The Chant of Savant

Sunday 21 November 2021

Barua kwa Rais Samia Kuhusu Mgao wa Umeme

Mheshimiwa Rais, kama ada, nakusalimia kwa jina tamu la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Ni kitambo sasa tangu tuwasiliane hata kama, mara nyingi, hujibu kwa maneno bali vitendo. Kwa heshima na unyenyekevu mkubwa, naomba leo nigusie suala kero na nyeti si kwa taifa tu bali hata kwako binafsi kama kiongozi wa nchi ambaye mambo, yanapoharibika mambo, hata kwa hujuma na uzembe wa wengine, ndiye unayelaumiwa. Kwanza, nikupe pole na hongera kwa ziara yako nchini Misri, japo nina maswali mengi kuhusiana na nchi hii ambayo imekuwa ikitaka kuziburuza na kuzidharau nchi za kiafrika hasa zile za kwenye bonde la mto Nile kwa kulinda maslahi yake kitaifa kwa kuyahujumu ya wananchi wa nchi husika. Niende moja kwa moja kwenye hoja. Kwa sasa, watanzania wanakabiliwa na jinamizi na zahama ambazo walishazisahau hasa baada ya awamu ya tano uliyokuwa mmojawapo wa wakuu wake ilikomesha. Hili si jingine bali ni mgao wa umeme na ukatikaji wa mara wa umeme mambo ambayo athari zake ni kubwa kwa maisha na uchumi wa taifa letu.
        Mheshimiwa Rais, unajua kuwa kwa sasa siishi Tanzania. Nipo masomoni Kanada japo moyo na roho yangu viko nyumbani. Hata hivyo, ndugu zangu na watanzania wenzangu wanaishi hapo. Hivyo, kama mtanzania halisi na mzalendo, kila linalowagusa, kwa namna moja au nyingine linanigusa. Hivi karibuni, ulikaririwa na vyombo vya habari ukisema “kuna watu wanalima karibu na vyanzo vya maji haya yote mawili yanapelekea vyanzo vya maji kupungua. Yanapungua na hayaendi kule yanapotakiwa yaende.” Je tatizo ni kilimo tu au/ima hujuma kwako binafsi, mazoea na ufisadi? 
        Mtangulizi na bosi wako aliyekuamini kuwa makamu wake na ambaye, kwa kiasi kikubwa, imani yake kwako na uamuzi wake, vimechangia pakubwa wewe kuwa Rais, Hayati Dkt John Pombe Magufuli (RIP) aliwahi kufichua kuwa mgao wa umeme nchi siyo sababu ya mapenzi ya Mungu bali binadamu wabinafsi, wachoyo na waovu ambao alisema kuwa walikuwa wakishirikiana na wauzaji wa majenereta kwa kufungulia maji usiku na kusema hakuna maji ya kutosha ili kuwawezesha wahalifu hawa kufanya biashara ya kuwanyonya watu wako. Je hapa tatizo ni mazingira au hujuma ukiachia mbali ufisadi na mazoea? Tafadhali chunguza.  Hili bila shaka, halina shaka hasa ikizingatiwa kuwa aliyeliibua alikuwa mkuu wa nchi aliyesifika kwa ufuatiliaji na uzalendo wake. Je         Mheshimiwa Rais, utakubaliana nami kuwa tatizo hili halikupatiwa suluhu? Je mchezo mzima bado unaendelea ili kuwanufunufaisha wenzetu ambao ni wachukuaji wanaojiita wawekezaji wakati hawawekezi chochote zaidi ya hujuma? Chonde chonde. Nakuomba uliangazie na kulitafakari hili.         Mheshimiwa Rais, kiti ulichokalia ni kikubwa na kina utamu hakuna mfano. Naamini umeliona na utaamini nisemayo. Ili kukipata, kwa wale ambao wanakinyemelea, lolote linawezekana ukiachia mbali ubinafsi, tamaa, upogo na uovu.
            Hivyo, nakuomba uangalie mbali zaidi ya matatizo ya kimazingira ambayo sina ubishi wala ugomvi nayo kuwa yapo na ni sababu tosha, kati ya nyingi, zinazosababisha uwepo wa mgao usio wa lazima wa umeme kwa nchi iliyojaliwa vyanzo vingi vya umeme isipokuwa ujuzi na utashi wa kufanya hivyo.
            Hivi karibuni, ndugu yangu mjasiliamali maarufu na mkubwa aishie Dar es Salaam aliniandikia ujumbe ufuatao akilalamika kwa kusema “huyu mama naona kama anachemka yaani juzi nimepata ahibu kubwa kwa mtu anatakuwekeza kwenye soko kubwa la frozen products ghafla umeme ukatika siku nzima na biashara yangu ikazimikia hapo tena mtu nimemtoa mbali.” Alipoandika ‘huyu mama’ alimaanisha wewe. Sijui alifikiaje hitimisho na uamuzi huu vipi na kwa vigezo gani. Binafsi, sina cha kuficha au kuchelea wala sababu ya kufanya hivyo hasa nikizingatia kuwa nimekuwa nikikushauri kizalendo si kwa kuchaguliwa, kuteuliwa au kutaka bali kusukumwa na mapenzi na uzalendo kwa nchi yangu. Baada ya kupata ujumbe huu–––ambao haupendezi hata kwangu––––nilijiuliza maswali mengi mojawapo myakiwa: je ni wangapi wameathirika? Je ni wangapi wana hasira, mawazo na maoni kama haya? Je hakuna haja hapa ya kuwafahamisha wadau ukweli ili kuepuka lawama kama hizi ambazo si nzuri kwa kiongozi na mkuu wa nchi ambaye hana shaka katika mapenzi na utumishi wake kwa umma?
            Kama wasaidizi na washauri wako, ima wanakuogopa au kuogopa kukwambia ukweli, haya ndiyio yanayozungumzwa. Hizi ndizo hasira na hisia za watu wako ambao hawana uwezo wa kuwasiliana nawe kama mimi.  Je nini kifanyike? Kuna mengi ya kufanya hapa ili kutatua tatizo. Hivyo nashauri yafuatayo:
            Mosi, napendekeza vyanzo vyote vya matatizo vikabiliwe vilivyo bila huruma wala simile. Mfano, watu binafsi wanaochepusha maji washughulikiwe mara moja si kwa hasira bali kuangalia namna umma na wao wanavyoweza kunufaika na raslimali hii muhimu.
            Pili, tashhisi za hujuma kama alivyowahi kuzifichua Hayati Magufuli zimulikwe kuangalia kama kweli kuna uhusiano kati ya ukosefu wa maji na biashara ya majenereta ambayo ni mambo ya mwaka 47 katika karne hii.
            Leo sitaandika mengi ili kukupa muda wa kutafakari, kuchunguza na kuamua. Je, kweli, Tanzania nchi yenye vyanzo vingi vya umeme visivyotumika, inastahiki kuwa na mgao au ukatikaji wa umeme katika karne ya 21? Maswali muhimu na stahiki ya kujiuliza ni: kwanini sasa na nini kifanyike kuyapatia majibu sahihi na haraka ili kuepuka ngoa na sintofahamu zinazoendelea? Je hii inajenga mazingira gani na matokeo yake ni nini kwako na kwa taifa? Sipendi kutoa fursa ya wananchi kuanza kulinganisha na kuanza kuishi kwa kutamani Hayati angerejea japo ni haki yao lakini si kwa kulazimika. Je kweli tuna uhaba stahiki wa umeme au wa kujitakia wakati tumejaliwa vyanzo lukuki? Je nini kinakosekana kama siyo uadilifu na utashi? Je hizi sababu ndizo vyanzo pekee vya matatizo yetu au ni zaidi? Je matatizo haya–––ambayo, kimsingi, ni ya kujitakia–––yataisha lini na madhara yake ni yake yawe ya muda mfupi au mrefu kwa taifa? Je tumekubali kuwa mateka wa kujitekea kwa wahujumu na wahalifu wachache? Leo, sisemi mengi zaidi ya kushauri kwa dhati na uwazi kuwa umeme ni haki ya kila mtanzania kwa maendeleo na maisha ya taifa na watu wake.
         Mheshimiwa Rais, tafakari hata kama matokeo ya kufanya hivyo ni kuwatumbua baadhi ya wasaidizi na watendaji wako husika kwenye maeneo haya ambao wanaonyesha kuwa mzigo kwako. Kuna haja ya kuwaelimisha hawa kuwa hapa muhimu siyo sura zao bali utekelezaji wa dhamana walizoaminiwa na umma unaohangaika kwa sasa tokana na ukosefu wa ubunifu na utekelezaji wa majukumu yanayofanya walipwe. Kila la heri dada yangu.
Chanzo: Raia Mwema kesho.

No comments: