The Chant of Savant

Saturday 24 June 2017

Uhuru wa habari: Mbona viongozi wetu wanapingana?


            Katika kuangalia haki na uhuru wa kukusanya, kusambaza, kutoa na kupata habari nchini, leo nitajikita kuonyesha mkanganyiko uliopo serikalini kiasi cha kugeuka tatizo kubwa kwa baadhi ya vyombo vya habari visivyokuwa “ndiyo mzee.” Kufungiwa gazeti la Mawio hivi karibuni kutatumika kama kigezo cha kudurusu hoja hii.  Katiba ya Tanzania inampa uhuru kila mtanzania kutoa, kupokea, kusambaza, na kupata habari ilmradi asivunje sheria. Gazeti la Mawio lilifungiwa kwa miaka miwili. Kosa? Kuchapisha picha za marais wa zamani wanaohusishwa na ufisadi. Chanzo cha habari? Wabunge waliosema wazi kuwa marais wa zamani walioshiriki ufisadi–kubwa likiwa ni kuingia mikataba ya kijambazi–washitakiwe. Je hapa kosa la gazeti liko wapi; kuripoti kilichotamkwa hadharani tena mbele ya kamera na vinasa sauti vya vyombo vya habari? Wengi walidhani kuwa gazeti lilikuwa limeandika uzushi. Je si kweli kuwa, mfano, rais Benjamin Mkapa alijitwalia mgodi wa Makaa ya Mawe wa Kiwira chini ya kampuni yake na mkewe iitwayo ANBEN yaani Anna and Ben ambayo ni majina ya kwanza ya Mkapa na mkewe?
            Wa pili kuhusishwa ni rais mstaafu Jakaya Kikwete. Je gazeti liliandika uzushi? Kama ni kukamata basi angekamatwa mbunge wa Singida Mashariki (CHADEMA) Tundu Lissu aliyeliambia bunge kuwa mikataba ya hovyo ya uwekezaji kwenye madini–uliogeuka uchukuaji hata wizi kama alivyosema rais John Magufuli–ilisaniwa na Kikwete hapo tarehe 5 Agosti, 1994. Je si kweli kuwa Kikwete alisaini mkataba unaomhangaisha Magufuli na watanzania kwa ujumla? Kosa liko wapi hapa? Je na Lissu atafukuzwa bungeni? Nadhani wapinzani wameonyesha uzalendo wa hali ya juu kwa kuliita koleo koleo na si kijiko kikubwa; na kumkosoa rais au serikali si kosa kisheria.
            Sasa ngoja tuonyeshe serikali inavyojikanganya kiasi cha kujipinga na kuzua mkanganyiko. Hivi karibuni mkurugenzi wa Maelezo Dk Hassan Abbas alisema kuwa vyombo vya habari vinaruhusiwa kuikosoa serikali. Abbas alisema “hakuna chombo cha habari kitakachochukuliwa hatua kwa kukosoa, haki hiyo ipo kwa mujibu wa Sheria ya Huduma za Habari ya Mwaka 2016 kifungu cha 51, tutaendelea kuthamini na kufanyia kazi ukosoaji huo.” Je Mawio nalo limo humu; nalo si chombo cha habari?
            Bahati mbaya, hakutofautisha kati ya kuikosoa serikali na kumkosoa rais ambaye kimsingi ndiye mkuu wa serikali. Je kweli serikali haikosolewi? Mbona bosi wake anasema vinginevyo? Aliyekuwa Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo Nape Nnauye aliyemteua Abbas kabla ya kutenguliwa uteuzi wake kwa kuwashika pabaya wasioguswa alikaririwa kabla ya kufukuzwa akisema “serikali ni rahisi sana kujisahau, ama inaweza ikaziba masikio, hivyo ni lazima pawepo na ‘very strong media’ zitakazofanya kazi ya kuiambia Serikali.” Je serikali haikujisahau kiasi cha kuingia mikataba ya kijinga? Strong media zinafungiwa; zinaachwa zinazojikomba. Huku ni kujipinga Dhahiri.
            Hata hivyo, kupingana kwa mteule na bosi wake hakuashii kwa Abbas.  Hata Nape anaonekana kupingana na aliyemteua yaani rais Magufuli ambaye alikaririwa akisema “nawaambia wamiliki wa vyombo vya habari be careful and watch it (kuweni waangalifu) kama mnadhani mna freedom (uhuru) ya namna hiyo not to that extent (siyo kwa kiasi hicho).” Kama haitoshi, Magufuli aliongeza kusema kuwa“uzalendo umepotea na unapotezwa na viongozi kwa interest (interests) (manufaa) zetu.” Kwanza, kwanini uzalendo uwe wa upande mmoja? Strong media hazijikombi; zinakosoa hata kama kufanya hivyo kunawaudhi wahusika. Bahati nzuri Magufuli anajua lilipo tatizo ila hataki kulishughulikia vilivyo.
            Mfano, Magufuli anasema “watoaji haki katangulizeni Tanzania, majaji mnafanya kazi nzuri katika kutafuta haki, tutengeneze Tanzania yetu, mimi nipo hapa temporary (kwa muda mfupi), makamu wa rais yupo temporary; everybody is (in power) temporary because the life is so temporary (temporal) (kila mtu yupo kwa muda mfupi kwa sababu maisha ni mafupi), lakini Tanzania yetu si temporary, itaendelea kuwepo tuilinde hii Tanzania yetu ambayo because it is suppose to (supposed to be) be there permanently (kwa sababu idumu).” Hii kidogo inashangaza. Mbona magufuli hatangulizi uzalendo kwa kukubali; Tanzania ni ya wote na wana mawazo hata kama ni kinzani? Kuna haja ya washauri wa rais kujitahidi kumkumbushwa anayosema ili asijipinge au kupingana na watendaji wake ukiachia mbali kuvunja sheria. Au Magufuli anafanya kile ambacho waingereza huita holier than thou kwa kutotaka kukosolewa wala kushughulikiwa watangulizi wake waliotenda uovu wa wazi bila sababu ya msingi zaidi ya tamaa na uroho wa kawaida?
            Tumalizie kwa kuwashauri washauri wa rais wawe wanamshauri vizuri kuhusiana na kupingana kwa serikali yake. Anaongelea uzalendo wakati akijua kuwa ni serikali za chama chake zilizoukosa na kuliingiza taifa kwenye matatizo ya ufisadi tunayopambana nao. Hata hivyo, nimshukuru Magufuli kwa kuanza kushughulikia kashfa makaburi kama vile Escrow. Ila asiume upande mmoja na kupuliza mwingine. Atende haki kimsumeno; akate mbele na nyuma bila kupatiliza wala kupendelea. Tanzania ni yetu sote bila kujali cheo cha mtu.  Kama serikali haitaki kukosolewa isikosee. Kama ikitaka kuheshimika ifanye mambo ya heshima; si ya hovyo kama kuingia mikataba ya hovyo. Tukiendelea kutishana, kupatilizana, kudanganyana, na kuogopana, kama taifa, tutaangamia. Hakuna asiyekosea.
Chanzo: Tanzania Daima Jumapili kesho.

No comments: