The Chant of Savant

Sunday 16 June 2013

Hongera Katiba Mpya "kuusuka" Muungano

Baada ya kugundua kuwa rasimu ya katiba mpya inanipa power ya kugombea urais kama mgombea binafsi, leo nawapongeza wananchi walioipendekeza na waliokusanya maoni hata kama walikuwa wanakwamua mabilioni ya njuluku.
Nampongeza jaji Jose Warioba kwa kusimama kidete na kuhakikisha anakuja na kitu ambacho kitaua muungano kistaarabu. Sijui kama jamaa zangu ambao wamekuwa wakilewa na kulalamikia muungano kama wameipata. Mlitchotaka sasa kitakuwa na tutagawana mbao baada ya kuvunja hiyo ndoa ya muungao ambayo kwa ulevi wenu mliiona kama mgongano badala ya muungano. Ila tukubaliane. Ukishavunjika sitaki nisikie vilio tena. Au vipi mkubali tuendelee kuachana taratibu kwa njia ya kuwa na sirikali tatu na marais mia kidogo. Sasa muungano umekuwa mgongano dhahiri.
Japo sipendi utitiri wa sirikali tena kwenye kaya kapuku na ombaomba kama yetu, hili la kuondosha viti vya ubunge wa kashfa rushwa na kila aina ya unyonyaji limenikuna. Huenda hiyo pesa waliyokuwa wakikusanya bila kufanya kazi yoyote ndiyo itaenda kwenye serikali tatu.
Hata hivyo, msiwe na shaka. Nikishashinda urais nitaondosha sirikali tatu na kutangaza moja tu. Atakayetaka matatizo apinge mbinu hii adhimu na takatifu ya kuwaunganisha walevi toka kwenye unafiki na kila kipande kutaka ulaji wa dezo na ujiko. Nasema wazi tena kwa kinywa kipana. Mkinichagua sahau sirikali mbili au tatu. Nitaunganisha kaya hata kwa ntutu wa bunduki. Atakayeona hili halifai basi kila mtu aende kivyake. Wao waende na Zenj yao nasi na Danganyika yetu au vipi? Kwanini kuendelea kunyimana raha bure? Kama wapo walioshiba ulaji wetu au sisi wao basi kila mmoja akale kwake ila aangalie isile kwake. Ngoja nibadili gea.
Hakuna kitu kilikuwa kinanikera kama kuwa na wabunge tena wakiitwa waheshimiwa wasiomwakilisha yeyote isipokuwa matumbo yao. Rafiki yangu Sofia Lion na Anae Andallah mnanipata siyo? Kweli imekula kwenu. Lazima hapa mtafuta kazi ama ya uhausigeli au kuuza nyanya. Hakuna kitu kimenikuna kama kuondoa upuuzi wa spika kuwa muishiwa sorry mheshimiwa tena mwenye kupendelea chata lake huku akiwaburuza waheshimiwa utadhani mjengo mali ya baba yake. Shame on her! Anna Makidamakida unapata?  Umekuwa ukiniudhi kwa kuvurunda kiasi cha kutamani siku moja nikushukie na kukupa kibano kama si kicha... we koma na ishia hapo. Hizi bangi na gongo vitakuja kunilaza lupango siku moja. Jobless Nduguy lazima uwe unalia kama kichanga kwa kunyimwa ulaji ambao ulikuwa ukiutumia kwa nyodo kana kwamba hakuna mwisho wa kila kitu chini ya jua.
 Yawezekana ni Danganyika pekee yenye wabunge watokanao na vitu vyenye kila aina ya kejeli, ubaguzi hata udhalilishaji chini ya dhana ya viti maalumu. Kwa wanavyochuma uchache bila kufanya kazi yoyote, kuna siku walevi watawaita MPigs kama ilivyotokea kule kwa Nyayo ambayo rais wake unachukua jina la nchi na kuongeza ta imetoka hiyo. Kuna mlevi husema eti waishiwa hawa huwa hawana na kazi yoyote mjengoni zaidi ya kungojea posho na sifa ndogo ndogo magazetini.  Jamani naandika kama mlevi asemavyo. Hakuna haya ya wahishimiwa kuanza kunitafuta waninyotoe roho au kunihoji kama vile niko mbele ya pilato. Mjumbe hauawi ati.
Juzi nilikuwa na maongezi na waziri mkubwa wa Ukanada ambaye aliomba nisimtaje jina ili wafisadi wasimjuejue wakati tukipata ulabu kwenye mitaa ya mji mmoja uitwao Arawa. Nilimuuliza anaonaje mfumo wa kuwa nauishimiwa wa msukule. Kwanza, alishangaa inawezekanaje mtu kwenda kwenye mjengo kuwakilisha tumbo lake!. Alisema wazi kuwa hiki nacho ni chanzo kizuri cha umaskini wa kaya. Aliongeza kuwa katika kaya yao hili haliwezekani kwa vile lazima kila mtu apambane kuupata uheshimiwa. Anasema wao wanapambanisha uwezo na si jinsia wala mitandao ya kifisadi ya kivyama kama ilivyo huko kulikoungua shoka ukabaki mpini. Nilishangaa aliposema kuwa uhishimiwa wa namna hii ni matusi ya nguoni. Hata hivyo, nilifurahi kusikia akiongea lugha ya kilevi ya kuliita kulego kulego na si kijiko kikubwa. Acha nitafsiri kwa lugha rahisi.  I call a spade a spade not a big spoon like some hypocrites who can’t tell those hishimiwas that they are screwing our hunk up. Shame on them all!
Walevi kusema ukweli hawajawahi kuona mantiki kwa mfano mtu anapochaguliwa kuwakilisha vijana kwenye mjengo huku vijana hao hao wakiishi kwnye jimbo lenye mbunge. Je huyu mbunge wa kawaida ambaye jimbo lake lina kila aina ya binadamu atawakilisha nani? Je vijana au wanawake wana nini hadi kuwa na wawakilishi zaidi ya mmoja? Hawa hawana tofauti na wale waishiwa toka Zenj wanaowakilisha majimbo yao kwenye muuganiko. Inatisha kuona kijipande cha ardhi sawa na wilaya ya Ushoto kuwa na maulaji kuliko hata mikoa. Japo huwa napenda umoja na kuunganika, nikiangalia ndoa ya sisimizi na tembo huwa uzalendo unanishinda na kusema waache wende zao na kipande chao cha ardhi wakamalizane. Sisemi hivi kwa ubaya wala ulevi.
Jamaa walituzidi akili. Baada ya kugundua kuwa tuna maulaji mengi ya kuwapa hawaachi kudai kila uchao ili tuendelee kupumbaa. Nimekumbuka kikao cha walevi juzi ambapo wengi walikandia muunganiko wakisema eti unawanyonya na kuwakosesha raha.  Hakuna ninachokumbuka kama maneno ya mgosi Machungi pale aliposema, “Ila siku wakiambaa na walevi wabara wakaamua kuwaambia kuwa kila mtu ave na kwao basi watazamisha kila kipande cha ardhi kutokana na wengi wao kuzaliana sana upande wa pili.”
 Baada ya kuona mgosi anavuka mipaka kwa kuanza lugha ya kilevi ambayo wasiopenda ukweli wanaweza kuiita ya kibaguzi, niliamua kuondoka zangu kwenda kusoma kitabu cha yule Mchungaji kidhabu Mtikisa kiitwacho Sera ya Magabacholi na Saa ya Ukombozi.  Hakuna mstari ulinichekesha kama ule usemao, “Wakituita machogo nasi twaita machokoo.”  Sikukisoma sana kutokana na lugha ya jamaa.  Inaoneka huyu jamaa alisoma volume langu la SAA YA UKOMBOZI nililotunga kuonyesha jinsi ya walevi wanavyoweza kuongoza wasiolewa kwa kuwapiga chini kwa njia ya kura ili wakose kula ya dezo kama ilivyo. Hata hivyo, tuache utani. Wazenj wanaopigapiga kelele kila uchao hasa baada ya kusikia kuwa kuna dalili ya kuwa na wese wajiandae kama tutaamua kila mtu aende kivyake baada ya mlevi kutaka kuunganisha pande la kaya na kipande cha kakaya na kutengeneza kaya moja.
Ngoja nikavute kwanza!
Chanzo: Nipashe Jumamosi Juni 15, 2013.

No comments: