The Chant of Savant

Saturday 7 September 2013

Mlevi ashukia `waishiwa` wezi na Foundations zao

Juzi wakati nikipita-pita kwenye mitandao na maeneo mengine ambapo ‘nyuzi’ huwa si siri, ‘niliinyaka’ ya mama mmoja mwizi muishiwa wa Chama Cha Mafisadi (CCM). Msichanganye hii CCM na ile inayowatawala. Sitaki shari bwana.
Nilinasa ‘kimemo’ cha ‘muishiwa msukule’ au wa kupendelewa aitwaye Catherine Magigez.
Alihomola madafu milioni kumi kwenda kununua madawati ayatoe kama takrima mkoani analotaka kugombea ‘uhishimiwa’ ili aibe zaidi.
Je, huyu si ‘kibaka wa kisiasa’ anayetumia cheo kujipatia ‘mafweza’ na kuhonga wapika kula ya kura? Wajua alichoraje `mchongo’ wake?
Simple, you just create a bogus foundation and go to government offices asking for dosh for development.
Yaani `kimakonde’ ni kwamba unaanzisha wakfu mfu na uchwara na kwenda kwenye ofisi za `lisirikali’ na kuomba msaada wa `njuluku’ ili, ima kuchangia maendeleo, au kutoa msaada. Utapeli mtupu!
Kama huna kitu hadi unaombaomba unawezaje kuleta maendeleo au kutoa msaada gani, kama siyo utapeli uchwara kama tunavyoushuhudia kila uchao?
Wewe mwenyewe ukiitwa msaada unaitika utatoa msaada kwa jeuri na `njuluku’ ipi? Yaani hamtumii hata chembe akili!  Shame on you!
Nilishastukia Wakfu au Foundations zenu. Hamna tofauti na ile kampuni ya Bi- Mkubwa ya MAWAWA yaani Maulaji ya Wake za Wakubwa.
Kila siku utamsikia Bi-Mkubwa msaka ngawira, mama Tamaa, akizurura kila kona ya dunia, akisaka misaada iishiayo mfukoni mwake kwa kisingizio cha kuwasaidia akina mama.
Unawasaidia akina mama au wanakusaidia kupata fedha za haraka kitapeli? Kwani hiyo wizara ya akina mama na watoto kazi yake ni nini?
Huu ni ujambazi mbuzi unaofanywa na walaji wetu, wake zao marafiki hata watoto wao.  Siku hizi Foundations au Wakfu mfu ni biashara inayoingiza fedha sana.
Hakuna siku nilipocheka kama Bi-Mkubwa fulani fisadi alipoteuliwa kwenye ulaji wa ubalozi kule ng’ambo.
Bibi huyu aliyesaidia ‘dili’ la Richmonduli kama mwanasharia, alipogundua kuwa mumewe hakuwa na kibarua ughaibuni, aliaamua kumuundia Foundation iliyoitwa Maajali Foundation.
Yeye na mumewe walianza `kuwashobokea’ wafadhili kama ilivyo mazoea ya waswahili wasiopenda kujigemea.
Walipata ‘mshiko’ kwa kisingizio cha kupeleka madawati kwa wanafunzi. Mlevi hakuacha kujiuliza. Kama unapenda sana elimu si ungepinga ujambazi wa Richmonduli?
Je, fedha za Richmonduli zingenunua madawati mangapi, tena bila kuombaomba na kuidhalilisha kaya yetu kama si utapeli na upunguani?
Kama unapenda wanawake na watoto, kwanini kutomshauri mumewe aache sera na siasa za kibabaishaji kama kuingia mikataba `fweki’ ya uchimbuzi wa midini na utoaji wa `minishati’?
Je, hiyo ‘fweza’ ingekomboa akina mama wangapi na watoto? Tumieni akili badala ya `masaburi’.
Kama unawapenda wanawake na watoto kwanini usipunguze kuzurura? Kama unapenda elimu kwa akina mama kwanini wewe ni `kihiyo’ usiyependa kutumia fursa iliyopo kujiendeleza ili uwe role model kwa hao akina mama zako na watoto wa kike?
Nikiwa nakata ‘kanywaji’, maswali mengi yalizidi kuniijia. Kama mnapenda elimu kama huyu mwizi muishiwa alivyofanya, kwanini mnaiua huku mkisomesha vitegemezi vyenu nje ya kaya yetu?
Kwa taarifa yenu, siku nikikutana na vitegemezi vyenu ughaibuni nitawapigia FBI wavipeleke Guantanamo kwa kosa la ugaidi wa kuangamiza walevi kielimu.
Hivi mgependa na kuthamini elimu mngegushi shahada na vyeti kweli? Hebu waulize akina Bill Lukuvison, Emmy Nchimbison, Makorongo Mahangason, Balozi Deodorusius Kamalason, Marry Nagudaughter na wengine walioghushi walivyopata shahada zao?
Kwa vile wakubwa zetu wameonyesha `kaungonjwa’ ka-kupenda PhD na `madude’ mengine makubwa, nina mpango wa kuanzisha dhehebu la dini na kuliita PhD yaani Prophecy, Healing and Deliverance au Utume, Uponyaji na Ukombozi (U3) ambalo litalenga maadui wakubwa watatu yaani Ukihiyo, Ufisadi na Utapeli hasa wa kughushi.
Hebu nimpashe huyu mama anayejifanya kupenda sana wanawake na watoto wakati hawapendi bali kuwahadaa. Mama mpenda haki za akina mama na watoto hasa elimu, kamwambie mumeo awatimue basi hao walioghushi.
Thubutu wakuchome kwa vile wanajua `madudu’ yako na hata ya huyo mumeo waliyemgeuza mateka kwa vile wanajua chafu yake.
Ngoja nimpashe hata huyu `muishiwa’ wa viti vya msukule aliyekwapua `njuluku’ zetu kule Ngorongorongo Conservation Area Authority (NCAA).
Kama unapenda sana elimu si ukasomee ualimu au ukafanye kazi ya kubwia vumbi la chaki, badala ya kukimbilia Mjengoni kupata posho ya mkao usio halali?
Huna aibu `kibaka we muishiwa’. Ungependa elimu ungeibia walevi au ungevumbua kitu lau uwaneemeshe?
Kaya yetu imegeuka shamba la chizi. Hii ni baada ya kuharibikiwa zaidi ya shamba la bibi. ‘Mijitu’ inajiita ‘mihishimiwa’ wakati ni miishiwa.
Hivi ni kuishiwa kiasi gani kwa ‘muishimiwa’ kwenda kwenye taasisi za umma akiombaomba? Au ni kwa vile ‘lisirikali’ lake nalo linaishi kwa kubomubomu ughaibuni?
Kwanini msibadili jina la kaya na kuwa Matonyaland au Ombaombaland? Ikizidi ikipungua basi ipe jina zuri la Bwimbwiland kama si Fisadiland or Venaland, hata Chiziland laweza kufaa kama mambo ya ‘kijichizi’ na ‘kijuha’, yanafanyika na hakuna anayestuka wala kuchukua hatua.
Kama si kuogopa kutukana mie ningependelea iitwe Goonland kama siyo Zombiland. Maana ukiangalia hata wizi mwingine wala wanaoufanya hawatumii hata chembe ya akili zaidi ya ‘masaburi’.
Ukiangalia huyu ‘muishiwa’ kibaya yaani Magigez na Foundation  yake utacheka. Eti aliomba apewa madafu milioni kumi toka NCAA, wakati nao walikuwa wakilililia ‘lisirikali’ kuwa bajeti yao haitoshi.
Ajabu baada ya NCAA kubanwa mbavu na wakubwa, ikatoa hiyo fedha wakati yenyewe ilikuwa na hali ngumu ya ‘ki-njuluku’.
Kama si ujambazi wa mchana unaofanywa na ‘wahishimiwa’ waishiwa ni nini? Siku hizi ukitaka kutajirika haraka au kuukwaa ‘uhishiwa’, uza ‘mibwimbwi’, anzisha foundation, uwe msanii, jipendekeze kwa Nambari Wahedi au jifanye mkereketwa wa maendeleo na haki za akina mama vijana na watoto.
Ila mjue.  Mmekalia bomu kwa kuwateketeza walevi. Siku wakizinduka, msinilaumu kuwa sikusema.  You betcha. Chanzo: Nipashe Jumamosi Sept., 7, 2013.

No comments: