The Chant of Savant

Monday 11 July 2011

Hizi ni Trust Funds au vichaka vya pesa za wizi?


Mke wa Rais na Mwenyekiti wa Taasisi ya WAMA Salma Kikwete (kulia) akizindua nembo ya (HMT) kwaajili ya uzinduzi ya Taasisi ya Hassan Maajar Trust na kuanzisha kampeni ya kusaidia kutokomeza uhaba wa madawati mashuleni jijini Dar es Salaam (juni 11.2011) (kushoto) ni Makamu Mwenyekiti wa Taasisis hiyo Shariff Hassan Maajar ,akifuatiwa na Mwenyekiti wa HMT Balozi Mwanaidi Maajar.

Kama maelezo hapo juu yalivyo, kuna jambo jema linafanyika ingawa nyuma ya wema huu kunaweza kuwa uchafu wa kutisha. Je tatizo la madawati nchini litaondolewa na taasisi za watu binafsi tena zenye kutia shaka?
Huyu Maajar ni nani? Analipa kodi vilivyo? Ni msafi kimaadili? Ametanganza mali zake na kueleza alivyozichuma? Wahusika wangejibu maswali haya muhimu kabla ya kutuaminisha kuwa wana nia nzuri na taifa letu. Watakuwaje na uchungu na taifa iwapo nao ni sehemu ya waliosababisha hali hii ya umaskini?

Maswali haya yanasababishwa na ukweli kuwa mke wa Hassan Maajar ambaye ni balozi wetu Washington Mwanaidi anatuhumiwa kuwa mmojawapo wa wanasheria waliosaini mikataba ya uhamishaji pesa ya wizi ya EPA.Je huyu Hassan Maajar ni nani na anafanya kazi gani? Tungepewa CV yake na historia ya utendaji wake kabla ya kuaminishwa kuwa mhusika na mkombozi wakati anaweza kuwa wale wale watokanao na urafiki, kulipana fadhila hata familia.

Mtuhumiwa hajawahi kukanusha wala mazingira yaliyomfikisha kwenye cheo hiki cha juu kisiasa hayajulikana zaidi ya mchirizi kuelekea kwenye wizi wa EPA ambao uliwezesha serikali ya sasa kuwa madarakani kwa kuwahonga wapiga kura mbali na kuchakachua kura.

Hata ukitazama historia ya anayefungua taasisi hiyo unaona mauzauza ya ufisadi. Kwani naye ana kampuni yake ya mfukoni ya WAMA inayotumia mgongo wa ikulu kuchumia mali. Nilishwahi kuuliza: kama NGOs za wake za wakubwa zilianzishwa kutokana na uchungu wa zinaodai kuwapigania, kwanini zianzishwe baada ya waume zao kuingia madarakani?
Turejee kwa Maajar. Je ana udhu na uaminifu kuweza kusaka misaada kwa ajili ya madawati na kuifikisha au kujitafutia sifa na ulaji na pa kufichia pesa ya ufisadi. Je anatafuta kutoa huduma au kukwepa kodi kwa kujifanya anahudumia jamii? Kazi kwenu.

No comments: