The Chant of Savant

Tuesday 26 August 2014

Njama za kumuua Slaa: Ni zaidi ya Masele


      12    Taarifa za kuchukiza na kutisha kuwa kada wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) mbunge wa Shinyanga Mjini na Waziri mdogo (Nishati na Madini) Steven Masele pamoja na wenzake, walipanga na kuratibu mpango mchafu wa kuwaua Katibu mkuu wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA), Dk Wilbroad Slaa na Mkurungenzi wa Mawasiliano na Uhusiano, mbunge wa Ubungo, John Mnyika zinaiweka CCM pabaya. Je Masele ni nani? Je yuko peke yake katika ugaidi huu unaoonekana kupangwa na watu wengi zaidi yake? Je atachukuliwa hatua au kufumbiwa macho kama mwenzake, Mbunge wa Iramba na Waziri mdogo wa Fedha, Mwigulu Nchemba, aliyetuhumiwa kwa vitendo vya kigaidi akapandishwa cheo? Je imeishia wapi kesi ya kubambikizwa ya mkurugenzi wa usalama wa CHADEMA, Wilfred Rwakatare? Si wameuia kimya kimya baada ya mbinu zao za kigaidi kufichuliwa? Je watanzania wataendelea kujiruhusu kutawaliwa na chama kilichoishiwa kiasi cha kujigeuza kundi la kigaidi? Je njama kama hii ingeelekezwa kwa Katibu mkuu wa CCM Abdulrahaman Kinana na Katibu wa Itikadi na Uenezi, Nape Nnauye serikali ingeendelea kujifanya hamnazo wala haijui kitu? Mbona tunatumia sheria kihuni na kibaguzi hivi?
          Diwani wa kata ya Ngokolo mjini Shinyanga, Sebastian Peter alifichua kuwa waliahidiwa mamilioni ya fedha kutekeleza mauaji ya wawili tajwa walipokuwa Shinyanga kikazi mwezi Februari. Peter alikaririwa akisema, “Baada ya maongezi ya aina mbali mbali na Mchange tulishindwa kupata muafaka lakini tuliendelea kuwasiliana na aliporudi Shinyanga akatueleza kuwa kuna mpango mzuri wa fedha na kwamba utasimamiwa na Waziri Masele na kwamba tutapata sh. milioni 180 kila mmoja.” Hivi kweli kuna ushahidi zaidi ya huu kupaswa kumfungulia mashtaka Masele na wenzake? Kama huu ni uzushi mbona mtuhumiwa haendi mahakamani kusafisha jina lake? Peter anaendelea, “Mkakati huo ulianza kuratibiwa na Mwenyekiti wa UVCCM, Abbakari Gulam ambaye ni mtoto wa Meya wa Shinyanga, wakiwa na Habib Mchange, kisha tuliona mkakati unatekelezwa na mbunge wa Shinyanga mjini, Stephen Masele, Nape Nauye, Januari Makamba, Mwigulu Nchemba na Ridhiwani Kikwete.”
          Kwanza, ni aibu kwa mbunge, anayepaswa kuwa mfano wa jamii, kugeuka gaidi. Pia ni aibu kwa serikali kutochukua hatua stahiki. Kitendo cha Masele kushiriki ugaidi na uvunjaji wa sheria licha ya kumuaibisha kama mwakilishi wa wananchi, kinawaibisha na kuwadhalilisha wale waliomwamini uwakilishi. Pia, kwa nafasi yake, Masele alipaswa abanwe aachie ngazi kwa vile ameaibisha kazi ya ubunge na bunge kwa ujumla.  Mbunge anayeweza kupanga kutekeleza ugaidi hapaswi kuendelea kuwa bungeni wala uraiani bali gerezani akingojea kesi yake kusikilizwa na kutolewa hukumu. Kunajengeka dhana kuwa Masele alitumwa na wenye serikali inayomilki taasisi na vyombo vyote, hatachukuliwa hatua. Ndiyo maana mamlaka hazimchukulii hatua. Je kweli Tanzania inafaa kuendelea kutawaliwa na chama na serikali na watu wanaoweza kudiriki kutenda ugaidi halafu wakaendelea kulindana?
          Pili, kwa wanaojua uhusiano  baina ya Masele na mtoto wa kigogo mkubwa wa CCM ambaye pia ni kigogo wa serikali, hawashangazwi na hisia kuwa anatumiwa tu na mtandao mkubwa. Wengi wanajua kuwa, pamoja na udhaifu wake kitaaluma, Masele aliteuliwa kwenye nafasi aliyo nayo kutokana na ukaribu wake na mtoto wa kigogo huyu ambaye ana ushawishi mkubwa katika masuala mengi yanayohusiana na mamlaka ya baba yake. Pia kwa wanaojua makundi ya kigaidi yanavyofanya kazi, Masele hawezi kuwa peke yake. Lazima kuna watu wakubwa na makundi makubwa yaliyomtuma kupanga njama hizi. Huenda ndiyo maana akapigiwa kampeni na kuteuliwa uwaziri wakati hana sifa. Walimuopoa mapema wakijua wanavyoweza kumtumia wakati ukitimu.
          Tatu, siasa za kichovu, kikatili na kuishiwa sera tulizoea kuzisikia na kuzishuhudia kwa majirani zetu hasa Kenya ambapo chama tawala cha wakati ule kiliwaua makada wake wengi kiliodhania walikuwa tishio kwa ulaji wa bwana mkubwa. Pia, tulizoea kusikia watoto wa watawala wa huko nao wakijigeuza watawala tusijue yatafika hata kwetu. Je imekuwaje tumefika hapa? Bila shaka,  ni matokeo ya ufisadi na siasa za kifisi ambapo kila mwenye kupata madaraka huyatumia vibaya kuibia umma na kujitajirisha kiasi cha wasaka tonge kuwa tayari kuua watu wasio na hatia ilmradi wapate madaraka ambayo ni hati ya kuibia umma kwao. Hivyo, si ajabu kushuhudia magaidi, majambazi hata wauza mihadarati wakijitokeza kutumia fedha zao zitokanazo na jinai yao kusaka nafasi za kisiasa na kuendeleza jinai yao bila kuguswa wala kuzuiliwa hata kama ni kwa kuua wenzao.
          Nne, wahanga wa mpango huu mchafu na CHADEMA wanapaswa kuomba vyombo vya kimataifa vinavyoshughulikia ugaidi kuingilia kati kwa sababu mamlaka za Tanzania haziwezi kufanya hivyo kutokana na kutekwa na CCM.
          Tano, watanzania wajulishwe kupitia mikutano mbali mbali aina ya utawala unaoanza kujengeka chini ya CCM ambayo imeamua, kwa tamaa ya madaraka, kujigeuza kuwa kundi la kigaidi. Chama kilichofikia kiwango hiki hakipaswi kuendelea kuvumiliwa kuwa madarakani. Kuna haja ya kuwahakikisha taasisi za kimataifa zinazoshughulikia ugaidi zinajulishwa angalau zitoe maelekezo hata maoni yake.
          Sita, walengwa wasijue yamekwisha. Wanapaswa kuchukua hatua madhubuti na tahadhari vya hali ya juu kwa vile kilichowasukuma CCM kutaka kuwaua bado kipo pale hasa ikizingatiwa kuwa CHADEMA ndiyo tishio lao. CCM iko tayari kufanya lolote liwe haramu au halali kuhakikisha inabakia madarakani ikifanya ufisadi na ugaidi wake kama kawaida. Hili halivumiliki. Upinzani unapaswa kulichukulia tishio hili kwa uzito unaostahili.
          Saba, kwa upande wake, licha ya kushinikiza Masele na genge lake la kigaidi lishitakiwe, kuna haja ya kumbana rais kuhakikisha anamwajibisha ili iwe rahisi kumshughulikia kisheria.
          Tumalizie kwa kulaani mchezo huu mchafu ambao kama hautazuiliwa kwa nguvu ya umma unaweza kulitumbikiza taifa kwenye machafuko na mauaji ambayo yangeweza kuzuilika.  Wakati wa kuzuia zahama hii ni sasa.
Chanzo: Tanzania Daima Agosti 27, 2014.

6 comments:

Anonymous said...

MASELE NI NANI KWANI KWANZA HATOKI SHINYANGA NASHANGAA KUUPATA UBUNGE WA SHY SHY INA WENYEWE CHA KUSHANGAZA KUUPATA UNAIBU WAZIRI
ANAIJUWA SHY HUU JK WAHASHAURIKI WAKO BOMU KAMA LA GAZA POLE SANA
AU NI RAFIKI WA RIZIWANI KANA NAIBU WA SHERIA ANJELA AYEKUWA AKIPATA MAKARAI ZANAKI HAKI CHUO KIKUU
TWAMBIENI MAWAZIRI NI CHA CHAGUO LA MTOTO RIZIWANI

Anonymous said...

Lisemwalo lipo kama halipo lipo njiani
CCM wanatapatapa 2015 kiboko yao

Anonymous said...

JK anamuandaa rais ajaye ni tajiri sijawahi wal kusikia rais anandaa rais baada yake ni Tajiri tena kwa tanzania 60% ya bajeti ni kodi zetu ulaya na USA

Anonymous said...

Riziwani yumo kwenye hili danga kwani ndiye msemaji mkuu wa ikulu

Anonymous said...

kuna virus vinanitafuta kila kona
oya masifisadi hamtuwezi watu wa dunia ya kwanza ukweli wetu isiwe nongwa
issssssssssssssssssssipendi CCCCCCCCCCCCCCCCCCCMMMMMMMMMMMMMMMM na watu wake

Ndugu Nkwazi N Mhango said...

Anon wote hap juu michango yenu imesikika. Nawashukuruni na kuwakaribisha tena na tena.