The Chant of Savant

Tuesday 30 August 2011

Hongera Luhanjo na Jairo



Kwa mara nyingine mhimili mmoja wa dola yaani utawala umeuumbua mhimili mwingine yaani bunge kwa kuuonyesha ukuu na ujabari wake.

Wabunge walipotoa shutuma za kuwepo rushwa na ubadhilifu kwenye wizara ya Nishati na Madini hawakujua kuwa walikuwa wakitaka kuwagusa wasiogusika. Zilipotolewa shutuma kuwa katibu mkuu wa wizara ya Nishati na Madini, David Kitundu Jairo alikuwa akitaka kujipatia pesa kwa njia zisizo halali kwa lengo haramu wengi walidhani Jairo angeshughulikiwa vilivyo. Walikosea hasa wakati huu ambapo mauzauza na mazingaombwe ni sehemu ya maisha ya kawaida. Wabunge walikosea kutaka kukata tawi kutokana na sumu ya mti mzima. Walikosea sana kudhani kuwa nyoka akivuliwa gamba anaacha kuwa nyoka. Wengi walitegemea matokeo haya. Unategemea nini kesi ya tumbiri inapohukumiwa na nyani?

Maneno ya Luhanjo yanaeleza hali halisi. Alikaririwa akisema, “Nawaonya watumishi wa umma wanaotoa siri za Serikali…, tutafuatilia tujue nani alitoa barua kwa mbunge, akipatikana atapewa adhabu,” Kumbe mchezo wote ulikuwa siri! Siri ya nini kama hapakuwa na namna?

Kwa busara zake na mapenzi wa taifa na uadilifu, katibu kiongozi Philemon Luhanjo aliamua kuwaacha uchi wabunge kama onyo kutowagusa wasioguswa. Wengi tulishangaa mantiki ya kumuandama Jairo huku tukiwafumbia macho mabosi wake yaani waziri wa nishati William Ngeleja na naibu wake Adam Malima.

Isitoshe, haikuwa mara ya kwanza kwa wizara ya Nishati na Madini kufanya madudu tena makubwa kuliko hili la kuhomola na kutaka kuwahonga wabunge. Nani haoni walivyofanikiwa kuliweka taifa kizani kwa miaka bila kuguswa? Nani haoni madudu haya ambayo kimsingi yanadhoofisha hali za maisha ya watu na uchumi wa nchi? Kuna kosa kubwa kama hili la kuhujumu taifa?

Hivyo basi, shutuma za mbunge wa Kilindi (CCM), Beatrice Shellukindo hata kama zina kiwango kikubwa cha ukweli kuliko uongo zimefanywa kuonekana fitina badala ya msaada kwa taifa hasa linalojidai kupambana na ufisadi na uvunjaji wa maadili. Nani hajui kuwa maadili yamepinduliwa na madili?

Kwa hukumu safi ya Luhanjo, kwanza, inaonyesha wabunge ni wambea na wafitini. Pili wabunge wanaonyeshwa kama wala rushwa hasa katika kupitisha bajeti za hovyo kama walivyofanya kwenye bajeti za wizara za nishati, utalii na mali ya asili.

Je wabunge watatahayari na kunywea au kujikusuru na kutaka wahusika washughulikiwe? Nani atawashughulikia wateule hawa? Je wabunge watanywea na kuonekana kama wala rushwa wa kawaida wanaoweza kuhonga pesa kidogo na kupitisha bajeti zinazowaumiza waliowachagua kuwawakilisha? Nini kitafanyika au ndiyo imetoka? Je namna hii tunajenga taifa la namna gani ambapo kila mhalifu anaposhitakiwa huachiwa na aliyemshitaki kuonekana mfitini na mtu asiye na lolote bali fitina?

Kwa uamuzi wa kumrejesha kazini Jairo, Luhanjo ameonyesha busara ya hali ya juu. Kwanini ahangaike na mjumbe wakati waliomtuma wanaendelea kupeta? Je alichofanya Luhanjo ni haki au kuwasuta wakubwa wasiowawajibisha wateule wao? Je rais atakubaliana na uamuzi huu wa kustua na kulindana huku ukimtia doa kuwa hana ubavu wa kupambana na mafisadi papa? Je ni wangapi wamepewa nguvu na kutiwa moyo na uamuzi huu wa aina yake unaowapa mwanya wa kuendelea kutenda watendavyo bila kujali kelele za wale watakaostukia madudu yao?

Baada ya kutolewa tuhuma waziri mkuu Mizengo Pinda alimwamuru mkaguzi mkuu wa hesabu za serikali (CAG), Ludovick Utoh na si TAKUKURU, “kumchunguza” Jairo. Baada ya “uchunguzi” wake Utoh alikaririwa akisema, “Pia taasisi hii ililipia gharama za tafrija iliyofanyika Julai 18 jioni katika Ukumbi wa St Gasper Dodoma kwa gharama ya Sh 6, 141,600, pamoja na kuwa bajeti haikupita, tafrija ilifanyika kwa kuwa maandalizi yalishafanyika na hata gharama ingelipiwa tu,”

Matokeo ya “uchunguzi” wa Utoh yanaacha maswali mengi kuliko majibu. Je Ewura waligharimia tafrija hii ya kuwalisha wabunge kama nani na ili iweje? Je wabunge kwa kufanyiwa tafrija siyo hongo? Je hapa kosa ni mkosefu kumshitaki mkosefu mwenzake? Kwanini serikali ilimtumia mkaguzi wa hesabu za serikali ambaye kimsingi alipaswa kuwa shahidi kama mtaalamu? Je kazi ya mkaguzi wa hesabu za serikali ni kuchunguza watuhumiwa au kukagua hesabu za serikali? Je huu si mgongano wa maslahi kati ya serikali na bunge? Hivi nani alitegemea mkaguzi wa hesabu za serikali ambaye naye ni mteuliwa kama Jairo aiaibishe serikali yake? Je kwanini Bunge halikuunda kamati huru kuchunguza kashfa hii?

Maswali yanazidi kuongezeka kutokana na majibu ya CAG. CAG alisema katika uchambuzi huo, imebainika kwa uhakika kuwa malipo yaliyofanyika yalihusu posho ya kujikimu, takrima na posho za vikao kwa maofisa walioshiriki katika shughuli nzima ya kuwasilisha bajeti ya wizara na kwamba hakuna ushahidi wa malipo kwa wabunge.

Je CAG hajui kuwa takrima ilipigwa marufuku kutokana na kuwa rushwa ya wazi? Je kwa wizara kutoa takrima na wabunge kuipokea wakati ni wao walioibatilisha si kutoa na kupokea rushwa?

Ukiachia mbali uamuzi wa Luhanjo kuacha maswali mengi kuliko majibu, umemvua nguo waziri mkuu ambaye alikerwa wazi na tuhuma hizi ila kwa vile Jairo hakuwa mteule wake aliichia jukumu la kumshugulikia Jairo mamlaka iliyomteua.

Kabla ya mazingaombwe na sarakasi kuingizwa, Pinda alikaririwa akitoa msimamo wake akisema,

"Kwa jinsi jambo hili lilivyokaa, hakuna jinsi mtu unavyoweza kulitetea hata kidogo, nilitamani sana kwamba nije hapa niseme kwamba uamuzi wangu mimi ni huu, lakini haikuwezekana," alisema Pinda na kuongeza: "Kwa dhati kabisa naomba wabunge tuwe na subira, mara tu mheshimiwa Rais atakapotua South Africa (Afrika Kusini) jioni ya leo (jana), nitamuarifu na ninaamini tutaelewana kuhusu hatua za kuchukua." Hii ni nukuu ya tarehe 18 Julai yalipotolewa madai haya.

Ukiachia mbali kuvuliwa nguo waziri mkuu, hata wabunge wa CCM waliotaka Jairo afukuzwe kazi kuwa ni pamoja na Christopher Ole Sendeka (Simanjiro), Esther Bulaya (Viti Maalumu), George Simbachawene (Kibakwe), Godfrey Zambi (Mbozi Mashariki), Henry Shekifu (Lushoto), Murtaza Mangungu (Kilwa Kaskazini), Alphaxard Lugora (Mwibara), Shellukindo (Kilindi) na Mwenyekiti wa Kamati ya Bunge ya Nishati na Madini, January Makamba ambaye pia ni Mbunge wa Bumbuli nao watakuwa wamevuliwa nguo pia.

Tuhitimishe kwa kuwapongeza Jairo na Luhanjo kwa kuokoana ingawa uamuzi huu hauna faida wala maana zaidi ya kuzidi kuionyesha serikali kama legelege kama walivyowahi kusema wapinzani. Je tutaendelea na madudu haya na kulindana hadi lini? Hata hivyo, bila kushughulikiwa Ngeleja na Malima, Jairo angeonekana bangusilo maana hawezi kufanya kitu bila wao kuridhia.
Chanzo: Dira Agosti 29, 2011.

Natafuta kijogoo cha kike kiniwowe

Haki ya nani mambo yanazidi kubadilika! Sijui haya ndiyo maendeleo, maanguko, kulipiza visasi au kusahihisha mahusiano ya jamii! I have no idea. Nani alitegemea mwanamama angeoa mwanarume tena wawili kwa mpigo? Anayedhani hizi ni rongorongo au pumba za gongo ameumia na atachekwa. Kama husomi magazeti kwa vile u kilaza au apeche alolo basi fungua masikio maneno ya injili ya mlevi yaingie. Imetokea openly and live. Are you thither? Usiniulize maana ya thither ingawa yaweza kuwa there au pale. Juzi si nilisikia walevi wakisema kuwa kule Mpanda ya Sumbawanga au Tupa uchawi, kuna mama kaoa walume wawili ambao wanamshea bila mitwalingo wala nini. Sijui wamepigwa limbwata wakingojea kahando au la. Mie sijui.

Huyu mother nimem-love kweli. Maana, baada ya kufanya usharmutah na kushindwa akaamua kufanya kweli. Heri yake ameamua kuchukua haramu yake kuliko makabila fulani yanayochukua kaka na dada na wajomba zao. Hayo tuyaache.

Hili la mama kuoa mibaba tena mibee si jipya. Juzi si mlimsikia yule balozi akifungua kampuni kwa jina la anayeonekana mumewe wakati ukweli ni mkewe wa kiume kule kwa Joji Kichaka.

Kwa vile kuna wanamama wenye ubavu wa kuweza kuwaoa warume, nami natafuta kijogoo cha kike kinioe lau naweza kuondokana na ukapa huu wa nanihii baada ya kuachwa na aliyekuwa wa ubani wangu. Najua viherehere weshaanza kusema eti mie ni mtoto si riziki. Hasha! Nataka kuolewa na kijogoo cha kike si cha kiume. Hivyo tuelewane barabara hapa tusijetoana nundu bure.

Hata hivyo nina masharti. Huyo kijogoo wa kike atakayetaka kunioa lazima awe tayari kuninyenyekea. Sitaki mama wa kunidunda au kuninyoshea domo hasa baada ya kuwa nimeutwika. Maana naweza kumnyotoa mtu roho bure nikaishia kunyongwa pasina ulazima. Najua kuna njemba zinazodundwa na wake zao. Ukikutana nazo mitaani zinavyojishaua. Juzi nilimsikia mmoja pale Uwanja wa Fisi akisema eti mwanamke hambabaishi wakati tunajua anakong’otwa na mkewe kama mtoto mchanga. Wapo wengine wanavishwa magagulo na kupiga deki tena vizuri ingawa hatuwaoni. Hata kama mimi ni mmojawapo yakuhusu nini? Mbona pale Kenya wababa walikimbia kwenda kuomba msaada baada ya kukunyugwa na akina mama yaani memsahib wao? Wadhani nchezo na uongo. Watu wanafanyiwa kweli sema hawasemi kwa vile nyumba zinaficha mengi. We ziache nyumba ziitwe nyumba.

Unakuta baba zima likikwidwa na halifurukuti kwa vile halina kitu. Linaogopa likipandisha Mwenembago mshirika wa bedroom atalitishia kuwa ‘nitagawa kama sina akili nzuri’ tuone. Na umeme huu, ndiyo usiseme lazima mulume mzima unywee. Ni Bakhresa na wenye nazo pekee anaweza kufurukuta na kusema kata mti panda mti mwenye nazo hakosi walaji. Kama ni apeche alolo what do you do zaidi ya kunywea au kufunika kombe mwanaharamu adunde?

Juzi kwenye ofisi yangu Uwanja wa Fisi nilimsikia mdada mmoja akimpa mumewe, sijui mshirika wake, akisema kama hunazo wenye nazo wala wewe waletewa makombo. Duh! Nilitamani nimnyotoe roho lakini kwa vile cha mtu mavi niliamua kula waya na kuendelea na mihanjo yangu au siyo? Unaweza ukajifanya kukomaa ukamkuta mkeo na kaka yake hasa wale jamaa zangu wa mlima ule. Akionyeshwa njuluku hata dogi anapewa kitu muhimu mnakula sahani moja. Hata hao wanaojiita uncles na kaka chunga sana. Hao hawaaminiki ni sawa na jiko la mchina. Jamani nanyi achene mambo haya mtaishia unung’aembe. Maana mtu aoelewa leo kesho yu ntaaani! Jamani punguzeni kuabudia na kupenda pesa na vitu ni vya kupita. Hata mbuzi hawafanyi hivyo zaidi ya mbwa na kuku.

Kumbe siku hizi kama huna kitu huna bao kama hizi njemba zilizotembezewa ndoa hata kama haramu na kijogoo cha kike! Kama umeingia mkenge na kuoa kwenye mlima ule ndiyo usiseme. Najua wengi wanaosoma walioingia mkenge wanatauna meno na kutikisa vichwa. Shauri yenu kwani mie ndiyo niliwatuma? Je ni wangapi wanafanyiwa hivi na wasifurukute? Nawaambia fanya kama mimi. Timua wapo wengi badala ya kuwa mtumwa wa ndoa. Huna haja ya kujinyong’onyeza na kiumbe asiye na shukrani wakati wapo wengi wanatafuta nafasi yake. Hata wanaume hivyo. Kama nkeo ni mali amelelewa vilivyo ukanchezea jua wapo wengi wanawinda. Hayo tuyaache.

Jamani ee siku hizi wanawake wako aina mbili-mosi vitega uchumi vya wazazi au wale wa ubani. Ukiangukia kwenye akina babangu “kinu lasima kijenge nyumba”, umeumia. Huko mie siko matajuana wenyewe. Kwani wakati mkikubaliana mie mlevi sikuwepo. Nilikuwa zangu Uwanja wa Fisi nikiweka vitu. Hata wanaume wapo akina toto la mother. Wao wanadandia akina dada wenye nazo au nafasi ili wawatumie kupiga pamba na kuishi wasijue ndiyo kuolewa kwenyewe! Hata akina dada wanaoulizwa na mama zao kama wachumba zao ni wafanyabiashara, wanasheria au wahasibu nao hawana maana. Si ujanja. Ni uvivu na umaskini wa kiakili. Kwanini utake mchumba wako awe nazo wakati baba yako hana kitu bali kukutumia wewe kama mtaji? Huu nao ni ufisadi na umalaya. Unamwambia mtu I love you kumbe una-love Pochi lake! Wapo walioambukizwa miwaya wakaacha mipesa nyuma wasiifaidi kutokana na kujiona wao wanjanja wasijue wapo wajanja kuliko wao. This is crazy so to speak. Upendo ndiyo msingi wa ndoa. Zaidi ya hapo ni kupoteza muda. Wewe unataka mie niwe nazo uchume. Je baba yako anazo? Kama unataka mie niwe nazo kwanini wewe usiwe nazo? Huu nao ni uvivu na umaskini. Wenye tabia hizi jamani acheni.

Turejee kwenye ndoa yaani kuolewa na kijogoo cha kike. Kama warume wanaoa, kuna ubaya gani wanamama nao kuoa? Si ndoa ni makubaliano bwana? Ila hapa lazima niweke shurti. Si kila makubaliano si ndoa. Naongopa wale akina saga na senge wasitumie mwanya huu kuhalalisha ufirauni wao. Mbona kuna warume wameolewa na tunawajua lakini hatusemi!

Acha niende kusaka kidumejike kiniwowe haraka mie. Sharti la mwisho kidumejike hiki kiwe waziri au balozi nje.
Chanzo: Dira Agosti 29, 2011.

Thursday 25 August 2011

Rais avunje na kusuka baraza la mawaziri

Hakuna ubishi. Baraza letu la mawaziri linamweka rais majaribuni na kwenye lawama bila sababu. Maana kila uchao zinafumka kashfa zinazoonyesha kuwa baadhi ya mawaziri hawafai au tuseme hawafanyi au hawajui kazi zao.

Waandishi wa habari watakuwa bado wanakumbuka kashfa ya Loliondo ambapo mwandishi mwenzao Stan Katabaro aliuawa kwa kuifichua na kuishupalia. Hii ilitokea wakati wa awamu ya pili ambapo mwarabu aitwaye Brigedia Ali alishirikiana na watendaji waroho na wapuuzi wa serikali kuliibia taifa.

Wakati ule, wanyama walikuwa wakiuawa hovyo huku wahusika wakishuhudia na kunyamaza kutokana na sababu walizojua. Ilifikia mahali mbuga zetu zikawa kama mali ya watu binafsi. Nani mara hii kasahau ilivyokuja kubainika kuwa baadhi ya mawaziri wa wakati na familia za baadhi ya vigogo walikuwa na maslahi ya moja kwa moja kwenye makampuni ya uwindaji? Kwa sasa sijui hali ikoje ila hali ilivyo itakuwa mbaya zaidi ya awamu ya pili na tatu. Ninachojua ni kwamba mchezo huu wa Brigedia Ali unazidi kunoga. Maana, hata kwenye sakata la mitambo ya Dowans Ali huyu huyu aliletwa na Rostam Aziz akidai ndiye mwenye kampuni wakati siyo.

Japo serikali imekuwa ikisema haina ubia, ukiangalia tangu awamu ya ruksa ya Ali Hassan Mwinyi, ulijengeka ufisadi wa ajabu ambapo wezi na matapeli wa kimataifa hutumia vimemo au mamlaka za wakubwa kuhujumu nchi bila kushughulikiwa. Hii ndiyo siri ya wezi wa EPA kutopatikana wala kushughulikiwa. Wangepatikana na kushughulikiwa vipi wakati watuhumiwa ndiyo hao hao waliopaswa kujikamata?

Hata ukienda kwenye kashfa ya ununuzi wa rada, ndege ya rais na ukarabati wa ikulu wakati wa awamu ya tatu mambo ni yale yale. Tapeli anakuja nchini kwa kutumia mgongo wa mkubwa mkewe au mwanae na kufanya kila uhalifu bila kuguswa.

Ripoti kuwa wanyama 116 na ndege 16 walitoroshwa kupitia uwanja wa kimataifa wa Kilimanjaro kwenda kusikojulikana ni upuuzi. Haiwezekani wanyama wengi kiasi hicho watoroshwe kusikojulikana. Je walikopelekwa hakujulikani? Bila shaka kunajulikana. Kama wahusika hawajui nani wa kumuuliza walipopelekwa hawa wanyama basi waende mamlaka ya anga. Maana hakuna ndege inayoweza kuingia na kutoka nchini bila kujulikana wala kupewa kibali cha kufanya hivyo. Watuhumiwa wa pili ni mamlaka za mbuga za wanyama zilizokabidhiwa jukumu la kulinda wanyama. Hivyo tusidanganywe kuwa wanyama waliotoroshwa hawajulikani walikotoroshewa wala aliyewatorosha. Hapa tutake tusitake lazima kuna mkono wa mtu au watu wazito. Maana itakuwa nchi ya ajabu ambapo madege yanaweza kuingia na kuchukua mali zetu sisi bila kujua. Achia mbali kuingia na kutua nchini. Hata ndege ikikatiza kwenye anga zetu lazima mamlaka husika ziwe na taarifa. Je ni ndege ngapi zimeishaingia mara ngapi na kwa muda gani nchini mwetu na kuondoka na madini, nyala hata dola? Kama ndege zinaweza kuingia na kutua bila kujulikana zinatoka wapi, kwenda wapi na kubeba nini, nini mantiki ya kuwa na mamlaka husika? Je hili haliweki usalama wa taifa letu hatarini hasa kipindi hiki ambapo uhalifu wa kimataifa kama vile kusafirisha mihadarati, silaha na ugaidi vimeongezeka?

Kwa kuangalia uzembe na uhujumu huu wa kutorosha wanyama, tupaswa kumshauri rais avunje baraza la mawaziri na kuwatimua mawaziri husika.

Kwanini tumeruhusu nchi yetu kuwa shamba la bibi tena linalosimamiwa na mataahira?
Siyo siri, kwa sasa kuna mawaziri ambao hawapaswi kuwa ofisini. Hawa ni waziri anayeshughulikia mbuga za wanyama na naibu wake, Ezekiel Maige, waziri wa Nishati, William Ngeleja na naibu wake Adam Malima ambao wameshindwa kutatua tatizo la umeme na uhaba wa mafuta, waziri wa mambo ya ndani, Shamsi Vuai Nahodha na naibu wake Sued Kagasheki ambao jeshi lao la polisi linasifika kwa kuua, na waziri wa ulinzi, Hussein Mwinyi na naibu wake ambao mabomu yao hivi karibuni yaliua watu wasio na hatia kule Mbagala na Gongo la Mboto.

Pia wapo mawaziri waliotuhumiwa kughushi shahada zao za kitaaluma ambao ni Mary Nagu, Makongoro Mahanga, William Lukuvi, na Emanuel Nchimbi.


Pia wapo mawaziri wanaopwaya kwenye nafasi zao kama vile Hawa Ghasia, Celina Kombani,Jumanne Maghembe, Shukuru Kawambwa, Sofia Simba aliyejipatia umaarufu kwa kuwatetea mafisadi.

Kwa wanaofuatilia utendaji wa mawaziri tajwa, watakubaliana nami kuwa wanapwaya kiasi cha kumfanya rais achukiwe kutokana na uzembe au makosa yao. Sina sababu ya kumtetea rais bila sababu. Hii si kazi yangu. Ila kama mwananchi wa kawaida, najua mbivu na mbichi kama ambavyo wengine wanaweza kuona. Bahati mbaya hatuna utamaduni wa kutafuta maoni ya watu wetu kuhusiana na watawala wao. Ungekuwapo utaratibu huu na ukawa ukitumika kuwatimua au kuwabikiza watu maofisini, bila shaka hali ingebadilika tena haraka. Hata hawa niliowaorodhesha kama watapigiwa kura ya maoni, wataonekana kuwa tatizo kwa serikali. Haiwezekani kwa mfano nchi ikae kizani zaidi ya mwaka mzima waziri husika apendewe au aonekane anafaa. Itakuwa ni ajabu ya aina yake. Haiwezekani wanyama waibiwe tena kwenda “kusikojulikana” mawaziri husika waonekane wanatimiza wajibu wao. Haiwezekani watu wapigwe risasi hovyo na kuuawa au kulipukiwa na mabomu mawaziri husika waonekane wanafaa. Haiwezekani kabisa.

Haiwezekani, kwa mfano, waziri anayehusika na utawala bora awalinde mafisadi wazi wazi na bado aonekane anafaa. Haiwezekani waziri wa sheria apinge mchakato wa kuandikwa katiba mpya aonekane anafaa. Haiwezekani. Hata kama wananchi wetu hawana nafasi na hawasemi, wanaona kuwa mambo yanavyokwenda siyo. Wanaishia kulalamika tu kwa vile hawana pa kwenda kushitaki wala wa kuwasikiliza. Badala yake wanatutegemea sisi wachambuzi tuwafikishie kilio chao. Na hii ndiyo maana, badala ya kumtwisha lawama rais moja kwa moja kabla ya kumweleza ukweli, nimeamua kuandika makala hii nikiamini atapata salamu zangu.

Tuhitimishe kwa kumtaka na kumshauri rais kuvunja baraza la mawaziri na kuondoa mawaziri wanaoonekana kuwa mzigo kwake bila sababu. Rais hana sababu ya kulaumiwa kutokana na uzembe wa watu wachache aliowaamini wakashindwa kuaminika. Kuna haja ya kusafisha safu yake ili wote wenye madoa waondolewe na kwenda kujisafisha wakiwa nje ya ofisi za umma.

Kichekesho ni pale eti waziri wa wanyamapori kumsimamisha mkurugenzi wa mamlaka hiyo wakati na waziri ni mtuhumiwa! Tangu lini mtuhumiwa akawahukumu watuhumiwa wenzake?
Chanzo: Dira Agosti, 2011.

Wednesday 24 August 2011

Binadamu anaweza kufanya lolote akiamua

Kuna ukweli unaoanza kujitokeza kuwa binadamu na nyani wana uhusiano wa karibu hata kama si uhusiano wa damu inawezakana uhusiano kitabia. Nani aliamini kuwa binadamu angeweza kufanya kama hawa binadamu wanavyofanya. Kwa taarifa zaidi, BONYEZA HAPA.

Msekwa naye ni gamba


Chama Cha Mapinduzi (CCM) kimekuwa kwenye mikakati ya kuuaminisha umma kuwa kinaweza kurudisha hadhi yake. Moja ya mikakati ya kurejesha hadhi na imani ya chama ni kujivua gamba. Dhana hii ya kujivua gamba ilianzishwa baada ya CCM kubaini kuwa ufisadi ambao umekuwa ukifanywa na baadhi ya vigogo wake haufichiki wala kuweza kulindwa. Dhana hii imeishapata majeruhi ambapo aliyekuwa mbunge wa Igunga Rostam Aziz aliachia ngazi hivi karibuni huku watuhumiwa wenzake wawili Edward Lowassa na Andrew Chenge wakipewa mwezi mmoja kujivua gamba kabla ya kuvuliwa.

Ingawa CCM ima kwa maksudi au bahati mbaya ilikuja na majina matatu kati ya mengi yaliyoorodheshwa na wapinzani kule Mwemba Yanga ya Septemba 15, 2007. Wengi hadi sasa hawajajua vigezo vilivyotumika kuwalenga mafisadi watatu kati ya wengi. Hata hivyo, idadi ya mafisadi imekuwa ikiongezeka ingawa watajwa hawajashughulikiwa. Mnamo tarehe 17 Aprili 2011, Dk Wilibrod Slaa, Katibu mkuu wa CHADEMA ambaye ndiye aliyetaja kundi la kwanza la mafisadi, alipanua orodha ya mafisadi wa awali kwa kuongeza wengine wapya.

Yeye badala ya kuwa humu ndani kusikiliza bajeti ya wizara hii, amekuwa akihangaika huko kutafuta watu ili aende kuwakatia maeneo na kuyauza huku akisingizia Rais Kikwete ndiye ametoa amri ya kuuzwa kwa ardhi husika.

Ukichunguza kwa makini, mafisadi au magamba yanayoisumbua CCM si yale tu yaliyotajwa na Dk Slaa tu. Kwa mfano, makamu mwenyekiti wa CCM taifa Pius Msekwa hakuwahi kutajwa kwenye orodha mbili za mafisadi zilizotolewa na ufisadi ingawa anadaiwa kuwa amekuwa akifanya ufisadi tena kwa kiwango cha juu.

Hivi karibuni msemaji mkuu wa kambi ya upinzani kwa wizara ya Maliasili na Utalii, Peter Msigwa CHADEMA alinakiriwa na vyombo vya habari akimueleza Msekwa ifuatavyo:

"Kambi rasmi ya Upinzani inaitaka Serikali kuchukua hatua kali dhidi ya Mwenyekiti huyu wa bodi mara moja kwa kukiuka mipaka ya majukumu yake, tunaahidi kuwa tupo tayari kuipa Serikali ushirikiano kuhusiana na tuhuma hizi,” Muhimu, hapa mwenyekiti anayezungumziwa ni Msekwa.

Shutuma za ufisadi dhidi ya Msekwa hazikutoka kwenye kambi ya upinzani tu bali hata kutoka chama chake kama alivyokaririwa Mbunge wa Ngorongoro, Kaika Terere (CCM) akisema kuwa Msekwa amekuwa akiitumia bodi kufanya mambo yenye mwenyewe ambayo ni kinyume cha taratibu za Bodi ya Ngorongoro.

Alisema Msekwa aliidhinisha ujenzi wa hoteli yenye hadhi ya nyota tano katika hifadhi ya Bonde la Ngorongoro ambapo hata wenyeji wa pale walikatwa kupitisha mifugo yao.

Telele alisema, "Rais gani anaweza kukubalina na uuzaji huu? Kama ni kweli amebariki, basi hatuwezi kukubaliana naye katika uamuzi wa kuharibu na kuiuza hifadhi ya Ngorongoro,"

Telele alitaka iundwe tume ya kuchunguza bodi ya Ngorongoro kutokana na mambo mengi yanayofanyika ambayo ni uvunjifu wa sehria na katiba.

Wengi wanangoja kuona CCM itamchukulia hatua gani kigogo wake huyu wa ngazi ya juu ambaye amewahi kushika nyadhifa nyingi ikiwemo ukatibu mkuu wa CCM, spika, uwaziri, ukuu wa mkoa na sasa umakamu mwenyekiti. Huyu si dagaa bali papa kwa viwango vya kitanzania. Ajabu ni kwamba ni huyu huyu Msekwa alikuwa akiwaita watuhumiwa wenzake kuwataka waachia ngazi yaani kujivua gamba kabla ya kuvuliwa. Je yeye atavuliwa lini? Bila CCM kujibu swali hili kwa kumshguhulikia mhusika, kelele zote za kujivua gamba zitaishia kuonekana kama danganya toto huku mchezo wa kulindana ukiendelea kama kawaida. Wengi wangetaka kuona Msekwa akivuliwa gamba hata kesho ili angalau haki ionekane imetendeka.

Pia, baada ya kufichuka kwa uchafu wake, Msekwa ameonekana mnafiki mbele ya jamii. Wengi wanashangaa alipata wapi ujasiri wa kuwataka wenzake waondoke au wajivue gamba wakati naye analo lake? Je ni kwa sababu yake yalikuwa hajafichuka? Je wako wangapi wanaoonekana kung’ara wakati ni wachafu kuliko hata wale wanaowanyoshea kidole?

Hata ukimwangalia rais Jakaya Kikwete ambaye alitajwa kushiriki na kunufaika na wizi wa EPA, utagundua kuwa hana udhu wa kumwajibisha yeyote. Je hii ndiyo sababu ya Kikwete kuchagua baadhi ya mafisadi na kuwaacha wengine? Je kwanini kulenga mafisadi watatu kati ya wengi waliomzunguka kama Msekwa? Je Msekwa anatuma na Kikwete kama alivyobainisha mbunge Telele kuwa huwa anasema ametumwa na rais? Mbona Kikwete hakanushi kama kweli auhusiki na ufisadi na hujuma hii?

Ukiachia orodha ya Dk Slaa, kuna magamba mengine mapya yaliyofichuka hivi karibuni. Hawa si wengine bali Idd Simba, Didas Massaburi. Hawa nao ni magamba yanayopaswa kuvuliwa haraka hasa ikizingatiwa walivyohujumu lililokuwa Shirika na Usafiri Dar es salaam (UDA).

Tuhitimishe kwa kuwahimiza wananchi wasiendelee kutoa nafasi kwa rais Kikwete kumaliza muda wake huku akiwa ndiye anashutumiwa kuwa kinara wa ufisadi hasa kwa kushiriki na kuwalinda. Wakati wa kumwambia Msekwa wazi wazi kuwa anapaswa kujivua au kuvuliwa gamba ni huu. Bila kufanya hivyo tutaendelea kuchezewa kana kwamba hatuna akili kama umma na jamii.

Chanzo: Tanzania Daima Agosti 24, 2011.

Wauza wese walichakachua sasa wanakwatua

Jamani kaya hii imechakachuliwa kila idara kulhali. Wewe umechakachuliwa hata mimi kadhalika. Bila kuchakachuliwa nani angekubali kuishi kwa mgao wa takribani kila kitu? Juzi mwenzenu niliumbuka. Nilipewa lifti na mlevi fulani mzito. Kumbe pamoja na uzito wake gari yake haikuwa na wese la kutosha. Kufika njiani si gari ikageuka kimeo! Mwenzangu alianza kupagawa akifikiri jinsi jeshi la vibaka litakavyotuvamia na kuchukua njuluku zake kama si uhai wake. Maana vibaka wana hasira na mibaka inayowafunga wakati yenyewe ikilindana. Wana usongo na maisha na wamechoka na maisha ya mgao wa kila kitu. Ukienda kwenye umeme mgao, wese mgao, mikopo ya ilmu dunia ya juu mgao, gongo mgao, maji mgao, matatizo mgao, ufisadi mgao, maulaji mgao. Jamani, hata kifo sasa kitakuwa mgao. Makapuku watapewa kifo kingi huku wazito wakipewa afya nyingi kama wanavyogawiana umeme mwingi na kuwapa walevi kiza kingi.

Baada ya shangingi la mfala wangu kugeuka kweche si niluliza kulikoni, mzito mzima tena mwenye cheo si kikubwa tu bali cha haja akaanza kulalamika na shumbwenga lake kugeuka kweche mchana kweupe. Mara alisema: “Hawa washenzi tusipoangalia watakuja pindua kaya hii na kusimika lisirikali lao la kijambazi.”

Mie kwa unoko nilijifanya simpati hivyo niliuliza. “Mkuu washenzi wapi hawa wanaotaka kupindua kaya na kuingiza ujambazi kuku?”

Naye bila kusika alijibu, “ Si hawa wauza wese ambao wengi wao wanaitwa wawekezaji wakati ni wachukuaji. Hivi huoni wanavyowalangua watu huku wakitorosha mipesa kibao kwenda ughaibuni?”

Nami sikujivunga. Nilimpa laivu, “Sasa wakubwa kama nyinyi mnalalama hawa waduchu wafanyeje? “

Nilitaka kumuongezea kigongo kingine lakini nikamuonea huruma. Moyoni nilitaka kusema hivi: kama nyinyi mnaowaruhusu hao wezi kuwekeza humu uongo na kuvuna pesa kwa vile nanyi mnakatiwa kitu kidogo na kikubwa sasa mnalalamika nini? Hamjui kuwa mmeuza watu wenu nanyi mkiwemo kwa uroho wenu? Ndiyo maana kuna mwizi mmoja amesema eti baadhi yenu wanafikiria kwa makalio wakati naye anafikiri kwa makalio hay ohayo. Wahuni nao wamemkomesha kwa kuzusha msamiati uitwao masaburi yaani wakimaanisha matako! Heri angesema kuwa wanaosababisha uwekezaji na ubinafsishaji kwa kijambazi wanafi…. Sorry wanalawiti… sorry wamekeketwa kiakili huenda wangetia adabu. Hayo tuyaache.

Kwa ufupi sitaki niseme yote tuliyoongea na huyu mzito kwa sababu za usalama wa kaya. Tuliyoongea ni top secret au tusema of high importance for national security. Isitoshe tuliyodurusu ni top secret ambazo zaweza kujulikana kwa FBI pekee yake baada ya kuibiwa na CIA. Upo hapo mlevi mwenzangu?

Kwa ufupi nawamegea kidogo. Ukweli ni kwamba huu mgao wa wese uliozaliwa baada ya huu wa umeme, ni mchezo wa wanene fulani kutafuna kaya. Jamaa walianza na uchakachuaji wa mafuta na siasa wakanogewa hadi wakajiweka reheni bila kujua na kujikuta nao wakichakachuliwa. Hukumsikia yule mfala wa kikaburu toka Sauzi aitwaye Sell no Nanduu akiwabwatukia walevi wenzie kwa kuwapa masaa 24 wakafyata mkia. Baada ya welevi hasa wambea wa magazeti kushupalia karipio na tishio lake si ndipo Lisirikali likaamka na kujivuvumua kwa kuamuru wese liuzwe. Kuonyesha lisirikali lisivyo na bao, baada ya kubanwa mbavu nyuma ya pazia si bei zilipandishwa tena baada ya masaa 24! Je hapa mfala huyu wa kikaburu hajatawala nchi yetu by proxy kama wasemavyo watasha?Je hapa mamlaka haijasweka kwenye mfuko wa fisadi huyu wa kikaburu? Je jeuri yote hii inatoka wapi kama siyo kujua uhovyo na siri zao? Wathubutu awavue nguo. Wao wamezoea kuvuana magamba. Jamaa atawavua nguo tena za ndani bila kubaki hata na godfather makalioni. Maana anawajua vizuri na wakiendelea kutishana atawaanika hadi walevi wawamwagie kahawa na tangawizi kwa mihasira waliyo kuwa nao dhidi yao.

Ingawa suala la mgao wa nishati haliwakutikisa wala kusababisha walevi wawatimue kwenye ulaji, hili la wese laweza kutupeleka Tahrir kirahisi na kwa haraka bila kutegemea. Hii itategemea uwezo wetu wa kusoma alama za nyakati. Ni kama tunafanya upuuzi wajapani waitao shinatako siyo sina tako. Najua waswahili walivyo mabingwa wa kubadili mambo ya wengine wakishindwa kubadilika wao wenyewe. Wenye kupenda kaya waombe Mungu haya mazabe yaendelee uone kama kuna mlevi mkubwa ataendelea na ulevi na matanuzi yake. Wainglishi huita hii to be pennywise and pound foolish. Kama nimechapia nisameheni ila jua mie sikughushi kama wale madaktari uchwara wanaowaibia na kuwachakachua nyie. Mie hanichakachui mtu kabla sijamshukia na kitanzi changu.

Kabla ya kuendelea naleta good news. Mwajua kuwa Pio Msekua naye ni gamba? Juzi jamaa zake na wapingaji walimvua nguo sina hamu. Mie sikuwa nimeinyaka kuwa kumbe yeye ndiye kuwadi wa jamaa wa kimanga wanaotorosha wanyama wetu na kujenga mihoteli ya bei mbaya kwenye maeneo yasiyoruhusiwa! Nilishangaa sana. Si ajabu hata haya mahoteli ya magenge ya mafia na wauza bwimbwi yaliyojazana kwenye beach zetu yameletwa naye. Je hapa kaya haijageuzwa kichwa cha mwendawazimu kwa mlevi kujifunzia kunyolea kama aliyesema mwasisi wa ufisadi huu mzee Ruksa ambaye ana bahati ya kutounganishwa na ufisadi wake? Nani mara hii kasahau kashfa ya Muhunidin Ndongala ambaye aliwahi kuipiga seli Loriondo zama zile za ruksa?

Kwa vile Pio ametajwa na hata chama chake cha mafisadi, nina mpango wa kuhamasisha walevi tumvamie na kumvua nguo ili tumzomee. Zaidi ya hapo kitakachoendelea waweza bunia mwenyewe. Kwani mtu akishavuliwa nguo unategemea kifuate nini? Bakora bila shaka. Kwanini asirambwe bakora iwapo amekuwa akibaka kaya yetu?

Najua hapa rafiki yangu Njaa Kaya ana kibarua kigumu. Maana kila uchao watu wake wanazidi kuvuliwa nguo kuanzia kitegemezi chake, nkewe hata yeye mwenyewe. Hata hivyo mhuni huyu ana bahati. Sijui aliwaroga walevi ama vipi? Maana kwa kaya inavyokwenda alipaswa afanyiwe alichofanyiwa yule imla wa kwa Farao Hoseini Kibarak. Hata hivyo nani ajuaye? Huenda walevi watatia akilini na kuamua kufanya kweli tena bila woga wa kuuliwa. Nani atawapiga watu risasi wakati madevu Mreno Okampo yuko macho? Walevi wasingekuwa mataahira huu ndiyo ulikuwa wakati mwafaka wa kumgeuzia Njaa Kaya na genge lake kibao. Walevi mwanisikia na kunielewa au mnaridhika na kuendelea kuliwa na kaya yenu kubakwa na akina Pio? Ya Pio tuyaache kwa leo.

Tumalizie na wauza wese. Nawapa masaa 24 wapunguze bei ya wese vinginevyo nitawa--- leo chichemi wakajipanga.
Wacha niwahi kufuturu!

Chanzo: Tanzania Daima Agosti 24, 2011.

Monday 22 August 2011

Hivi rais kufuturisha siyo kufuja pesa ya umma?

Rais Dkt.Jakaya Mrisho Kikwete akiwasalimia baadhi ya wakazi wa mji wa Lindi waliohudhuria futari aliyowaandalia jana jioni mjini Lindi
Baadhi ya wananchi na viongozi walioalikwa katika futari iliyoandaliwa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzanian Alhaj Dk Jakaya Mrisho Kikwete,wakichukua chakula katika utaratibu maalum uiloandaliwa huko viwanja vya Ikulu Mjini Zanzibar.(21/08/2011)
Watu wakifaidi futari iliyoandaliwa na ubalozi wa Tanzania mjini London




Ingawa nchi yetu haina dini, watu wake wana dini. Hivi karibuni rais Jakaya Kikwete ameanzisha mchezo mwingine wa hatari ambao, kimsingi, ni kuchanganya siasa na dini. Amekuwa akifuturisha umati wa watu kwenye maeneo mbali mbali ya nchi. Ameishafanya hivyo Dar es salaam Mtwara na Zanzibar. Je ni halali kwa rais kutumia pesa ya watanzania waislamu wasio waislamu na wasio na dini kufuturisha watu wake? Je hii futari anayotoa rais anaitoa kama rais au mtu binafsi? Kwanini hafanyi hivyo nyumbani kwake badala ya ikulu? Je huu nao si ufisadi na matumizi mabaya ya pesa ya umma? Je watanzania wana shida ya futari au mambo mengine muhimu? Rais wa Zanzibar, mkewe hata ubalozi wa Tanzania nchini Uingereza nao wanafuturisha! Kwa pesa ipi na ya nani na kiasi gani? Imefikia mahali futari imekuwa dhihaka kiasi cha wahusika kuwafuturisha hata wasio waislam!
Tunahoji maswali haya si kwa chuki na dini yoyote bali kutaka kuwepo uadilifu na ulinganifu katika matumizi ya pesa ya umma.

Sunday 21 August 2011

Go Gadaffi go

Go Gadaffi go ye Muamar Go without turning thy head back ever The game is up and over sir Go son of hell, a coward in your own light. Go Muamar go down standing like a dolt In flames go down like that In a shame go even faster Go go Abuminyal go go and others will go. Museveni will go Kagame will also go Go leave the mark back. Go like a goon and a stooge. Go the ignoble way go. Go the world will remember you. Just as a symbol of megalomania Go son of man. Go Muamar go. It is time to go. Never look back go Go Gadaffi go It is time to go. Go from thy man-made no-go Go go it's time to go go go go go Don't turn back go! Those that you called rats, Are now coming in scores Who's between you and em a rat? Cornered is you tyrant You are yourself indeed a rat You called em drugged braggarts, Little knowing you are but a rat, You wrongly thought you're smart Cornered is you braggart Go Gadaffi go. Tripoli is a no-go Libya is a no-go It is only to Zimbabwe you can go Go Gadaffi go Go Gadaffi go Go go go!

Friday 19 August 2011

Ngeleja na Malima acha utoto


Kwa wale wenye kufuatia mifumko ya kashfa za mara kwa mara nchini mwetu watakubaliana nasi: baadhi ya watendaji hawana hata chembe ya kujisuta wala nia njema na taifa letu. Wanafanya utoto na kutaka watendewe kama watu wazima wakati ni wa hovyo!

Ukiachia kashfa nyingine nyingi ambapo wahusika hawakuwajibishwa wala kujiwajibisha, kashfa ya hivi karibuni ya kukusanya pesa kwa ajili ya kuhonga wabunge wapitishe bajeti ya hovyo ya wizara Nishati inathibitisha hili. Kwanza, inashangaza kuona hata wabunge walioonyeshwa kama wapokea rushwa wamekaa kimya kuhusiana na kashfa hii! Ilishangaza zaidi pale wabunge walipopitisha bajeti ya wizara ya Nishati wala bila kumtaka waziri William Ngeleja na naibu wake Adam Malima kutoa maelezo ni kwanini walikuwa wakikusanya pesa kwa kisingizio cha kuwahonga wabunge. Je kwa kukaa kimya wabunge wamethibitisha ukweli kuwa pesa iliyokusanywa ililenga kuwahonga na hivyo kuridhia kuwa wao ni wapokea rushwa?

Kabla ya kashfa hii kulikuwa na kashfa ya mauaji ya Arusha ambapo jeshi la polisi liliua wananchi wasio na hatia kwenye mvutano baina ya Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) na Chama Cha Mapinduzi. Ni pale CHADEMA ilitaka kuwahamasisha watanzania nchi nzima waiwajibishe serikali kwa kutoshughulikia ufisadi.

Yalipotokea mauaji ya Arusha wengi walitegemea waziri wa mambo ya Ndani Shamsi Vuai Nahodha na naibu wake na mkuu wa jeshi la polisi wangewajibika kuwajibisha au kwajibishwa. Hawakufanya hivyo. Kadhalika, hawakupoteza muda hata kuomba msamaha zaidi ya kujifanya hayawahusu na kuendelea kung’ang’ania ofisi za umma. Hili lilithibitisha watendaji hawa wasivyothamini utu wala haki za binadamu. Ajabu hata polisi waliofyatua risasi Arusha au wanajeshi waliozembea hawakuchukuliwa hatua! Tunajenga taifa la namna gani lisilo na chembe ya kumbukumbu wala huruma? Ajabu wanaotenda madudu na jinai bado wanaitwa waheshimiwa badala ya wezi, wala rushwa na wauaji wakubwa wasiopaswa kuishi achilia mbali kuwa kwenye ofisi za umma wakiendelea kutapanya mali na pesa vya umma.

Wengi wanaojua jinsi madaraka yanavyotumiwa vibaya nchini mwetu hawakushangaa kilichotekea hasa ikizingatiwa kuwa wahusika huwa hawawathamini watawaliwa zaidi ya kuwachukulia kama punda wa kuwabeba watawala na mizigo yao yaani beasts of burden kwa lugha ya kuazima. Je hali hii itaendelea hadi lini? Je wahusika hawajawateka watawaliwa kiasi cha kuwageuza watumwa na hayawani wanaoweza kuua hata kuibia bila kuwajibika? Je umma uende kwa nani?

Si hilo tu, kabla ya kufufuliwa kwa kashfa tajwa hapo juu kulikuwa na kashfa mbili za ulipukaji wa mabomu yaliyoua watu wasio na hatia maeneo ya Mbagala na Gongo la Mboto. Wahusika wakuu yaani waziri wa Ulinzi, Hussein Mwinyi, naibu wake na mkuu wa majeshi hawakujihangaisha hata kuomba msamaha. Je tunajenga taifa la namna gani iwapo maisha ya binadamu yanaweza kuondolewa kizembe na wahusika wasichukuliwe hatua?

Matukio hayo mawili hapo juu ya mauaji ambalo ni kosa la juu sana katika jamii ya binadamu yalianza kuibua hisia kuwa kuna watu wenye ubia na serikali kiasi cha kutoguswa. Wengi tulidhani huu ungekuwa mwisho lakini wapi! Kumbe wasioguswa au untouchable wako wengi!

Turejee kwenye kashfa ya ukusanyaji pesa ili kuhonga wabunge kupitisha bajeti. Je mawaziri husika wanangoja nini hata baada ya ushahidi mwingine kutolewa kuwa walipewa mgao wa pesa hiyo? Ajabu wahusika, walivyo vichwa ngumu na wenye dharau kwa umma, hawakuhangaika hata kujitetea wala kukanusha kuwa walipewa mgao kupitia kwa wasaidizi wao waliotajwa hata majina! Hivi kuendelea kung’ang’ania ofisi ambazo wameishazichafua licha ya kuwa aina fulani ya ufisadi, wahusika hawajui kuwa wanamwongezea mzigo wa lawama rais aliyewateua? Hivi hawaoni kuwa kutojiwajibisha ni kuzidi kumburuza rais kwenye uchafu wao? Je watu wa namna hii wana heshima yoyote kwa rais ilhali wanaendelea kuhatarisha hadhi yake? Je watu wasio na uwezo mdogo tu wa kuona kosa walilotenda wafaa kuendelea kukaa kwenye ofisi za umma? Wahusika wanaongoja nini kuwawajibisha kama wao hawataki kujiwajibisha? Kwanini tunajenga na kuendelea kulea mazoea haya machafu? Je kama wabunge walioingizwa kwenye uchafu huu wameamua kukaa kimya kwa sababu wajuazo, umma nao unakaa kimya kwa sababu zipi iwapo ofisi na pesa inayochezewa ni vyao?

Yaani watanzania tumejiruhusu kugeuzwa mataahira na vihongwe wa wezi wachache wasio na chembe ya aibu wala utu? Kwa faida na sababu gani? Sitaki kuambiwa kuwa wahusika hawana kosa bali katibu wa wizara ambaye naye amelindwa kwa kisingizio cha kupewa likizo. Unampa likizo mtuhumiwa badala ya kumfikisha mbele ya vyombo vya haki ili iweje? Hakuna mbunge anayehoji ufisadi huu wa kimfumo wa kulindana! Je ina maana kosa la kujipatia pesa kwa nia mbovu ya kuhonga ni la David Jairo pekee yake iwapo yeye alikuwa ofisini kupokea maelezo ya waziri na naibu wake? Kama kosa ni lake, inakuwaje waziri na naibu wake wasimwajibishe kabla ya bomu kulipuka kama hawakuwa wakijua? Kama hawakuwa na habari huu nao si uzembe unaotosha kuwaondoa ofisini? Wako pale na wanalipwa kusimamia nini kama mambo yanaweza kuwapita wakiwa hawana habari? Hata hivyo hapa ukweli ni kwamba Jairo, Ngeleja na Malima lao ni moja.

Tukubali kuwa Jairo amepewa likizo ya lazima ili kuchunguzwa. Na hawa wakubwa zake nao wanangoja nini lau kupata hiyo likizo? Kwanini hatutaki kujifunza hata kutoka kwa majirani zetu pale Kenya. Waziri wa Elimu ya Juu wa zamani William Ruto aliposhutumiwa kujiingiza kwenye kashfa na mwenzake wa mambo ya Nje Moses Wetangula, waliwekwa kando ili kuchunguzwa. Ajabu hawa wakenya wanaoona mbali ndiyo eti tunaungana nao tukitegemea kusonga mbele wakati wao wakisonga mbele sisi tunarudi nyuma!

Hivi mawaziri wa Kenya wakikutana na wetu wataelewana iwapo wakenya wanaangalia maslahi ya umma wakati wetu wanaangalia matumbo yao? Bila kujenga utamaduni wa kujiwajibisha, kuwajibika hata kuwajibishwa Tanzania itaendelea kuwa kichwa cha mwendawazimu kwa kila mafisadi, majambazi, mibaka na wezi kuja kujichotea watakavyo kama shamba la bibi.

Je waziri Ngeleja na naibu wake Malima wanangoja nini iwapo wameishachafuka kiasi cha kutosafishika? Kwanini wanamtwisha rais mzigo wao wa dhambi? Wananchi tutafute jawabu na ufumbuzi kama mamlaka husika zimechemsha kwa sababu na nia wazijuazo.
Chanzo: Dira ya Mtanzania Agosti 16, 2011.

Is this the beginning of the end of Gadaffi?



True, Libya's kicking ass is on the verge of hitting the road if he will be given the chance. Let us put it this way: Muamar Gadaffi has nowhere to go except to the grave. Will America and EU allow him to flee or just seals his fate with bullet? Looking at how things are shaping up, Gadaffi is as good as dead. Let us pray that the tyrant goes down sooner than later to avoid losing many innocent lives.

Thursday 18 August 2011

Tanzania ni sanaa sanaa hadi kiama


The Qatar Emiri Air Force plane through which nearly 140 animals from Tanzania were smuggled from the Kilimanjaro International Airport in November, 2010. (Guardian)


Baada ya kufumka kashfa ya usafirishaje haramu wa mamia ya wanyama kwenda Uarabuni yaliyofanywa na vigogo waliomo serikalini eti serikali inapiga marufuku usafirishaji wanyama nje! Yaani baada ya wao kusafirisha wanyama na kupata dola zao ndipo wanatuletea usanii wa kupiga marufuku usafirishaji wanyama! Hii ni sanaa maalum ya ufisadi na kujitoa kimasomaso. Je watanzania waathirika wako wapi?

Huwa napatwa na majonzi na mshangao kusikia watanzania wakimsifia rais wa awamu ya pili Ali Hassan Mwinyi mwanzilishi wa ufisadi huu pale alipomleta brigedia Ali toka Falme za Kiarabu zama za kashfa ya uuzwaji wa Loliondo. Nani mara hii kawasahau majambazi wakubwa wakiongozwa na mkurugenzi wa wanyamapori wakati ule Muhidin Ndoranga? Nani kasahau kugundulika kwa njama za akina Zakhia Meghji na Seif Khatib waliokuwa wamejigawia miraba ya uwindaji?

Watanzania waguswe wapi ndipo wastuke na kufanya kweli? Kama wengine wameridhika sisi haturidhiki tutazidi kupiga kelele. Tunaamini kuna siku kitaeleweka. Je watanzania wameamua kutochukua hatua kutokana na ukweli kuwa kila mtanzania ni fisadi? Maana ufisadi sasa imekuwa sera na sheria vilivyobarikiwa na watawala na watawaliwa. Saa yetu ya UKOMBOZI itafika lini kufichua yanayofanyika NYUMA YA PAZIA? Mie sielewi. Kituko ni pale waziri mhusika na kashfa hii Ezekiel Maige kumsimamisha kazi mkurugenzi wa wanyamapori wakati naye ni mtuhumiwa na mhusika mkuu!
Kwa kituko hiki SOMA HAPA.

Wednesday 17 August 2011

Is Britain cascading into third “worldness”?


What recently transpired in the UK, unearthed a hidden malady of racism and hypocrisy. We used to believe that the UK is an ideal society that promotes and protects human rights, prosperity and equality. We goofed. UK we used to superficially know is different from the real and true one. Had this happened in Africa, it would be highly touted as revolution and thirsity for human rights. Riots resulting from police shooting, poverty, racism, unemployment, even corruption are mainly experienced in third world countries, which Britain is not.

Indeed, what transpired in Britain recently, especially in the capital city, London, speaks volume. Unrest first flared on Saturday after a peaceful protest in Tottenham over the fatal shooting of a civilian by police.

The Brits and other so-called civilized and developed countries used to cheat us that everything is spiffy. Who knew that racism and inequality are still rife in the UK? Unfairly enough, UK is among countries whose journalists go to third world countries and take nasty photos to show the world how the third world, especially Africa, are still living in pre-adamic era, little knowing that they are living in the same manner and time. If anything, what happened in UK, just like what happened in the US during Katrina mayhem, has opened the eyes of many people in the third world countries.

Tottehnham, the black spot of poverty, was the core and trigger of this entire imbroglio. All this, despite the police shooting dead a civilian, resulted from pent-up anger against the government that has always ignored inequality among the citizens. Areas occupied by poor people, understandably, are not taken care of. There is no policing in their areas compared to affluent ones. This is why rioters went on a rampage.

Poverty and unemployment are swelling as the authorities slash social benefits under the pretext of having no money. People do not subscribe to this. They query, how can government say it does not have enough money, whereby the monarch just recently extravagated millions on nuptial party of the grandson of the queen? What if this money would have been chanelled to the needy in lieu of making meriments?

Questions are many more than answers. How the authorites are able to feed the whole nation of queen’s clan they take care of at the tune of millions by just bilking money out of treasurer? Is Britain cascading into third worldeness it created? Currently the economy of Britain is on the standstill. Unemployment is rife, not to mention social and cultural rot resulting from decay of the whole system governing Britain.

When unrest broke out in London, before spreading to other regions, police termed it as just mere criminality. Looking at the core of this unrest, one finds that it’s nothing but inequality and uneven distribution of wealth. If what police termed as criminality, indeed the criminal is more a state than the citizenry. Police and politicians pleased themselves for the while before things got out of control. They thought the riots would be contained in the poor areas. When the riots broke up in Camden where the rich live, police found themselves with nothing to do.

If you mention Islington, Hackney, Croydon, Clapham Junction, Peckham, Lewisham, Stratford and Ealing, you mean poor communities by European standards.

Though Britain is regarded as the mother of democracy, looking at how things are unfolding, the citizenry is now tired of monarch and the way it exploits them, not to mention a do-nothing government that has always turned a blind eye on racism. The monarch is stinking to the core. It is getting older and older by days so as to force the citizenry to start the beginning of the end of it.

Those who are aware of the difference between who haves and who have nots noticed that London has been under fire for long save that the fire that was burning it was anger but not real fire. Now that the anger of the poor has exploded, should we expect to see the more flames? Politicians on behalf of the monarch need to put their acts together. True, what is going on can be contained. But again, the cracks on the monarchy are now visible and tangible.

Looking at much force employed by the government, African dictators are laughing the all way home. For this gives them a pretext of butchering their people who will think taking to the street to demand they be kicked out. In Uganda Yoweri Museveni, as well as Paul Kagame in Rwanda, they are laughing heartedly.

The difference between police and the way they sometimes act in Africa and Britain, is the fact that not all police are motivated to take on rioters-cum-looters as we all evidenced in London. This was evidenced when people looted whatever they put hand on as police witnessed. Nick Davidson said: “We’ve had enough of police just standing there while people are looting and ruining the whole area. Everybody here pays taxes and has had enough of it. We’re sickened by police doing absolutely doing nothing.”

Importantly, it must be noted. When demonstrators in Egypt used social media to bring down their long time strong man, the west was laughing and chestbeating that this is the tool that will emancipate third world. Unfortunately for them they were not aware that the same can be used against them. Riots in Britain is said to have succeeded due to the use of social network as it was in Egypt.

Again, being sacred lamb, Britain is no longer saying that social media is the tool of emancipation. Instead politicians and police were calling the new wave of protest thuggary and criminality. If it were in Africa, it would be referred to as revolution. What double standard under the sun!
Is UK cascading into third worldness it created? Time will surely tell.

Source: African Spear Toronto.

Tuesday 16 August 2011

Kwenda visiwani pasipoti tena!


Mbunge wa viti maalum, Mwanamrisho Taratibu Abama (CUF), hivi karibuni aliitaka serikali kurejesha utaratibu wa watu kutoka Tanzania Bara kuingia visiwani Zanzibar kwa paspoti ili kupunguza wimbi la ujambazi na mauaji linazidi kuongezea siku hadi siku.

Kauli hii ya kibaguzi na kashfa, licha ya kuwakasirisha na kuwasikitisha wenye akili, iliwashangaza wengi. Huyu mbunge anapata wapi jeuri ya kutoa matamko ya kibaguzi tena kwenye bunge la muungano? Nini mantiki ya Tanzania kupigana na kaburu kuondoa utawala wa kibaguzi kusini mwa Afrika yaani Apartheid? Je huyu mbunge anaijua historia ya taifa hili kwenye kupinga dhuluma naubaguzi? Kweli huyu mbunge ni mtanzania au wa kuja?

Ajabu, Abama alitoa kauli hii bungeni na bunge halikulaani ubaguzi na matusi haya kwa wananchi wote wa Bara akiwamo rais wa jamhuri ya Muungano. Pia hakuna mbunge aliyejitokeza kumuelimisha huyu mbunge ambaye uwezo wake wa kuelewa mambo ya kawaida achia mbali sheria unatia shaka. Ni hatari kwa mtu mwenye wadhifa wa ubunge kuwa na roho ya kibaguzi na hitimisho la jumla bila kuchelea nafasi yake. Kwanini Abama hataki kukubali ukweli kuwa kwenye nchi moja si rahisi wala haki watu wa upande mmoja kubeba pasipoti kuingia upande wa pili? Kwanini Abama hataki kukubali kuwa hata watu wa visiwani wanaweza kuwa tishio kwa mstakabali wa bara hasa ikizingatiwa kuwa wamejazana na kuzaliana bara kuliko hata Zanzibar? Hivi tukianza kuulizana nani ni nani katika nini kati ya bara na visiwani nani ataathirika hata kuadhirika ukiachia mbali kujua nani anamhitaji nani?

Kwanini Abama na wenye mawazo kama yake hawataki kusoma alama za wakati na kuuangalia ukweli kuwa bara imekuwa kimbilio la watu wengi wa visiwani wasio na pa kushika huko kwako? Kwanini ni halali kwa watu wa visiwani kuja bara, kufanya biashara na kuzaliana na kuneemeka lakini ikawa haramu hata kwa watu kiduchu wa bara walioko visiwani kuishi kama raia yoyote kwenye nchi yake?

Matamshi haya ya kijinga ya Abama yanathibitisha wazi kuwa hata uchomaji wa vibanda vya wafanya biashara toka bara una Baraka za baadhi ya wakubwa visiwani. Nani mara hii kasahau hotuba za chuki zilizokuwa zikiendeshwa na shehe mmoja aitwaye Azzan ambaye ukimtazama ni mwarabu kwa kila kitu? Mpuuzi huyu alikuwa akimtuhumu makamu wa rais Dk Gharib Bilal kuwa anataka kuigawa visiwani kwa bara. Kwa walioona alivyojibiwa kwenye jamii forum wachangiaji wakimtaka arejee kwao Oman akawagawe na kuwabagua huko watajua hasira walizo nazo wananchi dhidi ya ubaguzi huu. Ajabu mhusika hata akienda huko Oman hawatampokea zaidi ya kumuita Abdi yaani mtumwa wa kawaida! Watu wameshiba matunda ya muungano sasa wanaanza kuutapikia. Kama kuna watu wanauhitaji muungano zaidi si wengine bali visiwani. Maana bara nchi yenye ardhi kubwa na kila aina ya maliasili ahihitaji kijipande cha ardhi kisicholingana na hata baadhi ya wilaya zake ndogo. Hayo tuyaache. Ila tutahadharishe. Tukianza kuchokoana kama pweza wapo watakaoamsha hasira za akina Christopher Mtikila na kuanza kujilaumu. Kuna haja ya watawala wetu kuwakemea hata kuwatimua watu kama Abama ambao uwezo wao wa kufikiri unatia kila aina ya shaka.

Tukianza kuulizana asili yetu kuna wazanzibari ima watajikuta ni wamalawi, wacongoman, waarabu hata wahindi kiasi cha kutostahili kuishi hapo wanapopaona na kupaita kwao. Dhambi ya ubaguzi huwa haiachi kumg’ata mwenye kuitenda. Pia ni upofu na upogo kwa watu kuwekeza kwenye ubara na upwani. Maana kama tukianza changu kichungu chako kichungu tutaumbuana kiasi cha baadhi ya wenzetu kuathirika kabla yaw engine. Au ni kwa vile Abama ni mwanachama wa CUF chama ambacho siku zote kimekuwa na harakati za kichinichini za kuvunja muungano ili kiitawale Zanzibar?

Abama ni mbunge wa viti maalum ambaye hamwakilishi yoyote isipokuwa chama chake na tumbo lake. Hii ndiyo hasara ya kuwagawia watu ubunge kama ubuyu kwa kuangalia vyama na maslahi binafsi hata jinsia. Wabunge wa namna hii licha ya kutokuwa na uhalali na uwezo ni mzigo kwa walipa kodi. Wanakula bure kiasi cha kujipayukia watakavyo kwa vile wamefika pale kwa bahati. Nchi zenye demokrasia iliyokomaa hawana viti maalum bali mazingira sawia ya kuwania nafasi za uongozi.

Tumuulize Abama. Je wabara ndiyo wezi pekee duniani na wazanzibri malaika?
Je wazanzibari wanaoishi bara na kufanya mambo machafu nao waingie bara kwa paspoti?
Je wabara wakitaka wazanzibari wanunua visa ya kuishi bara wataona haki? Je mbunge ana habari kuwa bara inatunza kulisha na kwa kila wazanzibari wengi kuliko huko visiwani? Bila shaka mbunge, Abama yote haya sema ameamua kutafuta umaarufu naye ajulikane yupo bungeni. Si hilo, huyu mbunge anapaswa achunguzwe akili zake. Maana ukiangalia anavyofaidi marupurupu ya ubunge kwenye bunge la bara wakati huko kwao hatuna hata chembe ya mbunge, shurti awe ima ni mbaguzi mhafidhina au asiye na akili timamu. Tukianza kubaguana kwa tunakotoka, kuna watu wataiona dunia chungu kuliko hao wabara.

Okey wabara ni wezi. Na huo mpunga na ardhi vyao je? Kama wabara ni wezi kiasi cha kutishia usalama wa Zanzibar mbona mhusika anapata nafasi ya kuja bara kwenye bunge na kufaidi posho za makalio na kupayuka kama alivyofanya na asidhulike? Jamani tuache ulimbukeni wa kujiona bora kuliko wengine. Huu, licha ya kuwa ulimbukeni ni utoto na utovu wa nidhamu kuhukumu watu wa asili yao kama alivyofanya Abama. Hakika anapaswa kulaaniwa sin a waandishi wala watu binafsi tu bali bunge na serikali Au ni yale ya baniyani mbaya kiatu dawa? Au ni yale ya changu changu chako changu.Tujaribu kwa watu na wenye shukrani na kumbukumbu. Bila muungano Zanzibar itageuka Comoro nyingine. Na hao wabara mnaowachukia watakuja huko na mitutu ya bunduki kulinda amani mtakapoanza kupinduana kwa uhizbu afro na upemba na uzanzibari.

Hisia na mawazo mgando ya kubebeshana passports kwenye nchi moja hayawezi kutufikisha popote. Kama wapemba nao watataka wazanzibari wabebe passport kuingia Pemba kutokana na udogo wa kisiwa chao wazanzibari watasemaje?

Tuhitimishe kwa kumtaka Abama aombe msamaha huku bunge likimuonya hata kumshughulikia ipasavyo. Abama hafai kuwa hata mlinzi achia mbali mbunge kama ni mbaguzi kiasi hik
i.
Chanzo: Dira ya Mtanzania Agosti 16, 2011.


Pumba za Mlevi Mdanganyika

NIMEGUNDUA DAWA YA KUUA INZI

Baada ya kuona inzi wamezidi kuongezeka wakichafua kila kitu, nimejipa kazi ya kupambana nao. Nimeamua kufanya hivi ili kunusuru maulaji ya walevi. Kwa wale ambao hawajawahi kufikia Uwanja wa Fisi tunapojichana mapupu, utumbo au amfitifi kwa lugha nyingine na maulaji mengine, kuna inzi kweli kweli. Hivyo basi nimeamua kuchonga rungu ili niwasambaratishe inzi. Nimeamua kuchonga rungu kuepuka kutumia doshi kununua nyundo. Hivyo lazima nibane matumizi hata kama wadanganyika hasa wanywa gongo hawafanyi hivyo kama serikali yao. Naonya. Msianze sema eti nafanya uchochezi. Hasha. Nani hajui kuwa nchi hii inaliwa na kila fala kwa namna na wakati atakao? Anayebishia hili ajiulize mantiki ya kampuni la Usafiri Bongo and Around (UBA) limeuzwa kwa kabilioni kamoja wakati thamani yake ni mibilioni 12? Hii akili au matope? Huu ujanja au ujambazi mbuzi na ufala? Hivi hawa wanaouza mali ya umma kama njegere wana tofauti gani na inzi? Najua maswali yangu magumu kwa mtu mwenye akili ya kawaida kutokana nami kufikiri kigongo gongo na kibangi bangi. Sikupenda kuwa mnywa gongo wala mvuta bangi. Wanaouza mimali ya umma kwa manufaa binafsi ndiyo wamenifanya niwe mvuta bangi na mnywa gongo. Maana hii hunisaidia kuepuka kujinyonga ukiachia kunipa stimu ya kupanga kuwatokea siku moja na kuwabomoa sura zao kwa chupa za gongo.

Turudi kwenye inzi hawa wachafu kama wale niliotaja hapa juu. Si wanafanya ufska wao kiasi cha kujisahau na kudondokea kwenye kanywaji kangu wanadhani nitawaacha. Hawa hawana tofauti na akija Devil Jero Jeuri waliofanya ufuska wao na kuangukia mjengoni. Ingawa wao wamelindana na kupumzishana. Mie hawa inzi wangu nawapiga rungu bila kujali ni wadogo au hayawani. Kwanini niwavumilie inzi wakati wanakunya kila mahali kuanzia chooni hadi kwenye sahani?



Inzi ni wadudu wachafu na hatari sana. Wanaambukiza watu kipindupindu. Kwa wale inzi watu wanaambukiza watu ugonjwa wa kipindupindu mifukoni hata akilini. Nani atakuwa na akili timamu wakati muda wote anafukuzia gongo na ndururu lau aishi? Ni wangapi wamegeuka vibaka na vyangudoa bila kusahau matapeli kutokana na hali hii?

Mie nawachukia inzi wawe hayawani au vinginevyo. Wanakunya hata ikulu hawana adabu hawa tena wanaitana na kupatia uchafu. Hawajui hii ni ofisi tukufu ya rais ambayo Mchonga aliita patakatifu pa patakatifu ingawa inzi wamepafanya pawe pachafu pa pachafu!

Waarabu humuita inzi au afananaye naye Dhubab dhakar yaani mchafuzi wa kila kitu kwa lugha ya kimakonde. Huruka na kutua juu ya yule na kufanya ufuska wake hapo hapo humdandia mwinginie hivyo hivyo hadi anakufa. Wakati akifanya ufuska wake hasahau kunya hovyo hovyo. Huyu ni dhubab dhakar, marhun mkubwa.

Kweli wakati wa Mchonga hapakuwa na inzi ikulu hata kama walikuwapo walikuwa kidogo. Wengine wanasema eti ni kwa sababu nchi ilikuwa imefilisika kiasi cha kukosa ulaji wa kukaribisha mainzi. Yawezekana ni kweli. Ila alipoingia Ali ndiyo usiseme. Inzi walianza kualikana na kujazana kila sehemu. Wanaopamba utawala wanasema eti inzi waliongezeka kipindi cha Ali kutokana na ruksa ambapo ulaji mwingi ulitengenezwa kiasi cha kukaribisha hata kunguru wa india na inzi. Mara alipoondoka wakazidi kuzaliana na hatimaye kujazana zaidi na zaidi. Lazima tufanye mpango wa kupasafisha mahali hapa. Najua rais hapendi uchafu. Naamini ataniunga mkono kusafisha ikulu. Nitamwandikia barua ya kumtaarifu kuwa nakwenda kule kuwapigilia mainzi mbali kwa rungu langu. Mie sihitaji ufagio uchwara na wa uongo wa chuma.

Ukienda Baa unakuta mainzi. Kwenye dala dala nako inzi. Ukienda Airport yamejazana mainzi. Kwenye mbuga za wanyama ndiyo usiseme. Jamani! Kila mahali inzi! Jamani inzi mbona wanatusumbua hasa sisi walevi. Ukinunua mapupu utamuona katua achukue kitu kidogo. Ukikatisha barabarani yuko mgongoni mwako akitaka kitu kidogo. Ukienda maofisini kila unachofanya inzi yupo mgongoni hata mbele yako akitaka kitu kikubwa! Mwe! Jamani nyie inzi mmetumwa na nani yarabi? Mainzi yanapanda hata mashangingi! Haya yatakuwa yanafaidi kodi yetu. Lazima tuyasafishe kuanzia Igunga, Monduli, Bariadi, Chalinze hadi Mara na kwingineko.

Hakuna wanyama na wadudu nawachukia kama kunguru na inzi. Maana, kila unapokwenda kuna inzi. Ukinunua bia yako huyo! Kaisha tua na kuanza kufanya ufuska wake. Tena naona lile inzi lina kitambi utadhani jiheshimiwa! Linavyorukaruka hapa na pale utadhani linafanya kampeni ya kugombea ulaji wa bure ambapo hata makalio hulipwa posho. You houseflies, get out of the house. We are tired of you really. What a heck you are causing!

Kwa vile inzi hawaelewi lugha rahisi, nimeamua kuchonga rungu la kilo kumi ili nitakapowaona natwanga bila kujali kama nitavunja vyombo au nini. Hii ni kweli na si hadithi za Abunwasi wala Alinacha. Mie nitafanya kweli bila kujali nani atachukia wala nini.

Kwanini mainzi yanenepeana wakati walevi tunakondeana wakati yanakula jasho letu? Naona hata kunguru nao wananenepeana utadhani hii nchi ni yao! Kwanini tunafuga wanyonyaji hawa tena wachafu? Yaani tumegeuka jamii ya kunyonywa! Jana baada ya kutoka kupiga gongo nikajitupa kwenye kitanda changu cha kamba. Mbu walivyonishambulia sina hamu. Hii ikiongezewa na kiza na joto ndiyo usiseme. Hata kile kiyoyozi yangu chapa Mzaramo sijui kiliibiwa na nani? Maana sisi wanywa gongo kiyoyozi chetu si kingine bali feni ya mkono.

Mainzi yanavyozaliana siku hizi sina mfano. Kila siku utaona hili likiibuka pale na jingine kule. Kwanini yasipange uzazi? Lo! Sasa naanza kuchanganya! Kwanini mainzi yapange uzazi wakati uchafu upo jaro na yanakula bure? Kwa vile sijapata gongo tangu asubuhi, wacha nitimke kwa mama Betty nikaongeze mafuta tayari kukabiliana na inzi. Inzi mpo? Kaa chonjo bwana rungu naja. Sitaangalia rangi wala ukubwa. Inzi ni inzi kila nitakapomuona natwanga. Laiti wanywa gongo wote wangekuwa na moyo mkubwa kama wangu!

Chanzo: Dira ya Mtanzania Agosti11, 2011


Sunday 14 August 2011

Je Wabunge kweli ni wala rushwa wakubwa?

Waziri wa Nishati na Madini William Ngeleja na Naibu wake Adam Malima, wakipongwezwa na wabunge mbalimbali baada ya kupitishwa kwa Makadirio ya Bajeti ya Wizara yao ya mwaka wa fedha 2011-2012 jana mjini Dodoma
Hao ndege wana tofauti gani? Tofauti utakayopata ndiyo tofauti kati ya wabunge wako na wala rushwa.


Baada ya bunge kupitisha bajeti ya wizara ya Nishati bila kupingwa, wenye akili wamejiuliza swali moja kuu: Je ni kweli zile pesa alizokuwa akitaka kuchangisha katibu mkuu wa wizara aliyesimamishwa kazi David Jairo kweli zililenga kuwahonga? Kama ni vinginevyo, inakuwaje wapitishe bajeti ya wizara iliyotoka kuwahonga bila hata kuhoji shutuma hizi?

Wengi wanajiuliza ni kwanini wabunge, kama kweli siyo kutaka kufunika kombe mwanaharamu apite, hawakutaka waziri mhusika William Ngeleja na naibu wake Adam Malima wawajibishwe?

Je hii haiwezi kuchukuliwa au kutafsiriwa kuwa lao ni moja? Picha hiyo hapo juu inaweza kukupa picha halisi ya ndoa hii ambayo wakosoaji wanaiona kama ya wala rushwa wakubwa wa nchi yetu. Inakuwaje wampongeze? Wanampongeza Ngeleja na naibu wake kwa lipi kama wizara yake ilitaka kuwasingizia kuwa ni wala rushwa? Je wabunge wetu si wala rushwa wanaopitisha bajeti za hovyo baada ya kupewa chochote kitu? Wapo wanaoona kama hali ni hii tumekwisha na bunge hatuna bali klabu ya wala rushwa. Wako wapi wabunge wa upinzani?

Saturday 13 August 2011

Namna hii matajiri wetu hawana sababu kutaabika


Mankind has dreamt of a flying car for decades, and while most fictional examples appear to use futuristic hover technology, the engineers of Terrafugia have taken a decidedly more practical approach. The company's Transition aircraft has just received approval from the Department of Transportation and is slated to enter commercial production later this year. Taking proven aircraft technology and adapting it for road use has created a craft that performs admirably in both scenarios.

The Transition features folding wings that allow it to go from plane to highway cruising machine in just seconds. A few exceptions have been made in order for the vehicle to squeak by certain safety requirements. The craft's beefy curb weight — much of it due to road safety features — has been scrutinized, as has its polycarbonate windows which are considerably thinner than standard automotive safety glass.

Terrafugia was founded in 2006 by graduates of MIT, with the sole purpose of developing a "roadable aircraft," i.e. a flying car. The Transition is the fruit of the company's labor, and has already taken to the skies to prove its worth. The craft will be offered for sale in late 2012 with an estimated price tag of $250,000. If Terrafugia's plans come to fruition, it will be the first commercially available vehicle that can not only drive to an airstrip, but take to the skies as well.
For more on science's advancement just PRESS HITHER.

Chanzo: Internet.

Thursday 11 August 2011

Wizi UDA tutaendelea kuwa shamba la bibi hadi lini?




Taarifa kuhusu ufisadi na utata wa ubinafsishaji lililokuwa Shirika la Usafiri Dar es Salaam (UDA) zinatia kinyaa ukiachia mbali kuwa onyo kwa serikali kuwa wakati wa kuwashughulikia wezi ni huu. Habari toka bungeni ni kwamba UDA iliuzwa kwa shilingi 1, 200,000,000 wakati thamani yake ni mara kumi ya hii yaani shillingi 12, 000,000,000.

Utata ulizidi kuongezeka baada ya kugundulika kuwa kigogo mmoja ambaye ni mmojawapo wa viongozi wa wazee wa Dar es Salaam alikutwa akiwa amepewa shilingi 250,000,000 kwenye akaunti yake. Huu jamani ni ujambazi wa mchana hata kama unafanywa na watu wakubwa kwa kutumia kalamu. Je hawa wezi wanapata wapi hii jeuri ya kututenda hivi wakati mamlaka zikipata kigugumizi kuwashughulikia? Kazi ya mamlaka ni nini kama mali za umma zinaibiwa na fedha kuchotwa kila uchao?

Mbunge wa Mafia (CCM), Abdulkarim Shah alisema haiwezekani UDA yenye rasilimali za sh bilioni 12 ziuzwe kwa sh bilioni 1.2 kwa Kampuni ya Simon Group ambayo ununuzi wake wa hisa umegubikwa na mizengwe.

Shah alikaririwa akisema: “Mheshimiwa Mwenyekiti ni aibu kusikia shirika hili linauzwa ni aibu, kamata wote waliohusika kuliuza, Meya, Mkurugenzi wa Jiji, bodi yote kamata halafu Takukuru wafanye kazi yao.

Shah aliongeza: “Unakwenda kuuza terminal ya Kurasini, ni aibu, nasema Wallahi Wabilahi na Ramadhani hii, sintokubali, nasema watu hawa wawekwe ndani na wachunguzwe.

Je ushauri wa mbunge utafanyiwa kazi? Je ni wabunge wangapi wana mawazo kama haya ukiachia mbali wananchi wanaowawakilisha? Je tutaendelea kuwa shamba la bibi hadi linin a kwanini? Je wahusika kipindi hiki watafanya mambo tofauti au ni yale yale ya business as usual katika kulindana na kuokoana kwenye ufisadi na dhuluma kwa taifa?

Nchi yetu imegeuka shamba la bibi na wananchi wanaendelea kugeuzwa mataahira kila uchao. Nani mara hii kasahau kashfa ya Kiwira kuuzwa kwa shilingi 70, 000,000 kwa rais mstaafu Benjamin Mkapa, familia yake na marafiki zake ilhali thamani yake halisi ni bilioni 4,000,000,000? Tuliambiwa tumuache mzee Mkapa apumzike baada ya kuambiwa ana kinga kisheria. Je huyo mkewe, watoto wake na marafiki zake nao wana kinga ya urais ule ule wa Mkapa? Kwanini hatukuelezwa mapema kuwa kinga ya urais ni suala la kifamilia na marafiki? Kwanini hatuambiwi kuwa siku hizi urais wa Tanzania ni wa ushirika na si suala mtu mmoja tuliyemchagua na kumlisha kiapo kama inavyosema katiba? Wengi watajiuliza maswali yote haya ni ya nini.

Baada ya Mkapa kubainika kuwa alijitwalia Kiwira kinyume cha sheria nini kilifanyika zaidi ya kupigwa siasa na wananchi kusahau wakaendelea kusota kwa kulanguliwa umeme na mgao wa umeme? Nani mara hii kasahau kadhia iliyouawa kimya kimya ya Katibu Tawala zamani wa Mkoa kilimanjoro, Hilda Gondwe, kujiuzia gari aina ya Toyota Land Cruiser VX lililokuwa limenunuliwa miaka mitatu iliyopita kwa sh 155,000,000 kwa shilingi milioni kumi? Je mhusika alifanywa nini zaidi ya wahusika kutopoteza hata muda kujibu achia mbali kumchukulia mtuhumiwa hatua? Je ni magari au mali kiasi gani vya umma vimeishapotea kwenye mazingira kama haya nchi nzima na kwa muda wote tangu ufisadi uanze kuwa order of the day?

Nani kasahau ujenzi wa nyumba za TANESCO kwa mabilioni na hakuna ambaye amewaki kukamatwa wala kuhojiwa ukiachia mbali kupiga kelele na hatimaye kunyamaza? Nani mara hii haoni madudu ya waziri wa sasa wa Nishati na naibu wake walivyotaka kujipatia pesa kwa kisingizio cha kuwahonga wabunge wapitishe bajeti yao ya kimazabe? Na tunaambiwa wamekuwa wakifanya hivyo kwa muda mrefu. Nani kasahau utengaji wa mabilioni ya shilingi kila mwaka kukarabati ikulu? Je ni ikulu gani hii inayokarabatiwa kila uchao utadhani tunaishi mwisho wa dunia kwenye mabarafu? Hapa hatujaongelea nyumba za umma zilizonyakuliwa na wakubwa.

Ajabu katika bajeti ya bajeti ya wizara ya Ujenzi ya 2011/2012 huu shilingi 1,899,600,000 zimetengwa kwa ajili ya ujenzi za majaji wakati shilling 949,800,000 zikitengwa kwa ajili ya ujenzi wa nyumba za OCD, DSO, DAS na DMO kwnye wilaya sita! Je kwa uhaba wa namna hii wa nyumba nini mantiki ya wakubwa kugawana nyumba za umma?!

Ajabu ya maajabu hakuna anayeulizia mantiki ya kujenga nyumba nyingine wakati zile za umma ziliishia kugawanwa na wezi fulani wenye madaraka! Hapa hatujaongelea wizi wa iliyokuwa benki ya taifa ya NBC au wale majambazi wa Net Group Solution walioshirikiana na wezi wetu kufilisi TANESCO. Badala yake tunaendelea kuugeuza mgao na kulanguliwa umeme na mafuta vitu vya kawaida ambavyo hatuna budi kuishi navyo na kuvizoea! Shamba la bibi bila shaka. Nani kamroga nani na lini na hadi lini? I have no idea.

Kwa ufupi, ukiamua kuorodhesha wizi uliofanyika nchini kwa miaka kumi, unaweza kujaza msahafu. Pia utagundua kuwa nchi yetu ni tajiri wa kutupwa yenye kutawaliwa na wezi wa kutupwa kwa kutengeneza maskini wa kutupwa wanaounga mkono wizi huu wa kutupwa.

Turejee kwenye kashfa na ujambazi wa UDA. ATC imechezewa, TRC kadhalika. Je wabunge wataishia kupiga kelele na kujinyazia au kunyamazishwa au watafanya kweli kama walivyofanya kwenye kashfa ya Richmond? Je spika wa sasa ambaye ameonyesha anaegemea upande gani atawawezesha kushughulikia uchafu huu? Je watuhumiwa ambao ni wazito watatimuliwa maofisini na kuchunguzwa mara moja? Maana wanajulikana na majina yao yametajwa wazi wazi ingawa baadhi yao wameishaanza kuzusha tuhuma kwa waliowatuhumu ili kupoteza muda na kuuchanganya umma usiwashughulikie.

Kama tulivyoanza, swali kuu bado halijajibiwa. Je nchi yetu itaendelea kugeuzwa shamba la bibi wakati waathirika tukiangalia hadi lini? Nani wa kulaumiwa kati ya wananchi wasiochukua hatua na baadhi ya watawala wao wezi? Je uwajibikaji wa wahusika ni kurusha tuhuma kwa wenzao au kujiweka kando ili uchunguzi huru ufanyike? Ni vizuri watuhumiwa wakaanza kujiwajibisha ndipo wanaowatuhuma baada ya kuwatuhumu wao nao wafuatie. Je mamlaka zitaendelea kufumba macho na kuziba masikio kana kwamba hii hujuma haiwahusu? Kazi yao ni ipi kama hatawachukulia hatua watuhumiwa? Tuguswe wapi ndipo tustuke jamani?

Chanzo: Dira ya Mtanzania Agosti 11, 2011.

NIMEGUNDUA DAWA YA KUUA INZI

Pumba za Mlevi Mdanganyika

Baada ya kuona inzi wamezidi kuongezeka wakichafua kila kitu, nimejipa kazi ya kupambana nao. Nimeamua kufanya hivi ili kunusuru maulaji ya walevi. Kwa wale ambao hawajawahi kufikia Uwanja wa Fisi tunapojichana mapupu, utumbo au amfitifi kwa lugha nyingine na maulaji mengine, kuna inzi kweli kweli. Hivyo basi nimeamua kuchonga rungu ili niwasambaratishe inzi.

Nimeamua kuchonga rungu kuepuka kutumia doshi kununua nyundo. Hivyo lazima nibane matumizi hata kama wadanganyika hasa wanywa gongo hawafanyi hivyo kama serikali yao. Naonya. Msianze sema eti nafanya uchochezi. Hasha. Nani hajui kuwa nchi hii inaliwa na kila fala kwa namna na wakati atakao? Anayebishia hili ajiulize mantiki ya kampuni la Usafiri Bongo and Around (UBA) limeuzwa kwa kabilioni kamoja wakati thamani yake ni mibilioni 12? Hii akili au matope? Huu ujanja au ujambazi mbuzi na ufala? Hivi hawa wanaouza mali ya umma kama njegere wana tofauti gani na inzi? Najua maswali yangu magumu kwa mtu mwenye akili ya kawaida kutokana nami kufikiri kigongo gongo na kibangi bangi. Sikupenda kuwa mnywa gongo wala mvuta bangi. Wanaouza mimali ya umma kwa manufaa binafsi ndiyo wamenifanya niwe mvuta bangi na mnywa gongo. Maana hii hunisaidia kuepuka kujinyonga ukiachia kunipa stimu ya kupanga kuwatokea siku moja na kuwabomoa sura zao kwa chupa za gongo.

Turudi kwenye inzi hawa wachafu kama wale niliotaja hapa juu. Si wanafanya ufska wao kiasi cha kujisahau na kudondokea kwenye kanywaji kangu wanadhani nitawaacha. Hawa hawana tofauti na akija Devil Jero Jeuri waliofanya ufuska wao na kuangukia mjengoni. Ingawa wao wamelindana na kupumzishana. Mie hawa inzi wangu nawapiga rungu bila kujali ni wadogo au hayawani. Kwanini niwavumilie inzi wakati wanakunya kila mahali kuanzia chooni hadi kwenye sahani?

Inzi ni wadudu wachafu na hatari sana. Wanaambukiza watu kipindupindu. Kwa wale inzi watu wanaambukiza watu ugonjwa wa kipindupindu mifukoni hata akilini. Nani atakuwa na akili timamu wakati muda wote anafukuzia gongo na ndururu lau aishi? Ni wangapi wamegeuka vibaka na vyangudoa bila kusahau matapeli kutokana na hali hii?
Mie nawachukia inzi wawe hayawani au vinginevyo. Wanakunya hata ikulu hawana adabu hawa tena wanaitana na kupatia uchafu. Hawajui hii ni ofisi tukufu ya rais ambayo Mchonga aliita patakatifu pa patakatifu ingawa inzi wamepafanya pawe pachafu pa pachafu!

Waarabu humuita inzi au afananaye naye Dhubab dhakar yaani mchafuzi wa kila kitu kwa lugha ya kimakonde. Huruka na kutua juu ya yule na kufanya ufuska wake hapo hapo humdandia mwinginie hivyo hivyo hadi anakufa. Wakati akifanya ufuska wake hasahau kunya hovyo hovyo. Huyu ni dhubab dhakar, marhun mkubwa.

Kweli wakati wa Mchonga hapakuwa na inzi ikulu hata kama walikuwapo walikuwa kidogo. Wengine wanasema eti ni kwa sababu nchi ilikuwa imefilisika kiasi cha kukosa ulaji wa kukaribisha mainzi. Yawezekana ni kweli. Ila alipoingia Ali ndiyo usiseme. Inzi walianza kualikana na kujazana kila sehemu. Wanaopamba utawala wanasema eti inzi waliongezeka kipindi cha Ali kutokana na ruksa ambapo ulaji mwingi ulitengenezwa kiasi cha kukaribisha hata kunguru wa india na inzi. Mara alipoondoka wakazidi kuzaliana na hatimaye kujazana zaidi na zaidi. Lazima tufanye mpango wa kupasafisha mahali hapa. Najua rais hapendi uchafu. Naamini ataniunga mkono kusafisha ikulu. Nitamwandikia barua ya kumtaarifu kuwa nakwenda kule kuwapigilia mainzi mbali kwa rungu langu. Mie sihitaji ufagio uchwara na wa uongo wa chuma.

Ukienda Baa unakuta mainzi. Kwenye dala dala nako inzi. Ukienda Airport yamejazana mainzi. Kwenye mbuga za wanyama ndiyo usiseme. Jamani! Kila mahali inzi! Jamani inzi mbona wanatusumbua hasa sisi walevi. Ukinunua mapupu utamuona katua achukue kitu kidogo. Ukikatisha barabarani yuko mgongoni mwako akitaka kitu kidogo. Ukienda maofisini kila unachofanya inzi yupo mgongoni hata mbele yako akitaka kitu kikubwa! Mwe! Jamani nyie inzi mmetumwa na nani yarabi? Mainzi yanapanda hata mashangingi! Haya yatakuwa yanafaidi kodi yetu. Lazima tuyasafishe kuanzia Igunga, Monduli, Bariadi, Chalinze hadi Mara na kwingineko.

Hakuna wanyama na wadudu nawachukia kama kunguru na inzi. Maana, kila unapokwenda kuna inzi. Ukinunua bia yako huyo! Kaisha tua na kuanza kufanya ufuska wake. Tena naona lile inzi lina kitambi utadhani jiheshimiwa! Linavyorukaruka hapa na pale utadhani linafanya kampeni ya kugombea ulaji wa bure ambapo hata makalio hulipwa posho. You houseflies, get out of the house. We are tired of you really. What a heck you are causing!

Kwa vile inzi hawaelewi lugha rahisi, nimeamua kuchonga rungu la kilo kumi ili nitakapowaona natwanga bila kujali kama nitavunja vyombo au nini. Hii ni kweli na si hadithi za Abunwasi wala Alinacha. Mie nitafanya kweli bila kujali nani atachukia wala nini.

Kwanini mainzi yanenepeana wakati walevi tunakondeana wakati yanakula jasho letu? Naona hata kunguru nao wananenepeana utadhani hii nchi ni yao! Kwanini tunafuga wanyonyaji hawa tena wachafu? Yaani tumegeuka jamii ya kunyonywa! Jana baada ya kutoka kupiga gongo nikajitupa kwenye kitanda changu cha kamba. Mbu walivyonishambulia sina hamu. Hii ikiongezewa na kiza na joto ndiyo usiseme. Hata kile kiyoyozi yangu chapa Mzaramo sijui kiliibiwa na nani? Maana sisi wanywa gongo kiyoyozi chetu si kingine bali feni ya mkono.

Mainzi yanavyozaliana siku hizi sina mfano. Kila siku utaona hili likiibuka pale na jingine kule. Kwanini yasipange uzazi? Lo! Sasa naanza kuchanganya! Kwanini mainzi yapange uzazi wakati uchafu upo jaro na yanakula bure? Kwa vile sijapata gongo tangu asubuhi, wacha nitimke kwa mama Betty nikaongeze mafuta tayari kukabiliana na inzi. Inzi mpo? Kaa chonjo bwana rungu naja. Sitaangalia rangi wala ukubwa. Inzi ni inzi kila nitakapomuona natwanga. Laiti wanywa gongo wote wangekuwa na moyo mkubwa kama wangu!

Chanzo: Dira ya Mtanzania Agosti 11, 2011.

Wednesday 10 August 2011

President Kibaki Is Setting Good Precedent



Kenya’s president Mwai Kibaki’s recent take on who should inherit his office is commendable. He stated categorically that he is not going to busy himself looking for his stooge or protégé to take over from him as soon his term in office lapses. This wisdom should be emulated by other east African rulers who have shown no signs of relinquishing power even when the constitution states so. We recently evidenced some machinations in Rwanda and Uganda where the constitutions were tampered with to enable current rulers cling unto power illegally and unnecessarily.

Kibaki’s take shows the world that he does not intend to mess his legacy. Despite his dark side especially the way he secured his second term in office, Kenyans are likely to forgive him shall they consider the changes Kibaki ushered in. One of his legacies is the new constitution of Kenya. Through new constitution, accountability is now reality in Kenya. Bigwigs are paying tax and those that seem to be in slumber are forced to toe the line. Again, under Kibaki’s watch, Kenya’s economy has performed relatively well compared to other countries in the bloc. Kibaki will be remembered as the African president who harbingered power sharing in Africa ahead of Zimbabwe and partly Zanzibar.

Another feather on Kibaki’s hat is devolution of power. Kenyans are now used to the president that can be faulted when he goes wrong. Refer to how Kibaki’s choice of Chief Justice was shot down by the opposition. Kibaki did not superimpose his choice. Instead, he let the constitution produce the CJ everybody appreciated. This is different from former regimes under which the president was a demi-god who apart from being the law, he was above the law. Kenya’s president is now a mortal being that can make mistake and be taxed just like any other common mwananchi.

If anything, Kibaki’s take is a new wake up call for other rulers who still cling unto frozen ideas of ‘me forever’ as seen in Uganda where the strong man has been in power for more three decades and has never shown signs of retiring despite being above normal retiring age. If he does think about it, he’d like to see his son or his stooge takes over from him so as to protect him and be controlled by proxy.

In Tanzania, the current president came to power by suspicious means whereby public coffers were broken to enhance his rise to power. He has nary stood to defend himself, deny or take on those implicated in this heinous crime against the poor.

Currently, Kenya is an ideal and exemplary democracy ahead of all countries in East Africa bloc. Freedom of expression and freedom to receive and disseminate information is real. Media is awash with stories on corruption. The Kenya that used to kill, silence and force journalists into exile is long gone and forgotten. Kenyans can demonstrate at any time they deem fit. This cannot be done in Uganda. Refer to the recent beatings and humiliation of opposition leader Kizza Besigye when he decided to support the walk to work move that aimed at reminding the authorities that economic situation in Uganda was worse.

Thanks to Kibaki Kenyan police force is currently undergoing a lot of face lift among which is being taught human rights and accountability. Kenya’s army is for the protection of mwananchi instead of big men and their bootlickers.

To Kibaki’s credit, his spouse, sons and daughters don’t featuring high when it comes to running the country as in Uganda and Tanzania. During Daniel arap Moi’s notorious era, Moi’s children were power brokers to reckon with. This is still going on in Tanzania and Uganda where the names of the sons of the presidents Ridhiwan Kikwete and Muhoozi Museveni are featuring high respectively. Again, if those responsible watched how publicly Egyptian former strong man was presented lying in a stretcher in court, sick, caged and on drip, surely they might have gotten a very crucial lesson if they nicely use their brains.

Shall Kibaki live up to his promise of not planting his protégé in the office of president; he will be remembered as a statesman who shaped the future of Kenya. Retire well Mwai Kibaki. All this depends on how you are going to live up to your promise of honouring the constitution. Importantly, your colleagues need to borrow a leaf from you shall they want to leave good and sound legacies behind.

Source: The African Executive Magazine August 10, 2011.

Mpyayukaji the kila kitu

Ninarap ninarap ninarap

Nawakilisha mistari, ninarap

Machizi wanapagawa ninarap

Kama sina akili nzuri, ninarap

Yo yo yo yo ninarap

Nami siku hizi siachwi nyuma. I am Mpayukaji the jack of all trades so to speak. Acha nimwage ung’eng’e kuonyesha mie si kilaza kama Makambale au wale vilaza walioghushi PhD. Hamkumsikia mmojawapo aitwaye Diddy Masemburi akilalamikia waishiwa baada ya kumvua nguo kwwenye dili la UDA? Ajabu eti kilaza mwenzake Makorongo Muhanga anaamua kumtetea bila aibu asijue tunawajua walivyo vilaza walioghushi PhD! Siku hizi kila mtu, hasa matapeli, anapenda kuitwa dokta kama wafanya mazingaombwe.Hayo tuyaachane nayo ingawa yanatuathiri hasa sisi walevi wa Danganyika.

Pamoja na kuwakilisha mistari kuonyesha kuwa mie ni The Kila Kitu yaani TKK, nataka nitoke kivyangu vyangu na mistari yangu hapo juu. Sitatoa mistari mingi kuogopa wezi wa sanaa kuniibia mistari na kuanza kuwa masupa staaa hata kama ni wachovy wanuka jasho wa Danganyika. Kwa ufupi, ni kwamba kwenye mambo ya Uongofleva nimo kinomanoma nikimwaga mistari. Nawakilisha kama sina akili nzuri.

Kuonyesha ninavyoyanyaka ma-Uongofleva, nimetoka na minyororo mikubwa kuliko ya mbwa shingoni. Sorry si minyororo. Ni cheni. Hata kama ni za shaba na mawe na si dhahabu na almas. Bling bling ni bling bling hata kama ni ya mbao. Kwani niko peke yangu? Hamuoni hata wanaoitwa waheshimika wanajinoma mibling bling kwenye vidole masikio hata makalio kama yule mbunge machachari, Sonko wa kule kwa mzee Moi Kibaka sorry Kibaki? Hata bi mkubwa mwenyewe anajinoma kama hana akili nzuri. Mzee mwenzangu Dugong Ben wa Nkapa huwa hatupi mnyororo shingoni. Je hapa mtasema mie mbwa au mheshimika kama Dugong?

Ngoja nizidi kuwamegea. Nimetinga suruali ililyolegezwa hadi chini makalioni au sagging kwa kimanga huku nikidunda bega moja juu jingine chini kinoma. Mkononi nina justice au elephant. Wasiojua elephant au justice ni msoba au tuseme sigara kubwa. Nasema kimoyo moyo bangi nibangue nimwage vitu.

Kwenye masikio nimetinga mihereni kibao kuliko hata akina Ole. Japo natukanwa eti mtoto si riziki kwa kutoboa masikio, najifanya hamnazo hata sijali. Nadunda mwendo wa Dola si ndururu. Si juzi baba mdogo akasema eti atanitafutia mume aniozeshe! We palitaka kuchimbika bila jembe kama si mzee mwenyewe kuingilia. Hayo tuyaache ni ya wale wanaotuona limbukeni wakati tunafaidi fasheni za majuu zinakwenda na wakati. Mbona P Daddy anaweka vitu kama vyangu? Mbona akina senti 50 nao wanafanya vitu kama vyangu. Mungu akupe nini duniani, kuvaa kama mtasha hata kama unaishi kwenye kiza cha mgao? Hata kama hatuishi kama watasha bado tunafaidi na mapozi yetu ya mende. Heri yangu nimetoga masikio kuliko akina supastaa uchwara wanaofuga vichiwawa au vijibwa vidogo vidogo. Mie nikaamua kufuga dog nitafuga Germany Shepherd au Labrador Husky. Wasiojua aina hii ya mbwa ni kama ile aliyokuwa amefuga Bill Clinton. Na chiwawa ni kama yule wa Joji Kichaka. Upo hapo chizi wangu? Mie ni mchizani wala simlaunguwi mtu wese wala kuiba Uda? Mpo hapo majambawazi wenye nazo walanguzi na wala na watoa rushwa?

Ngoja niwakoge washamba hata kama mimi ni limbukeni. Kila nikipita mitaani naangalia huku na kule kuona kama kuna watu wananiangalia super star mie. Wengine wanakandia kuwa eti mimi ni super star uchwara. Mara utasikia wakisema: super star mwenyewe apeche alolo na alikimbia shule.

Nimepiga pamba zenye chata babu kubwa wafikiri maneno yenu yatafanya niache ulimbukeni? Siku hizi ulimbukeni unalipa. Waulize wahishimiwa wanavyomwaga ung’eng’e uchwara au tuseme kiswanglish wakiwaingiza wale wa kwa mama wasijue wale ni lugha yao! Je hawa nao si limbukeni?



Naingia na uongofleva kuwaibia malimbukeni waliojaa kayani. Nawapa vipande kupitia mistari lau waamke na kuacha ulevi na ushamba. Badala ya kushabikia upuuzi kama kitchen party na kuchangia harusi waanze kujenga mwamko wa kimapinduzi wa kuborosha maisha yao.

Kwa vile mie ni The Kila Kitu jiwe gumu, napanga kufanya kila sanaa lau niukate kama akina Roast Tamu, Ewassa, Endelea Chenga hata Riz-One. Kwa hiyo, msishangae kusikia mipango na mikakati yangu.

Juzi nilipita sehemu nikaona maajabu. Nikiwa nawaza kujifanya mtangazaji wa runinga bambataa si nikakuta CV ya mfala mmoja limbukeni mtangazaji anayepayuka sana pumba. Sikuwa najua kuwa jamaa ni Kilaza bin Kihiyo. Kumbe jamaa aliondoka na divisheni ziro kwenye mtihani wa kidato cha nne! EF Kivalley upo hapo? Ajabu kesho utasikia jamaa ana Masters na baadaye PhD kama za jamaa zangu walioshukiwa na Keine Mlongakweli. Hapa akina Billy Lukuveee, Chitaahira, Merry Nangu, Makorongo Mahanga, Diodorant Kamara, Emmy Nchimvi, Mwambalaswai, Chengeni,Diddy Masab—uri na wengine wengi ambao kughushi kwenu hakujafichuliwa mnaninyaka. Baada ya kugundua kuwa kumbe Kivalley ni kibonde kweli kweli nimeamua kuwa mtangazaji wa runinga. Nitaanza kubwabwaja kama sina akili nzuri. Ili kuwavutia walevi nitakuwa nacheza miziki ya X maana najua wanapenda mambo X X. Hata akili zao Mungu keshaziwekea X. Kila kitu kwao ni X kama nyumba zilizopangwa kubomolewa huku wahusika wakipaisha malipo. Wataacha kuiibia mijitu yenyewe kama ni hovyo kiasi hiki? Hayo tuyaache. Wenye vituo vya runinga jiandae kupata kifaa mithili ya mzee mwenyewe Larry King. Mie nitakuwa nikitumia jina la Larry Dog King Kong. Haya tuyaache. Ukifika wakati wake nitadurusu zaidi jinsi ya kutengeneza mchicha kama wale wachizi waliojitwalia UDA. Idd Lion upo? Nasikia uligaiwa madafu 250,000,000. Hii kweli imeniuma sana. Maana nilikuwa nikikuhusudu kwa utetezi wao wa uzawa kumbe uzawa wenye si mali kitu bali uliwa siyo? Mtu mzima hovyo.

Nimalizie na upande wa pili wa usupa staa uchwara. Juzi nusu mshirika wa bedroom ajinyotoe roho baada ya kutishia kunipa talaka kutokana na kumdhalilisha. Si nilikwenda nikachora tattoo mkononi ili nionekana kama akina Snoopy Dog. Nilitaka nibadilishe hata jina niitwe Big dog au mzinga wa mbwa. Pia nilitaka nianze kuimba muziki wa injili aina ya shamkwale.

Mama alizoza hadi nikatamani kujinyotoa roho kama siyo kuwahi kijiweni na kupata kahawa na tangawizi ambavyo viliyeyusha hasira zangu. Wale ndata mbona kama wanakuja huku! Ngoja nitimke kabla hawajanibambikizia kesi. Maana, wakitaka mshiko mie sina. Kulaleki!

Chanzo: Tanzania Daima Agosti 10, 2011.

Monday 8 August 2011

Wajua nchi ambako wananawake wanasifika kuwabaka wanaume?

Taarifa zilizokaririwa na vyombo mbali mbali vya habari zinadai kuwa kuna jinai ya kubaka wanaume iliyoibuka nchini Zimbabwe hivi karibuni. Kawaida hata kisheria ni kwamba mwanamke huwa habaki. Lakini kadri siku zinavyokwenda ni kwamba tunapaswa kubadili sheria na imani hii. Maana nchini Zimbabwe kumeripotiwa wanawake kuwabaka wanaume tena si kwa kuwategeshea vishawishi bali mtutu wa bunduki.
Kwa wenzangu wanasheria watasema mwanamke hawezi kubaka kwa vile hana uwezo wa kusababisha erection. Kwa ufupi tunarejeshwa kwenye kuchunguza tena uwezo wa ubongo wa binadamu hasa anaposhikiwa mtutu wa bunduki. Hata hivyo, wengi wataendelea kuhoji inawezekanaje kusimama wakati umeonyeshwa mtutu wa bunduki? Au ni yale yale ya kumsukuma mlevi?
Kwa habari zaidi BONYEZA HAPA

Friday 5 August 2011

Chenge na Lowassa wanangoja aibu zaidi?


Ingawa watuhumiwa wakuu wa ufisadi wanaopaswa kujivua gamba wanaamini kuwa hawana hatia, mazingira ya kuwajibishwa kwao yanaweza kuwa ushaidi wa kimazingira tosha kuwaona wana hatia. Baada ya aliyekuwa waziri mkuu Edward Lowassa mbunge wa sasa wa Monduli kutakiwa na kamati teule ya bunge kujipima na kuamua na akaamua kuachia ngazi, ilitosha kumfanya aonekane ana hatia. Vinginevyo asingeachia madaraka kama aliamini hakuwa ametenda kosa lolote. Kwanini aliamua kuachia ngazi kama kweli hakuwa amehusika na kashfa ya Richmond iliyoliingizia taifa hasara na kulitumbukiza kizani? Majibu sahahi ya maswali haya ni kumburuza Lowassa na wenzake mahakamani ili haki itendeke. Pia, kama watakutikana na hatia mali walizochuma zitaifishwe.

Baada ya kuachia ngazi baada ya kujipima, Lowassa hivi karibuni alisikika akijaribu kujitakasa bila mafanikio. Alikituhumu chama chake kinachomtuhumu kuwa gamba kuwa na ugonjwa wa kutofanya maamuzi mazito ingawa uamuzi wa kuwataka Lowassa na wenzake waachia ngazi si rahisi. Maskini Lowassa hakujua kuwa kumshughulikia yeye ni sehemu ya maamuzi hayo magumu anayohimiza wenzake wafanye bila kuchelea lawama. Na kwa kuzingatia ushauri wake, Lowassa hana sababu yoyote ya msingi kulalamika kuwa anaonewa au amelengwa kwa sababu ya azma yake ya kugombea urais ambayo hata hivyo hajawahi kuiweka wazi ukiachia mbali mikakati yake kuonyesha hivyo. Lowassa alikwenda mbali zaidi kutaka wananchi wawapime uwezo wa watendaji naye akiwamo wakati baadhi yao walikwishajipima! Wananchi, kwa mfano, wampime Lowassa kwa lipi wakati alikwishajipima na kuamua kuachia madaraka kutokana na kuridhika kuwa alitenda makosa? Hata hivyo Lowassa na wenzake wana bahati. Maana kwa makosa wanayotuhumiwa kutenda na matokeo ya makosa haya, ingekuwa nchi za wenzetu, maandamano ya kushinikiza wakamatwe yasingezuiliwa na risasi wala mabomu. Hata hivyo, taratibu tutafika huko kama wahusika wataendelea kuwaona wananchi waathirika kama woga na mataahira wasiojua lolote.

Tukija kwa Andrew Chenge waziri na mwanasheria mkuu wa zamani almaaruf kama mzee wa Vijisenti, naye kama Lowassa,hana bao tena ikizingatiwa kuwa hajawahi kutoa utetezi wowote kuhusiana na tuhuma zinazomkabili. Hawezi kukwepa kuhusika na ufisadi wa Rada kwa sababu rahisi kuwa hajawahi kukana kuwa na akaunti kwenye visiwa vya Jersey yenye pesa taslimu zaidi ya shilingi 1,500,000,000. Pili hajawahi kutoa maelezo ya jinsi alivyopata hiki kiasi kikubwa cha pesa na kwanini aliamua kuzificha nje. Hajawahi kueleza alivyosafirisha hiyo pesa ambayo kimsingi alitorosha.

Hakuna ubishi kuwa kikao cha Kamati Kuu (CC) Chama Cha Mapinduzi kilichomalizika hivi karibuni mjini Dodoma kimewaacha watu wengi hoi? Kimeionyesha CCM kama chama ‘kinachojipiga mtama’ hata kuchechemea na kuogopa baadhi ya makada wake ambao wanaendelea kukigharimu. Ingawa CCM imekuwa ikilaumiwa kwa mizengwe kujuana na kulindana, kwa kushinikiza watuhumiwa hawa papa waachie ngazi ni mwanzo mzuri kama kuna mpango wa kuwafikisha mbele ya vyombo vya haki.

Kinachogomba ni hii hali ya kuvuta vuta miguu kuwashughulikia vilivyo. CCM inawabembeleza watuhumiwa. Na pia bado hawa hawatoshi kuna wengine wanaopaswa kuachia ngazi mfano wale waliotuhumiwa kughushi shahada na jinai nyingine. Hawa matapeli nao ni magamba kwa chama. Hivyo kuna haja ya kuishauri CCM izidi kujichunguza vilivyo ili magamba zaidi yaporomoshwe. Kadhalika, chanzo cha magamba matatu ni tuhuma za CHADEMA pale Mwemba Yanga. Hivyo wahusika wajue kuwa orodha bado ni ndefu. Maana ufisadi unaodaiwa kufanywa unawagusa wengi.

Turejee kwa magamba ambayo yameishatajwa kwa majina na kupewa la kufanya-yaani kuachia ngazi kama lilivyofanya gamba la kule Igunga, Rostam Aziz. Kwanza, walipewa siku 90 zikapita na hakuna kilichofanyika zaidi ya mmoja wao kujiondoa siku ya 92.

Sasa wamepewa mwezi mmoja ambao ni siku 30 je watajiondoa? Je wakiendelea kung’ang’ania kama walivyofanya miezi mitatu iliyopita na CCM ikaendelea kuwagwaya, umma ufanyeje? Maana pesa iliyoibiwa na kufichwa nje au iliyolipwa Richmond si ya CCM bali watanzania wote bila kujali vyama vyao.

Siku moja baada ya kikao cha Kamati Kuu (CC), mmojawapo wa watahumiwa wakuu Chenge alikaririwa akikikejeli chama na maazimio yake kwa kusema: "Sijui kama mimi ni gamba," Sambamba na kejeli hii, Chenge aliendelea kuwataka wananchi wa jimbo lake kupuuzia uongo unaosemwa juu yake. Je hii ni dharau kiasi gani kwa mtu ambaye asingefika hapo alipo kama si chama kumuunga mkono? Je ni ile shukrani ya punda au mtoto umleavyo? Je CCM bado ina haja ya kuendelea kuwafunga mafisadi? Je jeuri ya Chenge na Lowassa inatoka wapi? Kuna wanalojua ambalo wakilimwaga hadharani kuna watakaoumbuka au ni jeuri tu na harakati za mfa maji? Je ni ile hali aliyoieleza katibu wa uenezi wa CCM Nape Nnauye kwa nukuu hii?

“Samaki ana nguvu akiwa ndani ya maji tu, ukimtoa hakuna kitu tena wala hana ujanja na hivyo hata hawa wanatusumbua wakiwa ndani ya chama lakini tukiwatimua hawana mahali pa kuegemea,’’

Je kama Nnauye anamaanisha anachomaanisha huku kusuasua na kuchelewa ni vya nini wakati wahusika wakizidi kukipasua na kusambaratisha chama kadri mambo yanavyozidi kucheweshwa? Je CCM itawatoa majini samaki wake baada ya mwezi mmoja kama ilivyoahidi? Wengi wangetaka kuona CCM ikijivua magamba mengine mengi makubwa na kuona itakuwa na sura gani.

“Ni heri kupoteza jimbo au kata halafu tukarudi kwenye uchaguzi maana ndiyo njia pakee ya kukisafisha CCM kuliko kuendelea kung’ang’ania wachafu kwenye chama chetu.” Kama maneno ya Nnauye yatatekelezwa, si haba CCM inaanza kurejea kwenye mwelekeo ilioupoteza baada ya kukumbatia na kutekwa na mafisadi wachache wakiitumia kwa maslahi binafsi.

Tumalizie tulipoanzia. Je Chenge na Lowassa wanangoja aibu zaidi au kutunishiana kwao misuli na CCM mwisho wake utakuwa upi? Yetu macho.

Chanzo: Dira ya Mtanzania Agosti 4, 2011.