The Chant of Savant

Wednesday 28 June 2017

Kijiwe chataka kujua nini sharia za madini zitaanza kubadilishwa


     Baada ya rais Joni Kanywaji kusema atalazimisha Mjengo kukaa muda zaidi ili kurekebisha sharia za madini, Kijiwe kililipuka kwa furaha kabla ya kuzimika matumaini baada ya porofwedheha Joni kutoka Ukanadani kuja kuweka mambo sawa na kuuzima moto wa mabadiliko ya sharia.
            Msomi Mkatatamaa siku hizi anaingia mapema akiwa na inshu kibao. Akiwa amesheheni mzigo wa magazeti anayokopa kwa muuza magazeti anautua mezani na kuamkua na kusema “wenzangu mnasemaje kuhusiana na ahadi ya kuuamrisha mjengo ubadili sharia za madini na mafuta ili kupambana na upigaji ulioigeuza kaya yetu makinikia? Naona kama sakata la Escrew limefuta kila kitu kana kwamba lina thamani kuliko madini na nishati ingawa nalo ni sehemu ya nishati. Sijui wenzangu mna mikakati gani ya kuwarejesha hawa ambao wanaonyesha kuwa wepesi wa kusahau na kulaghaiwa kwa ahadi za maongezi hadi kutelekeza ubadilishaji wa sharia?”
            Mijjinga anakula mic ‘mie naona mambo mengi yanaendeshwa kizimamoto tena kwa kutegemea usongo wa dingi lakini si kaya. Namna hii tutaendelea kupigwa; kwa sababu tunaonyesha kama hatuko serious wala hatuna maandalizi. Kama unakumbuka waraka uliotolewa juzi na jambazi akashia kuwa hawakukubaliana kurejesha njuluku zetu, basi unaweza kuelewa anachohofia Dk Msomi. Hivyo, napendekeza tuandike waraka maalumu kwa dingi kukumbushia ubadilishaji wa sharia na kuwanyonga wale waliotuingiza kwenye mkenge hadi tukapigwa kijinga hivi.”
            Mpemba anampoka mic na kudema “yakhe nami nkuunga nkono. Kama tutaendelea kukubali kila jambo wallahi tutajaendeleapigwa bila sababu bali ulimbukeni wa baadhi ya wale waniofanya vitu kwa kukurupuka. Hata hivo, kama dingi atakumbushwa, naamini atarejea nchakato huu wa ukombozi wa kaya yetu.”
            Kabla ya kuendelea Mipawa anampoka mic na kusema “hakuna cha kurejea nchakato. Uko wapi ule wa Katiba Mpya ambayo ilikuwa muarobaini wa kila kitu. Si imeuawa ili kuendelea kulindana na kukomoana kwa kufanya mambo kwa akili ya chama kimoja wakati wa utawala wa vyama vingi. Kusema ukweli mie sina imani na chochote wala lolote hadi nione sharia zikibadilika na kurejewa kwa mchakato wa Katiba Mpaya.”
            Kapende aliyekuwa akibofya ki-Samsung chake anaamua kutia guu na kusema “mie simlaumu dingi hasa ikizingatiwa kuwa ameachiwa afanye kila kitu kana kwamba hana wasaidizi. Ninachoona akisaidiwa si chochote wala lolote bali kumuimbia kwaya ya sifa kiasi cha kukera na kuchusha. Hakuna ninapoumia kama kuona madaktari na hata maprofwedheha wakimsifia hata pale anapotimiza wajibu wake. Hapa kweli ipo shughuli. Nadhani sisi tujichukulie wadhifa wa kumshauri dingi baada yakuona aliodhani wangefanya hivyo kumgwaya kila mmoja akitetea kitumbua chake hata kama ikibidi kwa kujikomba.”
            Kanji naye anaamua kukamua, “veve sangaa vatu jipendekeza. Kama hapana pendekeza kupendeza dingi nataka afukuze yeye veve tampa juluku na laji nakula bure? Kama profesa napendekeza veve nani hapana pendekeza. Basi naji jiwe pendekeze ilete katiba mpya ya vananchi ili mambo yote ive safi au vipi dugu yanguni?”
            Sofia Lion aka Kanungaembe anatia timu na kuchonga “kwa vile sisi si wateule wala wajipendekezaji na waimba sifa, lazima tuseme ukweli. Kwani hatuna cha kupoteza. Ninachomaanisha hapa ni kwamba kama hawatabadili sharia za mimawe na mifuta kila kitu ni bure. Ni sawa na kutwanga mawe. Nadhani hawa jamaa waliwahi kuja kujifanya wanajutia kosa lao na wako tayari kutapika njuluku ili kutuzuga tupoteze muda wakati wakijiandaa kutushikisha adabu.”
            Mheshimiwa Bwege anamchomekea da Sofi na kukwangua mic na kudema “Sofia umejuaje kuwa ilikuwa nawaza kusema uliyosema. Nakubaliana nawe mia kwa mia kuwa hawa jamaa wanataka kuendelea kutugeuza mabwege. Wanafanya kile ambacho watasha huita to buy time as you contemplate how to thwart your enemy outfront.”
            Kabla ya kuendelea mzee Maneno anamkatiza kwa kusema “Mheshimiwa Bwege lugha hiyo naona kama imepiliza.”
            Kila mwanakijiwe amepigwa na butwaa ile mbaya hasa ikichukuliwa kuwa hii ni mara ya kwanza kwa mheshimiwa Bwege kumwaga ung’eng’e. Wengi tulidhani haupati kumbe kifaa! Tena anaongea ung’eng’e mufti bila kubukanya na kuchanganya na broken.
            Mheshimiwa Bwege anaendelea kuchonga “samahanini kwa kuongea kingindo ndugu zanguni. Ibidipo hubidika. Nilidhani nilikuwa kwa mama wa ukoloni kule Londoni kumbe niko hapa Danganyika nikidanganyika kama kawa. Tusameheane sana ndugu zanguni. Yote yalinitoka katika ile hali ya kutoa mchango kwa kaya yangu ili kuiepusha na kupigwa pigwa na kugeuzwa shamba la bibi.”
            Mgosi Machungi ambaye aliingia akiwa amechelewa na akawa anafuatilia mjadala kwa makini anaamua kutia guu “wagoshi tikubaiane kuwa bia kuandamana kushinikiza kuejea mchakato wa kubadii shaia tinapoteza muda. Nadhani tokana na ukapa, baada ya jamaa kutiahidi wangeipa njuuku yetu, timeangaia kupata si kupatikana. Titakapopatikana ndipo titajua. Na hapo utasikia wanasiasa wakitafuta kia kisingizio ili tione hawana makosa.”
            Kijiwe kikiwa kinanoga si likapita shangingi la dingi wa Akashia. Acha tumtoa mkuku ili tumfanyie kitu mbaya kabla ya kwenda kutaifisha migodi yetu!
Chanzo: Tanzania Daima Jumatano leo.

No comments: