The Chant of Savant

Tuesday 18 July 2017

Kijiwe kwenda Ukonga kuwasalimia akina Escrew

          Leo Mgoshi Machungi amekuja na mpya. Si alikishangaza kijiwe aliposema kuwa alikwenda Keko kumuona Mgoshi Semtwashua na kuambiwa kuwa wale watuhumiwa wa Escrew wanaishi kwenye vyumba vya VIP lupango.
            Baada ya kuamkua anakula mic “wagoshi jana niishangaa sana.” Kabla ya kuendelea Mbwamwitu anadakia “kwani ulikwenda feri au bandari kushangaa namna vichwa 15 vinavyoweza kuingia na kupakuliwa bandarini bila kujulikana mwenyewe? Au ulikuwa chumbani ambako maji huingia sehemu na kugeuka kiumbe? Si ulisikia juzi namna watasha walivyotengeneza kondoo Dolly kwenye chupa tena kwa kutumia maji ya nonihino?”
            Mgoshi anajibu “hii hainishangazi hasa tikizingatia kuwa bado tina watu wanaodhani kuwa Dokta Kanywaji hawezi kuwatumbua kama aivowafanyia akina Eskoo ambao hata hivyo niiambiwa kuwa wanaisha kwenye vyumba vya VIP wakitanua kama vie hawako upango.”
            Kapende anampoka Mgoshi mic “ina maana Dokta Kanywaji amezidiwa ujanja na ndata wa lupango au ni uzushi wa kawaida? Nitashangaa na kusikitika kama habari hizi zitakuwa za kweli. Ama kweli ukishangaa ya Escrew utaona ya IPTL! hata hivyo, nani ajuaye? Lolote lawezekana kwenye kaya hii ya maajabu.”
            Kabla ya kujibu Kanji anakwanyua mic “na mimi iko sikia toka vatu yangu ya karibuni kuva ile vatu ya escrew naishi kama iko jumbani yao. Iko moja naambia mimi kuva napelekewa hata bibi kuburudisa yeye. Hii kaya iko complications mingi dugu yangu. Mimi ikodhani kuwa Svahili sana nagombea ile Singasinga kama bwabwa.”
            Kabla ya kuendelea mzee Maneno anamchomekea “hii kweli kali! acha ndugu yangu Kanji nikuchomekee. Mana sikuelewi. Unamaanisha nini unaposema kuwa Swahili nagombea Singasinga kama ubwabwa? Sasa kama napelekewa bibi kwanini isigombee hiyo bibi badala ya kugombea Singasinga au wanagombea yote kiasi cha Singasinga kulalamika kuwa haipati singizi tokana na hofu kama vilivyoripoti vyombo vya umbea hivi karibuni?”
            Kabla ya kujibu Mpemba anajibu “hapa mie ndhani huyu aongelea yale mambo ya Popobawa. Maana, nasikia haya mambo yako sana kule ati. Kwani yeye nani asiliwe? Mie ningependa nisikie kuwa nao yakhe waliwa kama walivokula njuluku zetu wallahi.”
            Mijjinga anakatua mic “mie Singasinga hanipi taabu. Nitasherehekea na kuwamwagia ofa ya kahawa kama nikisikia kuwa na Nshomile Rugetumbuliwa naye anashikishwa ukuta. Kwanini wao watutese wasiteseke? Kwanini wale vyetu vyao visiliwe? Natamani ningekuwa kule niwasheherehekee kama walivyosherehekea njuluku zetu.”
            Mchunguliaji anachomekea “mbona wanashikishwa ukuta sana kila wakitoka na kuingia. Mie nayajua maisha ya lupango. Ukitoka kwa pilato unavuliwa nguo zote ili kuhakikisha huiingii na mabomu kama vile bangi, fedha na mambo mengine. Jamaa kule wana laana ile mbaya. Wanakupekuwa kila mahali tena ukiwa uchi wa mnyama. Hivyo, kushikishwa ukuta wala si ajabu wala adhabu. Ni utaratibu wa kawaida.”
            Msomi Mkatatamaa aliyekuwa akibukua jarida moja la kimataifa liitwalo Corrupt Poor Countries anakula mic “Mtu binafsi akiliwa siyo real deal. Kama wao walituibia, kuna kosa gani yakawakuta haya? Hata hivyo, dua la kuku halimpati mwewe.  Kama alivyosema Mgoshi na Kanji, intelligence yangu inaniambia kuwa hawa jamaa wanaishi kama wako uraiani hasa ikizingatiwa kuwa wana njuluku ya kuhonga na kupewa upendeleo. Kama bangi na simu za mkononi zinapenyezwa, watashindwa kuhonga na kupewa upendeleo hasa ikizingatiwa kuwa kwao njuluku ambao hawakuzitolea jasho si tatizo. Sitashangaa kukuta madai haya ni ya kweli hasa ikizingatiwa kuwa bado kaya yetu ina ufisadi ambao umegeuka donda ndugu. Kinachofurahisha ni kwamba angalau Dokta Kanywaji amethubutu waliposhindwa wengi kiasi cha kuwatia kiwewe hadi wakamfuata kwake kumramba makalio kama alivyofanya Tunituni Makapi hadi akapayuka kuwa wapingaji ni wapumbavu asijue naye ni wale wale.”
            “Msomi usinikumbushe fisadi huyu mjivuni ambaye, hata hivyo, vyombo vya umbea havikumlazia damu zaidi ya kumpa kavu kavu aache upumbavu na upayukaji asijeishia walikoishia wenzake wa Brazil na Korea ya Kusini hivi karibuni walipofikishwa mbele ya haki bila kutarajia,” anachomekea Mipawa huku akiendelea kufyonza kipisi chake cha sigara kali.
            Mheshimiwa Bwege aliyekuwa akisikiliza kwa makini anaamua kutia guu “mie mpaka sasa sina imani na mazingaombwe na sanaa zinazoendelea mbele ya mapilato hasa kutokana na kuachiwa na wale jamaa wa Bandarini ambao walipiga wazi wazi wakaishia kuchomoka. Sijui walitembeza chochote kitu au waliowanasa hawakufanya homework yao vizuri. Maana system sasa inaonekana bwege na cha mtoto kiasi cha kuwadaka mafisadi wakachomoka kirahisi. Je hapa tatizo liko wapi au kuna namna mapilato nao wanafanya kama siyo mandata wanaochunguza kesi husika?”
            Sofia Lion aka Kanungaembe anakwanyua mic “kaka lolote linawezekana. Unategemea nini mapilato wanapokuwa kama yule aliyekwanyua njuluku za Escrew aliyelazimishwa kutema ulaji hivi majuzi? Sijui naye ataunganishwa na akina Bill Gereza na Endelea Chenga na profwedheha Anae Kajuamlo kwenda lupango lau kufanya vitu vyao kwenye mtondoo?”
            Kijiwe kikiwa kinaendelea si likapita shangingi la Bashite? Acha tumzomee tukitaka naye apelekekwe lupango kwa kughushi.
Chanzo: Tanzania Daima Jumatano kesho.

No comments: