehemu mojawapo ya malengo mahsusi ya serikali ya rais John Magufuli.
Kumi, sijui kama waziri alijiuliza maswali yafuatayo na kutoa haki kwa watuhimiwa kabla ya kufikia uamuzi wake:
a)      Je aliuita utawala wa gazeti na kuupa fursa ya kutosha ya kujitetea?
b)      Je aliotoa onyo au karipio kabla ya kufikia uamuzi wake?
c)      Je aliwaamuru wahusika kukanusha taarifa husika na kumwomba mhusika msamaha wakakataa?
d)      Je muda uliotumika kufikia hukumu ulikuwa unawatosha?
e)      Je Kama waziri alitoa haki hizo husika; kama alifanya hivyo, wahusika walitoa utetezi gani  na nini misingi ya waziri kukataa utetezi wenu na kutoa adhabu kali kiasi hicho?
f)       Je amewapa fursa ya kupinga uamuzi wake?
            Kimsingi, kuna maswali mengi hasa ikizingatiwa kuwa kisheria, hakuna anayepaswa kuhukumiwa bila kusikilizwa.
            Baada ya kupata habari za kufungiwa gazeti, niliwasiliana na mkurugenzi mtendaji wa kampuni ya Halihalisi inayomilki gazeti husika Saed Kubenea aliyesema, “Barua ya Maelezo - Idara ya serikali - ilifika ofisini kwetu Jumatatu saa 10 jioni. Kumbuka hii ni siku ya mapumziko hapa Tanzania - Nane Nane. Ikataka tueleze kwa nini tumeandika hiyo stori inayomtaja ‘rais aliyepo madarakani.’ Basi. Tukajibu. Tuliekelezwa majibu yafike ofisini Maelezo kabla ya saa 3 asubuhi ya kesho yake.”
            Kwa uchache, hivyo ndivyo ilivyokuwa hali. Ni vema msomaji ambaye ni mdau wa habari na haki za kiraia za kikatiba ukasoma na kuamua mwenyewe.
            Mwisho, kwa ukiukwaji huu wa katiba, nashauri gazeti liende mahakamani kuitaka ibatilishe uamuzi huu wa ajabu.
Chanzo: Mwanahalisi leo.

Saturday 13 August 2016

Mlevi aanza kuhisi anaanza kulewa madaraka

Man And A Half
Baada ya walevi kufanya makosa kwa kunichagua kuwa kiongozi wao, walisahau kitu kimoja muhimu. Walisahau kuwa walevi–hasa wana politiki– huwa hatabiriki wala kuaminika. Sawa na mwana politiki yeyote, baada ya kukaa kwenye kitu cha utukufu–nikiwa nimesheheni utukufu wangu–najihisi kuanza kulewa–si kanywaji bali madaraka. Najihisi kama mimi si gendaeka tena bali muungu-mtu ambaye hakosei wala hapaswi kukosolewa. Katika kujitathmini, nimejikuta nikihisi kuwa mimi ndiye kijogoo pekee kwenye kaya ya walevi. Waliobaki wote ni tetea wanaopaswa kunisikiliza, kuniamini na kupokea amri toka kwangu, tena kwangu pekee. Hivyo, zaidi yangu, hakuna anayeruhusiwa kufikiria kuwika achilia mbali kuwika. Wika nikusikie na kukukata hicho kidole na ushungi vinavyokupa kiburi. Kwa wale ambao hawajapata wala kuelewa somo, tafadhalini, nawajulisha kuwa Danganyika ina jogoo moja tu linalopaswa na kuruhusiwa kuwika yaani mimi munene wa wanene na mkuu wa wakuu. Yeyote anayetaka kuwika angoje nipige miaka yangu kumi ndipo afanye hivyo. Hivyo, kwa usalama wa maisha na ulaji wake anapaswa kufanya kitu kimoja tu–kuramba makalio na viatu vyangu na kutenda nitakavyo vinginevyo atakoma na kukiona cha mtema kuni. Nani hajitaki huyu usawa huu wa kulewa madaraka? Najua wengi wanadhani wataniingiza mkenge kwa kucheza na kuimba nitakavyo wakati kimsingi wanatetea ulevi wao. Mie sijali, uwe  unafanya kweli au kuzuga, ilmradi unakubali kuwa mimi ndiye kijogoo pekee anayepaswa kuwika, sijali huo usanii na usaliti wako kwa roho yako.
Kama haitoshi–baada ya kulewa ulaji sana–najihisi kujua na kuweza kila kitu kwenye kaya ya wadanganyika na walevi. Hivyo, amri zanguhisia na mawazo yangu ni sheria zisizopaswa kupingwa wala kuhojiwa. Kuhakikisha hili linatimia bila kukwama, nimeamuru walevi wengine wanaojitiatia kunipinga–eti kwa kuwatetea walevi wengine ambao hata hivyo, ni wangu tokana na kuwa mkuu wa walevi wote bila kujali nani alinipa au kuninyima–wafunge mabakuli yao vinginevyo nitawatia adabu. Wanapaswa kufahamu kuwa mimi najua kila kitu; na lolote nipangalo, lazima litekelezwe bila kusuasua, kuhoji, kushuku wala kuuliza maswali. Walevi walizoeshwa kudekadeka na kujipayukia hovyo hovyo na watakavyo. Kwangu hili halikubaliki.  Anayepaswa kusikika ni mmoja yaani mimi mlevi mkuu mwenye mamlaka na ulaji wote mikononi mwangu na sirikali yangu. Hata chama changu kilichoingia mkenge kikanidhamini hakifui dafu hata nisingekuwa mkiti wake. Mimi ni Alpha na Omega, mwanzo na mwisho, mbele na nyuma, kulia na kushoto. Ukitaka uwe salama, sikiliza na zishike amri zangu vingenevyo unahatarisha maisha yako.
Kama alivyowahi kusema Dan son of Mwai Kibaka kule kwenye kaya ya Nyayo na nyang’au, “Chini ya mzee Jomo nilikuwa naimba kama kasuku. Sasa nimepata ulaji. Kwanini nanyi msiniimbie kama kasuku?” sasa nasema, “Hapa ni kuimba tu.” Na hii ni amri; siyo ombi. Kama wahenga wa Kirumi walivyosema “Roma Lucuta est, causa finita est” yaani kilichoamriwa Roma ni mwisho na hakina rufani. Kama bi nkubwa wa Ku-Tulia pale mjengoni, langu lazima lisikike na kutekelezwa bila kusuasua wala kuwazawaza. Hivyo, wale wote wanaoota mchana kudhani watapingana na mimi wajiandae. Kwanza, wajue mambo muhimu yafuatayo:
Mosi, mimi nina shahada ya uzamivu ya utawala na ubunifu PhD in Creativity and Leadership.
Pili, wafahamu kuwa kila ninachopanga na kusema ni sahihi na hakina shaka yoyote.
Tatu, waelewe huu si wakati wa siasa bali kutekeleza yale niliyojipangia kwa ajili ya walevi.
Nne, waelewe kuwa kwenye kuwania nafasi hii ya kiongozi wa walevi, niliwashinda hawa wanaojitiatia kunikosoa chini ya kisingizio cha domoghasia. Ninataka mambo muhimu matatu yaani:
Wacheze, wafikiri na kutenda nitakavyo. Lazima kila mmoja acheze ngoma niamuruyo na si ngoma yake. Japo unaweza kuuita huu ulevi uliopindukia, kimsingi, ni utawala uliotukuka na kujitenga na utukutu wa domoghasia na ghasia nyingine. Nataka kaya yetu ya walevi iwe Bongolalaland kweli kweli aka Danganyika ambapo hakuna atakayedanganya tena isipokuwa mimi msemakweli. Ninachopanga, kuamuru na kuwaza mimi ndicho kinachofaa; na huu ulaji nimepewa na Mungu kupitia wapika kura ya kula. Kwani, kuna ubaya gani kula hata ikibidi kuwala wote? Kwani, mimi ni wa kwanza au wa mwisho kwenye zama hizi za kuburuzana?
Kwa vile nafaidi ulevi wangu wa madaraka, natoa fursa kwa wote wanaosoma waraka huu ambao umevuviwa na Muumbaji mwenyewe watafakari na kuwa tayari kutekeleza niwaamuruyo na niwaambiayo. Huu ndiyo uhuru wa kutumia madaraka. Nisisikie mlevi yoyote akisema eti mimi ni imla au dikteta. Dikteta gani wa kuchaguliwa tena kwa kishindo? Kama asemavyo munene fulani, meseji sent and received. Hivyo, namalizia kwa kusema wazi kabisa kuwa huu ni wakati wangu wa kufanya vitu vyangu. Sitaki wapingaji wanijazie mbu. Nitawatumbu…we! Koma na ukomae.
Sitaki niseme mengi leo. Acha niwaage kwa kuwataarifu na kuwaonya kuwa atakayekaidi ujogoo wangu ajue ameumia. Siko tayari kuona walevi wakinikwamisha kwa kuhoji au kupinga maagizo, mawazo, mipango na ndoto zangu hata kama ni za kukurupuka au za mchana.
Inshara tuonane wiki rijaro. Ni mimi lais wenu ambaye nimefulahi kufikisha ujumbe wangu. Jitu Pande Makwelini aka JPM.
Chanzo: Nipashe Jumamosi leo.

Friday 12 August 2016

Ujaji tusitangaze ajira bali kutumbua hata waliopo


 
            Hivi karibuni mahakama imetangaza kuwa sasa kazi za ujaji zitakuwa zikiombwa kama kazi nyingine ili kuepuka kuendelea na mfumo na utamaduni wa kizamani ambao ulijaza majaji vihiyo na wenye mafungamano kisiasa kiasi cha kuinyima mahakama hadhi inayopaswa kuwa nayo kama taasisi ya umma na mhilimi mmojawapo wa dola.
Kwanza, tunapongeza hatua hii ambayo bila shaka italeta mapinduzi na maendeleo makubwa katika utoaji haki nchini.
Pili, tungeshauri hata upatikanaji wa jaji mkuu utumie utaratibu huu kama ilivyo nchini Kenya na Afrika Kusini. Kwanini rais apatikane kwa uchaguzi lakini jaji mkuu apatikane kwa uteuzi?
Tatu, tunashauri mahakama isianzie hapa; bali irudi nyuma na kuhakikisha majaji vihiyo na wenye kutumiwa kisiasa au kwa namna yoyote wanaondolewa ofisini ili kutenda haki na haki ikaonekana inatendeka. Kwani, wa vihiyo ambao sifa zao hazilingani na kazi na mamlaka waliyopewa.
Nne, wa majaji wanaojulikana kuwa uteuzi wao licha ya kutia shaka na kudhalilisha mahakama na mamlaka zilizofanya uteuzi huu na taifa kwa ujumla, unajulikana ulivyosukumwa na kujuana kwao na mamlaka zilizowateua.
Tano, wapo majaji ambao kuna ushahidi kuwa walishiriki vitendo vya kukiuka maadili, hivyo, kutofaa kuteuliwa kuwa majaji ingawa waliteuliwa kutokana na utawala mbovu uliopita kuangalia maslahi binafsi badala ya taifa.
Kwa wale wanaotaka kubaini majaji vihiyo na mabomu wanaopaswa kutumbuliwa kwa kuachishwa ujaji, warejee malalamiko yaliyowahi kutolewa na mwanasheria maarufu Tundu Lissu tena bungeni akidai kuwa baadhi ya majaji hawakuwa na sifa wala hawakupaswa kuteuliwa kwenye nafasi hizo hasa baada ya kubainika kutenda vitendo vinavyokiuka maadili kama vile rushwa na madhambi mengine. Kwa mujibu wa gazeti la Tanzania Daima la Novemba 29, 2012, ulimkariri Lissu akisema, “Nilieleza jinsi rais alivyofanya uteuzi wa baadhi ya majaji pasipo kupata ushauri wa Tume ya Utumishi wa Mahakama. Wamekuwa wakijibu kiujumla, mimi niliwataja kwa majina yao na hata hili nilieleza katika Kamati ya Ngwilizi ambayo taarifa yake haikuwekwa hadharani pasipo sababu za kueleweka.”
 Lissu aliwataja majaji Mbaruku Salumu Mbaruku na Fatuma Masengi kama majaji waliteuliwa bila kuwa na sifa za kitaaluma kufanya kazi ya ujaji.
Wengine aliowataja Lissu ni majaji Latifa Mansoor anayedai alifukuzwa na manispaa ya Ilala kwa ubadhirifu na udanganyifu, Kassim Nyangarika aliyewahi kushinda kesi kutokana na urafiki wake na jaji na Zainab Muruke, Pelagia Khaday, Aloysius Mujulizi ambaye licha ya kutuhumiwa kupokea fedha ya Escrow inadaiwa alishiriki kuanzisha kampuni ya Deep Green Finance Co. Ltd iliyotuhumiwa kwa wizi mkubwa wa fedha za umma.
Je wapo majaji wengine ambao waliteuliwa na mamlaka za hovyo ambazo zilidharau au kutofuata vigezo zaidi ya kujuana au kusaidiana kama anavyodai Lissu kuwa kuna majaji waliteuliwa wakiwa wagonjwa mahututi ili waweze kusafirishwa nje kwa matibabu. Lissu anawataja hawa kuwa ni marehemu Jaji Kulwa Masaba na Jaji Madina Muro na majaji Stephen Ihema, Juxton Mlay, Augustine Shayo na Vincent Lyimo. Wengine ni Mwendwa Malecela ambaye hadi Lissu anatoa madai yake alikuwa hajawahi kutoa hukumu yoyote tokana na ugonjwa.
Madai ya Lissu yanazua maswali mengi kuliko majibu. Je inakuwaje mamlaka zinazopaswa kuheshimu na kutimiza sheria kama zilivyochaguliwa na kuapa kufanya vitu visivyoingia akilini mfano kuteua watu wasio na sifa kitaaluma au kusheria kuwa majaji? Je ni wangapi ambao hawajapigwa kurunzi? Je watu hawa wamelisababisha taifa na mahakama madhara makubwa kiasi gani? Je tuhuma za Lissu ni za uongo? Kama ni za uongo, kwanini hajawahi kufikishwa mahakamani kujibu tuhuma? Kama tuhuma za Lissu ni za kweli–na kama zinavyoonyesha ni za kweli kutokana na kutokuwapo shauri mahakamani–watuhumiwa ambao hawajastaafu au kufariki wanangoja nini kwenye ofisi za umma wakati hawana sifa na wamepatikana kinyume cha sheria? Je hili nalo linangoja rais Dk John Pombe Magufuli au jaji mkuu–kama anasoma habari kama hizi–anaweza kuomba ushauri kwa rais na mamlaka nyingine husika na kuwawajibisha wahusika? Je watanzania wataendelea kuumizwa na watu wasio na sifa kwa kuwanyima haki hadi lini?
Leo hatutaandika mengi. Badala yake tunaomba tuishie hapa kwa kutaka watuhumiwa wote  wajiwajibishe au wawajibishwe mara moja ili kulinda na kurejesha imani na heshima ya mahakama; na wasipewe nafasi na kurejeshwa kazini kwa vile kazi ya ujaji inahitaji mtu asiyekabiliwa na tuhuma yeyote. Kama watahitaji kuheshimika kama raia na wana taaluma wengine ima waende mahakamani kujisafisha au wajiuzulu kabla ya kuwajbishwa. Kwani madai yanayowakabili–hata kama yalifutikwa chini ya busati kwa muda mrefu–ni mazito sana kwa ofisi ya jaji. Kwa habari zaidi wanaweza kutembelea kiunganishi hiki: http://sheriayako.blogspot.ca/2012/08/tundu-lissu-afichua-mengi-juu-ya-majaji.html
Chanzo: Tanzania Daima Jumatano.

Wednesday 10 August 2016

Kijiwe chakumbushia Escrew, Lingumi na UDA

Image result for lugumi
          










Baada ya kufumka kashfa funga kazi kwenye utwahuti sorry utawala uliopita baadhi zikwa ni Escrew, Lingumi na UDA, na kunyamaziwa, wengi walidhani ujio wa dokta Kanywaji Joni Makufuli kungefanya mambo tofauti na upuuzi uliopita. Kadri siku zinavyozidi kuyoyoma na wachovu kusahaulishwa, kuna kashfa zinaonekana kuanza kuminywa kinamna kama siyo kufichwa ili wachovu wasahau kabisa waendelee na madili.
Mgosi Machungi aliyerejea hivi kaibuni kutoka Ushoto ndiye analianzisha. Anasema huku akiwa ameshikila kichwa kwa huzuni, “Mwenzenu pamoja na kuwaetea saamu toka kwa wagosi, kuna kitu kimoja kiinitia aibu kwei kwei.”
Kabla ya kuendelea, Mbwamwitu anamchomekea, “Ulifumaniwa nini?”
“Wewe Mbwamwitu acha utani. Unazani Ushoto kuna kufumaniana au kupigana zongo? Usidhani kue mambo yanafanyika Kizaramizi kama hapa ndugu yangu. Kiichonitia aibu ni kugundua kuwa watu wa vijijini wanajua mambo mengi ya maana kwa kaya kuiko sisi wa mjini,” anajibu Mgosi
Kabla ya kuendelea, Mipawa anamchomekea tena, “Una maanisha nini mbona hueleweki Mgosi? Eti washamba wa kwenu wanajua mambo mengi kuliko sisi watoto wa mjini siyo? Ya kweli hayo Mgosi?”
“Usiwe na haaka utanieewa tu. Je wajua kuwa niipofika kue kia mmoja aikuwa akiniiuizia uipofikia uchunguzi wa kufunga hata kunyonga majambazi ya kashfa za Eskow, Ingumi na UDA? Kusema ukwei sikuweza kupata jibu hasa ikizingatiwa kuwa wengi tiishasahau kashfa hizi. Sijui hata kama Dokta Kanywaji anazikumbuka,” anajitetea Mgosi.
“Kama hii ndiyo mada yako, Mgosi hapa una mashiko. Kuna ukweli japo si wote kwenye mada yako kuwa watu wa mjini wakati mwingine ni wasahaulifu kuliko wa vijijini kutokana na kuwa na unafuu wa maisha. Tunaumeme wa kumwaga siku hizi baada ya kuingia dokta Kanywaji. Wengine wanafaidi maji yaliyokuwa yameadimika miaka mingi kiasi cha kuwa bize na wengine kuridhika wasijue mapambano ya haki ni suala la kudumu na kufa na kupona,” anasema Msomi Mkatatamaa huku akibwia kahawa yake.
Msomi anaendelea, “Ni jambo la kushangaza na la kweli kuwa majipu uliyotaja yanaonekana kuanza kumshinda daktari wa majipu. Sijui kuna wanene zaidi nyuma ya majipu haya hasa wale aliowaahidi ulinzi kwenye madhambi yao au ni woga tu.”
Kanji anadakia na kusema, “Veve hapana iko saka dugu yangu. Rahis nasema takamata fisadi vote na funga. Patia yeye nafasi tafunga tu. Pia mimi ona rahis hapana veza kamata fisadi vote. Sasa kama fisadi ile kuba nakula na fisadi kubakuba ya siasa, ikotegeme veve funga yeye?”
Kapende anamuunga mkono Kanji, “Kanji nakubaliana nawe hasa ikizingatiwa kuwa ufisadi kayani haufanywi na watu wasio na ushirikiano na wakubwa. Ima ni ndugu, wake, zao au wao wenyewe kama si wateule wao. Tukizingatia kuwa kashfa tajwa hapo juu ziligusa wakubwa wengi tokana na utawala wa wakati ule wa kujihudumia, sidhani kama zitaguswa.”
Mpemba aliyekuwa kimya muda mrefu anakula mic, “Ami usemayo ni ya kweli tupu. Kama wale walobainika kuwekewa mabilioni kwenye akauti zao bado wamo bungeni wategemea huyu Kanywaji awafanye nini? Huoni akina Joni Chenga, Profwedheha Ana Kajuamlo, Ngeleza na wengine wanaendelea kutesa mjengoni?”
Sofia Lion aka Kanungaembe, “Hata nami ami hapa kanishawishi,” kabla ya kuendelea Mbwamwitu anachomekea, “amekushawishi vipi na ili iweje?”
Da Sofia hajibu; anaendelea, “Nikiangalia UDA yenyewe ilivyotolewa kama zawadi kwa wezi wale wale waliobainika kuitwaa kinyume cha sheria eti kwa kisingizio kuwa hakuna mzalendo mwenye uwezo wa kuendesha miradi mikubwa. Kwani kinachotakiwa hapa ni kufanya biashara yenye faida au kupeana ulaji kizawa? Mzawa mgeni na yeyote kama ni fisadi ni fisadi tu.”
Mipawa anakula mic tena, “Kaya hii kwa ufisadi mimi sina hamu. Umesikia juzi waliotumbuliwa baada ya kupenyeza watu wao kwenye msafara wa marubani ulioendea ndege mpya kule Kanada? Yaani watu hawamwogopi dokta Kanywaji! Ndege zenyewe hazijatua mmeishaanza kuzifanyia kitu mbaya kama mlichoifanyia Air Tanzia siyo?”
“Hata hii imenishangaza. Huu ni ushahidi na motisha kwa dokta Kanywaji kuwa kazi iliyoko mbele yake ni pevu kweli kweli. Kwani, wengi waliomzunguka ni wale wale walioifikisha kaya hapa. Hivyo, changamoto kama hizi zinapaswa kumfumbua macho kujua kuwa wengi wa mafisadi anaopaswa kuwatumbua wamo nyumbani mwake,” anaongezea Msomi Mkatatamaa.
“Tena Msomi umenikumbusha. Nilisoma mahali kuwa kuna mpango wa kuwatumbua vilaza na vihiyo. Hata hivyo, nina shaka sawa na ilivyo kwa kashfa kama hizi tajwa. Kwani nikiangalia vilaza kama Bill Lukuuvii bado vimo kwenye sirikali ya dokta Kanywaji. Je ina maana hajui kuwa huyu jamaa ni jipu na kihiyo ambaye alitajwa kwenye kitabu cha mafwisadi wa elimu au ameendekeza urafiki na kujuana kama si kufanya utumbuaji kibaguzi?” analalamika Kapende huku akiweka kamera yake vizuri mezani.
Kijiwe kilipokuwa kinanoga si wakapita majambazi wa Lingumi, UdA na Escrew wakitoka kwenye kikao cha kumzidi kete dokta Kanywaji. Acha tuwatoe mkuku ili kuwakamata na kuwafanyia kitu mbaya hadi wake zao waapige karata baada ya kujua hiyo kitu.
Chanzo: Tanzania Daima Jumatano leo.