Liberal Peace Conflict, Gender, and Peacebuilding

Liberal Peace Conflict, Gender, and Peacebuilding

Friday 6 September 2024

Tumechatwa Hadi Tumechakatika Haswa


Juzi, mtukufu doktari rahis alipofyatua na kuchakata, viherehere, vibwengo, na visebengo waso adabu wenye wivu waliawashwa midomo wakafyatua yasopaswa. Alipowaweka kando njemba wawili waliozoea kupayuka bila midomo kuwasiliana na bongo, wapo waliompongeza na kulaumu kwa kutumbua majipu, kujivua magamba, na kutua mizigo. Hakika, mafyatu si binadamu kama wajumbe! 
        Alipochakatua na kuchakata kwarejesha wakongwe wabee, vibabu tena chakatwa badala ya gen Z. walianza, mara “anatuletea Gen Zees makapi.” Jamani, mnataka afanye nini mfurahi au kuridhika? Akiteua wakweze, mnasema ufamilia na ufalme. Akinyamaza kama chura, mnasema mwoga!
            Ukizungukwa na jalala, kila kikufaacho ni uchafu tokana na kuwa nyenzo pekee jalalani. Jikumbusheni profedheha mwenye jina kama kabundi kadogo aliyechemolewa jalalani na aliyemfinyanga kisiasa. Ukitumia nyundo, kila tatizo ni msumari. Ukizoea kunyonga, yanini kuchinja?
            Mnafyatuka eti kazi sasa ni kuchakata na kuchakatua hata maiti. Kazi ya urahisi ni nini? Akisafiri, mnazoza. Afanye nini wakati urahisi ni uungu mtu unaompa madaraka yaso mipaka kufanya atakalo akasifiwa hata akikosea? Akirejesha vibabu, yawahusuni? Mwataka ateue wajukuu zake au wapingaji kama Looter kule kwa jirani? Kwani, hamuoni?
        Nawashangaa.  Mshindwe na waregee. Kitu gani siyo recycled? Mmesahau, uchakachuaji, sorry, uchaguzi uliopita uliochakata hawa mnaowaita recycled materials? Ebo! Nani, mara hii, kasahau mchakato wa bao la mkono? Je huku siyo kuchakata tena kisiasa ambako nyie huita uchakachuaji? Ni uchakataji kuanzia chini hadi juu, juu hadi chini na kila kitu kimechakatwa. Sera hazitoki majuu? Shopping na wachukuaji siyo majuu?
        Kwanini tumegeuka kaya ya uchakataji aka recycled kaya? Mosi, ni ukosefu wa nyenzo aka materials zifaazo. Jiulize. Kisiasa, maadili yamegeuka madili na siasa sasa ni sanaa na usanii bila kusahau misifa na usifiaji hadi njemba nzima zinampigia magoti mja utadhani Mungu.                         Tumeishiwa sera nini? Sifa zinageuka sera na sera zinageuka maudhi, uongozi umegeuka uongo, ukale umegeuzwa usasa na usasa ukale. Tunazalisha pamba. Tunavaa mitumba. Tunasomesha na kuzalisha mitumba. 
        Hizi ni zama za kujihudumia badala ya kuhudumu, na kutumikisha badala ya kutumikia. Haki na stahiki vimegeuzwa hisani, ukweli umegeuka uongo, ubangaizaji umegeuka kazi, haramu imehalalishwa na halali imeharamishwa. Akina Yero wamegeuzwa wakimbizi Kayani mwao. Kwani, hamuyaoni jamani? Mnasema ujanja kupata? Mwataka nifyatuke vipi mnielewe muache kulalama mfanye kweli?
        Pia, kijamii, ni kuchakata kwenda mbele. Jitu jeusi ja mkaa linatoja tojo (tattoos) nyeusi likiigiza watasha. Mingine mibwabwa na misagaji. Kama haitoshi, siku hizi, imbaba mizima inavaa hereni, vipuri, miregezo, kuonyesha ‘undaweya’ chafu bila aibu, kusuka na kutoboa masikio mbali na miziki recycled na wanamuziki walochakatwa kiubunifu waharibuo maadili nasi tukishuhudia kana kwamba haituhusu? Mwachakatuliwa na kuchakatwa bila chekeche. Mwacheza chakacha!
            Kiuchumi, zamani ulikuwapo uchumi si uchumiatumbo. Tulikuwa na wachumi si wachumaji, wawekezaji wamegeuka wachukuaji, watawaliwa wamegeuka watu waliwao, wafadhiliwa wamegeuka wafadhili. Wezi wanalinda fedha na mbwa kulinda nyama. Mnalalamika nini wakipiga njuluku na kutajirika mkageuzwa makapuku na walalamikaji wasiochukua hatua? Mnadhani kuna wafadhili watakuja kuwakomboa? Thubutu yenu!                             
Jikomboeni. Uchumi mmeugenisha. Mmegeuzwa manamba kwa kisingizio cha kutengeza vibarua muitavyo ajira. Kwanini kutegemea ajira? Kuweni wabunifu mjiajiri na kuwaajiri hao wageni wanaowaajiri? Imefikia mahali Afrika inakodisha ardhi kwa wageni kuzalisha chakula kwa ajili ya watu wao kukwepa kukinunua kwa bei mbaya wakati inaagiza hata nyanya na mayai visa toka ughaibuni halafu inasema iko huru. Uhuru au udhuru?                                     Wanene  watanuaji wanatanua sirkal na mikanda wakati nyie mkiambwa mfunge mikanda. Mtakula lini au mwangoja muingie peponi ambako hamna uhakika mbali na kuingia bila midomo wala matumbo? Mla kala leo kesho kalani.
        Siku hizi, uchatakataji umevamia hata anga za kiroho na kugeuza uroho kuwa dili na dini. Zamani, tulikuwa na mashehe kwelikweli siyo mashehena waliosheheni uroho hadi wanauza mali za wakfu au kugeuka wapiga ramli na waganganjaa wa kienyeji. Msiseme nazusha. Kumbuka mwendazake alivyoshupalia kurejesha baadhi ya mali za baadhi ya wale ambao siwataji. Wamejaa wachungaji waliogeuka wachunaji kondoo waliopaswa kuwachunga. 
            Wanawatoza njuluku eti kuwapa huduma wakati ni hujuma tupu. Kwani hawapo? Hamkusikia zile kashfa za ngono? Hamuoni kuibuka utitiri wa manabii na mitume uchwara?             
    Zamani, dini ilikuwa huduma si hujuma. Siku hizi, imechakatwa nasi tukiangalia tu na kugeuzwa biashara ya mabilioni. Utapeli na mauzauza vinaiitwa miujiza wakati ni wizi itumiayo mijizi iliyojificha nyuma ya imani sawa na ile imani ya amani katikati ya vurugu, utekaji, ujambazi, upigaji njuluku za umma n.k. Kwani, hayapo? Nasi tumevamiwa.Tuna makanjanja wanaosaka bahasha badala ya habari wajaze mitumbo yao isiyotosheka.
            Nimalize. Muacheni bibie achape kazi, kutanua hasa usawa huu anapokwenda kusaka kura ya kula ili kuendelea kukamua. Mwenye wivu ajinyonge. Msitupigie kelele vinginevyo tutawasweka lupango kama akina Tunda Lishe aka lion na wenzake. Juzi, nilisikia akichangisha njuluku kutengeza gari lake. Kwani halikuwa na bima? Nimesemaje?
Chanzo: Mwananchi Jumatano juzi.


No comments: