Kwanza, nakusalimia kwa jina la Ujamaa na Kujitegemea uliotekwa, kupotezwa na kuuawa na baadhi ya mafisi na wahuni kama wabongo wako uliokufa ukiwalilia. Hebu tujuzane kifalsafa mafala wafulie. Kwa sasa, tuna uhujumaaa na kujimegeae. Wachache wanajimegeaa huku wengi wakifa njaa, kwani, hawana cha kujimegea baada ya uhujumaa kuwahujumuu.
Una hali gani, ushaacha ufyatu? Je, huko ufyatu ni dili au mnalala tu? Vipi mzee Madiba na Kenneth Kaunda mshaonana? Basi, wape hi. Usiwasahau akina Sam Nujoma, Dawda Jawara, na mashujaa wengine walioko huko walioacha tuna na si uchafu kama mafisi wengine unaowaona huko kama vile Mobutu, Abacha, Bokassa, Bongo, Eyadema, Houphouet-Boigny, Kamuzu, Kenyatta, na wengine.
Pili, ujue sikukusahau kwa kuwasiliana nawe wiki moja nikiwa nimechelewa. Wajua? Siku hizi, mafyatu wenzako tunaisha mafichoni. Huko hakuna mtandao. Hata huu ujumbe unaoupokea leo ni kwa sababu nilikuwa mafichoni karibu na mpaka na kaya ya kufuata nyayo bila hata kufikiri wala kujua ni za nini. Sikwambii ni Lunga Lunga, Namanga, au Sirari. Hii ni chiri. Nikitaja, naweza kutekwa, kupotezwa, kuteswa, na kuteketezwa. Usijali. Nilimtwangia Madaraka na kumpa salamu amfikishie Mama Maria. Hayo tuyaache fyatu mwenzagu uliyesifika kwa ufyatu hasa kutetea haki na usawa na kupinga uhuni.
Siku hizi, kuna mashetani wasiojulikana japo wanajulikana, wanaoteka, kutesa, kupoteza na kuua kana kwamba hakuna lisirkal. Mchezo huu mchafu ulianza baada ya kangosha kenye hasira kama nyoka kujipenyeza na kuufyatua unene. Ni pale wanamitandao uchwara ya jinai walipofyatuana. Kajamaa kaliwazidi kete hadi kuwavurugia kila kitu kabla ya kufyatuka roho ghafla kwenye mazingira yanayotatanisha.
Juzi, kuna ‘mhuni’ mmoja aliyewageuka wenzake na kuanika uchafu wao hadharani. Si alijisahau akazoza bila kuchukua hatua! Walimnyaka. Mpaka sasa, hatujui kama bado yuko hai au mmeishaonana huko uliko. Huyu ‘mhuni’ mgeni kwenye kundi la wahuni aliibuliwa na kale kangosha. Kalimpandisha vyeo kama hakakuwa na akili nzuri. Ubaya ni kwamba jamaa mwenyewe alipewa usemaji wa chata lako na akajisahau na kusahau kuwa kutesa ni kwa zamu! Alizoza sana.
Ngoja nikupe inshu nyingine. Una habari kuwa kangosha kalihamishia makao makuu ya kaya Idodomya? Ila baada ya kufyatuliwa, naona kama waliokuwa wamefyatukia Idodomya sasa wanarejea Dar Si Salama. Je, wajua kwanini naiita Dar Si Salama? Misongamano baba.
Kaya imegeuka dampo la kila uchafuu toka Chaini, kaya yenye jina kama Bata mzinga, ugabacholiini, nk., usiseme. Viwanda ulivyoacha vikanusurika kufyatuliwa na mwanafunzi wako vilishapigwa mnada na kugeuzwa magala ya kupokelea uchafu sorry bidhaa toka nje.
Kabla ya kumaliza, ngoja nikufyatulie inshu. Zamani, tukiitana ndugu bila kujali dini au kabila. Sasa, tuna matabaka ya mafyatu, wababe, na machawa wasifikao kwa kujikomba na kujigonga huku wale wanaojigonga kwao wasiwakemee kana kwamba wanafurahia na kuunga mkono jinai hii ya fyatu wazima kujigeuza wadudu tena wachafu na wanyonya damu. Tuyaache.
Du! Ni usiku. Nasikia kama kuna watu nyuma ya maficho yangu. Acha nikuache nikitoe kabla hawajaninyaka na kunipoteza nikasahaulika. RIP Fyatu Mzee mwenzangu Nchonga.