The Chant of Savant

Wednesday 31 October 2012

Je CCM watamkumbatia Nagu au kumwangukia Sumaye?



 Chama Cha Mapinduzi (CCM) hujitahidi kuficha aibu zake kwa kuwabana wanaodhaniwa kutaka kukiaibisha, kashfa ya rushwa kwenye uchaguzi wa ndani wa chama uliopita haifutikwi chini ya busati. Hakuna mwiba unaoikabili CCM kama madai ya waziri mkuu wa zamani Fredrick Sumaye kuwa uchaguzi ulitawaliwa na rushwa.

Sumaye alipotoa madai yake CCM ilitumia busara ya kuepusha malumbano. Lakini taratibu zilianza kuibuka tuhuma nyingine za dhambi hiyo hiyo ya rushwa hasa baada ya kufanyika uchaguzi wa Umoja wa Vijana wa (UVCCM). Kuna madai kuwa rushwa ilitembea nje nje. Ingawa rushwa ni jadi ya CCM, kuzudi kwake kulimfanya mwenyekiti wake rais Jakaya Kikwete kusema, “Nawaambieni, mkifanya mchezo ipo siku mtakuja kujuta maana mkishamchagua kiongozi asiyefaa, mtalazimika kuwa naye huyohuyo hadi mwaka 2017 na kama waswahili wanavyosema majuto ni mjukuu,” 
Wengi walimuona Kikwete kama mnafiki na mwenye kutapatapa kutokana na ukweli kuwa ndiye aliyefunga rushwa ndani ya chama na serikali. Rejea kuendelea kuwakingia vifua watuhumiwa wa rushwa kama vile Andrew Chenge na Dk Idris Rashid waliobainika na mamlaka za Uingereza kupokea rushwa ili kununua rada mbovu kwa bei mbaya toka kwenye kampuni la BAE.
Rejea kuendelea kumlipa marupurupu na stahiki za kustaafu waziri mkuu wa zamani Edward Lowassa hata baada ya kubainika kushiriki ufisadi wa Richmond. Rejea kuwarejesha kwenye baraza la mawaziri watu walioshiriki kwenye kuuza nchi kama vile Dk Abdallah Kigoda.

Yote tisa, baada ya Sumaye kushupaa na kutamka hadharani kinyume na taratibu za chama kuwa aliyemshinda kwenye uchaguzi Waziri katika Ofisi ya Waziri Mkuu (Uwekezaji na Uwezeshaji) Mary Nagu kutokana na rushwa, CCM imejikuta msambweni. Sumaye bado ana ushawishi chamani. Je CCM itamkumbatia Nagu na kumtosa Sumaye au kumwangukia na kumtosa Nagu. Yetu macho.

No comments: