The Chant of Savant

Monday 14 July 2014

Mabilioni ya Uswizi yameishia wapi?

Hali ilivyo ni kwamba mjadala na mashinikizo juu ya kureshwa kwa mabiloni ya shilingi yaliyoibwa nchini na kuficha ughaibuni hasa Uswizi umezimwa kinamna. Pamoja na serikali ya Uswizi kutoa msaada wa jinsi ya kurejesha haya mabilioni huku serikali yetu ikiukataa, inaonekana wajanja wameufunga mjadala kwa kuleta maigizo mengine kama vile Katiba Mpya, Bajeti tegemezi zinazotumika kuiba mabilioni mengine na sarakasi nyingine kama kawaida.
Kinachostusha ni kwamba utoroshaji huu wa dola haukuanza jana wala juzi. Umekuwapo tangu tulipopata uhuru na hata kabla. Je ni kwanini tumeshindwa kupambana na ujambazi huu unaoathiri uchumi wetu kama taifa? Je nani wako nyuma ya mchezo huu mchafu wa mauti kwa watu wetu? Je tutaendelea  kulikubali na kulihalalisha balaa hili hadi lini?
Kwa mujibu wa msemaji mkuu wa kambi ya upinzani John Mnyika, Tanzania ilipoteza kiasi cha dola milioni 570.6 wakati wa awamu ya kwanza huku ikipoteza dola milioni 1,566 wakati wa awamu ya pili na dola milioni 1, 1010 wakati wa awamu ya tatu. Chini ya awamu ya nne ambayo imejipatia umaarufu kwa kuvumilia na kukingia kifua ufisadi bila shaka zitakazoibiwa ni kubwa kupita zote zilizotajwa hapo juu. Hata hivyo, takwimu hizi hazihusu pesa inayotoroshwa moja kwa moja kwa njia ya kuwahonga maafisa wa serikali kama ilivyokuwa kwenye kashfa ya ununuzi wa rada na ndege ya rais ambapo mamilioni ya shilingi yaliwekwa kwenye akaunti za wahusika moja kwa moja huko huko ughaibuni. Kuna uwezekano pesa inayowekwa moja kwa moja kwenye akaunti za maafisa fisadi ughaibuni ikawa kubwa kuliko inayotoroshwa hasa ikizingatiwa jinsi ufisadi kwenye uwekezaji wa sekta kama madini na nishati inavyowaingizia pesa nyingi. Swali linaloendelea kuwsumbua wengi ni kwanini viongozi wetu hawataki kupambana na jinai hii?
Kiasi cha fedha kilichokwisha kutoroshwa tangu uhuru kinaweza kuwa kikubwa kuliko kile kilichopatikana kutokana na mikopo na misaada. Hapa ndipo unaweza kugundua kuwa Afrika haipaswi kuwa maskini kama ingekuwa na uongozi wenye kuwajibika na si kushiriki kuliibia bara hili kama ilivyoshuhudiwa katika nchi mbali mbali chini ya tawala nyingi za kiimla na kijambazi kama tulivyoshuhudia nchni DRC chini ya Mobutu Seseseko kama mfano. Kwa sasa Afrika ina demokrasia sema inakosa uongozi makini na wenye visheni na uzalendo. Uongozi usio dokozi na tegemezi kimawazo na kimikakati. Hivyo, pamoja na kulaumiwa kwa utegemezi na umaskini wake, tunaweza kusema kuwa Afrika si fukara bali inafukarishwa na ukosefu wa uongozi wenye kujua unachofanya. Bila kupambana na ufisadi ambao ndicho kichocheo na kirutubisho kikuu cha utoroshaji fedha nje na utakasaji fedha, Afrika itaendelea kuwa maskini wa kutupwa Tanzania ikishika namba za juu.
 Wapo wanaoona kama utoroshaji dola nje hauwezi kuisha kwa vile unawanufaisha baadhi viongozi wezi kama hawa wetu ambao wao watoto na wake zao wanatuhumiwa kujisisha na watoroshaji huu wa fedha. Wakosoaji wanatoa sababu moja kuu mbili. Mosi, viongozi na familia zao kugoma kutangaza mali zao kama wanavyotakiwa na sheria. Na pili ile tabia ya kupenda kusafiri mara kwa mara bila kujali umaskini wa taifa. Wengine wanakwenda mbali na kutoa sababu kama vile kushamiri kwa biashara haramu ya mihadarati, rushwa, ujambazi na ufisadi kwa ujumla ambavyo haviihangaishi serikali ya awamu ya nne.
 Wapo wanaohoji kwanini serikali ya rais Jakaya Kikwete iko kimya kuhusiana na kurejeshwa mabilioni ya Uswizi? Wapo wanaotoa jibu kuwa ni ile hali ya kuwa baadhi ya watuhumiwa ndiyo hao hao wanaotakiwa na umma warejeshe fedha walizoficha ughaibuni. Hebu jaribu kujiuliza: Kama inafikia fisadi mmoja kuita bilioni 200 fedha za ugoro na asibanwe kuonyesha ana utajiri kiasi gani na ameupataje unadhani hawa wezi wataacha kutorosha fedha zetu? Hata hivyo, wapo wanaodhani kuwa hapa wa kulaumiwa ni mwananchi anayejifanya hayamhusu.
Hapa lazima wananchi yaani watawala na watawaliwa walaumiwe kwa kuacha mambo yajiendee huku taifa likisifika kwa kuombaomba, kukopakopa na ufisadi. Kiasi cha fedha kinachotoroshwa na kupotea ni kikubwa kuliko kinachopatikana tokana na kukopakopa na kuombaomba. Hatuwezi kuendelea hivi tukawa salama kama taifa. Kwa mfano, kwanini kusiwepo na kampeni za kubaini watoroshaji wa fedha na mbinu wanazotumia? Kwanini wananchi hawafahamishwi madhara ya utoroshaji huu wa fedha ambao kimsingi umechangiwa na mfumo mbovu wa kuruhusu baadhi ya watanzania wenye asili ya kigeni kumilki karibu uchumi wetu huku wazawa wakizuiwa kuwa na uraia wa zaidi ya nchi moja huku hawa wakiruhusiwa. Je wengi wa wanaosafishirisha pesa hii hawafahimiki? Kundi la pili ni la wezi wanaoingia nchini kwa kisingizio cha uwekezaji. Japo wanajulikana kuwa si wawekezaji kitu, wanawezeshwa na maafisa fisadi wa serikali wanaogawana nao chumo la utapeli na wizi wao.
Tumekuwa tukipendekeza njia rahisi ya kupambana na jinai hii. Ni rahisi, kulazimisha kila mkazi wa Tanzania kutangaza mali zake kila mwaka ili azilipie kodi na kueleza alivyozipata. Namna hii tutaondoa kundi wezeshaji la watanzania wanaoshirikiana na majizi ya kigeni. Hata hivyo, wengi wanadhani hili litakuwa gumu kukubalika kwa watawala wasiopenda kutangaza mali zao jambo ambalo wanalichukulia kama ushahidi wa kushiriki jinai hii ya kulihujumu taifa.
Tumalizie kwa kuwasihi wananchi wasibweteke na kupotosha na sanaa zinazoingizwa kwenye mkondo wa habari ili kuwaondoa kwenye mambo muhimu kama kudai kurejeshwa kwa mabilioni yaliyoko Uswisi. Bila kuibana serikali, wasitegemee miujiza toka mbinguni kurejesha fedha yao hata kukomesha utoroshaji huu unaowaacha maskini bila sababu wala ulazima.
Dira Julai 2014.

4 comments:

Anonymous said...

Hizi chenji bado tunafanyia uchunguzi na meneshehena mkuu wetu merehemu mpaka yesu atakaporudi tuu na uchunguzi utakamilika hakuna shaka sawa majuha

Anonymous said...

Chenzi Watu wanatolea misaada hasa mfungo wa Ramadhan lakini angalia Nanyi unao pokea motoni safari moja

Ndugu Nkwazi N Mhango said...

Anon hapo juu mmenena. Tumegeuka taifa la ajabu sana linaloweza kuhongwa pesa ya wizi na wahusika wakajisifu kuwa wataingia peoponi. Hiyo pepo hata nipewe bure siipendi. Ni ya wezi na majambazi na vitibakwiri.

Anonymous said...

Kama vibaka unawauwa kwanini na hawa hamuwauwi iwe fundisho kwa wengine
Uwa uwa uwa hawa ndo wanaleta problem in Tanzania
Uwa uwa uwa wote
Hamasa mpo fanyeni kazi nitawalipa