The Chant of Savant

Wednesday 20 March 2024

Sisi CcM Inapofyatua Kiki Kutufyatua Tikitiki

Marais sasa wa Danganyika waliodanganyika wakawadanganya wadanganyika Chiwawa na SSH (pichani).

Chama cha Mafyatu (CcM) kina sera ya Kisanii na Kizushi, sorry, ya Kishua na Kivungio (KIKI). Kutokana na KIKI kushika kasi, wapo mafyatu kaidi wanaoiita Kutapeli Institute in Kula Inchi, Kuzuga Ili Kufyatua Inji, Kudanga Ili Kupumbaza Inji nk. Juzi toto janja aliniuliza kitu chakufikirisha, kufundisha, na kufyatua nikakukumbuka KIKI iliyonipa kiki, makeke, na mikiki kufyatuka na kufyatua. Baada ya kushuhudia vimbwanga na vitimbwi vya KIKI, makeke, na mikiki, dogo fyatu alinifyatua tena kwa makeke na mikikii aliniuliza kaya ina marahis wangapi. Nilimjibu “doktari mazeri mwenyewe.” Alinicheka utadhani mie siyo profesa emeritus wala daktari ila dokatri. Nilitafakari, nikamuuliza “nitajie, wapo wangapi?” Alizoza “wawili?” “Wataje” niliuliza. Alijibu  "doktari, alhajat Ustaadha, alimuuminat, mazeri na kufari Bashiti aka Chiwawa.” La hawla wa la quwwata illa Billah! Kabla kuendelea kufyatuka na kufyatua, kijasho chembamba kilinichuruzika bila kufanya au kuacha nilivyozidiwa kete kiudodosi.

Dogo, kama Kadogo-Sir wa SgR uchwara, alinichanganya pamwe na udoktari na uprofesa wangu. Nilimuuliza “ulijuaje?” Alijibu “huoni huyu rahis chawa wa pili na wa kwanza anayeonekana runigani akipelekewa ‘matatizo’ kila aendako? Wa pili, anatanua ughaibuni.” Nilimuuliza “keshatatua matatizo gani?” Alifyatuka kimzahamzaha, mikiki, na kiki utadhani fyatu mzima “unadhani wana KIKI wanadhamiria kuwasaidia au kutufyatua waufyate tena kwa kutumia matatizo yao?” Aliendelea “ametatua matatizo sugu ya migao ya kila kitu? Kuona anavyofyatuka kunishinda, niliamua kuwajuza mafyatu mjue huu uchangu kisiasa.

            Nilitafakari kidoktari, kiprofesa, na kifyatu, nilikumbuka KIKI makabrashani ya kuwafyatuliwa mafyatu waufyatuke. Kama wale, tunayo sera mpya ya usahihi au political authenticity siyo yao olitical artistry Kisambaa. Kama wafanyavyo wasanii uchwara wa kisiasa majukwaani. Tumegundua. Mafyatu wamekata tamaa kiasi cha tapeli yeyote anayejifanya anawapenda hata kama anawaponda akiwahadaa anawajali wakati hawajali mbali na yeye na wenzake kuwa tatizo kubwa kuwafyatua! KIKI inatumia matatizo ya mafyatu kuwafyatua waamini wanene wanaowajali ingawa hawawajali wala kuwapenda bali kuwaponda.

 Mafyatu ni wagumu na wavivu wa kufikiri, hawaulizi kilichosababaisha matatizo kama migao ya maji, umeme, kupanda gharama za maisha, elimu mbovu, ufisadi, wizi, ubangaizaji, uzembe vinavyowayopeleka kwa waganganjaa wasio na tofauti na waganga wa kienyeji na wachunaji kutafuta utajiri au kuombewa ilhali wahusika ni makapuku na nyongeza na mazonge yao wakifyatuliwa kimasomaso?

Wamefyatua kibashiti wakidhani mafyatu hawajui na kuona matumizi mabaya ya njuluku zao. Misururu ya ndinga anazotumia si israfu na ufisadi? Je zingetumika vizuri zingetusaidia kiasi gani? Pamoja na yote, bado wapo wanaodhani bashiti aweza kutatua matatizo yao wakati anayazidisha. Hata waliomfyatua hawasaidii. Anawaponza. Kitambo, tulikuwa na sera hii kabla ya kundunguliwa tukawahiwa kuitumia. Sera yetu ni kufyatuana ili Kujenga Inji siyo hiyo KIKI uchwara ya akina Bashiti tuliyoshiti.

Turejee maswali muhimu ya dogo. Je wenzetu hawaoni wanavyojifyatua na kujifyatulisha kutegemea sanaa badala ya ubunifu mujarabu? Tunataka majibu ya matatizo sugu siyo ufisadi sugu na usanii. Inakuwaje vichanga vinawazidi akili mafyatu wanene na waliwao kuyaona na kuyatafakari yaliyowashinda? Je huyu rahis Chiwawa anamsaidia doktari mazeri au kuzidi kumrostisha huko tuendako hasa wakati huu ukapa unapotufyatua? Je wanaomshauri mazeri hawaoni balaa wanalotengeneza kwa mauti yao kisiasa hapo twenty twenty-five? Tangu lini tatizo likatatua tatizo? Bashiti na waliomfufua ni matatizo donda ndugu kwa mafyatu waelewe na kukubali. Huwezi kujifanya unawajali mafyatu wakati unawaibia na wale waliokutuma na chata lenu mnasifika kwa ubangaizaji, ufisadi, ufisi, ulafi na roho mbaya. Mnaitana majukwaani kuwafyatua mafyatu mkijifanya hamuelewani au kuwajibishana wakati ni karata tatu. Hayo matatizo mnayojifanya ‘kutatua’ yalisababisha na nani na yalianza lini kama siyo nyinyi? Tutakuwaje na mgao wa umeme na maji wakati wa mafuriko?

Hamuoni mnajifyatua na kujihadaa kwa kutaka kuendesha kaya kwa kamera majukwaani? Tunataka majibu na si maigizo, KIKI, na usanii. Kweli inaingia akilini chawa kuwatisha mafisi waliokubuhu waliotamalaki chatani na sirkalini? Kwa KIKI na ngonjera, sanaa, na kutaka ujiko, mmeishatatua matatizo mangapi? Umaskini unaengezeka. Bei za vitu muhimu hazishikiki. Tozo halikamatiki. Kikokotoo kinatukokota mifukoni. Taarifa za CAG zinapuuziwa Majambazi wanene wanazidi kuneemeka. Kuna matatizo yanayowasumbua mafyatu na kuwafyatua kama haya? Leo sifyatui mengi nisije nikaonekana nataka kiki kwa kutumia KIKI kama wale makeke na mikiki yao yatakayowafyatua tikitiki kama tikiti  lililodondoshwa mwambani mbali na kuwa tikiti ya kutokomea kisiasa.

Acheni kuwatia vidole machoni mafyatu. Msicheze na maisha yao mkidhani hawana akili wala kumbukumbu. Angalia mtoto alivyowaumbua na KIKI yenu ya kutaka kiki kikiri tena kwa makeke, mikiki, na mikukuliko.

Nimesema sera yao, sorry, yetu ni KIKI au ni makeke na mikiki ya kanywaji?

Chanzo: Mwananchi leo.

No comments: