Liberal Peace Conflict, Gender, and Peacebuilding

Liberal Peace Conflict, Gender, and Peacebuilding

Monday 17 June 2024

Misingi na Nguzo za Ndoa (2)

Leo tunaendelea tulipoishia kuhusiana na miiko na nguzo za ndoa. Karibuni tuendelee.
Maadili
Taaluma na taasisi yoyote lazima iwe na maadili ya kufanya ifanikiwe na kuheshimika. Ndoa kadhalika, lazima iwe na maadili vinginevyo haitafanikiwa au kuimarika. Kama ilivyo masharti ya udereva au uongozi, maadili ni nyenzo zinawezesha wanandoa kujifunza nini wafanye au wasifanye na kwanini. Maadili, licha ya kuwaongoza wahusika, huwapa fursa kuona madhara yanayoweza kuwapata wanapokiuka maadili ya ndoa kama tulivyogusia hapo juu juu ya changamoto na hatari za ndoa. Kuna usemi wa kimombo unaofasiri maadili kama kujua tofauti kati ya ulicho nacho haki kutenda na kilicho sahihi kutenda (ethics is knowing the difference between what you have a right to do and what is right to do). Pia, kuna busara nyingine inasema kuwa mtu asiye na maadili ni sawa nyamamwitu aliyeachiwa kwenye dunia hii (a person without ethics is a wild beast loosed upon this world).
            Tusisitize. Kama zilivyo nguzo nyingine, maadili ni muhimu au tuseme ni mojawapo ya matofali yanayojenga ndoa. Lazima wanandoa wayazingatie.
Miiko
Pamoja na mambo mengine, taasisi yoyote, ili idumu, ifanikiwe, na kuwa salama, lazima iwe na miiko yake ambao inaoingoza katika kuendesha mambo yake. Katika ndoa, miiko ni mojawapo ya nguzo zake. Kuna vitu mfano, hamuwezi kuitana au kufanyiana. Kuna kisa cha wanandoa katika nchi moja ya Amerika ya Kusini. Katika kisa hiki, mwanandoa mmoja alichukia hadi kufikia kutishia kuvunja ndoa kwa sababu mwenzie alijamba wakiwa kitandani wanaongea kabla ya kulala. Si kwamba hawa wanandoa walikuwa hawafanyi hivyo. Kilichogomba ni kanuni. Kila aliyetoa upepo alimtaka radhi mwenzake vinginevyo awe amelala fofo hajitambui. Hivyo, mwanandoa alioachia hewa na kushindwa kuomba msamaha, alikuwa amevunja kanuni moja kubwa. Jambo hili ni dogo, kama tulivyoonyesha hapo juu ila laweza kuwa na madhara makubwa kimahusiano kwani, lilitaka kuzaa makubwa kiasi cha kutishia ndoa ya wahusika. Hivyo, kanuni mlizojiwekea lazima mzifuate hata kama ni ndogo kiasi gani.
Upekee
Kama tulivyo viumbe. Kwa mujibu wa sayansi ya vinasaba (DNA science) kila mmoja wetu ana DNA tofauti na mwenzake na wenzake. Na ndoa kadhalika. Zina DNA za kipekee. Ndiyo maana hupaswi kufunga au kuendesha ndoa yako kwa kuiga ndoa nyingine. Hivyo, jambo mojawapo la muhimu ni kutambua na kuipa upekee ndoa yenu ili iweze kufanikiwa na kupambana na changamoto zake vilivyo bila ya kuigiza au kukopa japo si vibaya kujifunza kwa wengine wenye ndoa kongwe na zilizofanikiwa kuliko zenu. Hata hivyo, lazima muangalie mazingira na sababu za kufanya hivyo.
Siri na usiri
Japo siri na usiri (secret and secrecy) vinahusiana, havina maana moja. Ni rahisi kutengeneza siri japo ni vigumu kutunza siri kama hakuna nguvu ya ziada au sababu zinazokuzuia kufanya hivyo. Katika ndoa, siri na usiri vinakwenda bega kwa bega. Ili siri iwe salama, lazima kuwae na usiri. Na ili usiri uwepo lazima kuwa na siri ya kutunzwa. Ukiachana na misingi na siri za mafanikio ya ndoa hapo juu, msingi mwingine ni siri. Ndoa ina siri zake. Wenye ndoa pekee ndiyo waumbaji, watunzaji, hata wavujishaji siri. Tumegusia umuhimu wa kulishwa kiapo kabla au wakati wa kufunga ndoa. Mbali na kuwa ishara ya kukabidhiwa majukumu, kutoka hatua moja hasa ya chini kwenda ya juu, mantiki ya kiapo ni kutunza siri. Unadhani kinachofanya askari wawe watii wasitumie vibaya nguvu na silaha zao ni nini kama siyo kiapo na usiri wa kazi yao? Bila siri, hakuna taasisi. Ndoa siyo kama chumvi muazimane na majirani na marafiki.
        Kama ilivyo kwenye siri ya mtungi, muachie kata pekee ajue siri zake. Kama mume au mkeo ni tajiri au kafanikiwa katika jambo, huna haja ya kugeuza mafanikio yenu kuwa matangazo ya biashara. Wakati mwingine mafanikio yanaweza kuwa chanzo cha maanguko kama hayatahifadhiwa na kutumika vizuri. Kuna methali ya kiingereza isemayo kuwa thamani ya siri hutugemea dhidi ya watu unaopaswa kuitunza au kuiepusha (secret's worth depends on the people from whom it must be kept). Methali nyingine inasema kuwa kutunza siri yako ni busara lakini ukitegemea wengine waituinze ni upumbavu (to keep your own secrets is wisdom but to expect others to keep them is folly).
Wivu
Kama ilivyo petroli kwenye gari au mashini yoyote, ndoa bila wivu wa pande zote si ndoa bali maigizo. Kama tulivyodokeza hapo juu, binadamu ni kiumbe mwenye wivu wa kuzaliwa nao. Je itakuwaje utakapogundua kuwa mwenzio hana wivu nawe? Je ni kweli hana wivu au anao kwa mtu mwingine mbali nawe? Kwa wanaotoka Tanga wanajua. Kuna usemi kuwa siyo wivu tu bali hata limbwata kwa mume au mkeo linafaa ili muwe pamoja. Haya ndiyo mapenzi.  Mithali 6:34 inasema wazi kuwa wivu humfanya mtu achukie kiasi cha kutoonyesha huruma siku kulipiza kisasi. Japo si wote wanaoamini katika biblia, kuna ukweli katika aya hizi ambazo wakristo na waislamu huziamini. Tunaomba kutofautisha wivu huu na husda ambayo ni dhambi kama Muslim (V. 2) anavyoonya kuwa msichukie, kuwa na husda au kugeuka.
Chanzo: Mwananchi jana.

No comments: