The Chant of Savant

Monday 31 March 2008

Wizi EPA ni mkubwa kuliko tunavyoambiwa

GAZETI la ‘The East African’ la Machi 17, 2008 lilifichua kuwa serikali ilitoa waraka maalumu wa kuwatahadharisha na kuwazuia watu kununua mali za watuhumiwa na wanufaika wawili - Johson Lukaza na Beredy Sospeter Maregesi - wa wizi wa fedha kutoka kwenye mfuko wa madeni ya nje (EPA).

Bahati mbaya taarifa hizi hazikueleza kama watuhumiwa wamekamatwa au la.

Inavyoonekana watuhumiwa hawa wanaotambulika hawajakamatwa kwa sababu taarifa hii ya serikali inaonekana kuwa kimya, kuhusiana na kukamatwa kwa watuhumiwa hawa. Sababu? Serikali pekee na wao ndiyo wanaojua!

Hapa ndipo utata wa ‘seriousness’ ya serikali unapozidi kujitokeza. Je, hawa nao ni serikali ndani ya serikali au ni serikali sirini? Kuna nini hapa?

Kama kuna jambo linangojewa na Watanzania wenye mali, basi si jingine bali kuwaona wahalifu hawa wakiwa mbele ya vyombo vya sheria ili haki itendeke na ukweli ujulikane.

Taarifa zilizotolewa zilibainisha wazi kuwa watuhumiwa wana mali zenye thamani ya fedha zipatazo dola 20,000,000 nchini.

Kama Lukaza na Maregesi wana mali za dola 20,000,000, je, hao mabosi wanaofichwa waliowatumia kutenda jinai hii kwa taifa wana utajiri kiasi gani?

Na kama wameweza kuwekeza kiasi cha dola 20,000,000 je, wamefuja au kuficha kiasi gani? Maana, kuna uvumi kuwa mmoja wao amewahi kuagiza gari la thamani ya dola 200,000 kutoka Uingereza na kulipakiza kwenye ndege kutoka London hadi Dar.

Huyu hawezi kutumia shilingi mbili kwa siku. Lazima atakuwa ni mtu wa matanuzi na hatari kwa pesa. Pamoja na muda aliokaa bila kubainika, si bure pesa nyingi itakuwa imeshafujwa, kiasi cha kuwezesha mhusika kuozea gerezani kama haki itatendeka na kuonekana ikitendeka.

Je, ni kwa nini serikali imekamata mali za watu wawili tu kati ya wengi?

Dola 20,000,000 ni asilimia 15.037 ya pesa zilizoripotiwa kuibwa kwenye fuko la EPA, nashindwa kukubaliana na takwimu zinazotolewa.

Haiwezekani watuhumiwa, tena wadogo wawili, wawe na utajiri mkubwa kiasi hiki. Hii maana yake ni kwamba kama vidagaa waliotumiwa na wakubwa kuiba wana utajiri wa dola 20,000,000 basi waliowatumia wanaweza kuwa na hata mara kumi yao.

Hapa ndipo madai kuwa pesa iliyoibwa inaweza kufikia hata dola 800,000,000 na pengine zaidi ya hapo unapoanza kuwa na mashiko.

Kuna haja ya kujua idadi ya watuhumiwa na pesa waliyochukua kila mmoja, ndipo ukweli uwekwe wazi.

Hata ukizigawanya pesa hizi dola 133,000,000 tulizoambiwa kuwa ndizo zilizoibwa kwa makampuni uchwara yaliyotajwa 22 unazidi kupata shaka.

Je, wana mali kiasi gani zilizo nje ya nchi au ambazo hazijafichuka? Je, ni mali kiasi gani zimo mikononi mwa ndugu zao? Kuna maswali mengi yasiyokuwa na majibu. Wahusika si wapumbavu. Hizi mali zilizofichuka zaweza kuwa ‘tip of an iceberg.’

Kama watu wadogo kiasi hiki wana utajiri wa kutisha kiasi hivi, hawa kina Meremeta, Deep Green Finance na wengine wanao husishwa na vigogo walikwapua kiasi gani?

Kukadiria ni kiasi gani, rejea pesa iliyotumika kwenye takrima nchi nzima kwenye uchaguzi wa mwaka 2005 unaohusishwa na wizi huu.

Kama watu wageni wa pesa kama hawa wana utajiri kiasi hicho, hawa wenye Kagoda wana utajiri kiasi gani? Na Jeetu Patel atakuwa na utajiri kiasi gani?

Bado hawa si wezi wenyewe, bali vyambo vilivyotumika kuvua mabilioni haya kwa ajali ya mpango maalumu wa watu maalumu. Nadhani hapa ndipo serikali inaposhikwa na kigugumizi kusema ukweli ni upi na walioko nyuma ya wizi huu ni kina nani.

Wakati Rais Ali Hassan Mwinyi akiondoka madarakani mwaka 1995, dola moja ya Kimarekani ilibadilishwa kwa takriban sh 520 za Kitanzania. Angalia Mkapa anaondoka ameiacha wapi? Ilikuwa imezama kwa takriban asilimia 50.

Je, kwa serikali iliyokuwa inajisifu kuleta nidhamu ya matumizi na makusanyo, kwa nini iliporomosha shilingi yetu badala ya kuipa thamani zaidi ya iliyoikuta nayo? Hapa ndipo sanaa ya kutoa taarifa safi kwenye makabrasha wakati nyuma ya pazia mambo ni tofauti, inapowafumba macho wananchi wasijue ukweli na kuchukua hatua madhubuti.

Hapa ndipo Rais mstaafu Benjamin Mkapa anapopaswa kubanwa atoe maelezo ya ‘tambo’ zake za kufufua uchumi na kubana mfumko wa bei. Kama alifanikiwa kubana mfumko, alifanya hivyo si kwa kuzalisha bali kubana mzunguko wa pesa. Huu nao ni usanii.

Kashfa ya Goldenberg nchini Kenya ilikula takriban dola 200,000,000 na nchi ilinusurika kidogo kufilisika. Ikumbukwe Kenya ilikuwa na uchumi imara na mkubwa kuliko wetu. Sasa kama Tanzania haijafilisika inaendeshwa kwa muujiza upi?

Baya zaidi, tunaambiwa uchumi umeimarika. Lakini wakati tukiambiwa hivyo, tumeonywa: hali za maisha zitakuwa mbaya. Sasa nini ishara na faida za kukua kwa uchumi kama si kuboresha hali za wananchi? Hiki nacho ni kitendawili kinachotaka kutenguliwa na wachumi ili umma uelewe sanaa unazotembezewa.

Tanzania ina kila sababu za kuwa muflis. Taarifa zisizo rasmi ni kwamba serikali inamiliki mashangingi zaidi ya 6,000 yenye thamani ya zaidi ya dola 30,000 kila moja. Haya ni magari yanayokula mafuta sana (gas guzzlers).

Gharama ya kulitunza shangingi moja kwa mwaka nayo si haba. Kulitengeneza na kulilisha mafuta si mchezo. Bado hatujaja kwenye kufuja rasilimali za nchi kama nishati, simu na fedha maofisini ambako kumegeuka vijiwe vya kupigia stori na soga na serikali isifanye kitu.

Bado hatujaangalia posho na malipo kwa watu wanaokwenda kazini kupiga siasa au soga waliotamalaki nchi nzima. Bado hapa hatujaingiza matumizi ya matanuzi ya watawala ndani na nje ya nchi. Bado hujagusa kashfa nyingine kubwa zinazohusisha pesa nyingi kama Richmond, Independence Power Tanzania Limited (IPTL) na nyingine nyingi tu.

Tujiulize, kwa nini serikali inapata kigugumizi kuwataja watuhumiwa wote wa ufisadi tata wa EPA? Kwa nini serikali haiwasilishi ombi rasmi kwa mamlaka za Marekani kumrejesha Dk. Daud Ballali, gavana wa zamani wa Benki Kuu ya Tanzania (BoT), mwasisi na mtuhumiwa nambari wani wa kadhia hii? Je, wanaomzunguka Dk. Ballali kama mkewe waliotajwa kuhusika na kadhia hii wako wapi na mbona serikali haielezi kinachoendelea?

Je, hapa mchawi wetu si huyu tuliyempa mtoto alee ilhali tukijua atamnyonga na kumla kama ambavyo inajionyesha kwenye kashfa ya EPA?

Siku zote serikali inasema ipo madarakani kwa ajili ya umma. Hata katiba yetu viraka inasema hivyo. Mbona linapokuja suala la kutwambia ukweli inatuficha? Huku kuwajibika kwa wananchi ni kupi na kutaanza lini?

Wapo wanaomhusisha Rais Jakaya Kikwete na uchafu huu kutokana na kuwa mnufaika na aliyekuwamo kwenye serikali chafu ya Mkapa. Bahati mbaya naye ameshikwa na kigugumizi. Amebakia kuja na ahadi za nitawakamata wapi kama na yeye anahusishwa?

Rejea ile ‘List of Shame’ iliyotolewa na wapinzani mwaka jana na ikabainika kuwa kweli baada ya serikali kujaribu kuua madai yao bila mafanikio.

Pia kuna jambo linashangaza. Kwa mfano, kwa nini Gray Mgonja, mtuhumiwa kwenye wizi wa EPA, bado yumo madarakani huku watuhumiwa wengine kama Johnson Mwanyika, Mwanasheria Mkuu wa Serikali; na Edward Hosea, Mkurugenzi Mkuu wa Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (Takukuru); nao wakiendelea kushughulikia suala ambalo wana maslahi nalo?

Hapa si siri, kinachochezewa ni sisi na rasilimali zetu. Ajabu, nasi tumeendelea kumuunga mkono Rais awashughulikie watuhumiwa wakati naye ni mtuhumiwa. Kwa nini hatoi utetezi wala maelezo kama kweli si mtuhumiwa au hakushiriki?

Kimsingi kadhia nzima ya EPA ukweli bado haujajulikana. Hivyo ni jukumu letu wananchi kuusaka ukweli hadi tuupate utuweke huru.

Source: Tanzania Daima Machi 30, 2008


Maoni ya Wasomaji

nashangaa sana kuona watz tumekaa tu hatuandamani kuuliza ya hapo juu wakati maisha yetu ni magumu ile mbaya

na k - 30.03.08 @ 09:36 | #4116

mpayukaji kaweka mambo yote hadharani kazi kwetu watanzania,kila mara nasema wakati wa kuongea umeshapita,na sasa kilichobaki ni vitendo,mana hawa mafisadi wanafurahi na kuzidi kutuibia baada ya kuona hatusemi lolote,siku zote madarasani tunaanza na theory halafu practical,sasa watanzania wakati wa theory umepita tuanze practical ili wale wote wanaoiba waone ya kua watu wameamka,ila cha ajabu ambacho hadi leo sijapata jibu ni kwamba,2010 watakuja hawa mafisadi kwa maneno matamu na watapewa tena nchi,sasa sijapata jibu ya kua fulana na kofia na wali kwenye kampeni ndio vinawachanganya watu ama ni ushabiki tu,mana wengine ukiwauliza wanakupa majibu ya kipuuzi sana,kwamba kikwete ndio anafaa na hakuna mwingine anaeweza kuongoza,siku zote mtu km hapewi nafasi tutabakia kusema hawafai mpk mwisho wa dunia,na mwingine akasema kikwete anafaa sababu ni handsome huyu dada alinipa wakati mgumu sana kuamua nilie ama nicheke,ila mwishoni nikasema MUNGU atusaidie watanzania,ila tusikate tamaa tuendelee kuwasomesha ndugu zetu km hawa ili wasituletee viongozi km hawa tena,naamini hata MUNGU atakua anajisikia vibaya sana,kwani katuma akili na nguvu ila tunashindwa kuvitumia na kubaki kumsingizia na kumalaumu kua ndio kaleta umaskini wetu wakati tunaona na kujua kabisa wanaoleta umaskini wa watz ni watu wachache tena tunaowajua,sasa mtu ana utajiri wote huo wkt sumve huko hakuna zahanati,na wkt huohuo tunamkamua mwananchi ambae anaishi chini ya dola 1 kwa siku achangishe shule,jamani hii inakaaje.

na mstari wa mbele, calif/usa, - 30.03.08 @ 10:05 | #4124

sasa ni nani wa kulianzisha maana sisi tunasubiri mtu wa kuanzisha tu halafu nasi tuliendeleze nyie mnaoandika siyo mtuandikie tu,tuelelezeni na mahala pa kupata silaha sisi kwa sasa tuko tayari maana kama ni kufa tulishauawa sasa tutachoogopa ni nini tumechoka na longo za serikali

na mulokozi, tanzania, - 30.03.08 @ 11:55 | #4156

mimi ni koplo kwa cheo ila kwa habari zinazoandikwa na mambo tunayoyashuhudia sasa imefika mahala hatutasikiliza habari ya nani maana sasa mambo yanayofanywa na serikali yanatukatisha tamaa na hata kama sisi ndiwo walinzi wa amani pia hatuhitaji amani ya kutufanya sisi wajinga na hatuwezi kukubali kama hivi serikali inamuachia mtu mmoja tu tena mgeni huyu anayeitwa azizi amechukua hicho kiasi cha pesa bilion 200 halafu sisi tunateseka na watoto wetu pa kulala hakuna elimu ya watoto wetu ni duni sasa tunacholinda hapa tanzania ni nini?MUDA SIYO MREFU TUTALIANZISHA NA BAADA YA HAPO NDIPO TUTAHESHIMIANA

na koplo john, tanzania, - 30.03.08 @ 12:04 | #4158

serikali isitufanye wajinga tunachosubiri sasa hivi ni mtu wa kuazisha tu na baada ya hapo hawa mafisadi wote watakiona maana serikali imeshindwa kuwatia adabu kwa hiyo ni muda sasa warudishe mastaka kwa wenye nchi yao ambao ndiyo sisi wananchi hasira tuliyo nayo kwa sasa ni kubwa iliyovuka mipaka VIONGOZI GANI HAWA WANAKULA HAWASHIBI?!!!!

na chacha, tanzania, - 30.03.08 @ 12:12 | #4159

Naamini njia muafaka ya kuiwajibisha serikali kwanza ni kwa kura kwa kipindi kijacho cha 2010. Ila kwa sasa njia ya haraka ili hali isifikie katika vita kati ya uongozi wa serikali wakitumia vyombo vya dola dhidi ya wanachi wenye machungu, nivyema kama wapo wanasheria wazalendo wenye uchungu pia swala hili likachukua mkondo wa kisheria,maandamano ya amani, migomo ya nchi nzima na mashinikizo kwa kupitia vyama vya upinzani taasisi huru za kijamii,taasisi na mashirika ya kidini na wafadhili wa nje na mabalozi. Naamini kwa kutumia massmovement ya namna hii tunauwezo wa kuishinikiza serikali hii ambayo wengi wetu tumeiweka madarakani kuachia ngazi mara moja! La basi tuko radhi kutoa uhai wetu kwa kizazi kijacho kama ikibidi kua hivyo...Mungu aepushe hilo kwa mapeozi yake.

na Mtz pure, Hillbrow. Joberg. RSA, - 30.03.08 @ 13:01 | #4161

SIKU INAKUJA.........., nayo ipo!!!,chezeni tu

na imani - 30.03.08 @ 14:32 | #4178

Big up mulokozi, mesema sahihi, wewe koplo nakuunga mkono, silah atatupa huyo koplo hapo juu inaonekana yuko tayari na yuko upande wetu.

nchi hii tupigane kidogo baada ya hapo heshima itakuja , MAANA HATA SASA WATU WANAKUFA SANA HILA SIO KWA VITA, NA TUSPICHUKUA HATUA WATAENDELEA KUFA, AFADHALI TUPIGANE KIDOGO TUZUIE VIFO VYA KUDUMU MAHOSPITALINI, JELA, MASHULENI, WAMACHINGA nk....................Afande ebu weka e-mail yako hata kama si ya jina lako sahihi tuanze vuguvugu hili.

na yoooooooo - 30.03.08 @ 14:53 | #4182

Sasa naona pameanza pambazuka nchi hii. Kwa mawazo haya naona Tz yenye neema ya kweli iko malangoni. Makala zenye kuibua hisia mwanana na za kiukombozi namna hii zidumu luliko Chama Cha Mafisadi (CCM). Tuwafundishe watz ukweli huu kwa nguvu zetu zote ili kwanza waichukie CCM na serekali yake alafu tuone kama kuna mtz atauliza afanye nini. Tukisema tungoje 2010 hawa mafisadi na tume yao ya ubaguzi watajihalalisha tena kuendeleza sera zao za kutufisadi kiakili, kiuchumi na kiutamaduni, sisi na vizazi vyetu.

na emmanuel, songea, - 30.03.08 @ 15:40 | #4188

Kwanza ningependa kujua kama Prof Semboja, Prof Matamballya, kama wachumi, Prof. Haroub O, Prof Kabudi, wanasoma haya maandishi? Mimi sioni jumuiya ya wasomi inafanya chochote kuamsha na kuipa jamii uelewa wa kutosha kuhusu fani walizoshikiria. Ninavyofahamu Jumuiya za Wasomi ndizo zinzoendesha mabadiliko katika nchi zinazoendelea. Inakuwaje Profesa unakaa kimya mwaka mzima hujazungumzia chochote kinachotokea ndani ya nchi yako kiuchumi, kisiasa na kisheria? Hawa wananchi wa kawaida wasiopata nafasi ya kuingia madarasani watapataje mwamko na uelewa wa kinachojiri katika ardhi yao? Wasomi wanaiangusha sana jamii. Haya yote yanayotokea katika nchi zetu za kimaskini ni kwa sababu wasomi wameshindwa kuiamsha jamii. Nini tofauti yao na wale wananchi walioko vijijini huko makwao? Tunao wachumi waliobobea lakini tunamjua huyu Semboja, Matamballya, wanasheria kibao, tunamsikia Kabudi, Shivji na sengondo, elimu ya siasa Baregu na ukuchungulia hawa ni kwa maslahi fulani, au siasa au wameitwa kwa ajili ya kuhojiwa, vinginevyo wanapumzika tu pale Mimani. Aibu. Fanyeni (siyo kutimiza) wajibu wenu. Hawa walioko katika siasa tunawaona jinsi wanavyoendekeza njaa, hawana msaada. Hakuna hata Prof mmoja aliyekuja na mpango mbadala unaoleta tofauti katika taasisi na idara wanazoongoza. Magufuli ni bora kuliko Msolla, Maghembe, Kapuya, aaah basi bwana.

na Christopher , Dar Tanzania, - 30.03.08 @ 17:22 | #4198

Watanzania kwa muda mrefu sana wamekuwa kimya wahesabiwa kama wapole au wajinga,mtajaza wenyewe.Imefikia mahali wamechoka na wanalalamikia hali halisi inavyokwenda.Tamko la ajabu na la kuvunja moyo toka kwa Rais wetu ni kuwa,kelele za wapinzani hazimnyimi usingizi.Hii si nchi ya wapinzani wala ccm,kwani rais hajui kuwa wapiganapo fahari nyasi ndo huumia? Kwa kusikia hizo kelele ni ishara kuwa hazitabakia kelele,wakati unakuja ambapo itakuwa ni zaidi ya kelele.Hatasikia kelele ila ataona yatokanayo na kelele.Sikio la kufa halisikii dawa.Haoni waliojidai kutawala kwa ubabe leo hii hawana hata kauli kwa kisingizio kuwa wameacha siasa,huo ni woga na aibu.Ataongea nini aeleweke na anajua watu si wa enzi zile.Watu wanabadilika.OLOE WENU WEZI NINYI,DAWA YENU IKO TAYARI.NI KIASI CHA KUINYWA TU.

na KERO, TZ, - 30.03.08 @ 17:37 | #4202

ndugu zangu tukisema tunamsubiri wa kulianzisha,anaweza kua hayupo au akaja ila akawa amechelewa,sasa kikubwa ni kujua hata mimi,wewe na yule tunaweza kulianzisha,ila kikubwa ni kwamba tuanze kwanza kuwapa somo ndugu zetu hasa wa vijijini ambao habari hawazipati au wanazipata zikiwa zimepitwa na wakati,ingawa sipendi tuanze huko mana muda umeshaenda sana ndio mana nasema tukisubiri wa kulianzisha tutakaa maisha yote na asije wa kulianzisha,km swala ni silaha sio ishu sana mana zipo nyingi sana kwenye black market ambazo wengi tulio huku tulipo tunajua wakina nani wanauza silaha kongo,swala ni kujuana km kweli wote tuna lengo 1 au wengine wametumwa na ccm,hapo ndio watu wengi hatuna uhakika,kuna watu wengi tu ambao wanafanya balaa huko kongo wanasema wapo tayari kutusaidia tukishajipanga bado hatujapata watu wa kuwaamini,mana isije tukafanya kitu halafu kikaishia kua aibu na tukaonekana wapumbavu badala ya wakombozi,kwa hiyo tujipange tu na tukiwa tayari mtaona tu kinaumana km kenya walivyofanya,na ilikua kidogo tu nchi ile iingie vitani watu walishajipanga haikua ajali tu,MUNGU tupe nguvu na ujasiri watz ili tuokoe nchi yetu kutoka mikononi mwa wajanja wachache,na kinachouma zaidi hawa watu wa nje wakina rostam ambao kwa dili 1 wanakula pesa ambayo ingetusaidia watz kwa miaka mingi sana mbele,sielewi kikwete anamkumbatia vp rostam ama nae kikwete sio mbongo ndio mana hawasikilizi wabongo wenzake,leo hii naamini kikwete yupo tayari kuona mbongo akifa,ila hayupo tayari kuona mtt ama ndugu wa rostam ama dewji wakifa sasa tumuweke pembeni mtu km huyu na kuweka watu wa kazi ambao watajali watu wao na maliasili zao na tukisema siku inakuja tunajidanganya kwa nini hiyo siku isiwe leo,ifikie wakati tuishi km makonda kwamba wanatafuta cha leo na cha kesho watajua kesho,sasa watz tufanye mapinduzi leo ya kesho au siku kuja tutajua siku hiyo itakapokuja,ila linalowezekana leo lifanywe leo.

na mstari wa mbele, calif/usa, - 30.03.08 @ 20:47 | #4219

ENOUGH IS ENOUGH , NAWAOMBA NDUGU ZANGO WOTE WA KITANZANIA MNAO ISHI NJE YA TANZANIA KIPINDI CHA KUSOMA MAGAZETINA KUTOA MAONI KWENYE INTERNET HAISAIDII HATA KIDOGO ,MIMI NAAMINI TUNAWEZA KUFANYA MABADILIKO.TUKI UNGANA NA KUIPA SHINIKIZO SERIKALI PAMOJA NA WAPINZANI WALIOKO TZ ,NINA IMANI MABADILIKO YANAEWZA KUTOKEA.WEWE NA MIMI NDUGU ZETU WAKIENDA HOSPITAL HATA PANADOL WANAKOSA LAKINI SPIKA WA BUNGE ANADAI DAWA ZA 2MILIONI INATIA HASIRA SANA SPEKA WA BUNGE LA TANZANIA AMETENGEWA MAGARI MAWILI WAKATI SPIKA WA BUNGE SIDHANI KAMA ANA GARI 2

No comments: