How the Berlin Conference Clung on Africa: What Africa Must Do

How the Berlin Conference Clung on Africa: What Africa Must Do

Friday 4 October 2024

Barua ya Wazi kwa Waziri, IGP, na Bosi wa TISS


Wapendwa,
Kwanza, nimshukuru mhe. Rahis kwa kuwapa muda mjitafakari na kufanya maamuzi kabla hajawawajibisha kuliko tumuwajibishe tokana na ushauri wangu. Sijawahi kuwasiliana nanyi. Hii ni mwanzo hadi kieleweke. Kwa uchungu, japo kichizani, nina hisia, mapenzi, maoni, mawazo, na haki kama nyinyi. Naomba niwaulize maswali yafuatayo nikiwakilisha mafyatu kama kiongozi wao:
            Kwanza, mna hisia kama machizi mnaowaangusha? Je mnaonaje hii jinai, kadhia, na kashfa isiyoisha ya utekaji, upotezaji, ufungaji, na uuaji wa mara kwa mara­­­–––kama wahusika, mnaionaje? Kama mnaifahamu na kuelewa, mmefanya nini kutatua na kukabiliana na janga hili? Mwajua wajibu wa nyadhifa zenu? Kama wazito, nini kazi yenu? Mmechukua hatua gani? Je nafsi zenu huwa zinawasuta? Wanaotekwa kupotezwa wangekuwa watoto, wake, ndugu, hata wakubwa zenu mgefanya nini? Mmewahi kuvaa viatu vya wahanga na wapendwa wao lau kihisia? Je, mmeshindwa tatizo hili, kwanini? Nini kifanyike kwa nafasi na nafsi zenu? Mnajua maana ya neno kuwajibika au mnangoja kuwajishwa? Kama hamjui, makelele na mashinikizo na ushauri vya bure kufanya maamuzi magumu mnavisikia na kuvielewa au la? Kama hamvielewi, kwanini? Kama mnavielewa, mmefanya nini au kwanini? Msaada gani mngetaka wahanga na umma wa machizi wahanga wawape kuepusha aibu kwenu, taifa, na bosi wenu na umma walioaamini dhamana hii? Mnataka wangapi wafe, kutekwa, kupotezwa, kuuawa, kuteswa, kudhalilishwa, kudhulumiwa, na kuhujumiwa iwaingie akilini? Je, mnapokea mishahara na marupurupu kwa nini? Mmewahi kujitathmini lau kiduchu? Kama mngeambiwa mjitathmini, mngejipa maksi kiasi gani, na kwanini na nini mungeamua? Kuna ugumu katika hili au mngependa/kutaka muwajibishwe?
            Mkitafakari maswali, mengine kapuni, ngoja nizamie historia iliyotukuka yenye mafunzo mengi ya mzee Ali Hassan Mwinyi (RIP Sana bro) walipouawa watu kule Kanda ya Ziwa––––mmojawapo akiwa [N]zegenuka kama sikosei––––hakungoja kuwajibishwa.  Roho ilimuuma. Nafsi ilimsuta. Imani yake ya kidini ilimkaripia. Nadhani hata washirika zake wa bedroom walimuonya. Kwanza, hakuhusika. Pili, hakuweza kuvumilia uoza. Tatu, alifanya maamuzi magumu. Nne alijiuzulu Januari 22, 1977. Tano, tokana na uadilifu, usafi, na weledi, baadaye kitendo hiki kilimwezesha kuwa dingi wetu kwa miaka kumi akiacha urathi uliotukuka. Sita, aliepuka kumfedhehesha bosi wake na kumtishwa mzigo wake japo haukuwa wake peke yake. Saba, alikubali yaishe kumondolea bosi wake taabu ya ima kuwajibishwa au kujieleza kama siyo kuonekana wa hovyo, asiyefuata sheria na viapo, au asiyewajali waliomwamini na kumpa maulaji aliyompa katika vicarious liability (kwa kisambachikwa wasomi wenzangu. Kama si wanasharia, niulize au waulize wenzangu walioko karibu yenu.
Tuache usomi kisheria, tuongee na kuulizana kichizani. Je mnajua kadhia hii? Kama hamjui, kwanini? Kama mnajua, inawafundisha nini? Je mnaielewaje na mantiki yake? Je mnaweza kuidurusu lau mpate somo na uamuzi mujarabu wenye faida kwenu, wahanga, na taifa? Mnaelewa madhara na uzito wake? Mmetafuta ushauri kisheria?
            Nataja majina. Bw. Hamad Yusuf Masauni, Camillus Mongoso Wambura, na Suleiman Abubakar Mombo mpo? Mwangojani?  Kwanza, mnaichukuliaje kashfa hii inayoishia milangoni mwa ofisi zenu? Inawahusu au la? Kama ndiyo, mwangoja nini? Kama haiwahusu, inamhusu nani zaidi ya bosi wenu? Mngependa au kupanga mujiwajibishe, kuwajibishwa, au kutaka hata bosi wenu awajibike wakati hahusiki moja kwa moja ingawa anahusika hasa ikizingatiwa kuwa ndiye aliwapa nyinyi maulaji? Kwa kashfa hizi za kinyama zilizogeuka donda ndugu, huwa mnalala usingizi kama mimi na wengine? Kama mnalala, kwanini? Kama hamlali, mpaka lini? Majina yenu ni ya dini hata kama ni za kigeni. Mnaamini kweli? Kama kweli, mmezitumiaje kuona mwanga? Je mmepuuzia imani zenu au ni waumini jina? Mlipoapishwa na mkaapa, mlibeba vitabu tulivyoaminishwa ni vitakatifu hata kama ni suala kujadilika? Kama mlivishika na kuviinua juu, mnavitenda haki au kuvihujumu mbali ya kujihujumu binafsi, taifa, bosi wenu, hata familia zenu mbali ya ufyatu na uumini wetu?
            Mkitafakari/kupanga kujibu maswali yangu­­­––––hata kama msiponijibu bali kujijibu––––tafakarini sana. Mngekuwa familia, jamaa, na ndugu za wahanga, mngetaka mfanyiwe nini au nini kifanyike? Je mmewahi kuwashirikisha washirika zenu wa bedroom kupata jicho la pili/ushauri? Juzi, nilimsikia bosi wenu ‘akiamuru’ vyombo vya uhasama, sorry, usalama vijichunguze. Je hii ni sahihi au vunga ili joto lishuke? Nani aweza kujichunguza akatenda haki hasa kama si mchizani na si malaika au Chizi Mchizani mwenye nguvu za ajabu za kanywaji? Je hii ni haki na sahihi? Je mmeshaurina naye au la? Kwanini? Kama mmemshauri, anasemaje  na mnasemaje? Je hili la kuwajibika, kujiwabisha, au kuwajibishwa ni gumu kiasi cha kuhitaji PhD kama yangu? Kati yenu na bosi wenu, nani mngetaka abebe hili zigo la kashfa na uchafu, maana naona Chakudema wameamua kukinukisha kama mbaya, mbaya japo ndata nao wametunishia misuli. Je watawazuia bila kukomesha utekaji na upotezaji machizani.
            Du!  Kumbe nafasi imejaa! Ngoja niishie kabla sijatekwa na kunyotolewa roho.
Chanzo: Fyatu Mfyatuzi.

Nilivyojinusuru Kutekwa

Nikiwa kwenye basi naelekea zangu home si zikaja njemba saba hivi zikiwa na defender uchwara yenye nambari fichi. Bila hili wala lile, si zikaniamuru nishuke ziniteke. Weee! Nilijiinua kwenye siti na kupiga samasoti za ki-Bruce Lee na kupaa hewani usiambiwe! Bila kufanya ajizi, nilichomoa pingu zangu na kusema “mnarekodiwa na kurushwa mtandaoni live.” Kabla ya kutafakari, nilikunja ngumi na kujiweka tayari kana kwamba niko kwenye goju ryu session. Nilifanya Banguazhang, Choy Li Fut, Hua Quan, Wudang, Wing Chun, na mitindo kama ishirini hivi kwa kasi ya umeme. Njemba hazikuamini macho yao.
Kuona na kusikia hivi, njemba zilianza kuonyesha kugwaya waziwazi huku zikitazamana na kuishiwa maneno zisiamini kuwa mie ni fyatu asiyefanyiwa masihara hata na siafu. Nami bila kungoja, nilipiga tena samasoti na kusimama yowe tayari kufanya maangamizi. Nilisema ‘hatekwi fyatu hapa. Mie ni bwanga la mjini kwa kisambaa. Kabla ya kuendelea, nilitoa cha moto na kuweka kidole kwenye usalama tayari kufanya maangamizi, maana siku hizi tunaruhusiwa kuwa nacho. Sikupindisha maneno. Nilisema “nikienda home nitaangalia sura zetu halafu nami na mafyatu tuwatafute tuwateke na kuwapeleka kwenye runinga ya mafyatu ili mafyatu wote wawaone.” Nilipiga tena samasoti, kutunisha misuli huku nikinguruma kama chui alindaye vichaga vyake, na kuzoza “ tuhesimiane. Mjue tutawanyaka na kuwataabisha kabla ya kuwapoteza. Tutawateka bila kuwapoteza kabla hamjatwambia nani aliwatuma na kwanini mlitaka kunifyatua msijue mie ndo mwenyewe Fyatu Mfyatuzi aliyefyatuka na afyatuaye bila kuogopa lolote wala chochote.”  Njemba kuona na kusikia hivyo, zilitoka harakaharaka na kuingia kwenye defender yenye namba za kutia shaka na kutokomea. Mafyatu waliokuwapo walianza kuzoza kuwa huyu si bure. Ima ni mwenzao au ni komandoo. Mie nilichuna.
            Kwa taarifa ya watekaji, mimi natembea na kamera fichi inayorekodi kila ninapokwenda isipokuwa nikichepuka, huwa naizima ili bi mkubwa asinifyatue. Kutekana, kwangu, ni mambo ya kizamani na kinyama. Ni ushamba na ukumbaff ambao sasa nimeamua kuukomesha haraka ili tuishi kwa amani na ustawi.
            Hivyo, nashauri mafyatu wote, kuanzia leo, wajichue kwenye madojo ili wawe fit kupambana na watekaji na ikibidi nao wawateke ili waonje joto ya jiwe ka jusi. Pia, nawashauri mafyatu wote kuanza kutembea na kamera fichi ili kuwafichua hawa watekaji waliojificha. Pia, nina mpango wa kuiomba sirkal ituruhusu njemba zilizomanya makung Fu na magujulyo kama sisi kumilki na kutembea na pingu ili tuisaidie kuondoa aibu na kadhia hii ya kishamba. Kama nyie mnateka mafyatu wasio na hatia si muende mukawateke mafisadi. Kumbaff zetu kubwa. Unapomteka fyatu na kumnyotoa roho, unaumiza familia yake na jamii. Unanyotoea mlipa kodi na mpika kura ya kula ya wanene. Mnataka wanene wasichaguliwe na kunenepa siyo? Mshindwe na mlegee. Nawachukieni sana nyie wana hizaya. Mnafanya mafyatu wachukie ndata na sirkal bure tokana na ujuha wenu. Sisi ni mafyatu wa amani hata kama ni ya imani. Hatutaki utekaji. Sasa nawaamba msikie na muelewe. Nasi wahanga tuaanza kuwateka ili mjue raha ya kutekana ilivyo. Haiwezekani njemba kama mimi niliyesomea Uchinani na Ujepu mambo ya karate, Kung Fu na madude mengine ya kutisha ninyamaze wakati mafyatu wangu wanateketea kwa kutekwa na kunyotolewa roho. Si utani wala mkwara. Nitakula nanyi chungu kimoja tuone. Mkizidi kujito akili, najitoa ufahamu. Hatuwezi kugeuka kaya ya watekaji utadhani wote woga.
            Ili kuepuka kuwateka bi mkubwa na vitegemezi vyangu, kuanzia juzi, nimeanza kuwafundisha madude yangu ili nao wasaidie kupambanana kansa hii ya kishenzi. Senzi kabisa na mkome na kukomaa kabla hamjakomolewa na hao mnaodhani na nyanya kuteka na kupoteza. Nasema, tena kwa herufi kubwa. Hatekwi fyatu hapa. Ukiteka tunateka, ukipoteza tunapoteza ili tuone. Kama mbaya mbaya. Loh! Mna habari mie ndiye nilikomesha komando yoso na panya road? Kama hamjui, mtajua hamjui. Dawa ya fire ni fire au siyo?
            Sasa msiseme sikusema. Nasema tena kwa kujimwambafy. Ukija kuniteka, jua nitakuteka kabla hujaniteka. Ukija kunipoteza, utapotea na kupotezwa ukijiona. Nataka nianzishe chuo cha makarate na makung fu ili nitoe mafunzo bure ili kuhami na kulinda mafyatu wangua. Hawakunichagua niwe mzigo kwao. Nitawakomboa liwalo na liwe.
            Hivyo, natangaza hadharani, kuanzia leo, watekaji wajue. Ukija kuniteka, nakuteka. Ukija kunipoteza, nakupoteza. Ukija kunifanya kitu mbaya, nakufanyia mara mia. Mie sina mchezo wala utani na maisha. Kwanza, tunaishi mara moja. Pili, msidhani wote ni wachovu wa kutenza kichovu na kijinga. Kwa wasionijua. Mie ni komandoo aliyesomea vyuo vyote vya kikomandoo duniani. Nina mikanda kama sabini hivi ya Karate na Kung Fu. Na kuanzia leo, mjue, nina cha moto, pingu, vitoa machozi, pilipili washa, na zana nyingine ambazo ni top secret. Cha mno, mjue nawajua watekaji na mafyatu wasiojulikana. Nitawaambia mafyatu nyinyi ni nani pale nitakapowateka kabla ya kuwapoteza.
            Ngoja. Hii defender inataka nini? Ngoja nitoke nduki wasije wakaniteka nikawateka na kuwapoteza bure. Tuonane wiki ijayo jamanini.
Chanzo: Mwananchi J'tano iliyopita.