The Chant of Savant

Saturday 1 August 2015

Mlevi kumfuata mkuu ughaibuni kumuaga

Rais Jakaya Mrisho Kikwete na Mama Salma Kikwete wakiwasili katika ...
Baada ya kuona Munene amekuja na staili mpya ya kuaga kwa kwenda ughaibuni kiasi cha walevi kungoja waagwe wasiagwe, wamemtuma Mlevi amzamie huko huko ughaibuni mkuu ili amuage. Lazima nimzamie na kumpa salamu zake hasa tathmini ya walevi ya ulaji wake na bi mkubwa, familia, marafiki na waramba makalio kwa miaka kumi inayoisha mwezi mmoja na ushei ujao.
Baada ya kuona jii huku usongo wa kukutana na jamaa yetu ukizidi, tulipanga kupeleka salamu za kumuaga Munene Njaa Kaya kwake nyumbani. Baada ya kugundua kuwa kumbe na bi mkubwa naye anakwenda kivyake ughaibuni kuwaaga mashoga zake, walevi wameamua nimfuate mzee hata kama itakuwa ni gharama kubwa kwa walevi. Hata hivyo, si unajua tena. Ngoja ngoja huumiza matumbo. Katika kipindi hiki cha kungoja Munene aje kutuaga asitokee, nilivuta na kunywa sana kiasi cha kuhisi kama naanza kuathiri afya yangu.  Hivyo, kitendo cha walevi kuniteua lau kimeokoa maisha yangu. Heri nimuage yeye popote alipo kuliko kuagwa mimi baada ya kurejesha namba bila hatia.
Walevi wananasema watamkumbuka jamaa kama bingwa wa matanuzi na mpenda michezo na sanaa. Kitendo chake cha kupenda sanaa na wasanii kimefanya baadhi ya walevi kuanza kufikiria kuwa wasanii ili nao angalau wasogee karibu na ulaji ingawa nimewashauri wangoje waone nani ataingia ikulu. Maana, kama ataingia mtu serious na tofauti asiyependa wasanii kama jamaa yetu, watakuwa wameula wa chuya bure.
Wanasema kuwa kama ungetokea msiba huenda angeweza kukaa kayani ila si busara kwenda kumuaga mtu kwenye matanga.
Kwa hiyo, ninavyoandika najiandaa kuelekea ughaibuni kumfuata mkuu ili nimpe salamu za lala salama. Kwanza, nikifika nitampamba ili wakati wa kurejea anipe lifti kwenye mchuma wake nami nitanua kama marafiki na washirika zake waliotanua kwa miaka kumi wakizunguka dunia na kumshinda mzee Vasco da Gama yule jambazi wa kireno aliyeizunguka dunia akipora na kusaka makoloni.
Ngoja niwanyofolee kidogo mambo nitakayokwenda kusema baada ya kukutana na mkuu. Kwanza, nitamuuliza siri ya kupewa tuzo nyingi za uongo ziii bora ughaibuni badala ya home. Hii maana yake ni kamba mkuu amefanya kazi pevu kwa walevi wa ughaibuni huku akiambulia ziro kwenye kutumika walevi wa kayani aliowaahidi maisha bora yakaishia kuwa bora maisha.
Pili, nitamuomba anipe siri ya kuweza kutanua huku uchumi wa kaya ukiendelea ku-tank na asijali. Nitamuuliza nini ushauri wake kuhusiana na jinsi ya kuziba pengo alilosababisha kwenye kasma ya umma. Maana, si haba. Maanuzi yake yamesababisha kuumka kwa deni la kaya ambalo hata hivyo halikumshughulisha kwa vile alijua wakati wa kulipa hatakuwepo kwenye ulaji na saa nyingine kwenye anga za Wadudi. Who knows?
Tatu, nitamuuliza kama atakwenda zake Mondulie kumuaga rafiki na mshirika wake aliyempiga chini kwenye kinyang’anyiro kilichopita.
Nne, kwa vile aliahidi kuwa baada ya kuachia ukanda atashughulika na kuhakikisha fisi hawatoweki kwenye kaya yetu.nitamuuliza kama atahusisha pia mafisadi kwa vile wao na mafisi lao moja.
Nitamkumbushia ile kashfa ya EPA ambapo aliwaambia washirika waliokwapua warejeshe njuluku ili mambo yaishe badala ya kuwekana lupango. Nitamuuliza ni kiasi gani aliweza kupata toka kwa washirika na angeshauri tufanye nini watu wanapokwapua kati ya kuwasweka lupango na kuwaomba warejeshe japo uchache kidogo ili kufunika kombe mwanaharamu apite.
Pia, nitamuomba anipe zile orodha za majambazi, wauza bwimbwi, mafisadi, walioghushi na vidokozi ili kama nitashinda kwenye uchakachuaji wakipate cha moto.
Kwa vile tutakuwa ughaibuni, nitamuomba tupite zetu Uswizi ili kupata orodha ya walioficha njuluku nje ili niwashughulikie inshallah nikiibuka mshindi baada ya kumpiga chini Dk. Kanywaji Makufuli.
Kwa vile na bi mkubwa wake naye anakwenda ughaibuni kuaga, nitaomba aniambie anayeratibu na kugharimia safari zake na faidi zinazopatikana kwa kaya tokana na safari zao wawili hawa.
Pia nitataka anieleze nini wosia wake kwa kaya na angependa akumbukwe kwa lipi ukiachia mbali ubingwa wa kutanua na kuacha kaya iende kwa autopilot.
Pia nitataka kusikia wosia atakaowapa washirika zake aliowateua kwenye nafasi mbali mbali kama vile ukuu wa wilaya na mkoa. Ujaji, ubalozi na makandokando mengine. Hili ni muhimu kuwaandaa kisaikolojia. Maana mtarajiwa ajaye anaweza kuwapiga chini wakajikuta apeche alolo wasijue la kufanya. Hapa lazima niwakumbuke akina Makondakonda na wengine waliounyaka kwa sababu ambazo hazikustahiki wala kutegemewa.
Pia nitamkumbusha changamoto aliyoipata wakati friend wake Dittto Likupatile Mzurimzuri alipomdedisha mlevi akaamua kumkingia kifua. Nitataka kujua anavyojisikia hasa akizingatia kuwa kitendo kile kilidhulumu uhai wa mchovu kabla ya Bwana God kuingilia kati na kutenda haki aliyokuwa ameikalia mkuu.
Baada ya hapo nitamuita chemba anieleze mantiki na sababu ya kuchakachua na kudedisha katiba mpya. Nitataka anipe faida na hasara za kufanya hivyo huku akitoa maelezo juu ya nini kifanyike kuridhisha pande zote yaani walaji na waliwa, watawala na watawaliwa ingawa maslahi yao ni pinzani na tofauti.
Kwa vile mkuu aliingia na falsafa ya ANGUKA yaani Ari mpya, Nguvu Mpya na Kasi mpya, nitataka anipe tathmini ya falsafa hii jinsi ilivyofiti jina lake kiutendaji na kimakakati.
Kwa vile nitakuwa mwanafunzi katika matanuzi, nitafanya kila kitu kiwe kifupi ili nikatanue. Hivyo, swali langu la mwisho litakuwa kumuuliza mantiki ya kuwanusuru akina Rugemalayer na Singasinga, Kagoda na majambawazi wengine walioibia kaya.
Kwa ufupi ni kwamba, kabla sijapanda pipa kuelekea ughaibuni kumsaka na kumuaga Munene, napendekeza wenye hoja na mawazo wanayotaka nimfukishie wanitumie kupitia uwanja huu. Namba yangu ya simu ni top secret. Hivyo, wasilianeni na mhariri atafikisha ujumbe wenu kwa haraka na salama.
Bye bye. I am leaving for ughaibuni to bid farewell to our outgoing Biggie Njaa Kaya.
Chanzo: Nipashe Agosti 1, 2015.

No comments: