The Curse for Salvation

The Curse for Salvation

Wednesday, 5 November 2025

Kumbe Mafyatu waweza kufyatuka na kufyatua wawafyatuao!



Haiwi haiwi, huwa na imekuwa! Si Nepali na Madagascar mafyatu walifyatuka na kufyatua kikaumana! Nani alitegemea mafyatu waliodhaniwa kutoweza kufyatuka au kufyatuliwa wangefyatuka na kufyatua wafyatuzi? 

            Watani wao waliwaita maiti. Hawakujua wangeweza kufufuka na kufyatuka wakawafyatua wawafyatuao! Hili liwe somo hata kama ni la kifyatufyatu. Hakuna aliye salama kama mafyatu watafyatuliwa wakafyatuka na kufyatua.

Huwa sipendi fujo wala dhuluma. Ni mpenzi kindakindaki wa haki ya kweli. Sipendi maigizo wala sanaa. Nachukia ngonjera, nyimbo, na mashairi vya sifa uchwara ilhali mafyatu wanafyatuliwa na matatizo yanayoepukika. 

        Fyatu ana nini hadi asifiwe na apende na kuridhika na kusifiwa? Waweza kuchukiwa na kusutwa hata kupondwa ukahadaika wapendwa. Hapendwi fyatu hapa. Ukiona mafyatu wanakupenda, jua kuna kitu wanataka kwako. Wakikusifia ukakubali, kubali na kupondwa ukubali hata kuchukiwa. Hayo tuyaache.

Leo, nitafyatua kisa cha Mafyatu waliofyatuka na kuwafyatua wawafyatuao huko kaya jirani ya Madagascar na Nepali hadi dunia ikafurahi, kushangaa, na kuogopa. Walidhani hawawezi kufyatuka na kufyatua. 

        Mafyatu si mawe yasiyobadilika. Ni wajanja usipime. Wanaweza kujifanya hawafyatuki wala kufyatuliwa ilhali wakipima situations na kudurusu namna ya kufyatuka lau kijulikane pale wafyatukapo wakafyatua kama walivyofyatua mafyatu wa Madagascar hadi dogo akakimbia ulaji wake kinomi. Sasa ishakuwa. 

        Nashauri tuache kuishi kwa mazoea tukijipa matumaini ilhali hali ni tete tokana na onyo dhahiri walilotoa mafyatu kuwa wakizidiwa, wanaweza kufyatuka na kuwafyatua wawafyatuao ambao wamepigwa na bumbuwazi wasiamini macho na masikio yao. Tujifunze toka kwa wenzetu.

Sasa nini kifanyike?

Jibu ni simpo. Wawafyatuao mafyatu wawajibike na kuonekana wakiwajibika kwa kuwatenda haki kabla ya mafyatu hawajafyatuka au kufyatuliwa zaidi na kufyatua zaidi. Wasikilizeni mafyatu na kujua matatizo yao ambao hata kuku wanayajua. Wawezeshe mafyatu badala ya kuwafyatua au kujifyatua akili kuwatisha mkidhani wanatishika wasifyatuke na kufyatua. Mafyatu wakifyatuka, huwa hawazuiliwi wala kufyatuliwa. Ukapuku umezidi ilhali  waneneo wawafyatuao mafyatu wakizidisha ukwasi utokanao na ufyatuaji wa haki zao.

Nini kifanyike?

 Ufyatuaji na matumizi mbaya ya mali na njuluku za umma vikomeshwe mara moja. Wajibikeni. Mjue, kama nyinyi, kila fyatu anataka amani na ufanisi. Je, amani yawezekana bila kutenda haki? Tendeni haki. Haki huleta amani na upendo, tofauti na dhuluma na ufyatuaji wa mali na njuluku za mafyatu huwafyatua mafyatu wakafyatuka na kuwafyulia mbali wawafyatuao. 

            Si mmeona wenyewe walivyofyatuka hadi kikataka kunuka pale jirani?  Wanene walijifyatua wakatuma ndata kuwafyatua nazo zikafyatuka na kuacha kuwafyatua mafyatu na kuwaacha wawafyatue wanene wao. Je, hii maana yake ni nini? Jibu ni simpo. Mafyatu waliodhaniwa kufa wamefufuka na kufyatuka hadi kuanza kufyatuana na wale wasiofyatuliwa ambao kazi yao ni kuwafyatua mafyatu na mali na njuluku zao.

Ushauri wa bure

Mafyatu wakifyatuka, wote tutafyatuwana na kufyatuliwa. Hakuna fyatu au fyatuzi wala fataki atapona katika mfyatuko huu. Mafyatu weshazoea maisha ya kufyatuliwa. Hivyo, wakifyatuka au kufyatuliwa na kufyatua, watakaoumia ni wale ambao hawajazoea ufyatu isipokuwa kuwafyatua mafyatu wasijue nao wanaweza kufyatuka na wakafyatua kama walivyofyatua tena kwa kuchovya tu.

Nini zaidi kifanyike?

Wanene wawafyatuao mafyatu waache kiburi na kujidanganya kuwa mafyatu hawawezi kufyatuka wakawafyatua wakati ni rahisi kuwafyatua wakafyatuka na kufyatua hata kaya kwa ujumla. Mafyatu si mazwazwa. Ni wajanja. Wanajua mambo mengi. Wanajua nani alifyatua nini na ameficha wapi. Jiulize. Kwanini baadhi za mali mafyatuzi zimefyatuliwa. Wangezijuaje kama wasingekuwa wanajua? Usione mtego umeinama ukajifyatua na kukadhani hauwezi kufyatuka ukakufyatua. Mafyatu ni kama mtego ulioinama ukingoja kufyatuka au kufyatuliwa halafu ukafyatuke na kufyatua.

Kipi kifanyike?

Lipo la kufanya. Nalo, ni kuacha kuendelea kuishi kwa mazoea na kujifyatua ufahamu kwa kujipa matumaini yasiyokuwepo. Ukiona mwenzio kanyolewa, tia maji. Tujue hata kwa kulazimika kuwa mafyatu ni kama volcano. Huwa haifi bali hulala au kulazwa. Ila hufyatuka au kufyatuliwa ikafyatua na kufyatuka. Suala hapa si ni kama bali lini itafyatuka na kufyatua. Je, itafyatuka na kufyatua lini na vipi? Si rahisi kujua. 

            Hivyo, ajidanganyae na kuandaa mauti yake ni yule ajifyatuaye na kuifyatua ikafyatuka ikamfyatua bila na wakati asiotegemea. Kadhalika, Mafyatu wakiamua kuwafyuka au hata kufyatuliwa, ni wazi. Hakuna wa kuwazuia wala kuwafyatua. Kama volcano, watafyatuka na kufyatua tu na kuwaacheni majeruhi mkiwa mmefyatuliwa vilivyo bila kuamani.

Chonde chonde

Msijifyatue na kuifyatua volcano mkadhani mtaifyatua isiwafyatue mkafyatukia mbali. Kadhalika, mtawafyatua mafyatu waliofyatuka wawafyatue bure. Watawafyatua vibaya sana. Mjue. Kizazi fyatu cha sasa kina hasira. Chochote na yeyote na wakati wowote chaweza kufyatuka au kufyatuliwa kikafyatua wafyatuzi. Kwani, hakina cha kupoteza zaidi ya kuandika historia fyatu mpya na mbaya. Huwa siku zote nafyatua kuwa kuna siku tutafyatuana. Si yamefyatuka na kutimia! Naonya tena. Mafyatu wamefyatuka. Wawafyatuao wajiandae kufyatuliwa zaidi. Kumbe visa yangu ya kuishi Madagascar imeisha! Ngoja nijifyatue kabla hawajanifyatua.

Chanzo: Mwananchi Jtatu leo.



No comments: