The Chant of Savant

Thursday 18 February 2010

Mwamini changudoa lakini si mwanasiasa

Kabla ya kuwaletea za leo, ninayo furaha kuwafahamisha kuwa nimepokea barua toka Sauzi ambapo Bwana mkubwa Jack Zuma ameniomba niache kusiliba na kutangaza upuuzi wake.

Makombora yangu yalimlazimisha kuomba msamaha kwa kuzini na kuzaa na Sonono Khoza binti wa rafiki yake tena yanki kuliko babu huyu kiwembe kama jamaa yangu pale ambaye simtaji.

Taarifa nyingine ni ya masikitiko. Kijiwe kinasikitika kutangaza kifo cha ripoti ya tume ya uchunguzi wa wizi wa pesa ya kununulia mkaa ambayo tuliibatiza Richmondulo ya kijiwe uliosababishwa na Mbwa Mwitu a.k.a Ewassa na Rosti Time.

Sambamba na hili ni taarifa kwamba wakuu wa kaya, hatimaye, wamewazidi nguvu makamanda wa ufisadi kiasi cha kuwasilimisha na kuridhia kulala bed moja.

Sikuamini kama Spika Sammy Sixx angejiingiza kwenye mtego wa Ewassa kiasi cha kugeuka kikaragosi ghafla na kuua sifa zote alizojizolea na imani ya walevi! Ama kweli unaweza kumwamini hata changudoa lakini si mwanasiasa!

Anyaway, wanasiasa ndivyo walivyo hawana tofauti na tuvyangu pale Oh.. lo! Hapa nataka kulikoroga! Kwa ufupi ni kwamba pesa ya walevi imeliwa na yale mapapa na majoka aliyesema meku huku Cheka Cheka akichekelea na mlamba viatu wake Mgosi Makambale wa Machungi. Shenzi nyote kabisa! Mkiambiwa kaya hii mnaliwa mnapandisha ilhali ni ukweli usiopingika. Ole wenu mrudie makosa.

Tuendelee. Juzi nami nilijitutumua pale kwenye mashine ya ATM au Automatic Teller Machine kwa lugha ya kitasha. Nilikwenda pale kuchukua vijisenti vyangu ili kuwazuzua walembo wa Bongo wanaoabudia wenye nazo hata kama ni mafisadi.

Kwanza mimi si waziri wala fisadi. Hili lifahamike kwanza. Ingawa si chochote si lolote ukiachia mbali ukuu wa kijiwe, huwa najiona kama malaika na wengine hasa walalahoi ni takataka mbele yangu.

Kufika nikiwa na kirongaronga changu cha kisasa kiitwacho Broadband, nilibofya machine nikaanza kukamua huku nikichonga na kimada wangu aliyekuwa akiningoja kwenye Hoteli ya White Cliff.

Wanukajasho wengine walikuwa kwenye foleni wakingoja zamu zao kuchukua sabuni ya roho ili waende kukosha na kukonga roho. Upo hapa mshirika?

Niliona watu wanaanza kuchukia huku wakitoa maneno machafu. Hawakujua kuwa kumbe pale kulikuwa na kibopa tena mwenye kaya yake yaani mimi niliyekwenda kuchukua pesa niliyokuwa nimewekewa na Kanji baada ya kumpa dili la kusambaza mkaa kwa kijiwe. Upo hapo ndugu yangu.

Usianze kusema mimi ni yule Ngeleza wa madili ya IPTL na Richmond au Kiwila. Mimi nakula rushwa itokanayo na dili za kijiwe si kaya yenu.

Basi mwanawakwa, kutokana kuendelea kuongea kwa pozi na madenguzi huku umati wa wataka sabuni ya roho ukizidi kuumka, mlinzi wa ATM ile aitwaye Mnoko si alikuja kunipa somo kuwa nifanye chap chap kwa vile kulikuwa na wateja wengine wakingojea. Maskini hakujua kuwa mimi ni nani!

Maongezi yalikuwa hivi: “Bosi, naomba ufanye haraka. Kuna wateja wengine wanangojea kuhudumiwa kama wewe.”

Kwa vile Mnoko ni mtu mdogo sikujihangaisha kumjibu. Niliendelea na kuchonga.

Mnoko hakuridhika sawa na wateja wake. Alirudi tena na kusema; “Bosi, kuna wateja wanangoja huduma hivyo naomba ufanye haraka ili nao wapate huduma.”

Mnoko hakujua amechokoza nyuki. Kwa ghadhabu nimjibu. “Unajua mimi ni nani?”

Mnoko alijibu. “Mie hayo hayanihusu zaidi ya kutimiza wajibu wangu.”

Mimi: “Kijana huna adabu na hujui mimi ni nani. Neno moja linatosha kukufuta kibarua na mke na vitoto vyako vitateseka.”

Mteja mmoja alimnong’oneza mwenzie na kusema: “Yule jamaa ni waziri wa kijiwe anayeshughulikia mkaa.”

Mwenzie alisema: “Sasa anapouliza kama mlinzi anajua yeye ni nani inaingilianaje na biashara?”

Mwingine alidakia, “Yule si fisadi wa kisukusi tena mshamba aliyeukwaa ukuu kutokana na kijiwe kutawaliwa na mafisadi tu.”

Huku Mnoko akiwa amepigwa na butwaa akiendelea kunidai nifanye haraka mteja mwingine alisema tena kwa sauti ya juu, “Huyu anayesema yeye ni nani zaidi ya kuwa mshamba mmoja mwenye kijicheo cha kupendelewa? Hebu sikiliza hata lafudhi yake ya unanijuaga mimi ni nani. Wewe ni nani zaidi ya kuwa limbukeni wa kawaida?”

Kutokana na wanakijiwe kuwa na tabia ya kujichukulia sheria mikononi, sikumjibu huyu mkota kwa kuhofia kuzushiwa na kuchomwa moto kama kibaka. Nilifanya haraka na kuchukua pesa yangu tayari kwenda ofisini kwangu kumfukuzisha kazi Mnoko kwa unoko na ukosefu wake wa nidhamu.

Pia sikutaka kuendelea kuwa pale nikizozana na Mnoko kuhofia wambea wajiitao waandishi wa habari kurekodi maongezi yetu nikaibika. Kweli hasira wakati mwingine hasara. Maana niliumbuka siku ile hakuna mfano!

Nasikia na lisilikali fisadi na jizi liliwahi kumwambia Sammy Sixx: “Unajua sisi ni nani?” Matokeo yake wameichinja Richmonduli tena kwa kutumia mikono ya Sixx mwenyewe ambaye sijui ataweka uso wake wapi kama kweli ana chembe ya roho!

Juzi nasikia Ewassa na Rosti Time, waliangusha bonge la pati kusherehekea kuzikwa aibu zao! Ama kweli kaya hii ni Danganyika tena danguro la mafisadi kutanua na kuiba watakavyo! Sijui hata mantiki ya msanii kwenda akijigamba kuwa atapambana nao ilhali ndiyo wanaoamua akae ukuuni.

Angefanya fyoko wangemtimua na kukichagua kikaragosi kingine tayari kusimamia wizi na ujambazi wao. Kumbe mzee Butuka alipobotuka na kubwatuka akisema mkuu wa Kaya yetu hapa kijiweni ni mtumwa wa mafisadi hakudanganya!

Wengi walikuwa wanamtaka afanye maamuzi magumu wasijue hatafanya. Unadhani ni mchezo kufanya uamuzi mgumu wa kujivua nguo hadharani na kutembea kama hayawani kama kuendelea kutumiwa na kina Richmonduli na Kagodoka?

Laiti walevi wangekuwa wana akili na si kuendeshwa na matumbo yao. Huu ulikuwa wakati wa kumtimua bwana mazingaombwe na kujikomboa. Kwa vile aliyewaloga alikwisha kufariki, ni mganga gani atawasaidia?

Kwa vile walevi na wakubwa zao wameamua kufanyiana uchangudoa, hakuna wa kuwalilia bali wajilaumu na kujililia wenyewe. Ukitaka kujua kuishiwa, aanza kuuliza. Unajua mimi ni nani? Kwani we Mungu au gendaeka wa kawaida ngurumbili mwenye kila mapungufu.

Hata wapuuzi kama Saddam Hussein, Chemical Ali na majuha wengine walizoea kuwauliza Wairaki: “Unajua mimi ni nani?”

Wewe si sawa na inzi anayeshida na kutapika kwenye viatu vya wafadhili kama alivyosema balozi wa Uingereza. Je na Richmonduli na Kagodoka ni nani?

Ngoja niende zangu Idodomya nikawalambe bakora waheshimiwa wa mjengoni.
Chanzo: Tanzania Daima Feb.17, 2010.

No comments: