The Chant of Savant

Friday 13 October 2023

Leo Nafyatua al Jinun Finun Imarati

Na Nkwazi Mhango
Leo naja na fununu na tena kindavandava. Kwanza, niwashukuru mafyatu wote walionikaribisha kwa shangwe na nderemo wiki iliyopita nilipokanyaga hapa kwa mara ya kwanza. Niwatonye chapchap. Nimeanzisha chata liitwalo Al Jinun Finun wanuni na nune (AJFnn). Msichanganye na twambombo tununu kule kwa akina Mwakafwilafwila na Mwakafaga. Chata lina jina nono na tamu la kimanga. Huu nao uwekezaji wa kimanga. Chata halina usununu, ushakunaku, na usongombwingo wala vinyongo. Litakuwa na manufaa makubwa sana. Washikaji wake watakuwa tumbili ili wawaandame chawa hadi kieleweke. Tunashuhudia rafu uchafuzi, sorry, uchakachuaji wa uchaguzi ujao. Tumenyaka ukweli, si fununu. Chawa weshatangaza wagombea wawafugao wakikiuka katiba. Hii haki na demokrasia au domoghasia? Wanawahi nini? Kunani? Chawa na uchaguzi mmhh! AJFnn itajibu.
         Nilimsikia Juli, senzi, sorry, Shonzo akichachawa kama chiwawa kule walikosongwasongwe na dhiki eti 2025 watamchagua chifu Yangaya kumshukuru kutoa njuluku ya miradi ya maendeleo. Kwani, alitoa njuluku yake? Nani anataka chifu usawa huu? Uchawa mwingine kigegezi. Kwa ubongo wa chawa usioweza hata kuonekana, unategemea awaze mambo makubwa kama kuendesha kaya kwa haki na weledi badala ya uchawa?
        Kwa vile kaya imevamiwa na kujaa chawa, imebidi nianzishe chata harakaharaka ili kuikoa na uchafu kabla ya kunyonywa damu hadi kukauka na kunyatuka. Ni baada ya mafyatu wengi kunilalamikia kuwa wamechoka kung’atwa na kunyonywa na chawa mbali na adha, hadaa, na kula mihogo tokana na gharama za maisha kupanda kiasi cha kukosa njuluku ya kula kalimati, keki, mahanjumati, na mikate kama wanene. Wanataka kula halua na tende si adha. Lengo la AJFnn si kudai kitabu wala kuzuia kubinafsisha maji, madini wala majini. Tutaka kaya ibadilishwe jina na kuitwa Al Jinun Finun Fir’aun Imarati. Mafyatu niliohoji wamesema wamechoka na jamhuri isiyo na uhuru ulogeuzwa mhuri wa unyonyaji tena wa machawa na wachafu wawafugao. 
Nitawasilisha maombi kwa msajili wa vyama atusajiri tuanze kufyatuka na kufyatua. Nadhani akina Tunu na Nunu waso wanuni watajiunga kwa wingi ili kufyatua mafyatu wanaotufyatua. Ninapendekeza wanakaya waitwe majinun al mujirmun al mufilis ili nao wajidai kwa kimanga na kula raha kama jamaa zetu wa Dubei. Nani asiyetaka kujulikana na kutanua kama Dubei? Tunapendekeza kubinafsisha kile kitu kuanzia ikuu hadi wanakaya wenyewe. Ila chawa hawatahusishwa. Tutawafyatulia mbali wasichafue dili hili takatifu.
Kwa sera yetu ya ubinafsishaji siyo uwizishaji, tutaanza na katiba ili tujipangie wenyewe tuepuke kubishana na kuumiza, kufyatuliwa, kufyatishwa, na kufyatuana. Pia, tutaokoa njuluku ambazo zingefyatuliwa bure kwenye kutoa elimu isiyo elimu na kukusanya maoni ambayo yangeishia kupuuzwa na kuoza kwenye makabrasha kama yale ya majaji Wariboa na Kisago. Ili kuepuka wambea kutuletea umbea na ufyatu, tutafanya dili siri ili kuepuka kuhatarisha usalama wa kaya na ulaji wetu au vipi? Pili, tutaepusha migogoro ambayo imefikia pabaya hadi wanakaya kurokoroniana, kutukanana, na kuitana majina mabaya. Tatu, tutaokoa njuluku ambazo zingetumika kuwagharimia baadhi ya mafyatu kuzunguka kaya nzima huku wakipoteza muda kutafuta kinachojulikana. 
    Nne, tutabinafsisha ikuu, waliomo, na vilivyomo ili kuukata. Shurti tuwaite wamanga waje na katiba yao ili nasi tufaidi kwa kutawaliwa kimangamanga na kimangaa. Nadhani kwa kuwauzia katiba na kwenda Dubei bila visa na visasi, tutawakaanga wamanga kwa mafuta yao kama wanavyotaka kutuchemsha kwa maji yetu. Hapa ngoma droo. Sipati picha kuwaona akina Mgosi na Njomba wakimwaga kimanga kama hawana akili nzuri. Kama alivyosema fyatu mmoja kule Mwanza, lazima tuchanganye damu ati. Tutakwenda umangani, kuishi, kuongea, na kutanua kimanga. Pia, kaya itapata faida kubwa sana nakwambieni. Msiniulize vipi. Mkiuzwa au kuliwa, sawa.
    Mwisho, tutawataka Al Finun Jinun wa al Mujirmun al mufilis wote wachague kati ya wao kubinafsishwa na kupewa visa visivyo na visa na visasi kwenda kutanua Dubei kama akina Maulaji Kitengi na Zekabwela waliopelekwa kule kutanua hadi wakatanuka, kufyatuka, na kuwapa faida mashakunaku. Pia, tutauza kaya kila fyatua achukue chake na kufyatukia umangani, bondeni hata majuu Watakaobaki watajiju.
Faida gani mtapata? Kawaulize wamanga na maza.
Chanzo: Mwananchi Oktoba 11, 2023.

No comments: