The Chant of Savant

Tuesday 19 April 2016

Tanzania haipaswi kuwa ombaomba


            Akiongea kwenye ibada ya pasaka, rais John Pombe Magufuli aliwataka watanzania kuchapa kazi ili Tanzania iweze kuondokana na uombaomba na utegemezi wa makombo ya misaada toka ughaibuni. Na kweli, siku chache baada ya rais Magufuli kuyasema  haya Bodi ya Shirika la Changamoto za Milenia (MCC) ilitangaza kusitisha msaada wa dola za kimarekeni milioni 700 tokana na kutoridhishwa na uchakachuaji uliotokea Visiwani kwenye uchaguzi uliobatilishwa mwishoni mwa mwaka jana bila sababu. Hata hivyo, ni bahati mbaya kuwa taifa letu–ukiondoa serikali ya awamu ya kwanza–limekuwa ikitawaliwa na viongozi wenye mawazo tegemezi na mafisadi kiasi cha kutegemea kuombaomba bila hata kuona aibu. Wazo la kujitegemea ni la kimapinduzi kama litafanyiwa kazi na pia kujitegemea huku kutalenga kutenda haki na si kufanya madudu kama ya Visiwani. Inatia aibu kuona kiongozi wa nchi kwenda kwa viongozi  wenzake wa nchi nyingine kujidhalilisha kana kwamba hana ubongo na anaongoza watu wasio na ubongo wala mikono. Ni aibu hasa kiongozi anayefanya hivyo anapokwenda kule akidai anaongoza taifa huru lakini lisiloweza kujitegemea hata baada ya kuwa huru kwa miongo zaidi ya mitano. Taifa ombaomba si huru. Taifa tegemezi si huru. Kwani wanaolifadhili ndiyo wanaoliwatawala kwa mlango wa nyuma kama ilivyo kwa mataifa mengi ya kiafrika ambayo yamekalia raslimali lukuki lakini watawala wake wakazivuja na kwenda kuomba bila hata chembe ya aibu. Tunampongeza na kumshajihisha Magufuli alifanyie kazi hili kwa vitendo na haraka sana ili taifa letu liweze angalau kuwa huru.

            Haiwezekani nchi iliyojaliwa raslimali kama vile ardhi nzuri yenye rutuba na madini kila aina, bahari, mito maziwa, mbuga za wanyama wa aina mbali mbali na watu kuendelea kuishi kwa kujidhalilisha ikiombaomba. Kuendelea kuomba –hata kama hili laweza kuonekana kuwa tusi –ni ushahidi kuwa ima tuna matatizo ya kiakili, na kama siyo sisi bali wale wanaotutawala wawe ni wafadhili au wafadhiliwa.  Ili kuweza kujitegemea, tunahitaji kufanya yafuatayo:

            Mosi, tuwe na uongozi na usimamizi bora wa raslimali zetu. Hapa lazima tupambane na maadui kama vile ukwepaji kodi, uvivu, misamaha ya kodi, uwekezaji wa kijinga na kifisadi na pia matumizi mabaya ya raslimali zetu.

            Pili, lazima tujenge utamaduni wa uwajibikaji unaoandamana na uchapakazi wa kweli na si kwa viongozi tu bali watanzania wote kwa ujumla wao. Mfano, watanzania wanapaswa kujua kuwa wana mchango mkubwa katika ubomoaji wa taifa letu. Kadhalika, wana mchango mkubwa katika ujenzi wa taifa letu. Wapo wenzetu wanaowasaidia wageni kuibia taifa letu kwa kupewa vijisenti kidogo wakati wageni hawa wezi wakiondoka na mabilioni ya shilingi. Rejea utoroshaji wa wanyama, madini na raslimali nyingine. Hawa wanapaswa kukamatwa na kunyongwa ili kuwa onyo kwa wote wanaodhani Tanzania ni shamba la bibi.

            Tatu, lazima kuwepo na mfumo unaosimamia na kutekeleza nidhamu ya matumizi ya mapato na fedha ya umma tena wenye uwazi na ukweli.

Nne, lazima tuwe na mfumo wa sheria zenye kusimamia uwekezaji ambao utasaidia kupambana na kuwashughulikia wale watakaokwenda kinyume na dhana nzima ya uwajibikaji na matumizi bora ya mali za umma. Mfano, sheria itamke wazi wazi kuwa atakayeshindwa kuelezea namna alivyochuma mali zake, atafikishwa mahakamani na mali husika zitatwaliwa na serikali. Pia sheria hii itasaidia kurejea mikataba ya kijambazi na kipumbavu tawala zilizopita zilizoingia kwa sababu ya maslahi ya watu wapumbavu, vipofu na waroho wachache. Ni bahati mbaya kuwa tangu aingie madarakani na kuanza mapambano dhidi ya ufisadi, rais Magufuli hajagusia namna atakavyofumua mikataba hii ambayo imegeuka mashimo makubwa ya kuzamisha fedha za taifa. Wengi wangependa kusikia mikakati yake juu ya kupambana na kadhia hii ambayo watangulizi wake waliogopa kutokana na kufaidika nayo.

Tano, bila kuwa Katiba mpya yenye kuanisha wajibu na haki za watanzania, tutakuwa tunatwanaga maji kwenye kinu. Mfano, unapokuwa na rais ambaye yuko juu ya sheria, ataweza kuitumia nafasi hii kujitajirisha na kufanya atakavyo kwa vile hakuna anachochelea. Tawala zilizopita zimetupa somo kuwa rais anapokuwa juu ya sheria inakuwa rahisi kwa waliomzunguka kuyatumia madaraka yake vibaya kuwaibia wananchi huku wakijitajirisha na wananchi wakiendelea kuwa maskini bila sababu. Uzoefu wa kashfa kama Kiwira na EPA unapaswa utupe somo kubwa juu ya namna madaraka ya rais yanavyoweza kufujwa na wahalifu waliofanya hivyo wakaepa mkono wa sheria kutokana na rais kuwa juu ya sheria. Hata hii kadhia ya ukwepaji kodi, ufisadi na misamaha ya kodi imechangiwa kikubwa na hali ya rais kuwa juu ya sheria.

 Sita, ili kufanikisha yote hapo juu, lazima–kama taifa na jamii ya watu wanaojua wanachofanya–turejeshe maadili ya utumishi wa umma na ikiwezekana kwa watanzania wote kama ilivyokuwa wakati wa awamu ya kwanza. Kila mtanzania ajaze ripoti ya mwaka ya mapato na matumizi yake, kutangaza mali zake na kutoa maelezo ya namna alivyozichuma ili kubaini kama ni kwa kufuata sheria au kifisadi.

Tumalizie kwa kumsisitizia rais na serikali yake wajenge mfumo wa kitaasisi utakaoliwezesha taifa kujiondoa kwenye aibu na kadhia ya uombaomba usio na ulazima. Watanzania lazima tujisute na kuonea aibu kadhia ya kuishi kwa makombo kama mbwa.
Chanzo: Mwanahalisi.

No comments: