The Chant of Savant

Saturday 4 February 2017

UDARt na mwendo kasi wa kupunyua mali za walevi

          Alipozindua mradi wa mabasi ya mwendo kasi jijini Bongo hivi karibuni, rahis alionyesha shaka ya kutojua faida ambayo kaya itapata au imeishapata tokana na mradi wenyewe ambao ni mazonge na madudu matupu kama tutaidurusu historia ya mbia katika mradi huu. Kwa tunaojua historia ya mradi, tunajua fika kuwa imekula kwa walevi. Najua wengi watashangaa kusikia habari mbaya hii ambayo ni ukweli mtupu. Hakuna kilichonichefua kama jina la mradi wenyewe yaani UDART. Jina hili linanikumbusha lile Shirika la Walevi la Usafari Dar (UDa) ambalo lilianzishwa na mzee Nchonga wa Burito kuondoa msongamano kwenye jiji hili la salama isiyo salama.
          Leo nataka nihoji baadhi ya masaala hata kama kilevi kama ifuatavyo:
          Mosi, je sakata la kashfa ya unyakuliwaji UDa limeishia wapi hadi sasa? Kwa kumbukumbu za kilevi ni kwamba aliyekuwa waziri ndogo wa njuluku Adama  (siyo yule wa Gambia) Milima aliwahi kuutonya mjengo kuwa hisa za lisirikali hazikuwa zimeuzwa kwa kampuni la Simian Group; na zile zilizokuwa zimedaiwa kuuzwa zilikuwa zimeuzwa kwa bei ya kichaa au kutolewa bwerere baada ya wahusika kutembeza mlungula kwa waliokuwa wakubwa wa shirika hili mfu. Bado nakumbuka. Milima alikuwa ima akijibu swali la bi Iron lady Halimaaa Mdzee au Joni mwana wa Nyika wote wahisimiwa wa Chakudema tena njengoni.
          Pili, inakuwaje lisirikali linatoa sadaka shirika na njuluku za umma kana kwamba mradi ni mali yake binafsi bila kutaka kutumia asasi zake kuchunguza na kufikishwa kwa pilato waliojitwalia UDa yetu kama alivyoshauri Mdhibiti na Mkaguzi wa njuluku za lisirikali? Nashauri lisirikali liitumbue UDa kwanza kabla ya kujisifu kuwa imefanya makubwa kwa kuleta mradi wa kipekee wakati upekee wake unaonekana ni wizi kasi na si mwendo kasi. Je dokta Kanywaji hayajui haya madudu na majipu yote haya tena yanayojulikana na kunuka wakati alikuwapo wakati yakifanyika? Hivi lisirikali halijui kuwa UDa ilianzishwa kwa njuluku za walevi ukiachia mbali huu mradi mpya lililozawadia hiyo kampuni ya Simian nao umegharimu mabilioni ya dola tena za nkopo toka Benki ya Dunia ya mabwanyenye na mabepari? Hii akili au matope?
          Tatu, je kwanini lisirikali limefanya siri hii ndoa haramu baina ya UDa na Dati iliyotengeneza kitu kinaitwa UDATA? Kwa nchezo huu sitashangaa kusikia kuwa siku moja Simian Group imegawiwa Air Bongolalalander.
          Nne, nani wako nyuma ya hujuma hii inayohalalishwa kwa mlango wa nyuma huku walevi wakishangilia wasijue haya ni mauti yao? Sasa nawaambieni hata kama ni kwa nguvu ya kanywaji na majani kuwa hii UDAT ni bomu na jipu linalopaswa kutumbuliwa haraka badala ya kuwekewa utuli. Hivi nyie walevi, nani aliwaroga hadi mkaaminishwa kuwa UDAT ni big deal wakati ni wizi mtupu? Je hamjui kuwa watasha watakapotaka njuluku zao mtalipa nyinyi au vizazi vyenu?
          Tano, tujalie kuwa Simian Group walilipa cash na kuuziwa UDa. Je walichunguzwa kujua walivyotengeneza hiyo njuluku? Nauliza swali hili kuepuka ushenzi wa wenye mamlaka kuwatumia waramba makalio wao kulinda na kuendesha miradi yao itakanayo na kuwaliza walevi. Pili, nahofia kuwa tusipokuwa makini, tutajikuta tukiwasaidia watakatishaji njuluku za bwimbwi na ujambazi mwingine.
          Nimalizie kwa kuwaonya walevi kuwa kama wataendelea kulishwa kila urongo na takataka watakuja kustukia siku moja nao wametwaliwa kama UDa na kubinafsishwa kwa mafisi watakaowachuuza watakavyo. Huwezi kuridhia ndoa ya ya UDAT bila kuuliza najisi na usharmuta (ukahaba) ulioendelea hadi kufikia ndoa hii ya haramu. Kinachopaswa kufanyika ni kujibu maswali ambayo wahishimiwa wenye uchungu na kaya wamekuwa wakiuliza kuhusiana na kashfa hii. Hakuna aliyeniacha hoi kama mstahiki wa jiji la Bongo aliyeapa kufumua uchafu wa UDa kusikia kuwa juzi amepiga kura kuunga mkono kutumia madafu bilioni 5 yanayodaiwa kulipwa na Simian Group kuitwaa UDa bila kueleza namna ulipofikiwa uamuzi wa kupewa njuluku kidogo wakati thamani ya UDa ilikuwa kubwa kuliko haya madafu. Kama haitoshi, leo tunaambiwa mradi wa mandinga yaendayo kasi ni wa mabilioni lukuki lakini unakasimiwa kwa  wale wale waliotuchomolea UDa yetu. Tieni akilini;msimame na kuhakikisha ndoa ya UDAT inabatilishwa na UDa yetu inarejeshwa na kuuzwa kisheria.
Nipashe Jumamosi leo.

No comments: