The Chant of Savant

Wednesday 24 August 2011

Wauza wese walichakachua sasa wanakwatua

Jamani kaya hii imechakachuliwa kila idara kulhali. Wewe umechakachuliwa hata mimi kadhalika. Bila kuchakachuliwa nani angekubali kuishi kwa mgao wa takribani kila kitu? Juzi mwenzenu niliumbuka. Nilipewa lifti na mlevi fulani mzito. Kumbe pamoja na uzito wake gari yake haikuwa na wese la kutosha. Kufika njiani si gari ikageuka kimeo! Mwenzangu alianza kupagawa akifikiri jinsi jeshi la vibaka litakavyotuvamia na kuchukua njuluku zake kama si uhai wake. Maana vibaka wana hasira na mibaka inayowafunga wakati yenyewe ikilindana. Wana usongo na maisha na wamechoka na maisha ya mgao wa kila kitu. Ukienda kwenye umeme mgao, wese mgao, mikopo ya ilmu dunia ya juu mgao, gongo mgao, maji mgao, matatizo mgao, ufisadi mgao, maulaji mgao. Jamani, hata kifo sasa kitakuwa mgao. Makapuku watapewa kifo kingi huku wazito wakipewa afya nyingi kama wanavyogawiana umeme mwingi na kuwapa walevi kiza kingi.

Baada ya shangingi la mfala wangu kugeuka kweche si niluliza kulikoni, mzito mzima tena mwenye cheo si kikubwa tu bali cha haja akaanza kulalamika na shumbwenga lake kugeuka kweche mchana kweupe. Mara alisema: “Hawa washenzi tusipoangalia watakuja pindua kaya hii na kusimika lisirikali lao la kijambazi.”

Mie kwa unoko nilijifanya simpati hivyo niliuliza. “Mkuu washenzi wapi hawa wanaotaka kupindua kaya na kuingiza ujambazi kuku?”

Naye bila kusika alijibu, “ Si hawa wauza wese ambao wengi wao wanaitwa wawekezaji wakati ni wachukuaji. Hivi huoni wanavyowalangua watu huku wakitorosha mipesa kibao kwenda ughaibuni?”

Nami sikujivunga. Nilimpa laivu, “Sasa wakubwa kama nyinyi mnalalama hawa waduchu wafanyeje? “

Nilitaka kumuongezea kigongo kingine lakini nikamuonea huruma. Moyoni nilitaka kusema hivi: kama nyinyi mnaowaruhusu hao wezi kuwekeza humu uongo na kuvuna pesa kwa vile nanyi mnakatiwa kitu kidogo na kikubwa sasa mnalalamika nini? Hamjui kuwa mmeuza watu wenu nanyi mkiwemo kwa uroho wenu? Ndiyo maana kuna mwizi mmoja amesema eti baadhi yenu wanafikiria kwa makalio wakati naye anafikiri kwa makalio hay ohayo. Wahuni nao wamemkomesha kwa kuzusha msamiati uitwao masaburi yaani wakimaanisha matako! Heri angesema kuwa wanaosababisha uwekezaji na ubinafsishaji kwa kijambazi wanafi…. Sorry wanalawiti… sorry wamekeketwa kiakili huenda wangetia adabu. Hayo tuyaache.

Kwa ufupi sitaki niseme yote tuliyoongea na huyu mzito kwa sababu za usalama wa kaya. Tuliyoongea ni top secret au tusema of high importance for national security. Isitoshe tuliyodurusu ni top secret ambazo zaweza kujulikana kwa FBI pekee yake baada ya kuibiwa na CIA. Upo hapo mlevi mwenzangu?

Kwa ufupi nawamegea kidogo. Ukweli ni kwamba huu mgao wa wese uliozaliwa baada ya huu wa umeme, ni mchezo wa wanene fulani kutafuna kaya. Jamaa walianza na uchakachuaji wa mafuta na siasa wakanogewa hadi wakajiweka reheni bila kujua na kujikuta nao wakichakachuliwa. Hukumsikia yule mfala wa kikaburu toka Sauzi aitwaye Sell no Nanduu akiwabwatukia walevi wenzie kwa kuwapa masaa 24 wakafyata mkia. Baada ya welevi hasa wambea wa magazeti kushupalia karipio na tishio lake si ndipo Lisirikali likaamka na kujivuvumua kwa kuamuru wese liuzwe. Kuonyesha lisirikali lisivyo na bao, baada ya kubanwa mbavu nyuma ya pazia si bei zilipandishwa tena baada ya masaa 24! Je hapa mfala huyu wa kikaburu hajatawala nchi yetu by proxy kama wasemavyo watasha?Je hapa mamlaka haijasweka kwenye mfuko wa fisadi huyu wa kikaburu? Je jeuri yote hii inatoka wapi kama siyo kujua uhovyo na siri zao? Wathubutu awavue nguo. Wao wamezoea kuvuana magamba. Jamaa atawavua nguo tena za ndani bila kubaki hata na godfather makalioni. Maana anawajua vizuri na wakiendelea kutishana atawaanika hadi walevi wawamwagie kahawa na tangawizi kwa mihasira waliyo kuwa nao dhidi yao.

Ingawa suala la mgao wa nishati haliwakutikisa wala kusababisha walevi wawatimue kwenye ulaji, hili la wese laweza kutupeleka Tahrir kirahisi na kwa haraka bila kutegemea. Hii itategemea uwezo wetu wa kusoma alama za nyakati. Ni kama tunafanya upuuzi wajapani waitao shinatako siyo sina tako. Najua waswahili walivyo mabingwa wa kubadili mambo ya wengine wakishindwa kubadilika wao wenyewe. Wenye kupenda kaya waombe Mungu haya mazabe yaendelee uone kama kuna mlevi mkubwa ataendelea na ulevi na matanuzi yake. Wainglishi huita hii to be pennywise and pound foolish. Kama nimechapia nisameheni ila jua mie sikughushi kama wale madaktari uchwara wanaowaibia na kuwachakachua nyie. Mie hanichakachui mtu kabla sijamshukia na kitanzi changu.

Kabla ya kuendelea naleta good news. Mwajua kuwa Pio Msekua naye ni gamba? Juzi jamaa zake na wapingaji walimvua nguo sina hamu. Mie sikuwa nimeinyaka kuwa kumbe yeye ndiye kuwadi wa jamaa wa kimanga wanaotorosha wanyama wetu na kujenga mihoteli ya bei mbaya kwenye maeneo yasiyoruhusiwa! Nilishangaa sana. Si ajabu hata haya mahoteli ya magenge ya mafia na wauza bwimbwi yaliyojazana kwenye beach zetu yameletwa naye. Je hapa kaya haijageuzwa kichwa cha mwendawazimu kwa mlevi kujifunzia kunyolea kama aliyesema mwasisi wa ufisadi huu mzee Ruksa ambaye ana bahati ya kutounganishwa na ufisadi wake? Nani mara hii kasahau kashfa ya Muhunidin Ndongala ambaye aliwahi kuipiga seli Loriondo zama zile za ruksa?

Kwa vile Pio ametajwa na hata chama chake cha mafisadi, nina mpango wa kuhamasisha walevi tumvamie na kumvua nguo ili tumzomee. Zaidi ya hapo kitakachoendelea waweza bunia mwenyewe. Kwani mtu akishavuliwa nguo unategemea kifuate nini? Bakora bila shaka. Kwanini asirambwe bakora iwapo amekuwa akibaka kaya yetu?

Najua hapa rafiki yangu Njaa Kaya ana kibarua kigumu. Maana kila uchao watu wake wanazidi kuvuliwa nguo kuanzia kitegemezi chake, nkewe hata yeye mwenyewe. Hata hivyo mhuni huyu ana bahati. Sijui aliwaroga walevi ama vipi? Maana kwa kaya inavyokwenda alipaswa afanyiwe alichofanyiwa yule imla wa kwa Farao Hoseini Kibarak. Hata hivyo nani ajuaye? Huenda walevi watatia akilini na kuamua kufanya kweli tena bila woga wa kuuliwa. Nani atawapiga watu risasi wakati madevu Mreno Okampo yuko macho? Walevi wasingekuwa mataahira huu ndiyo ulikuwa wakati mwafaka wa kumgeuzia Njaa Kaya na genge lake kibao. Walevi mwanisikia na kunielewa au mnaridhika na kuendelea kuliwa na kaya yenu kubakwa na akina Pio? Ya Pio tuyaache kwa leo.

Tumalizie na wauza wese. Nawapa masaa 24 wapunguze bei ya wese vinginevyo nitawa--- leo chichemi wakajipanga.
Wacha niwahi kufuturu!

Chanzo: Tanzania Daima Agosti 24, 2011.

No comments: