The Chant of Savant

Friday 13 November 2015

Mlevi akumbuka Kiquete kuingiana EPA kuondoka na Escrow

            














Utawala wa rahis mtaafiska Njaa Kaya Kiquette ulisifika kwa mambo mengi ya hovyo mojawapo ikiwa ni kukumbwa na kashfa mara kwa mara. Kwani lilikuumbwa na kashfa hata kabla ya kuundwa huku jamaa akituhumiwa kushiriana na rais Mstaafika Ben Makapi kuchota njuluku Banki kuu kwenye fuko la madeni ya nje almaaruf EPA. Wote wawili hawa kukiri au kukanusha. Hata hivyo, ushahidi wa kimazingira unaonyesha ukweli hasa pale Kiquette alipowataka waliochota fedha hizo kurejesha badala ya kuwafungulia mashtaka.  Hata ukimya wake na kukwepa kukiri au kukanusha unaweza kuwa ushahidi mzuri tu unaoelekeza kwenye ukweli wa mambo.
            Jamaa alipowambia wenzake kurejesha njuluku na si kuwashughulikia, wenye akili walijiuliza; Je ni waarabu wa Pemba? Je kuamuru kurejeshwa chumo la wizi si kushiriki wizi ule ule kwa mlango wa nyuma? Je si motisha kwa wezi wengine –hata ambao hawakuwa na mpango wa kuiba –kuiba wakijua hakuna adhabu wala maumivu?
            Bahati mbaya, jamaa hakuwahi kueleza mantiki na sababu za kupinda sheria kuwanusuru wezi kama hanao ushirika. Wengi walitaka kusika utetezi wake.  Jamaa ameondoka na EPA kama alivyoingia navyo. Ameondoka amechafuka zaidi kwa kashfa nyingine ya Escrow. Hapa ndipo usemi kuwa aliingia kwa EPA na kuondoka na Escrow unapata maana.
            Jamaa anaingia kwenye vitabu vya historia kama rahis aliyewaonea huruma wezi kiasi cha serikali yake kusifika kwa ufisadi zaidi ya mema. Atakumbukwa kwa matumizi na matanuzi yake yaliyoongezea uchungu kwa walipa kodi walioibiwa haya mabilioni ya EPA na Escrow. Nani anaweza kusamehe au kusahau kashfa ya Richmond ambayo ilimhusisha mshirika na rafiki yake mkuu waziri wake mkuu Eddie Lowassa ambaye hadi kesho anasema alitolewa kafara. Je waliozoea kuuibia umma kwa maslahi binafsi na kisiasa walikuwa nyuma ya wizi huu, ni juu ya msomaji kuamua mwenyewe.
            Licha ya kuzidi wizi wa mabilioni, utawala wa jamaa ulishuhudia deni la taifa likifumka kupita viwango tokana na matumizi ya hovyo na ukwapuaji ambapo wahusika hawakuchuliwa hatua. Nani mara hii atasahau utamaduni mpya wa kuficha majina ya walaji aliokuwa akiandamana kwenye mamia ya safari zake ughaibuni?
            Pia, utawala wa jamaa unasifika kwa kuvumilia mafisadi wengi walikingiwa kifua bila kujua sababu za msingi za kufanya hivyo. Rejea, mfano, mamlaka za Uswisi zilipolalamika kutopata ushirikiano toka lisirikali kurejesha mabilioni yaliyofichwa huk, bada Badala ya kushangilia kitendo hiki cha utu, tulishuhudia balozi wa Uswisi nchini Olivier Chave akitishiwa na mwanasharia mkuu wa wa wakati ule Freddie Werema aliyejizolea sifa ya kutetea uoza kuliko uadilifu. Ni huyu huyu aliyetishia kumkata kichwa mheshimiwa mbunge aliponyooshea kidole ujambazi wa Escrow ambapo matapeli wa kitanzania na kimataifa waliweza kutumika kuwaibia watanzania jumla ya shilingi zipatazo bilioni nyingi.
            Wakati baadhi ya washirika wa jamaa wakikerwa na kufichuliwa madhambi yake, yeye alikuwa kimya akitabasamu kama kawaida kana kwamba hakuna kilichotokea! Wengi walianza kuuliza. Ndiyo haya Maisha Bora kwa Wote au kwa baadhi tena wateule, wake na watoto, waramba viatu na marafiki zao?
            Mtangulizi wa jamaa aliondoka akinuka kwa kashfa ya kufanyia biashara ikulu na kujitwalia mali za umma, jamaa amempiku. Kwani ameondoka akinuka wizi kwa kutoshughulikia waliovunja Benki kuu na kuiba mabilioni.
            Wapo wanaodhani wizi wa Escrow –sawa na wa EPA –una mkono wa chata twawala. Kwanini wizi huu wote ulifanyika karibu na uchaguzi ambapo chama kilikuwa kinataka kushinda kwa udi na uvumba? Hapa ndipo ulipo mkanganyiko ambao ulimhusisha wore waliopo na waliotimka.

            Hata hivyo, kilichowazi ni ukweli usiopingika kuwa Kikwete anaondoka madarakani akiwa ameweka rekodi ya kuingia na kuondoka madarakani kwa kashfa za wizi wa mabilioni ya watanzania maskini ambao serikali yao licha ya kuruhusu wizi inaendeshwa kwa fedha za kukopa na kuomba. Hapa hujaongelea ni namna gani ofisi yake imetumika kuanzishia NGO za bi mkubwa kwa ajili ya kutunisha fuko la baada ya kuondoka ofisini. Hapa hujagusia kashfa zilizowahusisha watu wake wa karibu na hata yeye mwenyewe.
Chanzo: Nipashe Nov., 14, 2015.

No comments: