Baada ya mafyatu kufyatuka na kunichosha kwa kunisingizia baadhi ya mambo, nina mpango wa kuunda na kutumia timu–––siyo tume–––ya kujichunguza na kuniweka huru. Hii ni kutokana na kuwafyatua mafyatu waliojitia kufyatukakufyatuka wakitaka kunifyatua wasijue ningewafyatulia mbali. Si niliwafyatua tena bila huruma. Baada ya kuwafyatua, si wakatokea mafyatu wakilalamika mie sina huruma wakati mie nasifika kwa kuhurumia wadudu hata wanyama. Hivyo, basi, kuondoa mzizi wa fitina, nimeunda timu ya ‘kutumika’ kunichunguza.
Kwa vile hii ni timu yangu na inanichunguza, lazima itoe ripoti kwangu. Hii ni ripoti ni mali yangu siyo ya mafyatu. Naweza kuizima au kufanya nitakalo. Ataye fanya fyoko, namfyatua. Ole wa owaje na mauzauza na rongorongo kuwa niliwafyatua mafyatu. Watakoma. Hata kama kweli niliwafyatua mafyatu waliotaka kunifyatua, walitaka nimfyatue nani? Je, walitaka nifyatuliwe kirahisi hivi bila kufyatuka na kujitetea?
Katika kuunda timu hii, nimezingatia yafuatayo:
Mosi, nitaiunda mwenyewe bila hata kumshirikisha mshirika wangu wa bedroom. Sitafanya kosa niwahusishe wengine. Nani ajua wanaweza kufyatuka wakanifyatua kama wale waliotaka kunifyatua nikawafyatua kabla hawajanifyatua?
Pili, nitawalipa wanaounda timu kwa njuluku zangu na si za mafyatu. Maana, nikifanya kosa nikatumia njuluku za mafyatu, mafyatua nao wenye njuluku zao watataka washiriki katika kuunda timu hii ya kunichunguza ili wanifyatue. Nani afanye kosa hili la wazi usawa huu wa kufyatuana kifyatufyatu? Hivyo, mkiona washirika wangu kwenye timu msishangae wala kupoteza muda wenu kufyatuka.
Tatu, ripoti ya tume, sorry, timu hii itabidi niipitie kwanza kabla haijawekwa wazi. Hapa, nalenga kuondoa makandokando yoyote yanayoweza kusababisha au kuwapa mafyatu fursa au ushahidi wa kunifyatua.
Nne, nitahakikisha timu hii inanyonga ushahidi wowote unaoweza kusababisha nifyatuliwe. Hapa, lazima wana timu wapewe darasa kabla ya kutoa ripoti ya ujichunguzaji. Nawajua fika mafyatu. Ukizubaa wanakufyatua tena kwa kujifyatulisha. Bila kuwabana, wapo tena maswahiba zako, wanaweza kukugeuzia kibao ukaishia kujikuta umeunda tume ya kujifyatua badala ya kujichunguza na kuwachuuza mafyatu watakao ufyatuliwe.
Tano, tokana na kuwa na uhuru wa kuunda timu na kutengua, nitahakikisha watakaoleta jambo lolote la kunihusisha na ufyatuaji nilioufanya, nawafyatulia mbali bila huruma. Kama hii italeta shobo, nitapokea ripoti ya timu ya kujichuguza na kuiweka kapuni hadi mafyatu wangoje, wachoke na kusahau. Kwani, nitakuwa wa kwanza kufanya huu ufyatuzi ambao kitaalamu huitwa ufyatuzi wa kuepuka kufyatuliwa. Inshu inakuwa hivi. Unaita kadamnasi ya mafyatu tena kwa mbwembwe. Unakabidhiwa makabrasha na kuyaweka kapuni. Wakizidi kukubana, unawafyatua kwa kuwafunga kamba kuwa una mambo mengine muhimu ya kikaya. Hivyo, unawazuia wasiwe na mbambamba. Wangoje tu. Maana, haraka haraka haina baraka na mvumilivu hula mbivu hata kama wakati mwingine ni mbovu.
Sita, nitapiga marufuku vyombo vya umbea kupewa nakala ya ripoti ya timu ili visianze kusambaza umbea unaoweza kusababisha nifyatuliwe tena kwa kazi niliyoanzisha mwenyewe. Lisrikal langu litafanya ripoti ya timu kuwa siri. Hivyo, atakayejitia kiherehere na kujifyatua kuijadili, ataozea lupango au nitamtumia wasiojulikane wamjue na kumteka na kumpoteza ili kupoteza kila kitu mbali na kuwatisha na kuwanyamazisha mafyatu ili wagwaye. Unacheza na mimi siyo?
Saba, nitahakikisha wataalamu wangu wanaandika ripoti na kuipa timu inikabidhi harafu niikalie kifyatu na kinomi ili kufunika kombe wanaharamu wapite.
Nane, sitatoa hadidu za rejea. Najua. Kufanya hivyo ni sawa na kuwapa vichaa rungu wanifyatulie mbali. Kwa mfano, nitatoa idadi ya mafyatu walionyotolewa roho. Kwa vile sitaki nionekane mie ni nduli kweli, napanga kuiambia timu itoea idadi ya mafyatu watano tu walionyotolewa roho. Tena, timu iseme kuwa walinyotolewa roho wakiwa wanakwapua mali kwenye maduka. Hii ni kutokana na asili na ukweli kuwa ndata wa Fyatuland karibia wote, walitaka kuwa makasisi lakini kale kamjezo kanakofanywa na wenzao wenye majoho ya uroho wa roho mtakakitu, kaliwashinda.
Hivyo, hawawezi kuua hata chawa. Abishaye ajikumbushe. Nani haoni chawa wanavyonenepeana Fyatuland? Hii ni kwa sababu ya upendo na kujali viumbe wote. Hivyo, ripoti ya timu itasema kuwa imegundua kuwa hakuna fyatu hata mmoja aliyenyotolewa roho isipokuwa watano waliojitakia kwa kutaka kupora mali za wenyewe ambao waliamua kuwakomesha kwa kuwafyatua.
Tisa, nitaiamuru timu iseme kuwa waliofanya uzwazwa wa kutaka kuvuruga amani na mshirikiano wa Fyatuland ni mamluki waliokuwa wamelipwa bangi na gongo ili wavuruge tunu hizi kwa sababu ya wivu wa kike tu.
Kumi, sitataja kiasi cha njuluku ilizopiga timu. Maana, nikifanya hivyo, nitakuwa nawachokoza mafyatu na kuwakumbusha ile kitu. Kutaja kiasi cha njuluku, licha ya kufanya wajue ni kiasi gani nimepiga, itawapa sababu mafyatu kufyatuka tena na kunifyatua. Nani afanye ufyatu huu? Thubutu yako! Timu imekula kiasi gani? Hii, huitwa chiri chirini njomba.
Kwa vile leo nimeupiga mma vilivyo, sisemi mengi. Hivi, nimesemaje? Fanya kila kitu usomacho hapa siri.
Chanzo: Mwananchi leo Jtano.