The Chant of Savant

Tuesday 22 December 2015

Wanakijiwe walaani kubomolewa mijengo yao



            Baada ya kaka Dk Kanywaji kuja juu na kubomoa majumba yaliyojengwa uswekeni, wanakijiwe wamepokea uamuzi huu kwa shingo upande.
            Mpemba anaingia akiwa na ndita usoni. Baada ya kuamkua anasema, “Yakhe mmepata simu ya Mgosi Machungi?”
            Kabla ya kuendelea, Mbwamwitu anadakia, “Kwani simu yake imepotea au amekupigia? Unamaanshani Ami?”
            Mpemba anajibu, “Mgosi Wallahi kanpigia simu na kusema eti nyumbaake yabomolewa kesho. Hivo, anaomba yoyote mwenyeweza kumhifadhi afanye hivo.”
            Kapenda anachukua kirongaronga chake na kumtwangia Mgosi. Mara simu inapokelea.     Tunasikia “Hao hamijambo huko?”
            Kapende anajibu, “Sie wazima vipi huko Mgosi? Maana habari tulizopata si nzuri hasa kuhusiana na ubomoaji wa mjengo wako.”     
            Mgosi anajibu, “Ni kwei sote tiiojenga mabondeni timeambiwa tibomoe kabua hawajaja kubomoa wenyewe.”
            “Pole sana Mgosi,” anajibu Kapende na kukata simu. Baada ya kukata simu kijiwe kinaanza kujadili zali zima.
            Msomi Mkatatamaa anakuwa wa kwanza kutongoa, “Japo naunga mkono mpango mzima wa kubomoa majumba yaliyojengwa kinyume cha sheria, lazima niseme wazi, sikubaliani na kuwaadhibu wahanga peke yao huku waliowasababishia madhira haya wakisimamia zoezi la ubomoaji.”
            Mijjinga anakula mic, “Hapa Profesa Msomi umenena. Haiwezekani wale waliowaacha watu wakajenga wasiadhibiwe nao. Maana ukiangalia majengo haya ambayo hayakuota kimiujiza, unagundua kuwa serikali iliona kila kitu ikajinyamazia bila kutimiza wajibu wake kwa watu wake.”
            Mipawa anakula mic, “Wewe unaongelea la kuzembea kuwazuia wananchi kujenga mabondeni! Nani angemzuia nani wakati wazito nao walikuwa kazini wakijipa viwanja na kuvamia vya umma?”
            Mheshimiwa Bwege anakwanyua mic, “Unadhani sababu ni hiyo tu? Ilikuwaje wahusika wakapewa maji, umeme na wengine kutozwa kodi za viwanja na majengo kama serikali haihusiki na balaa hili?”
            Msomi anarejea, “Serikali inahusika japo si awamu ya dokta Kanywaji. Hata hivyo, kuna haja ya kumtaka Dk Kanywaji kuwapa hifadhi wahanga hasa ikizingatiwa kuwa makosa ni ya pande mbili. Nadhani jambo la muhimu kufanya ni kuchunguza wote walioruhusu balaa hili tangu mchezo mzima ulipoanza na kuwachukulia hatua za kisheria.”
            Kanji anakula mic, “Somi sema juli sana. Ila veve nasahau kuwa mingi ya vatu nakula juuku likwisa staafu au kufa. Sasa kama nachunguza tasitaki vatu yote nastaafu au kufa?”
            “Wewe unaonaje?” Msomi anamuuliza Kanji huku akikwanyua kombe lake la kahawa na kubwia kabla ya kuendelea kuongea bila kungoja Kanji ajibu.
            Anakohoa na kudema, “Tunafahamu wengi wameishastaafu hata kufa. Je mali walizochuma tokana na jinai hizi nazo zinastaafu au kufariki? Tungeshauri wahusika wasakwe, wafilisiwe na wengine kufungwa. Maana huu ndiyo ufisadi wenyewe na majipu ambayo Dk Kanywaji anapania kuyatumbua bila mzaha. Haiwezekani kaya yetu ikaendelea kuwa shamba la chizi.”
            Da Sofia Lion aka Kanungaembe ambaye alikuwa ameshika tama anaamua kula mic, “Mwenzenu hata mimi naona kuna namna. Kwani hata mjomba wangu naye amebololewa nyumba yake aliyojenga zaidi ya miaka 30 iliyopita. Mtu mwenyewe anaumwa vibaya sana ukiachia mbali kuwa alishafiwa na mkewe. Mzigo wote tumetupiwa sisi. Kweli nakubaliana nanyi. Kuna haja ya kutenda haki hasa kwa wahanga wa zoezi hili linalotokana na utawala mbaya.”
            Kapende anakula mic, “Kumbe nawe dada Sofi umeanza kuona mwanga! Siku zote tulipokuwa tunasema kuwa serikali zilizopita zilikuwa fisadi , ulikuwa ukituona wazushi usijue kuwa yakikugusa utastuka.”
            Mzee Maneno anakwanyua mic, “Ama kweli hujafa hujaumbika. Nadhani Sofi siku zote ametetea chama bila kujua nyuma yake kunani. Sasa uchaguzi ndiyo umeishakwisha na wenye kupeta wamepeta mnadhani kuna atayesikia la mwazini au mchota maji hapa?”
            Mijjinga naye anaamua kurejea, “Jamani tuwe wakweli. Tuseme ukweli kama alivyosema Dk Kanywaji kuwa msemakweli ni mpenzi wa Mungu. Watu wetu walizidi sana kiasi cha kusahau kuwa kuna sheria. Nadhani hapa tujadili jinsi ya kuwasaidia wahanga binafsi badala ya kuipa mzigo serikali ingawa chama chake kilihusika kwa asilimia kubwa. Nashauri –kama serikali itatusikiliza –ikamate waliosababisha maafa haya na kuwafilisi na hiyo fedha iwatunze wahanga wakati wakitafuta namna ya kusonga mbele.”
            “Nadhani sasa watu watajifunza kuheshimu sheria na kuzifuata huku na mamlaka nayo yakipaswa kutoacha watu wajenge ndipo yaje kubomoa. Tunatiana hasara na kuumizana tokana na kutofuata sheria. Somo kubwa nadhani hapa ni kwa wachovu kujifunza kutii na kufuata sheria badala ya kupenda vya mteremko. Nashauri tupitishe mchango kwa ajili ya Mgosi na da Sofi lau wapate pa kuanzia wakati kijiwe kikitafuta namna ya kuibana serikali isiwatupe watu wake iliyowadanganya kwa muda mrefu nao wakadanganyika.”
            Kijiwe kikiwa kinanoga si akapita meya wa zamani wa Jiji ambaye ni shikaji wake da Sofi. Acha tumtoe mkuku kabla ya ndata hawajamuokoa. Maana hawa ndiyo chanzo cha mabalaa yote haya. Na shauri yao. Tukiwakamata watu kama hawa wanaokalia madaraka bila kufanya kazi tutawafanyia kitu mbaya.
Chanzo: Tanzania Daima Desemba 23, 2015.

No comments: