The Chant of Savant

Tuesday 3 November 2015

Kijiwe champongeza Dk Kanywaji kwa urahis


 














            

Baada ya wapingaji kufanya kosa la mwaka kwa kumkumbatia adui yao waliyembomoa hadi akabwaga uwaziri mkubwa kiasi cha kuiwezesha Chama Cha Maulaji (CCM) kushinda kirahisi, Kijiwe kimeamua –kwa makusudi na roho safi –kumpogeza Dk Kanywaji Makufuli.
             Mpemba anaingia akiwa na bashasha kidogo. Anakula mic, “Yakhe mmesikia jinsi wapingaji walivokiwezesha chama twawala kuendelea kutula?”
            Mgosi Machungi anachomekea, “Utaiwa wewe au kuana wao kwa wao haiwi mtu hapa.”
            Kapende anakamua mic,”Kama mkikumbuka, nilikuwa mpenzi wa upingaji kabla haujaingia kitanda kimoja na Luwasa. Kwa vile wapingaji walituona sisi mabwege na wasio na kumbukumbu kwa kumkumbatia yule yule waliyetuaminisha ni fisadi, kura yangu niliharibu.”
            Mijjinga anakamua mic, “Ni kweli usemayo ndugu yangu. Hata mimi nilitaka hata kugombea uishiwa. Lakini baada ya kuona chata nililotaka kutumia limemkumbatia huyu jamaa, niliamua kuachana na ndoto za ubunge na kuharibu kura yangu. Utadhani tuliambiana.”
            Mipawa naye hajivungi. Anakula mic,”Kusema ukweli jamaa wametunyima fursa ya kuleta mageuzi kwa ajili yetu na vizazi vijavyo. Inasikitisha na kukatisha tamaa ukiachia mbali kuudhhi. Sijui tutafanyaje baada ya jamaa kuondoka na vyama vinne kwa mpigo?”
            Sofia Lion aka Kanungaembe aliyeingia punde akiwa ametinga kwenye mavazi ya CCM huku akishangilia kwa sana anakula mic,”Yako wapi? Tuliwaambia hashindwi mtu hapa piga ua. Sasa mtasemaje zaidi ya kuufyata.” Anasimama na kuangalia huku na kule na kuendelea, “Jamani, hamna haja ya kusikitika. Amkeni tushangilie ushindi wa ndugu yetu mwenzetu Dk Kanywaji Makufuli ambaye –kama alivyoahidi kwenye kampeni –lazima awafunge mafisadi akiwamo mtu wenu aliyemgalagaza chari.”
            Msomi Mkatatamaa anakwanyua mic, “Japo sikubaliani na da Sofi kwa yote aliyosema, nakubaliana naye kuwa tunachopaswa kufanya hapa ni kumzonga Makufuli atimize ahadi zake. Hakuna kitu kimenivunja moyo kama kuona watu wanavyoshindwa kuisoma na kuelewa historia kiasi cha kujifunza toka kwake. Nimehuzunishwa sana na kushangaa sana kuona kuwa wanasiasa wetu walishindwa kujifunza toka kwa Mremavu aliyeua NCCR-Mageuko mwaka 1995. Kwa upande mwingine naweza kusema kuwa upogo wa kumkubali Luwasa azike vyama vinne kwa mpigo ulitokana na ruiya ya kudhani kuwa kuondoka kwa Luwasa CCM kungesababisha vigogo wengine wamfuate kama ilivyo kuwa kwa rafiki yake Dk Kanywaji, Raira Odinga alivyofanya kule kwenye kaya ya nyayo wasijue siasa za Bongo ni tofauti na za kule. Kama walivyesema wasemaji waliotangulia, sijui hawa jamaa wataweka wapi sura zao baada ya kutuletea balaa hili?”
            Kanji anaamua kutia guu, “Somi veve iko sema zuri. Hapa napaswa laumu pingaji. Imepiga tama yenyeve sasa talia na nani dugu yangu. Mimi furahi san asana ona chaguzi nakwisha salama ili vatu iendelee na biashara yake.”
            “Pamoja na kumkubali Dk Kanywaji ambaye tulisoma wote seminari tukitaka kuwa makasisi kabla ya kushindwa kwa uchapakazi wake, sitegemei jipya toka kwake. Utakuwa ubwege kutegemea mtu mmoja aubadili mfumo uliomlea na kumkuza. Sana sana mfumo wa ulaji utambadili naye awe kama wenzake. Mmesahau kuwa kambale wote wana sharubu siyo?” anajibu mheshimiwa Bwege huku akikuna kidevu chake chenye mvi kama Dk Kanywaji anayedai walisoma wote seminari kabla ya miili yao kushinda roho zao.
            Msomi anarejea tena, “Sina haya ya kupingana nawe. Ila ukimlinganisha Dk Kanywaji ambaye mimi nilimfundisha kemia pale chuo kikuu cha Manzese, bado ana udhu. Kubadili au kubadiliwa na mfumo itategemea na shinikizo letu katika kumtaka atimize na kutekeleza ahadi zake lukuki alizotoa kwenye kampeni. Nadhani pia inabidi tumponge Luwasa kwa ushindi mnono hasa kufanikiwa kulipiza kisasi kwa waliomshitaki akautema uwaziri mkubwa na kuweza kuua vyama vinne kwa mpigo kama inzi. Pia nashauri tuanze kuangalia namna ya kubadili kijiwe chetu kuwa chama mbadala baada ya vyama vyote vya siasa vilivyopo –ima kugeuka CCM B au kusambaratishwa na upogo na uroho wa kutaka kutumiana vikaisha kutumiwa na kuuawa mchana kweupe.” Anakohoa kidogo na kuendelea, “Tukubali tumeingizwa mkenge na wale tuliodhani ni wenzetu wakati ni wenzao.”
            Kabla ya kuendelea, Mbwamwitu anachomekea, “Mnashangaa nini wakati wenzenu waliuza mechi? Hamkuona akina prof Pumba na Dk Slaa walivyostukia dili? Kumbe hamkujua hili?”
            Msomi anamtazama Mpemba na kuendelea, “Nadhani sasa tuelekeze macho na masikio yetu kule Zenj ambapo jamaa wa madevu anang’ang’ana angalau aendelee kuwa kwenye serikali ya umoja wa ulaji kitaifa. Tuombe Mungu wasinyotoeane roho kwa sababu ya ngurumbili wawili wanaogombea ulaji. Hapa lazima busara itumike ili kuendelea kutanua kama walivyozoea. Hata hivyo, naweza kusema kuwa ufa mkubwa umeishatokea.”
            Mijjinga naye anarejea, “Nakuunga mkono msomi mwenzangu. Tunachopaswa kufanya hapa ni kuunda kikosi mbadala ya kukomboa kaya hii. Najua Dk Kanywaji atakwamishwa na wenzake vinginevyo afanya kile alichofanya Mutharika wa Malawi, aunde chata lake akiwa humo humo ili kuwasulubu wale mafisadi aliotwambia anawajue ili asiishie kuwa kama njaa Kaya aliyesema anawajua mafisadi na wauza bwimbwi akaishia kula nao.”

            Kijiwe kikiwa kinanoga si likaja kundi la wakota wa CCM likinengua na kushangilia!
Chanzo: Tanzania Daima Nov., 4, 2015.

No comments: