The Curse for Salvation

The Curse for Salvation

Tuesday, 2 December 2025

Nimeamriwa kufungua hekalu la God la KGBJRJFRM


 Nikiwa sina hili wala lile, juzi, nilitokewa na Malaika wa Bwana akaniminyaminya na kuniamru nianzishe Kanisa ili kuikoa dunia hii inayoangamizwa na uzwazwa. Mwanzoni nilikataa kufanya hivyo nikidhani ni ndoto tu. Mara ya pili, si nilimezwa na samaki aina ya changu kwa siku tatu kule Manzese mpaka Bi Mkubwa alipostuka wakati nilikuwa napitia kwenye majaribio aliyopitia Yona yule mjanja aliyemezwa na Nyangumi wa kike kwa siku tatu. Hayo tuyaache.
         Baada ya juzi kusikia Askopo moja wa kujipachia ambaye duka lake la kuchuuza na kuuza roho za mafyatu waliokata tamaa na kutapatapa, si nikaijiwa na wazo la kifyatu la kufyatua njuluku kirahisi. Hapa, lazima nifyatue ukweli. Lazima nifyatue njuluku tena kiulani. Soon, sitaitwa Fyatu kapuku bali Fyatu mkwasi. Najuta. Sijui kwanini nilipoteza muda vyuoni wakati kuna fursa rahisi kwa hata vilaza na vihiyo kupiga njuluku ndefu! Maana, unene wa NGO kama hii ni wa kujipachika. Auhitaji kupiga shule mpaka ukafyatuka na kuonekana chizi.
            Kusema ule ukweli, tuache utani. Sikuamini kusikia madai ya ajabu kuwa ndata wetu waaminifu na watiifu waliokuwa wakilinda duka hilo la Ufu na Uendawazimu eti walikwapua mabilioni! Du! Wamejua kutufyatua! Inakuwaje kwa mwizi anaiba mwizi kama kweli njuluku ilipigwa? Kumbe mkuki ni kwa nguruwe!  Hekalu la Sir God na njuluku wapi na wapi wakati mwana wa Adam alikuja na kuondoka akiwa kapuku? Ajabu, wezi, sorry, wapigaji wenye roho mtakakitu wakimuita roho mtakatifu wanawafyatua mafyatu wasiofyatuka na kuhoji kuwa wanamhubiri mwana wa Adam huyu ambaye mie namjua kwa sababu ni wa ukoo wangu.
            Jina la kanisa langu linaitwa The Kasri of all God's, All Binadams and Jinni for Redemption and Jannah Firdaws Roho Mtakakitu Mtakatifu (KGBJRJFRMM). Usishangae urefu na utata wa jina la nyenzo yangu. Kuwapata mazwazwa wakaamini umepiga vitabu lazima utumie kimombo na majina marefu. Pia, lengo jingine ni kuunganisha din izote na kuepuka mchezo wa kutumia dini, udini, na udini kuwagawanya na kuwadhoofisha mafyatu japo hawafutuki na kushutukia huu ufyatuaji tunaotumia kuwafyatua.
        Kuwafyatua mafyatu vizuri, lazima nishughulikie matatizo yote Hivyo, wale wote wenye matatizo kama vile uzwazwa, umaskini, ugumba, uchungu, huzuni, mawazo, wasiwasi, waliovimbiwa, wenye njaa, waliotekwa, waliopotezwa nk.nk. Mie nitawapatia majibu ya matatizo yenu yote. Unatoa sadaka kidogo au kununua maji ya uzima na matatizo yako yote yanaisha hapo hapo. Mfano, shoo yangu ya kwanza ni kuahidi kumfufua Aminia Mfupa au kujifanya nimepooza halafu nikajitibu mwenye japo ukweli ni kwamba mganga hajigangi. Nitahakikisha natengeza maji ya uzima ambayo nitayajaza urahibu ili atakayeyaonja awe anarudi kununua mengine nami nafyatua njuluku. Hapa, dhambi iko wapi? Si tuliaswa kwa wajinga ndio waliwao?
            Najua wengi wataanza wivu wa kizwazwa. Watahoji kwanini mwana wa Adam alihubiri umaskini nami nataka njuluku. Simpo. Ufalme waliwao ni wa mbinguni. Sie, wajanja ufalme wetu ni wa hapa duniani. Msishangae. Kwanza, kuna vishawishi vingi ambavyo muovu sheitwan kaniletea. Mfano, ukifungua duka la kawaida TrA wanakuandamana wakati la kiroho hakuna kulipa kodi japo unawatoza wachovu kodi. Pia, kwa kutumia hii nyenzo, naweza kuingiza bidhaa zangu toka ughaibuni tena zisizo za kiriho na za wengine free. Hawa, nitakaowasaidia kutumia nyenzo yangu kupitisha bidhaa zao, lazima niwatoze kodi mwenyewe japo sitozwi. Nani hataki ulaji huu wa dezo tena unaotaka ubunifu na kutumia akili kiduchu?
            Kwa vile wachovu hawana njuluku kama nitakazowakamua, nitawahimiza wamtegemee Mungu awalinde. Ila nashauri wasishangae kwanini mimi nitakuwa nalindwa na mabaunsa. Ni kwa sababu shetani anayeniandama ahitaji kupambana na Mungu bali mabaunsa. Ili kuhakikisha nafaidi hii fursa na ubunifu mpya, nitahakikisha natumia hii kitu yangu kugombea urahis. Maana, nao nimegundua ahuhitaji elimu wala chochote isipokuwa urahisi na utayari kuhomola na kuhondomola. Hapa, lazima nijifunze kwa tapelo mmoja aliyewahi kucheza haka kamchezo. Si alijiunga na chata twawala hadi akazawadiwa uhishimiwa hadi alipolikoroga akataka kuwatumia waliomtumia ili watumiane wakaishia kumtimua na kufunga duka lake akabakia kubweka kama dogi tena akijifanya kulaani yale aliyokuwa akiyashabikia zama zile za Mwendaze. Hapa, nitachanganya duni na siasa japo twaonya kuwa havichanganyikani. Mbona vinachanganyikana. Upaswacho kufanya ni kupiga siasa ukiwa ndani ya chata twawala. Duni na siasa japo vyote ni duni, havichanganyikani kama uko upingajini kwa akina Tunda Lishe.
           Ili kupiga njuluku ndefu, nitaanzisha mradi wa Kutenda miujiza. Hapa, lazima ‘nifufue’ wafu na kuponya vilema. Naona yule anashangaa. Kwani, kufanya mazingaombwe, sorry miujiza ni vigumu hivyo? Si unacheza mchezo na kupandikiza vilema feki ambao mkipata mnagawana. Unacheza na miujiza? Ukiachia hadithi na ngano za kufikirika na amewahi kuitenda?
            Mwisho, nitajipachika mavyeo mazito. Kuanzia leo, naitwa Alhaj, Mtakatifu, Mchunaji, sorry, Mchungaji, Askopo, sorry, Askofu, Kardinali, Papa, Paroko, Bruda, Darwesh, Daktari, Profesa, Maulana Muadhama, Shehena, sorry, shehe Ulama, n.k, n.k, etc. Hivi, nani walinileta hapa Mirembe?
Chanzo: Mwananchi leo Jtano.

1 comment:

Anonymous said...

πŸ˜…πŸ˜…πŸ˜…πŸ˜…πŸ€­