The Chant of Savant

Tuesday 15 August 2017

Kijiwe tokea Nairoberry

Image result for photos of raila and uhuru
            Baada ya baadhi ya wanakijiwe kutia timu kwa siri Nairoberry maeneo ya Ngara, Muindi Mbingu, Kawangware, Kanunganga, Uthiru, Mukuru kwa Njenga na vijiwe vingine, walipokwenda kusimamia uchaguzi, watalazimika kutoboa siri na kubakia kule ili kuwasuluhisha akina Njoro na Owino ili wasinyotoane roho wakigombea koo zao mbili tawala baada ya kudhulumiana kwenye uchakachuaji uliopita kiasi cha kuacha baadhi ya walalahoi wakiwa wamenyotolewa roho na ndata baada kulianzisha tokana na kutokubaliana na matokeo.
            Owino analianzisha “eti ni aje jadwong madwong (mkubwa) kaibiwa kura yawe (yarabi). Haiingiangi kwa akili (haingii akilini). Tumevoti (kupiga kura) kwa wingi halafu wanasema Baba ameshindwa. Je lazima tukaange na kuangalianga wakati tunaibiwa kweli au kama kuumana kiumane? Kila elections ni machezo yale yale why?”
            Mpemba anamchomekea “yakhe ongea Kiswahili kinichoeleweka lau nasi wenzio tuchangie. Sijajua wamaanishani unposema tukaange mwakaanga nini wakati kinachoongelewa hapa kura au mwataka kuendelea kukaangana kama mlivokwishaanza? Kumbuka kaya itakuwapo wakati waja twapita.”
            Kabla ya kuendelea mzee mzima naamua kumchomekea Mpemba. Maana najua angeuliza swali jingine kiasi cha kuwafanya wenyeji wetu wejisikie ndivyo sivyo.
            Nakula mic “Ami hujui kuwa hapa Nairoberry (Nairobi) watu huongea sheng (lugha ya mjini) yaani lugha ambayo si kiswahili wala kimombo? Anyaway, Owino hapa anamaanisha kukaa anaposema kukaanga. Pia, anaposema kuangalianga anamaanisha kuangalia; anaposema kuumana anamaanisha kama ni mbaya mbaya. Kumbuka kuwa Afrika Mashariki ina Kiswahili kila aina. Ukienda UG (Uganda) wanayo yao ya warungwana, Burundi wanacho cha kidini huku DRC wakijidai na chao cha ukuye tukule nyama (njoo tule nyama).”
            “Yakhe nkushukuru sana. Kwani jamaa ameniacha Solemba wallahi; maana atumia maneno magumu mie ndhani kikabila hapa,” Mpemba anajibu. Kabla ya kuendelea namwambia kuwa naye anawaacha Solemba hivyo hivyo tokana na Kiswahili chake.
            Kabla ya kuendelea Kamau anakatua mic “Mathee (wazee) hivi kwanini kwenyu (kwenu) hakunanga hizi mambo ya kupinga kura kikabila na kupunyuliana kura kama hapa?”
Mgoshi Machungi ambaye ni mojawapo wa mjumbe wa msafara anaamua kutia guu “kwei, kwetu hatichagui kikabia kama hapa ila uchakachuaji upo. Kwani kuna nchi katika Afiika kunaweza kufanyika uchaguzi bia uchakachuaji. Nashangaa hata Dan arap Mwai aivyofanya kuuhusu Moi Kibaka amshinde UK mwaka 2002!”
            Njoro aliyekuwa anampasia kipisi Waititu anakwanyua mic “hi inatishia amani haki. Hapa walichukua doo kibao wakasema wanaweka kompyu wakaishia kupunyua. Huyu anasema TZ nako huwa wanapunyua, haki hawafikii hapa. Hukuona walivyomkil Msando kabla ya kuvoti? Je kama hawakupunyuka, kwanini waliuanga yeye? Hapa Baba Tinga has a point.”
            Msomi Mkatatamaa aliyekuwa akisikiliza kwa makini anaamua kula mic “nadhani hapa tatizo liko kwenye namna uongozi wa kwanza wa kaya hii ulivyoweka misingi. Naambiwa baba yake UK mzee mwenyewe alipora ardhi kila kona na kuwazawadia watu wa kabila lake. Hapa unategemea nini? Sisi tuko tofauti na nyinyi kutokana na mzee Mchonga kutokuwa na tamaa ya mali wala kuendekeza ukabila vinginevyo hatuna tofauti. Nawashauri muwe mnakuja Dar nanyi mjifunze tunavyohussle na kugawana na siyo kunyang’anyana kama nyinyi hapa.”
Kamau anakula mic “Hii ni haki (hii ni kweli). Tz haina ukabila kama sisi ambapo mkyuk (mkikuyu) haoni kama kuna mwingine aweza rule country hii sawa na mkale (mkalenjin) anavyodani kuwa baada ya UK lazima atawale. Hii ndiyo maana arap Mashamba asema atawin 2022 kwa vile yeye ni deputy.”
            Kabla ya kuendelea, Macharia anakula mic “yenyewe. Maana hapa kama hupunyui (huibi) unaonekana kama umezumbaa. Lazima kila mtu apunyue kwenye aliko. Kama naweza, naweza call Magufuli akuje hapa atie heshima kama anavyofanya huko Tz.”
            Kabla ya kuendelea, Ochuodho anakula mic “yenyewe (hakika). Napenda prezi (rais) wa TZ akuje hapa hata kama ni kwa one month ili achukue shamba atupeane kwa sisi squatters. Naumia sana kuwa wamepunyua. Hawatafanya changes. Wataendelea kupunyua. Jana naona arap Mashamba akisheheka kupunyua na kuendelea kulanga (kula).”
            Mijjinga aliyekuwa kimya akionyesha kushangaa namna Kiswahili kinavyowapiga chenga jamaa anamua kula mic “ndugu zangu, lazima tukubaliane kuwa mkitaka kusonga mbele lazima muachane na siasa za kikabila. Maana, hazina tija zaidi ya kukuza ufisadi na ufalme kwa mlango wa nyuma. Kawaida, baada ya kupigwa kura, washindi na washinde hutangazwa na kupongezana na mambo kuishia hapo. Nadhani hii ndiyo tofauti yetu nanyi au vipi?”
            Kinyanjui anaamua kula mic “sikubalianangi na madai kuwa Tz hakuna ukabila. Upo sema siyo kama hapa. Nimeishi Tz tena kule Zanzibar. Mbona suala la kupunyua liko nako. Mnadhani wale wa chama cha Kafu wanakubaliana na mawazo kuwa mambo ni shwari Tz? Nadhani tofauti ni kwamba sisi tunazidisha hapa. Na hii haki haiwezi kulisongesha mbele taifa.”
            Kijiwe kikiwa kinanoga si kanjo (ndata) wakatuamuru tuondoke kabla hawajatumwagia tea gas (mabomu ya machozi). Kumbe ndata wote baba na mama yao mmoja! Maana walivyotutoa mkuku sina hamu. Lazima kesho nikitoe kurejea Bongo.
Chanzo: Tanzania J'tano leo.

No comments: