The Chant of Savant

Tuesday 5 February 2013

Tumehamia Nipashe



Ile safu ya Jicho la Kijiwe imehamia rasmi Nipashe kutokana na sababu ambazo si vizuri kuzieleza. Safu hii ilisifika sana kwenye gazeti la Tanzania Daima. Ilikuwa safu ndefu karibia kuliko zote kwenye gazeti hilo. Safu hii chini ya kichwa cha  Hekima na hekaya za Mlevi itakuwa ikitoka kwenye gazeti la Nipashe la Jumamosi. Tunawashukuru wasomaj wetu wa safu hii wa zaidi ya miaka mitano.
Tukutane huko

Wapendwa wasomaji wa mipasho na umbea, habari za zali,
Ninayo furaha kuwaleteeni habari njema ya ukombozi itakayo wajaza furaha na wengine majonzi. Tusameheane. Kama mjuavyo, kwa vile hii ni ngoma mpya kwenye uwanja huu ingawa mtambo si mpya, kama ada, lazima nifanye kitu wazungu huita intro.
Kwa ufupi naitwa Dk, Profesa, Al Haj, Mwalimu, Field mashall, shehe, ulamaa,maulana, Man and a half, askofu Nkwazi Mhango aka Mpayukaji Msemahovyo bin Wapashe bin Waelewe bin Mtoboasiri aka Kiwanda cha Maneno aka Ngoma Kubwa. CV au Resume yangu ni ndefu kiasi kwamba nikiandika sifa zangu zote naweza kujaza barabara. Nitawapa kiduchu tu. Nina PhD (Commonwealth Nonexistent University), PhD (Havazard), PhD (Edenbug), PhD (Quacks’ Open University of the World (QOUW), New York na PhD (Make-believe University), Bangalore, India. Pia nina Masters nyingi toka vyuo kama Msoto University, Uswekeni, Uswazi na Kijiweni universities.
Kitaalamu naitwa Seer, nobleman, PhD Phil, MA (Abracadabra and Hypothetical Thinking), BSc (Lies and truth), Dip (Corruption and Mafia Management (CCM), Masters (Public funds Terrorizing), MBA, Masters (Money-making and Forgeries), etc.
Najua wengi wananifahamu kutokana na kuchezea timu ile ambayo nimeitema kutokana na sababu ambazo ni Top secret kwa ajili ya usalama wa walevi na wavuta bangi wenzangu.Kama akina Messi wanahama timu kwanini nami nisifanye hivyo? Nauza ujuzi wangu bwana hata kama ni wa kilevi. Mie nilizaliwa nikiwa nimelewa kiasi cha kuitwa Mlevi. Nilianza kuongea nikiwa na miezi miwili ndio maana niliitwa Mpuyukaji. Haya si makosa yangu bali bi mkubwa aliyekuwa akipiga ulabu wakati wa ujawepesi wangu. Ninayoandika siku zote huwa ni mawazo ya kilevilevi. Kama nikikushika pabaya huna haja ya kwenda kwa pilato. Maana ukinishitaki na akiniona mahakamani, atanitoa mkuku right away. Nilishashitakiwa sana kwa ulevi. Ndata walishaninyaka sana hata kunibambikizia kesi. Kila wakifanya hivyo pilato hunitema kwa vile ana ushahidi tena toka kwa daktari wa akili kuwa mambo upstairs kwangu si normal. Hivyo, kama ukiona nimekugusa pabaya umezee na kunisamehe huku ukijirekebisha.
Pia huwa ninao wenzangu tunaokunywa na kuvuta pamoja. Sisi hujichukulia ni kama bunge la kutetea walevi na wale wote wanaotendewa kilevi na walevi wakubwa wenye maulaji ya mamlaka.
Nilipata bahati ya kusoma hadi ng’ambo japo haikuzuia kuendelea kuwa mlevi. Wahenga walisema: Elimu ya mtu haiondoi ujuha wake. Tusingekuwa na watu wenye madigrii gunia wakifanya ufisadi kiasi cha kuwaacha watu hoi? Hivyo, msinishangae bali msome niandikayo ili yawe darasa msiwe kama mimi. Kitu cha kujivunia ni kwamba ulevi wangu unalipa. Kwani kuna kipindi wazito huniita lau wanikatie mshiko nisiwaumbue au niwape ushauri. Wanajua nimebukua kama sina akili nzuri. Bahati nzuri, pamoja na ulevi wangu, sikughushi wala kufeli. Wakati nikiwa chuoni kule Uskochi alikosoma Mwalimu Mchonga niliondoka na GPA ya 4.00 kiasi cha kuombwa nisirejee nchini badala yake nifundishe chuoni pale. Jina la chuo usiniulize ila siyo Edinburg.
Katika shahada yangu ya kwanza nilisomea Upayukaji yaani Rhetorics. Shahada ya pili nilisomea uhalisia yaani Realism.
PhD nilisomea Uchakachuaji na Usemahovyo. Nina masters na PhD kadhaa.Nasisitiza. Sikuzipata online wala kughushi wala kupewa za heshima. I toiled for my degrees. Hivyo, nimebukua kama sina akili nzuri. Najua wengi wakibahatika kuonana name hawataamini kutokana na pombe, bangi na bwimbwi vilivyonibangua na kuninyuka. Ila aminini nimesoma sana. Ndiyo maana nilikataa hata kuajiriwa kwenye ofisi za umma ili nisipate vishawishi na kuuma umma kama wenzangu wenye shahada za kweli na za kughushi wanavyouuma umma. Mie nauma mma.
Kwa vile waswahili wengi huamini kuwa kusoma ni kumwaga umombo, huwa siachwi nyuma. Nachonga umombo hadi ufransii. You know what? I speak English like the Queen. So too I speak French like Napoleon Bonapatre. C’est tres vrai. Je parle Francais comment Parisiennes ou quelque un qui habit au France.
Loo! Nshahararibu! Kwa vile leo nakuja na inshu ya introduction, acha nitambae na misifa yangu.
Nimeishawaeleza kisomo changu. Ngoja niwape kidogo juu ya maisha yangu hapa Bongo. Ninaishi Uswazi na mtaa na nyumba navyo ni top secret. Kwa ninavyowananga mafisadi na wengine wanaofanya mambo ambayo siyo, siwezi kutoa anwani yangu. Niaminini. Hata mhariri hajui mitaa yangu. Maana ninavyochukiwa na jamaa zangu hasa ndata wanaoniwinda ili wanitie nguvuni kwa kunywa gongo, nikitaja nitakuwa nimejihukumu kifo.
Mie ni mpenzi wa gongo, kahawa na bwimbwi. Kwa vile bwimbwi na gongo ni chanzo kizuri cha mapato kwa ndata wanapokubamba, huwa sitaji mitaa ninayoishi wala kunywa.
Huyo ni mimi. Kuna wazee wenzangu tunaoshirikiana kuendesha bunge la walevi. Hawa leo siwatambulishi ili wasiharibu intro yangu. Loo! Nilitaka kusahau mtu muhimu kwangu! Huyu si mwingine bali bi mkubwa mama Kidume Nesaa Mpayukaji Msemahovyo almaarufu Mother Lioness. Huyu si mlevi wa gongo kama mimi; ni mlevi wa migold na mapambo. Ukimuona huwezi kuamini kuwa anashare bedroom na mlevi kama mimi. By the way, yeye akiulizwa alinipendea nini husema siri ya mtungi aijuaye kata. Je lipi bora kati ya mlevi kama mimi na mafisi na mafisadi mnaowaita waheshimiwa?
Kwa wasiojua ukweli ni kwamba hata wale wanafalsafa maarufu mnaopenda kuwanukuu akina Socrates, Sophocles, Heraclitus na wengine wengi walikuwa walevi wa ukweli kama mimi. Hii ndiyo sababu ya kupenda ulevi kuliko ushufaa na uheshimiwa wa shilingi mbili utokanao na hongo, uchakachuaji na ufisadi.
Leo sitasema mengi. Mengi mtayaona kwenye nondo zangu zitakazofuata. Onyo: mafisi, mafisadi, warongo, wezi, wauza unga, wala rushwa, wasanii, wababaishaji, matapeli, wanaoghushi na wengine hawa ndiyo target yangu.
Au revoir and Sii yu!
Chanzo: Nipashe Februari 2, 2013

1 comment: