Liberal Peace Conflict, Gender, and Peacebuilding

Liberal Peace Conflict, Gender, and Peacebuilding

Monday 16 September 2024

Ndoa ni darasa jifunze na ufunze


Tuanze na kisa cha wanandoa wawili marafiki na wageni waliotutembelea hapa nyumbani. Walitoka Toronto kuja Manitoba. Hivyo, ilibidi walale lau tujadili hili na lile. Baba ni kutoka nchi jirani ya Tanzania. Mama ni mkanada mzaliwa wa Toronto. Ilipofika wakati wa kulala, tuliwakumbusha watoto wetu kwenda kupiga miswaki na kwenda vyumbani kwao. Baada ya hapo, na sie tuliwaaga wageni wetu kuwa tulikuwa tunawenda maliwatoni kupiga mswaki. Hawakuamini kama ambavyo nasi hatukuamini baada ya kueleza mshangao wao. Wale wanandoa walitushangaa kwanini tunapiga miswaki kabla ya kulala. Nasi, tuliwashangaa. Mama alisema kuwa akipiga mswaki wakati anakwenda kulala, asingeweza kupata usingizi mbali na kinyaa cha kufanya hivyo! Nesaa naye alimwambia kuwa akilala bila kupiga mswaki, asingepata usingizi. Hivyo, tulishangaana kama ambavyo hushangaana kwenye mbalimbali ambapo huishia kujisuta wakidhani wanawasuta wenzao.

Sasa unaweza kujiuliza. Kama una mazoea safi ya kupiga mswaki kila ulalapo , utajiuliza hata kushangaa inakuwaje walale bila kupiga miswaki. Ukiangalia kisa hiki, kinahusu jambo dogo lakini lenye umuhimu mkubwa na la binafsi lakini kinaweza kukufunza mengi. Je ni mangapi wanandoa hawayajui japo ni muhimu?

            Mnapofunga ndoa, kila mmoja anakuja na mambo yake, yawe mazuri au mabaya. Kila mmoja anakuja na mazoea yatokanayo na malezi, mazingira hata uchaguzi na utashi wake. Ni kapu mchanganyiko. Hivyo, mnapoanza kuishi kama wanandoa, jambo kubwa na la muhimu ni kuwa tayari kujifunza na kufundisha. Ndoa ni kama darasa au shule isiyokuwa na mwisho. Ili kuifanikisha, wanandoa, bila kujali viwango vya elimu au umri, lazima wawe tayari kuwa wanafunzi na walimu kwa wakati mmoja. Ukiangalia hili la kutopiga mswaki wakati wa kulala, pia laweza kuwapo la kulala bila hata kuoga. Binadamu ni viumbe wachafu. Unapalala mchafu, unategemea kweli mambo yaende vizuri? Umeshinda unakula, kujisaidia, kutoa jasho na mengine. Sasa inakuwaje unalala m chafu? Je kwa wale waliozoea kulala bila kupiga mswaki au kuoga hawajapata la kujifunza hapa? Je wale wenye utamaduni wa kuyafanya haya hawana la kuwafundisha wasioyafanya?

            Binadamu tuna mazoea na mila tofauti na saa nyingine kinzani kiasi cha kuchekana na kuishia kujicheka bila kujua. Mfano, kuna jamii huko bara Asia ambayo huamini kuwa kuramba vidole ni kuonyesha kuwa chakula kilicholiwa ni kitamu! Ukila na kumaliza bila kuramba vidole wanakushangaa kama unavyowashangaa kwa kuramba vidole. Pia, huko huko, wapo wanaokula kwa kupwakia na wengine wakiongea. Ukila kimya, bila shaka watakushangaa kama utakavyowashangaa. 

        Pia, kuna mazoea mabaya zaidi kwa wanandoa kula chakula cha usiku (wakubwa mnatuelewa) kwa kupigishana makelele bila kujali watoto hata kama wapo chumba cha pili hasa kwenye jamii za kibinafsi za Magharibi. Wakati kwa Waafrika hili ni mwiko, kwa wenzetu hutushangaa inawezekanaje kula chakula cha usiku cha baba na mama bila kupigishana makelele. Nasi huwashangaa inakuwaje wapige makelele kama nguruwe kiasi cha kuharibu watoto wao.

 Kwa watu hasa wa Pwani, haya ni makufuru. Je wanapooana watu toka kwenye hizi jamii tofauti, kweli hawana la kujifunza na kufundisha? Inakuwaje mtu ule kama mbwa, kuramba vidole, au kupwakia kama fisi? Unaweza kuhoji.

Turejee kwenye ndoa kama darasa hata shule. Je wewe au mwenzako alishawahi kukutana na mazoea, mila, au tabia ambazo ni tofauti hata kinzani na za mwenzako. Je huwa mnafanya nini mnapojikuta kwenye hali kama hii? Kama hamjawahi, mkijikuta kwenye hali kama hii, mtafanya nini? Hapa hakuna jibu moja. La muhimu, ni wote wawili kuwa tayari kujifunza na kufundishana bila kila mmoja kushikilia lake ndiyo sahihi. Mfano, katika kisa cha kutopiga mswaki, kupiga mswaki wakati wa kulala ni bora kuliko kutofanya hivyo. 

       Pia, katika kisa cha kupwakia kama wanyama na kuongea wakati wa kula, kukaa kimya ni bora kuliko kutofanya hivyo. Hata hivyo, tuonye. Mazoea ni magumu kuyaacha hasa yanapokuwa sehemu ya makuzi na malezi ya binadamu.

Tumalize kwa kushauri kuwa, katika kutatua matatizo kama hayo, wanandoa wanapaswa kuwa flexible (hatuna Kiswahili chake). Wawe tayari kujifunza na kufundisha na si mara moja bali miaka yao yote.

Chanzo: Mwananchi jana.

No comments: