The Chant of Savant

Thursday 30 April 2009

Kwa siri hizi za li-government nitajinyonga

WASOMAJI wangu wapendeka na waheshimika,
Huu unaweza kuwa waraka wangu wa mwisho kama mambo yataendelea hivi. Msiposimama kunitetea, nitajinyonga kuepuka kifo cha ghasia za hawa wahuni.

Katika pita pita zangu juzi, nilinunua vitumbua kwa mama Msoto pale jirani. Hamadi! Kumbe alifungia vitumbua siri za Lisirikali! Ngoja nikuibie kidogo chanzo cha mauti yangu. Kwa juu karatasi zimeandikwa, “Li-governnement top secrets and confidential. When you see this, commit suicide and don’t show them to akina Silaha”.

Soma taratibu wasisikie. Ndani kuna siri nyingi mojawapo, EPA, Richmond , wizi wa kura, ajira za kujuana (refer to Shemeji Hawa mwenye Ghasia et et et yada yada) shehe Abullah mfalme-ardhi), Mzindikaya hunting blocks Khatibu, UBT ulaji.

Baada ya mama wa Ghasia za hawa kutishia kumfishia lupango Dokta Will-upana Silaha kwa kuiba na kutoboa siri za nchi, Mpayukaji nilijikuta nonihino ndogo ikinitoka bila kujua!

Kwanza, nililaumu tabia ya kupenda vitumbua na kuwaka kwangu. Kwani, ningekuwa kama wao nakula bure kwenye mahoteli ya kitalii nisingeona balaa hili. Sasa tazama niko usoni mwa mama Hawa wangu wa ghasia akiapa kuninyongelea mbali ili mambo yao yasijulikane!

Najua atasema mimi mwizi wa siri? Mijitu mingine kwa kupenda ghasia na ufyatu, kwanini niibe siri badala ya fweza? Kwanza , siri utamuuzia nani iwapo watu wanapanga mikakati ya kuiba na kuuza kura kwa ajili ya kula? Siri zenyewe wizi mtupu! Hebu angalia wizi unaoitwa siri. EPA, Richmond , Kiwira, Deep Green Finance, ANBEN, grand project between CCM and Richmond bogus pipeline to KG and MZ. Naona kinyaa.

Kama mbaya mbaya. Kabla ya kujinyotoa roho lazima nihakikishe makabrasha haya ya siri za Lisirikali namkabidhi Silaha. Yeye kachaguliwa na walevi kuwawakilisha. Hivyo, hatishwi na kiumbe yeyote hasa yule anayemwakilisha shemeji yake Njaa kaya. Loo! Nshalikoroga! Kumbe na hii siri tena ya Lisirikali!

Mama wa ghasia akijua najua alipewa ulaji kwa sababu ni shemeji yake jamaa atanifanyia ghasia kabla ya kuninyotoa roho. Tena alivyoshirikiana na yule mama simba si ndiyo basi nitanonihino kwenye kaptula kabla ya kufikishwa majilini.

Ngoja nifikirie kwa mara ya mwisho. Hivi anayeiba siri na anayeiba EPA, Richmond, IPTL, ANBEN, Fosnik, Kiwira na mabilioni mengine mengi, nani anastahili kunyongwa? Kwanini tufanyiwe ghasia na hawa vibaka na mibaka wa mchana jamani?

Mbona kijiwe cha Dom kimegeuzwa nepi hivi? Yaani majizi yanatishia watu wema mchana kweupe na serikali inaangalia tu! Hivi kosa langu ni kujua siri kuwa wao ni wezi waheshimiwa wakubwa wachuuzao roho za watu au kununua vitumbua na kupata siri zao?

Kumbe hawa wavivu wa kufikiri kama alivyojisemea na kutenda Tunituni na Anna Tamaa siyo!

Kwa nini mama wa ghasia anataka kutufanya wote majuha kama yeye? Mbona siri anazodai ni siri kwa usalama wa taifa ni kwa ajili ya kulibomoa? Siri gani wizi na ubabaishaji mtupu?

Hawa kweli wasohaya wana mji wao wa ghasia! Ghasia za huyu mama zimenikumbusha utumbo wa Bill Ngereja aliyesema eti siri za wizi hazipaswi kutoka nje hasa kuhusiana na Wawekechukua. Kwani zinaweza kuvuruga biashara hii ya wizi na uuzaji wa mali na roho za walevi. Yaani wizi maofisini ni siri kweli wakati tunaona migari na mijumba yenu? Hivi siri ya kuficha mapesa nje ya akina Chenga na Idrishi nayo ni siri kweli?

Ngoja niangalie kabrasha hili la mikataba ya ujambazi na uchukuaji kuhusu madini. Inasema. Cha juu 10% uchaguzi 5% kusomesha vitegemezi vyetu 2% na mengineyo kama kuchangia kiama 25%.

Du! Jamaa inakomba kweli kweli! Yaani hata kulea vitegemezi vyao ni siri za Lisirikali!

Alaa kumbe! Wao wanauza watu kusomesha vitegemezi vyao kwa kula 10 percent. Kwanini wanyonywaji wanaohenyeka kwenye maofisi yao ya gharama yanayolipiwa na kodi zetu wakishuhudia kufuru zao nao wasinyake kitu kidogo wakawavujishia siri akina Silaha? Sasa mimi nampelekea Silaha bila hata ya kukatiwa chochote ili naye awalipue tuone. Huenda walevi wanaweza kuamka na kuwapiga kibuti au kuwafanyia ghasia kama mama hawa wanavyotufanyia.

Hawa hawajui hii kaya ya kitu kidogo na ten percent. Sasa tuone mpambano huu kati ya kitu kidogo na ten percent utawastua vipi walevi kushika patamu baada ya mafisadi kupang’ang’ania.

Kwa vile mama Maghasia kasema asiye na kinga atanyongwa, basi nitajinyonga mwenyewe baada ya kamkabidhi Silaha hizi siri nzito. Najua hana kinga wala hirizi. Yeye kinga ya nini wakati si kibaka kama Mkapaa?

Yes yes! See? Nimegundua kwa nini Silaha haogopi ghasia na taka taka yoyote. Kinga yake ni walevi waliomchagua kuwawakilisha! Yeye amechaguliwa. Hajaingia kwa mgongo wa shemeji au mafisadi wala takrima. Yeye kijogoo wa siasa asiyeogopa ghasia wala simba wala Njaa kaya. Yeye si kuku wa kufugwa na shemeji akila vya bure kwa kuwaibia walevi. Yeye ni kanga wala si kondoo bali mbwa mwitu.

Kwa vile nimeishatoboa siri nyingi za Lisirikali na zinasema atakaye fanya hivyo ama ajinyonge kabla ya kufanyiwa ghasia au kufikishwa kwa pilato, lazima niandike wosia wangu.

Ndugu zangu walevi, walevi wenu wakubwa nao ni hovyo kama nyinyi. Wanawaibia kwa vile nyinyi ni walevi wa pombe za kienyeji. Nao wanalewa lakini pombe za wazungu waendako ulaya kukagua ulaji wao na kusaka njuluku nyingine kwa kuwatumia nyinyi.

Sisi tumejitoa mhanga kuwaletea siri zao ili mzitumie lau kuwanyima kula. Basi tunashauri msituangushe. Mkifanya hivyo mtajimaliza wenyewe. Heri yetu tunaojinyonga kuliko nyinyi mnaonyongwa. Je lipi bora? Kunyongwa kwa kukataa kunyonywa au kunyongwa kwa njia ya kukubali kunyonywa ukinyongwa taratibu? Ila mjue, mwisho wa yote ni kifo. Ila kifo cha heshima ni bora kuliko cha fedheha.

Mpayukaji hamtaniona tena. Nawashaurini kila mkiimba nyimbo za ukombozi na kusali litaje jina langu kwa ukumbusho wangu. Msikubali kutawaliwa na ghasia ila msikubali ghasia kuwatisha.

Baba yenu sina tunu ya kuwapa zaidi ya kuwaamba mjikomboe kwa herufi kubwa. Kateni mikatale. Siri mnazo. Kazi kwenu kuzitumia kuwavua nguo hata wawatishieni na ghasia. Fanyeni hivi kwa ukumbusho wangu ambaye damu yake imemwangika kwa ajili ya ukombozi wenu na vizazi vijavyo.

Nachukua kitanzi na kukifunga na kuongea na wasomaji wangu nikisema, twaeni nchi yenu mle na kunywa wote kwa ajili ya ondoleo la umaskini. Na iwe hivyo.
Chanzo: Tanzania Daima Aprili 29, 2009.

1 comment:

Anonymous said...

وظيفة جيدة جدا.