The Chant of Savant

Sunday 11 June 2017

Wahamiaji Haramu: Kuna siku Tanzania itatawaliwa na mgeni



Baptista Marco raia wa Burundi aliyekamatwa nchini hivi karibuni akifanya kazi kama mwanasheria wa TBS kinyume cha sheria.
                Matukio ya wageni kukamatwa wakifanya kazi nchini–tena nyingine nyeti–kinyume cha sheria yanazidi kuongezeka kiasi cha kuanza kujenga shaka juu ya usalama wa taifa na wananchi kwa ujumla. Hapa lazima tujiulize tatizo liko wapi; na nini kifanyike kuondoa hatari hii ambayo inaweza kutugharimu kama taifa. Wahenga walinena: usipoziba ufa, utajenga ukuta; jambo ambalo ni gharama baada ya nyumba kubomoka.
            Kuna matukio ambapo wakimbizi wa kiuchumi wa kigeni wamemeajiriwa nchini na kufanya kazi kwa muda mrefu bila kustukiwa. Je vyombo vyetu wa usalama vinafanya kazi gani na kama vinafanya kazi je vinaifanya vizuri? Mtu anaajiriwa kwa ngazi ya juu. Je anapataje kazi kama hakuna rushwa? Je wako wangapi wahalifu wa namna hii? Je wako peke yao au wana mitandao ya watanzania wanaowasaidia kutekeleza jinai hii? Je mamlaka zinachukua hatua gani dhidi ya mitandao hii ambayo bila shaka itakuwa inajulikana?
            Japo mimi ni muumini wa umoja na ushirikiano vya kweli kwa Afrika, si mpenzi wa ushirikiano wenye kuvunja sheria ambapo baadhi ya wahalifu hujipenyeza kwenye nchi nyingine kinyume cha sheria na kujipatia kazi na elimu wakati wananchi wakikosa vitu hivi. Si mpenzi wa uchoyo wa baadhi ya mataifa hata watu kupenda kwenda kuchuma kwa wenzao bila kujali madhara wanayosababisha au bila kuruhusu watu kutoka huko wanakohujumu kwenda kupata kazi au kuishi kwenye nchi husika. Uumini wangu wa Afrika ni kwa nchi zote kuunganishwa na kurejea kuwa moja kama Afrika ilivyokuwa kabla ya kugawanwa na wakoloni kwenye mkutano wa Berlin 1884-85.
Kwa taifa kuondokana na kadhia hii, kuna haja ya kutunga sheria kali zinazowapa adhabu ya vifungo virefu sana hawa wakimbizi wa kigeni waliojipenyeza na kupata kazi au elimu nchini kinyume cha sheria ili wasifaidi vitu hivyo nchini na nje ya nchi ama makwao. Pia wahalifu hawa wanapogundulika, wasipewe dhamana ili wasitoroke. Hapa ndipo umuhimu wa kubadili sheria ili kuondoa dhamana unajitokeza kama kweli taifa lina nia ya kuondokana na kadhia hii.  Maana uzoefu unaonyesha kuwa wengine hupewa dhamana na kutoroshwa na washitiri wao ili wasiumbuke kama ilivyotokea kwenye kashfa ya kutorosha wanyama hai kwenye Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Kilimanjaro ikimhusisha mhalifu wa kipakistani ambaye alitoroshwa nchini.
Pia kuna haja ya mamlaka kujua; kwa sasa Tanzania inao raia wengi wa kigeni wanaoishi na kufanya kazi nchini kinyume cha sheria tokana na mfumo wetu mbovu na ile hali ya wananchi kutoelimishwa vya kutosha ili kusaidia kuwabaini wote wanaofanya hivi.  Haiwezekani watu wetu wakose ajira wageni wapate. Hapa lazima kutakuwa na tatizo kubwa mojawapo ikiwa ni ukosefu wa uzalendo na umakini katika kulinda mipaka na maslahi ya taifa letu. Nchi nyingine ukiingia tu, kila mtu anajua; na taarifa zako zinaifikia serikali mara moja. Tuachane na mambo ya kizamani. Kwani wakimbizi hawa wa kiuchumi wanadhoofisha uchumi wa taifa letu kiasi cha kufanya serikali ishindwe kutoa huduma bora kwa wananchi wake.
            Jingine, wote watakaobainika kutenda jinai wafilisiwe mali walizochuma nchini kwa kutumia elimu na fursa ya ajira nchini ili liwe somo kwa wengine wanaopanga kutenda jinai kama hii. Twende mbali; sambamba, tuwafunge waliowawezesha, kwa kuwahifadhi hata kuwatoza rushwa na kuwapatia ajira kinyume cha sheria.  Hapa lazima tuwe wakali na kuhakikisha kuwa yeyote anayeshirikiana nao , bila kujali cheo chake au uraia wake, anaadhibiwa vilivyo ili kuondoa uwezekano na vishawishi vinavyoshamirisha jinai hii nchini. Maana, tukiendelea na uhovyo na ulegelege huu, kuna siku Tanzania itatawaliwa na raia wa kigeni bila kujua; jambo ambalo ni hatari kwa usalama wa taifa letu.
Kuondokana na kadhia hii, tuwabane marais wetu waunganishe nchi zetu ziwe nchi moja ili kuondoa kadhia kama hizi zinazoweza kuvuruga uhusiano wa mataifa.
            Tumalizie kwa kuitaka serikali hasa rais John Magufuli ambaye anasifika kwa juhudi zake za kuanzisha vita dhidi ya kughushi sifa na vyeti vya kitaaluma, apanue wigo hadi kuwashughulikia matapeli hawa wanaojipenyeza nchini na kupata elimu na kazi nchini bila stahiki yoyote kiutu na kisheria. Inatosha kusema kuwa wakati wa kuigeuza Tanzania shamba la baba inabidi ufikie mwisho. Hili litawezekana tu pale wananchi wetu watakapoelimishwa juu ya madhara yanayosababishwa na wakimbizi wa kiuchumi ambao wengi wao wanapata usaidizi toka kwa watanzania wenyewe wasijue wanajikomoa na kujichelewesha. Haiwezekani nchi yenye kila aina ya vyombo vya usalama iendelee kuhujumiwa kirahisi hivi huku vyombo husika vikipoteza muda kuwachunguza wapingaji, wapinzani na mambo mengine madogo badala ya kutoa kipaumbele kwa usalama wa taifa kwa maana ya usalama wa taifa badala ya kuwa usalama wa chama kama ilivyo kwa sasa ambapo vyombo vyetu vya usalama vinatumika vibaya.
Chanzo; Tanzania Daima Jumapili leo.

No comments: