The Chant of Savant

Sunday 14 June 2009

Kirini mmeshindwa tena vibaya

Ni miaka minne tangu tujitutumue na kujidai. Mbele ya kadamnasi na mataifa tulitembea vifua mbele tusijue tutakuja zamisha vichwa michangani! Kulikoni? Si unakumbuka tulijidanganya: tumeandika historia tusijue tumesaini hati ya kifo! Hatukujua. Ubuguyu-ubuguyu wote kumbe kibafute;mwe!

Bado sijasahau kibapara mie nilivyomnunulia mke wangu kikuba kusherehekea ushindi wa kuondokana na mzee wa majisifu kwa kila aina ya mbwembwe na hoi hoi! Hadi leo nashangaa tabasuri tuliyotumia kuita mafamba tukidhani tunayafukuza! Sijsahau muda niliopoteza kuhudhuria vigwena vyao watulao tukilalamika wasisikie.

Walishapata walichotaka wana shida gani? Japo tunajikaza na nyonde nyonde yetu ambapo kidhabu mmoja habithi na marhuni alitukoga eti twapaa wakati twazama tena kwa kasi. Tukubali mbele yetu kuna vita japo tumeishaula wa chuya Mungu tusitiri na uwapige tafrani na nuksani wasiendelee kutufanyia ngenga ilhali wenzao twaangamia. Watu watung’onga kwa kujikonga tuloonyesha enzi zile!

Nani anaridhika na ulimpyoto,ulafu na ukuba huu? Basi huyu majinuni na afkani wa kuhurumiwa. Uliza twenda’pi au tuseme twaswekwa na kuswagwa kwenda wapi? Utaambwa huku! Huku wapi wakati kote ni huku hata kuno kwaweza kuwa huku? Washikilia huku! Huku huku wapi? Hata machinjioni huku! Peponi na motoni kote huku! Tukubaliane hapa hakuna jema bali hadaa na kupelekwa kisengesenge!

Twaliwa kama DECI na wachungaji fisi waliotamalaki kila kona ya Kaya!

Juzi tuliambiwa nyota tena ya jaha. Ebo! Mbona twapewa mbichi tulipoahidiwa mbivu? Mbona uvumilivu watulisha zilizovia! Jamani hamjastuka nyie mtendewao kama kisagaliwa! Je Mpayukaji nitumie lugha gani lau muenge?

Yule babu babu yuleee. Alisema hili koroma nyie mashikilia nazi! Alisema hili teke teketeke nyie mwaamba tena kwa minato na mbwembwe, kuwa dili. Toba! Dili liso maandili si dili kitu nakataa katu! Baya zaidi eti nao wajitia taraghani kwa sana ! Wanadhani tumesahau maneno ya babu?

Kila siku wenzenu wafaidi maghusubu nyie mwandanda na kudai “tulieni mambo yataiva na nuru itawaangazia wakati kiza ndiyo hicho kinazidi kunema na kushamiri! Ebo! Kweli limbukeni na limpyoto wana mambo tena mambo mambo!

Waachwa wasema wangojewa! Waliwa wasema wala! Wala walani? Kwetu Funzi husema, aso mato akipata mato chunga asemato. Mana yu mteke na weledi hana. Kwani yu agogota na kigovyache asijue wasomi tu wengi! Kama wataraji mwana basi umtegemeaye ana kigwaru shurti azae wafe hata mimba itoke. Kwani pale kwenye mambo ya fulusi hamjaona walivyochota na kuchuma siye tukabakia twalia huu!

Alichotaka ni mali ya mahonyo. Kaisha ipata yeye na kundile mwesha nyie. Mungu ampeni? Kilema au upele? Wenye kazi nyie mliotoa bure ili mliwe bure na kweli mwaliwa si bure! Audhubillahi mina shaitwan rajiiim! Ingekuwa yangu nafasi basi ndumo yangu ingekuwa amkeni kuzacha tumwinde bundi huyu. Ningepiga nyungwanani wasikie hata wa Likawage na Kivinje waje tumtwange kenge lau mayai yapone.

Walau hayo mayai? Ni yale aloacha Mchonga alotarazaki na kuadibu akinena kinabii: mtahadhari wajao si wote wasemao twaweza waweza!

Lahaula! Kumbe kwenye msafara wa kenge na mamba wamo! Mlipuuzia mkidhani alikuwa na lake msijue kumbe lenu mwalikoroga! Nani aliwaroga nyie? Nambe nielewe lau nilizoe gogo lililokingamana njiani mwenu muweze pita.

Hata wavikwe kiswa madhambi yao yatawaandama. Wametutenda kwanini tusiwatende tena kwa ghadhabu na munkari mara mia? Nani alitegemea maharamia yaiokoe meli wakati lengo lao kuizamisha? Ishazama zama gani! Tulonusurika angalau tulo nazo siyo hao hamnazo jama tusikizeni tuwaambacho. Hamkusikia: simbiko halisimbuliki ila kwa mikukuriko? Je m’ tayari lau kuondoa nuksi mambo yende tutegemeavyo? Tusiogopane. Maana tumejaribu kuwaauni.Wemetupuuza na kutuona hamnazo kama wao!

Kama yupo kiumbe namchukia si mwingine. Ni yule jambazi wa enzi za yule Mchonga maneno na meno alosema, “Angalieni wanangu. Si wote wasemao bwana bwana ni wangu” Mbona aliwakataa miaka ile! Wapi wamezaliwa upya tuwarejeshe kwa madoido huku jana waliiba mdomdo? Je anayetudanganya hajidanganyi? Nani huyu awezaye kuiandika historia upya au kuukamata upepo?

Tuwambe waelewe siyo walewe. Tuwambe kini’owalevya ni mali yetu

siyo ya mama zao wala umbu zao. Je wajua? Kama wajua kwanini wajifanya majuha wasijue? Nani aweza kuishinda kadamnasi ikiiamua? Kwanini tungoje iamue iwapo twaweza kurekebisha mambo? Tuseme na kurudia. Bwana mkubwa timua hao mabugu walokijaza kiwingu siyo ukichezee gungu la sivyo kesho tutakuputa wewe.

Heri kufa umesimama kuliko kuishi umepiga magoti. Niulize aliyeapa kututumikia si kututumikisha ni nani? Sasa ushoga watokapi?

Nani huyo alozaliwa jana asojua kuwa tushadoya na kujasisi aloyasema yule babuu? Hatusahau. Ni sehemu ya dafina yetu.

Leo twawapa paka watunze maziwa ya watoto! Watoto watanusurika kukonda, kunyongea na kufa kwa ngoa? Nani anamdanganya nani? Toba!

Tunataka lau tuone kikome kama mazao yapo. Nani anaweza kushiba kwa vikwakwa vyenu wakati siye twanuna?

Yule babu mwenye jina sawa na kikuku alisema, “Msipowauliza wenda kule mbio wana nini na kunani, mtajikuta tafrani” Yameishatufika tukubali. Lazima tulisake jibu hata kama kwa kuchenjiana kama alivyowahi kusema Arawa yule machachari na bingwa wa miruko kwa namnaye kama Mnana.

Husuma hii lazima ipate mwamana. Tusiposema watasema hamkusema. Sasa tumesema na tutasema hata wanetu watasema Mpayukaji alisema na kusema. Jamani nahau au lugha gani nitumie lau muambue japo ndururu!

Kaya yasedekea wao wahazahaza tutulie! Tulotegemea wanene wameingiwa na shake! Nani atawasemea? Neneni mnenalo tujue twendako vinginevyo huko twendako yatakuwa mafutu matupu!. Nani alaumiwe? Kuendelea kunyamaa si jibu bali kukikirika kiasi cha kuzua la kuzua tusijue jinsi ya kulizuia. Kwanini kuzua badala ya kuzuia? Mshaambwa kaya si mali binafsi bali kikoa. Sasa ushoga na uswahiba wajaje? Tuondoleeni maharamia na vipanga kwenye hekalu letu.

Tuleteeni watu wenye udhu siyo wanuka nongo na ugaga tuloambwa tuwatahadhari. Jamani kuna kesho na keshoye siyo mbali.

Nawapeni uchanjaa toune weledi au utobwe wenu japo tushawamaizi bado twawapa fursa japo ya mwisho ili tukiamua kuchegama na kuchenjiana tusionane wabaya.

Naregea nilikoanzia. Jamani jama twambieni basi lau tujue la kushika.
Chanzo: Tanzania Daima Juni.

No comments: