The Curse for Salvation

The Curse for Salvation

Wednesday, 26 March 2025

Tusichachawe, kuchawishwa, tukachawishana

 

Kuna usemi wa hovyo. Kila nikiusikia, natamani nifyatuke na kuwafyua wadudu hawa wawe ni wadudu au ngurumbili waliofilisika kimawazo hadi kuwa hivyo walivyo hovyo. Msemo unaonichachefua na kunifyatua si mwingine bali ule wa chawa na uchawa ambapo chawa wenyewe ni mafyatu. Mwanzoni, nilidhani chawa wamepata miujiza kiasi cha kufyatuka kama mafyatu na kugeuka mafyatu lakini si mafyatu kufyatuliwa hadi wakajigeuza au kugeuzwa chawa. 
Kwanza, siamini wala kukubali kuwa fyatu mzima na akili zake anaweza ima kujifanya, kufanywa, kujiita, kuitwa, kugeuzwa au kujigeuza chawa. Chawa na fyatu wapi na wapi na katika nini na lini na iwe nini kwa ajili ya nini na nani? Fyatu mwenye akili timamu hawezi kuvumilia achia mbali kufuga chawa. Sijui kama chawa wana akili au ubongo hata uwe kiduchu kiasi gani. Sijui hata kama wana utashi au utambuzi wa kujua wafanyacho zaidi ya kusukumwa na silika kama hayawani wengine kama wao.
Chawa anapoitwa fyatu ni poromosheni na fyatu anapoitwa chawa si dharau na matusi tu bali demosheni. Kwanza, sijui. Inakuwaje fyatu mzima akubali kuitwa au kuita wenzake chawa asione aibu wala kuhofia kuonekana hayawani na zwazwa. Inabidi nirejee kwenye kabrasha langu la mabuku ya saikolojia nijikumbushe kitu hii.
Tofauti na chawa, kazi ya mafyatu ni kufyatua kila kitu, fyatu, na chawa bila kujali ukubwa wala unene wao. Hivyo, siamini hata kidogo kuwa fyatu mwenye akili timamu anaweza kuchawawishwa na kuchachawizwa hadi akakubali kuwa au kugeuzwa chawa. Ili iweje? Ili apate nini? Hata kama mie ni fyatu, lazima niseme tena bila kufyatuka. Hakuna binadamu anaweza kuwa chawa wala chawa kuwa binadamu. 
Kuwa, kufanywa, au kuitwa, kugeuzwa hata kuihisiwa kuwa chawa ni kufuru na maudhi kwa mwenyezi Mungu mwenyewe na mafyatu hata wadudu. Ni hayawani na vichaa pekee wanaweza kunyonywa na chawa kwa vile ni hayawani. Hawana uchaguzi wala uwezo kama mafyatu. Sitaki kufikiri. Sijui inahisika au kuwa vipi kwa fyatu kujilinganisha au kugeuzwa hayawani kama mdudu chawa. Sitaki kujua wala ku-imagine.
Kwa wale waliokua na kwenda shule wakati wa Ujamaa, tuliozoea kuwaita wanyonyaji kupe, si kwa sababu ya ufyatu wao bali hatari, madhara, uchafu, udhalili, na uhovyo wao. Tofauti ni kwamba, mafyatu wanyonyaji walipoitwa makupe, hawakupenda tusi hili. Nasi, tuliwaita vile si kwa kuwasifu wala kutaka watusifu bali kuwakatisha tamaa waache ukupe au unyonyaji. 
Kuna tofauti gani kati ya uchawa na ukupe? Kama wahusika wanamaanisha chawa kwa sababu ya unyonyaji na uchafu wao, hapa sina neno. Nijuacho, hakuna kupe waliojitangaza kuwa makupe au sisi tuliowaita makupe kuwavumilia na kuwafanya sehemu ya maisha au harakati zetu. Tuliwachukia. Walituchukia. Tulichukiana. Je kwa chawa hali ikoje? Mie si chawa. Sijui chawa wanajiteteaje kama wanao utetezi kutegemea na uteuzi wao.
Je ni kwanini tuliwachukia kupe? Nani anapenda kunyonywa? Nani anapenda kufuga viumbe visivyo na faida bali hasara na hatari? Wale watunzao wadudu wanyonyaji hufaidikaje nao? Je kunyonywa kuna raha au karaha? Nani anaweza kufuga maradhi kilio kisimfichue? Ni mpumbavu gani huyo anayengoja kufichuliwa na kilio badala ya kutibu ndwele? Wanyama kama ng’ombe, nyati, tembo na wengine hunyonywa na kunguni. Kwanza, ni kwa sababu wao ni wanyama. Pili, hawana dawa na nyenzo nyingine za kuwaangamiza japo wana utashi. Tatu, wana damu nyingi kuliko mafyatu. Nne, pamoja na kutokuwa na dawa na nyenzo, hawawapendi kupe.
Turejee kwenye chawa au machawa kama wasemavyo watoto wa njini siku hizi. Nina swali. Je chawa anaweza kuishi bila ya kuwanyonya awanyonyao? Je anayenyonywa anaweza kunyonywa bila kuwa na damu na uchafu, bila kusahau ujinga au kukosa uwezo kabisa wa kuwateketeza wadudu kama wanyama hapo juu? Je sasa nani hawa wanafuga machawa na kwa nini ili iwe nini? Je chawa wanaweza kuwapo bila damu na uchafu? Je nani hawa wachafu wanaofuga chawa na ili iweje? Kuna haja ya kuwasaidia ima kuwaosha wawe safi na kuachana na mateso ya kunyonywa na aibu ya kuitwa wafuga chawa au kuwapulizia dawa ya kuua wadudu kama tufanyavyo kwa mbuzi na ng’ombe ambao huwa tunawapelekea joshoni mara kwa mara.
Kimsingi, fyatu anayekubali kunyonywa na chawa bila kuwaua au kujisafisha, anahitaji msaada sawa na chawa wanaomnyonya. Unachoweza kufanya hapa, ni kuua machawa ima kwa kumuosha mhusika, kusafisha nyumba yake huku mkimfundisha faida za kuwa safi na madhara ya kufuga chawa au kupulizia dawa za kufyatua wadudu. Je anayefuga chawa na chawa nani mjanja? Je kati yao, nani anahitaji ukombozi? Kumbe nililewa na kulala kwenye mtaro!
Chanzo: Mwananchi leo.

Monday, 24 March 2025

Shemeji, huwezi kumpiga mke wangu


Kisa hiki kinamhusu rafiki yetu. Siku moja, rafiki yetu alisimulia kuwa kulikuwa na mabishano juu ya suala la kifamilia baina ya mkewe na kaka zake wawili ambao ni mashemeji zake. Katika ubishi huu, mke wa jamaa aliwapinga kaka zake juu ya jambo fulani kiasi cha kuwaudhi. Mmojawapo wa wale makaka ambaye ni mkubwa kwa kufuatana na mke wa jamaa alimtishia dada yake kuwa angeweza kumpiga. Kwanza, alisahau kuwa, pamoja na kuwa dada yake, alikuwa mke wa mtu. Pili, alisahau kuwa jukumu walilomkabidhi shemeji mtu alipomuoa dada yao ilikuwa ni kumlinda na kumtunza dhidi ya hatari au tishio lolote. Tatu, hakujua au alijua lakini akasahau kuwa shemeji yake alimpenda na kumheshimu sana mkewe kiasi cha kutoweza kuvumilia kuwa shahidi wa udhalilishaji au utesaji wake.
            Kaka mtu alipomtishia dada yake kuwa angempiga, shemeji mtu aliamka kwenye kiti pembeni ya mkutano wa ndugu na kumwambia shemeji yake “huwezi kumpiga mke wangu nami nikuache. Tutapigana liwalo na liwe.” Kwa vile wale wakaka hawakutegemea kitu hiki, walishangaa na kuogopa kiasi cha kuwataka radhi dada yao na mumewe na ugomvi kuishia hapo. Baada ya tukio hili, kaka mtu walimheshimu dada yao kiasi cha kuwa wakisimulia kisa kile mara kwa mara kwa kuangua vicheko.
            Kwa mujibu wa mtoa taarifa, kaka mtu walizoea kusema kuwa mumewe alikuwa amemfundisha kuwa na roho ngumu, yaani ugaidi. Kwani, hawakutegemea kuwa shemeji yao angeonyesha hasira na kuamua kuingilia ugomvi wa kifamilia. Badala ya kukuta ndugu wakigombana na kuchukua jembe akalime kama wahenga watuhusiavyo, mume mtu aliamua kuingilia kati akimkingia kifua mkewe. Jambo hili liliwapa somo kubwa wahusika. Kadhalika, jambo hili linatoa funzo kwa wengine kuwa, kama utamlinda mwenzio, hakuna atakayehatarisha maisha yake kwa kuwa tayari kumdhuru. Isitoshe, kama mke au mume ni mwili mmoja, kama mmoja atadhalilishwa au kupigwa, na mwingine, kadhalika atakuwa amedhalilishwa na kupigwa.
            Jamaa alitwambia kuwa baada ya mkasa kusuluhishwa hivyo, mashemeji zake walizoea kumuuliza ni kwanini aliamua kuingilia ugomvi wa ndugu badala ya kuchukua jembe akalime? Aliwajibu kuwa, kama angelaza damu na mkewe akadhalilishwa au kupigwa, angeenda kulipia nyumbani mbali na kushindwa kumlinda na kumheshimisha mkewe. Hivyo, alizoea kuwajibu kuwa walipompa dada yao amuoe, walikoma kuwa na mamlaka juu yake. Kwa maana nyingine, wahusika siyo walitaka kuwadhalilisha na kuwaumiza hawa wawili tu bali kupora madaraka ya shemeji yao. Je ni wangapi wanaliona hili hivi kiasi cha kumhami wenzi wao kama alivyofanya jamaa huyu? Ni wangapi wangechukua majembe na kwenda kulima wakati wakiacha mambo ya familia kama yalivyo japo aliyekuwa akiumizwa ni mke mtu? Je wewe ungefanya nini katika hali hii? Je hili limewatokea wangapi na walichukua hatua gani? Si vibaya kumlinda na kumhami umpendaye hasa anapokuwa mke au mumeo. Tuna wajibu kwa wenzetu kama walivyo nao kwetu pia.
            Hivyo, unapokutana na changamoto au tishio kama hili, wala usisite wala kuona aibu kumhami mwenzio. Kwani, kumhami ni wajibu wako na kutomhami ni kushindwa kutekeleza wajibu wako kwake na kwako. Hisani, siku zote, huanzia nyumbani. Kupenda siyo kuambizana nakupenda bali kuonyesha upendo kwa matendo. Hata sheria nyingi ziko wazi kiasi cha kuzuia mke kuwa shahidi dhidi ya mumewe. Chini ya kile kinachoitwa spousal testimonial privilege au haki ya ushahidi wa mwanandoa dhidi ya mwenzake, mwanandoa ana haki ya kukataa kutoa ushahidi dhidi ya mwenzie. Hata hivyo, sheria hii humpa haki haki hii mwanandoa kwa makosa yaliyodaiwa kutendeka wakati wakiwa katika ndoa si kabla au baada ya kuachana. Sheria, mara nyingi, ni kipofu na haina huruma. Ila katika kuleta amani katika ndoa, inatoa haki hii kwa wanandoa. Hivyo, wanandoa wasiojua sheria wasilazimishwe kutoa ushahidi dhidi ya wenzi wao kwa vile jukumu lao ni kulindana na kuhamiana katika kila hali. Pia, kumhami au kumlinda mwenzi wako si hisani kwake bali wajibu wako kwake.
Chanzo: Mwananchi, Machi 16, 2025.

Tulifyatuliwa, tunafyatuliwa, tutafyatuliwe tena

Mwaka jana, Mkaguaji mkubwa wa njuluku za sirkal aka KAGO alitoa taarifa ya kuchefua baada ya baadhi ya mafyatu kufyatua mafyatu wote waliokataa kufyatuka wakafyatua wapigaji wakaishia kuufyata. Alionya kuwa, kama ufyatuaji unaoendelea usipofyatuliwa, kaya nzima ima itaendelea kufyatuliwa kama inavyofyatuliwa na itakavyofatuliwa kiasi cha kufyatuka na kuanza kuwafyatua wanaoifyatua. Na hapa, itakuwa pata shika na shaka, nguo kuchanika.
            Si ubishi wala uchawa kukiri kuwa mwaka ulofyatuka tulifyatuliwa na kuufyata bila kufyatuka. Njuluku zilifyatuliwa na maisha yakaendelea kuwafyatua mafyatu waliogoma kufyatua ima kutokana na ufyatu uchwara au kukosa ufyatu kabisa zaidi ya sifa za kipuuzi. Kazi na sifa ya mafyatu ni kama bomu au upinde. Lazima wafyatuke na kufyatua na si kujikomba na kusifia hata ukumbaff. Ila wasipofyatua wakafyatuliwa wanageuka bomu yaani kitu kisichofaa wala kufyatuka na si bomu linalofyatuka na kufyatua. Hata upinde, lazima ufyatuke. Usipofyatuka, hugeuka upondo.
            Sasa turejee na kufyatua inshu ya KAGO na ufyatuaji wa njuluku za mafyatu uliofanywa na mafyatu waliopaswa kufyatuliwa wasifyatuliwe wakaishia kufyatua, bila mafyatu kufyatuka na kuwafyatua hawa mafyatu, watafyatuliwa tena tena hata mwaka huu. Mwaka jana tulifyatuliwa. Mwaka huu tushafutuliwa. Je tutakubali kuendelea kufyatuliwa na wanaotufyatua na kufyatua njuluku zetu au tutawafyatua kabla hawajatufyatua tukafyata na kufyatuliwa kama tulivyofyatuliwa bila kufyatuka bali kufyatuliwa kama tutakavyo fyatuliwa tusivyofyatuka na kufyatua kabla ya kufyatuliwa kwa vile hatufyatuki tukafyatuka? Naona. Hapa nimefyatua hadi mafyatu wanafyatuka kizungumkuti tokana na ufyatu na ufyatuzi wa fyatu mfyatuzi bingwa wa ufyatu na ufyatuzi asiyeufyata wala kufyatuliwa kama mafyatu waufyatao wakafyatuliwa na wale wawafyatuwao wanaopaswa kuwafyatuwa wasiwafyutue.
            Pamoja na KAGO kufyatua ripoti ya ufyatuzi kayani mwaka jana, hadi unaisha, sikuona wala kusikia wafyatuaji wakifyatuliwa na wale wanaopaswa kuwafyatua ili kukomesha ufyatuaji wa njuluku za mafyatu fyata. Pia, kwenye salamu za kuukaribisha mwaka, sikusikia mikakati ya kuwafyatua wafyatuaji wa njuluku za mafyatu. Ajabu, pamona na mafyatua wapaswao kuwafyatua mafyatu wanaowafyatua mafyatu kuufyata, sikusikia mafyatu wakifyatuka na kudai hawa wanaowafyatua wafyatuliwe au wawafyatue hawa wanaopaswa kufyatua wawafyatuao wasio wafyatua!
            Kwanini mafyatu wanaofyatuliwa hawakuwafyatua mafyatu wanaolipwa njuluku kuhakikisha wanasimamia njuluku za mafyata au kuwafyatua wanaowafyatua hizo njuluku wasiwafyatue? Mwaka jana, nilimsikia mwenyewe kwa masikio yangu mtukuka asiyefananishwa na muungu akisema "sababu dosari zilizotolewa hapa, tutakwenda kukaa tuzifanyie kazi, turekebishe na mwakani pengine hizi hazitajirudia, na tutakuwa tumesogea.” Ajabu ya maajabu, katika hutba yake ya kufunga mwaka uliofyatuka, sikumsikia akikumbushia namna atakavyowafyatua hawa wafyatuaji wa mafyatu waliogoma kufyatuka na kufyatua. Je ni kwanini hakufyatuka lau kiduchu juu ya namna atakavyowafyatua hawa mafyatu wafyatuaji wanaohitaji wafyatuzi ili wakome kufyatua njuluku za mafyatu walioamu kuufyata?
            Mwaka jana, tulivyatuliwa matrilioni. Kama wanaopaswa kuwafyatua wanaofyatua mafyatu njuluku wasipowafyatua, sitashangaa KAGO kuja na ripoti kilio cha ufyatuzi wa madafu gizilioni kama siyo quadrilioni. Kwa vile hawa wafyatuaji hawakufyatuliwa na wale wanaopaswa kuwafyatua, sina shaka, watafyatua njuluku za mafyatu tena kama walivyozoea. Kwa kimakunduchi hii huitwa bizinesi ezi usual. Unafyatua hapa na kuhamishiwa pale ili uendelee kufyatua. Kinachoweza kukuzuia kufyatua hapa ni kifo tu. Kama kikufyatua, kila kitu ikiwemo ufyatuzi wa njulu za kaya vinaisha. Ajabu ya maajabu, hata ufyatue vipi, hakuna atakayeondoka na njuluku za mafyatu anazofyatua. Kwa maana nyingine, ni kama unajifyatua kufyatua visivyoweza kukusaidia bwana Godi akikufyatua.
            Japo ukisema haya unaonekana chizi au zwazwa, fyatu ana nini juu ya uso wa ardhi? Ana nini kiumbe aliyekuja bure na kuondoka bure? Laiti mafyatu wengi wangejua ukweli huu, wasingedhulumiana, kuibiana, hata kuuana kwa ajili ya vitu wanavyovikuta na kuviacha hapa. Ukisema ni utaahira, mafyatu wengi wanakushangaa na kuchukia kuwa umewatukana wakati ukweli ni kwamba ni mataahira wasioona zaidi ya usawa wa matumbo na pua zao. Wangapi waliwika dunia hii tena kwa madaraka makubwa lakini walishafyatuka na kusahaulika kiasi cha mali na ushaufu wao kuviacha hapahapa hata wengine kuharibika? Nani hakumbuki fyatu jambazi kama Mobutu Nseleko wa Kongwa alivyojenga kwao kwenye kijiji cha porini cha Gabadolite? Ukiangalia kilichosaliwa baada ya kufyatua na kuunguza njuluku za mafyatu, unakubaliana nami kuwa wanaofyatua njuluku na mali za umma, wengine ni machizi watakaoacha kila kitu hapa wakiondoka watupu kama walivyokuja.
            Wapo wapi akina Mafarao, Nabukadneza na mashaufu wengi uchwara waliojifyatua kwa kuwafyatua wenzao wakidhani hawatafyatuliwa? Tutankhamun, Farao aliyesifika sana, alikuwa na umri wa miaka chini ya 20. Sasa hawa wanaopiga njuluku za mafyatu na kuwafyatua wataishi milele? Unaweza kuacha mijengo mikubwa, akaunti nono, jua kufa ni kufa tu. Heri kuwaneemesha mafyatu kuliko kuwafyatua hadi inafikia mahali unashindwa kujua ni kwanini tumefyatuliwa, tutafyatuliwa,kama hatutachunga kufyatuliwa tena. Hivi niko wapi?
Chanzo: Mwananchi, Machi 24, 2025.

Tunashangaa, Tunashangazwa, na Kushangaza

 

Huwa nashangaa. Sijui kama nawe hushangaa kushangaza? Kama hushangai, unashangaza. Kama unashangaa, pia, unashangaza. Hata nami nashangaza kwa kushangaashangaa bila kufyatua. Huwa nashangaa kwa ninayosikia bila kuona ukiachia mbali ninayoona bila kuyasikia. Katika kaya yetu ya kushangaza, kuna vitu vinashangaza. Kila siku nasikia mafyatu wakilalamikia ukapuku wa kutengenezwa wakati kuna wanene waliofyatua njuluku hadi wanakufuru. Hawa hunishangaa kama nishangaavyo. Tunashangaana, kushangazwa, na kushangaza. Hapa, sijaongelea upigaji wa kutisha kila siku. Unashangaza. Unashangaa kwanini tunapigwa tukaendelea kushangaa hadi tunashangaza. Kwa kushangaa kwetu, tunashangaza na kushangazana. Ukinishangaa, nakushangaa. Usiponishangaa kwa kushangaa, nakushangaa kiasi cha kushangaza kwa kushangaana na kushangazana.

            Siachi kushangaa. Hushangaa kusikia mapambio, mashairi, ngonjera, na sifa tena vya kushangaza. Waimbaji ni mafyatu, wanyama, hata wadudu tena wanaoshangaza. Mfano, wapo waishio kwenye ukwasi wanaoshangaza wanaowashangaa waishio kwenye uchochole wa kushangaza. Licha ya kushangaana, wote wanashangaza. Wapo wanaoshangaa. Wanashaangana na kushangazana. Inakuwaje fyatu awe kapuku kwenye kaya inayosifika kutenda miujiza karibu katika kila jambo? Inashangaza. Wakati wenye njuluku wakiwashangaa wasio nazo, nao wanawashangaa namna walivyozipata wakati wao wakikosa. Inashangaza. Wanashangaa na kushangaza.

Hakuna kitu hunishangaza kama taarifa ya Mkaguzi mkuu wa njuluku za kaya (KAGO). Je huwa kweli anazikagua au zinamkagua? Inashangaza. Kwanza, hizo njuluku ziko wapi na ni kiasi gani? Inashangaza. Pili, kwa zinavyopigwa, sijui kama kweli zipo za kukagua. Inashangaza.  Kwanini asikague hata njuluku za wenye nazo waliozipiga toka kwa mafyatu wnaoashangaa na kushangaza? Nashangaa. Kago anashangaza kiasi cha kumshangaa. Sijui kama naye anajishangaa kwa taarifa atoazo za kushangaza. Je huwa anatushangaa? Kila mwaka, huwa anaripoti upigaji na madudu kibao udhani kazi yake ni kufyatua habari mbaya kwa mafyatu. Inashangaza. Kingine kinachoshangaza ni ile hali ya waliofyatua tena njuluku ndefu kuhamishwa vituo kwenda vingine badala ya kupelekwa lupango. Inashangaza.

 Wakati nikishangaa hili, huwa nashangaa namna Mwendesha Makesi wa Kaya (Dipipii) anavyoweza kukukamatisha, ukapozwa hata kusahaulika lupango halafu anajitoa welewa na kusema eti amekufutia mashtaka. Inanishangaza. Huwa namshangaa na vitu kama hivi vya kushangaza. Je huu muda fyatu wapotezao lupango unalipwa na nani? Inashangaza. Huwa nashangaa kama hii nayo ni haki, sheria, na utawala bora. Juzi, nilimuona mzee Silaha, akiwa amechakaa. Nilishangaa. Alikaa lupango kwa mwezi na ushei. Inashangaza. Ukiuliza nini mbaya alifanya? Unashangaa. Unashangaa ni kwanini ndata walimnyaka na kumsweka lupango bila kupeleka kwa pilato! Unamshangaa yeye kuswekwa lupango bila kosa. Unawashangaa ndata hawashangai hili. Pia, unawashangaa wanene wanaoshangaza kwa kudai kuwa wameleta maendeleo na ustawi. Inashangaza. Hivi vinaweza kupatikanaje bila haki? Inashangaza!

Wakati nikiwashangaa Kago, Dipipii, na ndata wa kushangaza pia, humshangaa munene anayeshughulikia njuluku asifikaye kwa kutoa misamaha ya kodi kwa wenye nazo huku akizidi kuwakamua wasio nazo kwa njia mbali mbali kama vile maokoto, tozos, na madude mengine ya ajabu ajabu na kushangaza. Inashangaza. Kabla ya kumaliza kumshangaa jamaa wa njuluku, huwa nashangaa kusikia kuwa kaya imefunguliwa. Inashangaza. Kwani, nani alikuwa ameifunga na kwanini na ili iweje? Inashangaza.

Hakuna kitu nashangaa kama kukatikakatika kwa umeme. Inshangaza sana kwa namna tunavyoahidiwa kuwa migao ingegeuka historia wakati wowote. Inashangaza namna ambavyo mambo ya kushangaza hutokea na ahadi za kumaliza migao kugeuka donda ndugu. Inashangaza ni kwanini hawa wanaotoa ahadi za kushangaza hawajishangai pamoja na kushangaza! Inashangaza na waathirika wasivyowafyatua. Inashangaza sana kwanini wanaofeli katika kutoa huduma nyeti kama hii kutoachia ngazi ili wenye uwezo waingie na kurejesha heshima ya kaya. Huwa nashangaa. Nashangaa sana kuona kuwa wale wale wanaotudanganya, wanafanya hivyo si mara moja wala mbili. Inashangaza.

Ngoja nifyatue mfano japo mmoja wa kushangaza mjue kwanini nashangaa na kushangazwa.Waziri mkubwa alikaririwa mwaka jana akisema “kwanini Muentertain wizi? Watu wanaiba mara ya kwanza, mara ya pili mmeshindwa kuchukua hatua za kuwadhibiti wasirudie tena?” Inashangaza. Nasikia mafyatu wanafyatua hata pesa ya wagonjwa. Je nini kimefanyika badala ya kulalamika? Inashangaza. Waziri mkubwa, pamoja na mamlaka yake, anashangaa. Inashangaza kweli kweli.

Naendelea kushangaa haya mambo ya kushangaza. Mfano, rahis, akihutubia buge, mwaka 2021 alisema “naomba kutumia jukwaa hili la Bunge lako Tukufu kuwaonya wale wote wanaodhani kuwa usimamizi wa mali ya umma kwa maslahi ya wananchi, kukataa ukwepaji wa kodi, wizi, na kukemea uzembe vitasimama kwa sababu tu Rais Magufuli hayupo.” Inashangaza.

Kwa ufupi ninashangaa, inashangaza, nawashangaa japo mnanishangaa kiasi cha kushangaza na kushangazana kama siyo kushangazwa. Wakati mwingine natamani tuitwe washangaaji kama siyo washangazaji. It’s too much. I wonder.

Ninashangaa kwanini nashangaa! Je wewe unashangaa au unashangaza? Hakika. Tunashangaa, kushangaana, na kushangaza. Mafyatu itikieni ‘kweli inashangaza na mseme amina.

Chanzo: Mwananchi, Machi 12, 2025.

Sunday, 9 March 2025

Sasa Kanji nafyatuka nageuka fyatu dugu yangu!


Juzi natoka Bombei ona mama na toto. Iko furahi kuba sana. Naacha toto moja. Nakuta mama nakwisazaa toto sita. Yote faida. Nakaa Bombei. Woo! heva iko chafu veve hapana ona. Sikia tu. Nalala naota Tanjania. Baada ya peleka faida, sasa narudi tafuta faida nyingine.
        Napanda dege. Nafika hapa. Swahili moja fyatu nataka fyatua mimi. Nalalamika kama toto eti fyatu fyatuzi iko nafyatua mimi hadi nafyatuka! Swahili nakuta mimi iko soma gazetini. Nauliza kwanini juluku naibiva kila siku? Nasikia hii iko chava. Kama nasema baya sirkal, nachukia veve. Kwanja, naanja. “Hii hindi iko chafu nachanganya Swahili sana. Napenda sana siasa na iko na multiple citizenship.” Nalalamika eti hapana piga kura lakini kama ongozi nachaguliwa, yeye nakaribisa na kuwa karibu nayo. Naongeza kuva Kanji nafanya ongozi sahau ile nachagua yeye. Sasa iko kosa ya yangu au ongozi? 
        Hii jinga naita mimi choli! Lini swahilihindi nakuwa safi dugu yangu? Kama nafyatua hindi nachanganya na Swahili nafanya juli sana. Naondoa baguzi ya luga na rangi dugu yangu. Sasa kosa nini veve nataka fyatua mimi dugu yangu? Mimi iko penda veve sana na juluku yako naleta dukani yangu nunua witu. Vote napata faida. Veve chukua witu. Mimi chukuva juluku. Hapana pendeja hiyo dugu yangu?
Nafika jumbani. Nakuta Swahili nalalamika sana. Nauliza “iko nini veve nalalamika owo kama toto dogo? Swahili iko sangaa kama paka naona juluku! Nauliza tena. Veve napata sida gani nasangaa hiwi? Nasema eti mimi hapana ongea Swahili juli. Nasangaa hadi nataka fyatua Swahili. Nauliza yeye “kwani Swahili iko ongea hindi juli? Sasa Swahili nataka fyatua kila kitu. Nataka hata kuoa totoz ya hindi! Kwanini nakuwa chokoji? Veve iko ona hindi naona totos ya Swahili? Sasa kama siyo nafyatuka, kwanini taka oa totos ya hindi veve Swahili choli?
        Swahili iko tabu mingi sana. Maisha iko gumu au fyatu iko gumu fyatuka na kufyatua ile nafyatua yeye? Naona vatu ikolalamika maisha iko gumu kama jiwe. Kwani, swahili siyo gumu? Swahili nalalamika kama toto dogo. Hindi nalalamika kama vatu kuba. Kama maisha nakuva gumu, kwanini hapana fyatua ile nafanya maisha kuwa gumu? Sasa lalamika nageuka sera ya vatu vote kwa kayani. Hindi nalalamika. Sirkal nalalamika. Tajir na sikini yote lalamika! Kama sirkal nalalamika, nan tasaidia nani? 
            Maisha iko gumu. Sasa hindi nafatyatuka nageuka fyatuzi dugu yangu. Sasa nauliza polepole. Juluku kayani nakvenda vapi? Mbona ile kuba naishi peponi? Kama Swahili napata juluku, naoa vake mingi. Hii hapana lalamika! Natumia juluku mingi fanye serehe. Juzi nakwenda Bembei. Kule jimboni yangu India, vaziri moja ya koa nasamehe juluku rupia laki moza nafukujwa kaji. Hapa vaziri nasamehe, trilioni napandishwa choo! Sasa hapa laumu nani na nini dugu yangu? Kvanini hapana fyatuka ikafyatua ile nafyatua veve dugu yangu?
Svahili iko tabu sana. Nakwenda sule. Napata digrii mingi. Hapana fanya biasara. Naogopa hasara lakini naishi kwa hasara. 
        Swahili iko penda faida. Vapi tapata faida kama hapana biasara? Au nataka kwenda kwa sirkal na kuibia chofu na fyatu juluku? Ile nasoma nayo howo kabisa. Napata digrii ya chumi nakuja chuma chovu na fyatu! Ile napata kazi kwa sirkal nageuka fisadi kuba. Kama hindi nasindva kwepa kodi, hapana lalamika. Hapa svahili nalalamika. Nasema hindi fisadi kuba. Kwani, hindi dio naongoza kayani?
         Sasa sirkal kama nalalamika hapana juluku, kvanini nasamehe kodi ile fanyabiasara kuba kuba? Hapana ona nafyatua na kuumija vatu yake? Nasikia kwa bungeni vaziri naulizwa kwanini nasamehe kodi bila kufuata sharia. Yeye nanyamaza kama jusi nabanwa na lango au chura kuba!
Sasa fyatu vote nakaa kimya hapana fyatukia vaziri lakini nafyatua kelele tu! Napiga kelele mingi kama chura ya bawani. Chura iko imba “yangu yangu.” Kama naokota jive napiga yeye, nakimbia! Natoka bawani hapana guo ya mvilini. Mingine naita chava. Naitwa chava nafurahi! Chava iko dudu chafu. Iko dogo na howyo sana dugu yangu. Je Swahili natofautina na chava guoni na chura bawani? 
        Kama nataka pata juluku, napasa kwenda fyatua ile fyatu kuba nafyatua juluku yao. Napasa zuia choli na mizi kuba. Kama naiba juluku na fyatu naomba yeye saada, sasa taacha kuiba juluku? Hapana nunua gari mingi ya sirkal. Naharibu kusudi. Nanunua vatu kuba kuba. Nakaa jumbani kuba kuba. Naoatesa tumbo kuba kuba. Naitwa kuba. Kila kitu ya kuba, kuba tu. Sasa dogo naishi vapi na wipi? Hapana tumia gari ya sirkal sereheni. Hapana nasafiri sana. Hapana fanya sanii na babaisaji mingi mingi. 
Kama nafanya mambo kuba na veve iko dogo na akili dogo, hapana ona naleta balaa na fyatu mingi nakosa juluku hadi nafyatuka nataka kufyatua veve kwa sababu ya jinga yako na akili dogo? Du! Kumbe naota!!
Chanzo: Mwananchi Alhamis iliyopita.

Chunga yasikukute ya Aziz na ndoa ya majuu

Aziz ni kijana wa miaka 24 wa Kipalestina aliyekimbia udhalilishaji kwao akaishia kudhalilika majuu. Kisa cha Aziz kinafikirisha, kusikitisha, na kufundisha. Wapo wengi kama Aziz walioharibikiwa maisha baada ya kuolewa wakidhani wameoa majuu. Kijana huyu, akiwa hajui hata Kiingereza, alijikuta akijiingiza kwenye ndoa ya mateso. Nkwazi alimjua Aziz. Alikuwa rafiki wa kaka yake aliyemlalamikia kuwa mdogo wake alikuwa akipoteza mwelekeo.
Tokana na kuwajua wote wawili, Nkwazi aliamua kuingilia kati kumsaidia Aziz. Kaka mtu aliwakutanisha Aziz na Nkwazi nyumbani kwetu walikozoea kuja kupoteza muda na kufundishwa Kiingereza. 
        Baada ya kaka mtu kueleza kisa kizima mbele ya mdogo wake, kama marafiki na walezi, tulimuuonya Aziz asijiingize kwenye uhusiano ambao ungemletea majuto baadaye. La kufa halisikii dawa. Azizi alichukia hadi kutwambia “hii ni Kanada nchi huru ambapo kila mmoja anaweza kufanya atakavyo.” Kwa maneno mengine, alitaka tusimuingilie katika maisha na uhuru wake hasa ikizingatiwa kuwa Kanada, vijana huweza kuamua kufunga ndoa hata bila kuwahusisha wazazi na ndugu japo si wote. Ghafla, Aziz aliacha kuja kwetu. Tulijua sababu. Aziz alikuwa kwenye mapenzi na mama aliyemzidi umri tutakayemuita Meg japo si jina lake aliyetaka wafunge ndoa. 
Pamoja na kumuonya asisikie wala kujali,  tulijua ni haki yake kufanya hivyo japo tulimtahadharisha juu ya tofauti za mila na dini. Mfano, tulimjua Meg kama mama aliyekuwa amempenda akipanga kufunga naye ndoa, alipenda sana kuongelea mbwa wake ambaye alikuwa akisema kuwa hata hula na hulala naye wakati mwingine. 
        Si ajabu huku kwa baadhi ya watu kula na mbwa kwa sababu kwao, mbwa ni sehemu ya familia. Hivyo, tuliona hatari itokanayo na kutofautiana kidini na kimila ambavyo vingemkwaza Aziz japo hakusikia. Baada ya kugundua kuwa Aziz alianza kutuchukia mbali na Meg ambaye alikuwa ameambiwa juu ya ushauri wetu, tulimuacha. Maana, yalikuwa ni maamuzi na maisha yake.
Hakika, Aziz na mama wa Kizungu walifunga safari kwenda kwenye visiwa vya Saint Lucia na kufunga ndoa na Meg.doa ilifungwa. Ndoa ilifungwa na fungate ikafanyika. Aziz na Meg walirejea Kanada wakiwa mke na mume. Baada ya muda mfupi, tuliamua kuhama mkoa tuliokuwa tunaishi na kusahau mambo ya Aziz na Meg.
Siku moja, Nesaa alikwama kwenye theluji usiku akitoka shule. Alijitokeza baba mmoja wa Kiarabu aliyekuwa na familia yake akamsaidia kwa kujaribu kukwamua gari asifanikiwe. Hivyo, alishauri ampe lift hadi nyumbani. Yule baba alimfikisha Nesaa nyumbani. Tuligundua kuwa kumbe aliishi mtaa wa pili toka kwetu. Alimsaidia Nkwazi kukwamua gari na tangu siku hiyo wakawa marafiki.
Baada ya miezi kupita, yule Mwarabu alikuja kutuaga kuwa alikuwa anahamia Toronto. Tulifurahi sana na kusikitika. Hata hivyo, alituuliza kama tunamjua Aziz toka kule tulikokuwa tukiishi mwanzo. Alituelezea namna Aziz alivyomuomba atuombe msamaha kwa kudharau ushauri wetu.             Tulimuuliza yule Mwarabu sababu za Aziz kukimbia na kujutia ndoa yake. Alitwambia kuwa Meg hakuwa tayari kubadili dini wala kuheshimu mila ya Aziz mbali na kutokuwa tayari kuacha kufuga mbwa wake kipenzi pamoja na mambo mengine binafsi kama nani mwenye madaraka zaidi ya mwingine kati yake na mkewe. 
        Kwa ufupi, Aziz alijikuta kwenye ndoa ya mateso hadi akakimbilia Toronto kuepuka ndoa ya mateso. Tulifurahi kusikia kuwa Aziz alikuwa amegundua makosa yake na mchango wetu na kujutia. Hata hivyo, maji yalikuwa yameishamwagika. Aziz, licha ya kuonja mateso na kuumia, alipoteza malengo na muda wake. Kwani, tulimshauri akasome kwanza akaghairi. 
Sasa tujiulize. Kisa hiki kinafundisha nini? Mosi, usilolijua litakusumbua hata kukuuumiza. Pili, asiyesikia la mkuu huvunjika guu. Tatu, vijana waepuke kujiingiza kwenye makubaliano ya ndoa bila uzoefu wala ushauri.
        Nne, tofauti za dini hata mila ni muhimu katika kufikia maamuzi ya kufunga ndoa. Mfano, Aziz, muislam, asingeweza kuishi na hata kuchangia kitanda na vyombo na mbwa.
        Tano, umri katika ndoa ni muhimu. Japo hatukatazi waliozidiana umri kuoana, kuna haja ya kulidurusu na kulijadili hili kabla ya kujifunga kwenye ndoa. 
        Sita, si kila ving’aravyo ni dhahabu.
saba, ingawa haya yanaweza kuchukuliwa kama masuala binafsi, yana somo kubwa kwa vijana wanaofikiri kuwa kuoa majuu ni kuukata. Wakati mwingi na mwingine, kufanya hivyo si kuukata bali kukatwa kama ilivyo kwa Aziz na wengine kama yeye.
Chanzo: Mwananchi Leo J'pili.