The Chant of Savant

Wednesday 15 January 2014

Hivi Lowassa na ulanguzi umeme bado anaota urais?

 
Kwa wanaokumbuka ndoa ya waziri mkuu wa zamani Edward Lowassa na kampuni la kitapeli la Richmond lililosababisha atimuliwe madarakani, hawana shaka kuwa ndoa hii haiwezi kuvunjika. Hata ikivunjika, bado mirindimo na legacy yake haviwezi kumuacha Lowassa huru. Kama kongwa shingoni, Richmond itaendelea kumuandama Lowassa hadi kaburini. Huu ndiyo ukweli.
Hivi karibuni Shirika la Ugavi wa Umeme Tanzania (TANESCO) liliomba Mamlaka ya Udhibiti wa Huduma za Nishati na Maji (EWURA) kuliruhusu kupandisha bei ya umeme kuanzia Januari 2014 na 2014 kwa kiwango cha aslimia 40. Hii si habari njema kwa watanzania hasa wale akina yakhe ambao mizigo ya utawala imeishawajeruhi vibaya sana. Binafsi niliposoma habari za ulanguzi huu wa umeme, picha ya kwanza niliyoiona ni ya urais wa Lowassa ukiyoyoma. Niliona ulanguzi huu kama msumari wa mwisho kwenye kaburi la Lowassa kisiasa. Nina sababu za kuona picha hii.
Kwanza, licha ya kuwakumbusha watanzania kashfa iliyosukumizwa chini ya busati ya Richmond, upandishaji bei za umeme ambao kimsingi ni ulanguzi, unawakumbusha skandali nzima kama vile ilitendekajana.
Pili, kupandisha umeme, mbali na kuamsha kumbukumbu za watanzania, kutaamsha hasira zao hasa ikizingatiwa kuwa akina Lowassa, licha ya kujinadi kutaka kugombea urais, wanaendelea kuwakoga kuwa urafiki wao na wenye madaraka si wa kukutana barabarani. Hii ndiyo siri ya Lowassa kutofikishwa mahakamani hata baada ya kukiri kuhusika na Richmond. Rejea alivyopewa kitanzi cha kujipima na kuamua na kweli akaamua kuachia madaraka ikiwa ni ushahidi kuwa alihusika vilivyo na kashfa hii.
Wapo wanaokwenda mbali na kusema kuwa Lowassa hakupenda kuwajibika. Kilichomsukuma ni kunusuru serikali ya rafiki na mshirika wake rais Jakaya Kikwete.
Pili, ni kuepuka yasifumuliwe mengi ambayo mwenyekiti wa Kamati Teule ya Bunge iliyochunguza kashfa hii Dk Harrison Mwakyembe alisema kuwa kama wasingeficha baadhi ya mambo nchi isingetawalika. Na kweli, baada ya akina Mwakyembe kuficha waliyoficha walipewa vyeo kama malipo ya fadhila. Samuel Sitta, spika wa bunge aliyeanzisha mchakato ule alinyamazishwa kwa kupewa uwaziri sambamba na Mwakyembe huku mjumbe mwingine Stella Manyanya akipewa ukuu wa mkoa.
Japo kugombea urais ni haki ya kila mtanzania, kuna haja ya wale wanaotaka kufanya hivyo kujipima. Leo tutatoa ushauri wa bure kwa Lowassa kuwa anafaa kujipima na kufanya maamuzi magumu ambayo ni kuachana na ndoto za urais. Sidhani kama watanzania waliwahi kumsamehe kwa harasa na karaha aliyowatia. Maana huu upandishaji holela wa bei za umeme ni matokeo ya kazi ya mikono ya Lowassa na wenzake aliowafia msalabani ili kuwakoa.
Bahati nzuri Lowassa amekuwa bingwa na mwalimu wa kuwaambia wenzake wafanya maamuzi magumu. Naye anapaswa kufanya maamuzi magumu hayo hayo kwa kuwekeza kwenye kujisafisha au kueleza ukweli na kuomba msamaha badala ya kuotea urais akidhani watanzania watakuwa wepesi wa kusahau hivyo.
Kimsingi, mzigo wa ugumu wa maisha utokanao na ulanguzi wa nishati unaowakabili watanzania kwa sasa una mkono wa Lowassa. Lowassa hawezi kukwepa lawama ingawa amekuwa akijtahidi kujisafisha kwa kutoa matamko yanayoonekana kuwatetea wanyonge ukiachia mbali kumwaga mamilioni ya shilingi ambayo haelezi alivyoyapata. Wapo wanaoona kuwa anachofanya Lowassa ni sawa na kumuua samaki halafu ukatumia minofu yake kuwalisha samaki wengine. Tofauti ni kwamba fedha anazomwaga Lowassa zinatokana na hao hao anawapa. Mwalimu Nyerere aliwahi kusema kuwa ukiona mtu anawanunua wenzake jua naye amenunuliwa. je ananunua nini kama siyo kujenga mazingira ya kujilipa baada ya kupata madaraka ambayo yamegeuka biashara kubwa yenye kutengeneza utajiri haramu haraka? Natamani Lowassa ajitokeze na kukanusha madai yangu ili nimuumbue zaidi. Najua hatafanya hivyo. Kama kawaida yake, atasoma na kupuuzia akidhani tatizo litajiondoa, ataendelea na umbuni wake ambaye huona adui akaficha kichwa mchagani akidhani na adui atafanya hivyo wakati siyo.
 Wanaompenda na kumtakia mema Lowassa wanamwambia wazi wazi kuwa hafai ingawa hapendi kusikia ukweli huu: Achana na urais na ashukuru Mungu kwa rafiki yake kumwepusha na kesi mahakamani. Je watanzania ni wasahaulifu au mataahira hivyo wamzawadie mtu aliyewaingiza kwenye matatizo kama yeye?  Ni ajabu kuwa Lowassa katika matamko yake ya “kuwatetea” aliowanyonga na kuwateketeza kwenye dili la Richmond haongelei ufisadi na ulafi unaoangamiza taifa letu. Nadhani kama Lowassa anataka kuwatendea haki wanyonge, basi ajadili mambo muhimu hasa ufisadi, wizi, rushwa, kulindana, kujuana na mengine kama hayo. je anao udhu wa kufanya hivyo? Thubutu!
Japo Lowassa amekuwa akiwalaumu maadui zake kuwa wanahujumu mipango yake ya kumrithi rafiki yake, anapaswa kujilaumu na kukubali ukweli kuwa alichofanya hakiepukiki. Kama kuna mtu ameamua kumuumbua Lowassa na kuzamisha ndoto zake za kuwa rais si mwingine bali aliyetoa wazo la kupandisha/kulangua umeme hasa kipindi hiki tunapokaribia uchaguzi mkuu wa mwaka ujao.
Lowassa si kwamba hafai tu kugombea achia mbali kuwa rais, hata atakayemuunga mkono atamponza. Japo ana mtandao mkubwa, sambamba nao anayo dhambi kubwa ya kuhujumu watanzania kwa kuwaingiza kwenye matatizo yasiyokwisha ya mgao na ulanguzi wa umeme wa kila mwaka. Ana mzigo wa kusababisha maisha magumu kwa watanzania. Maana unapopandisha bei ya umeme unasababisha kila kitu kipande kiasi cha maisha ya watanzania wa kawaida kuzidi kuwa magumu. Kinachofanya dhambi ya Lowassa iwe kubwa zaidi ni ile hali ya yeye kuendelea kutesa akimwaga mamilioni ya pesa huku watanzania wakifa kwa magonjwa yanayozuilika na ambayo serikali ingeweza kuyatokomeza kama si kuruhusu madudu kama Richmond ukiachia mbali mengine kama IPTL. Lowassa hana pa kukimbilia. Ataendelea kuandamwa na jinamizi la Richmond linalosababisha maisha ya watanzania yazidi kuwa magumu na kukosa maana.
Kwa machache haya, je pamoja na kupanda na kulangua umeme Lowassa bado ana ndoto ya urais? Je watanzania watakubali kuchagua mtu ambaye alishawaumiza ili awaumize zaidi? 
Chanzo: Tanzania Daima Jan., 15, 2013.

2 comments:

Anonymous said...

Namna mojawapo ya kuwatala watu ili nchi isiwe na maendeleo nikuwa wafanya wananchi wawe wajinga na washindwe kujitambua inawezekana huyu Bwana analijua suala vizuri na kwa sababu yupo ndani mfumo huo...

Basi hana shaka na hilo...Ukitaka uthibitisha angalia washabiki anaowapata katika hizo pilika pilika zake za ndoto alizosema hivi karibuni

Ndugu Nkwazi N Mhango said...

Anon
Ni kweli ujinga na umaskini ni nyenzo nzuri za kutawalia. Ila kwa dunia ya kitandawazi na kitandawizi ya sasa ni tofauti. Hakuna kitu kitaibadili ramani ya siasa za Afrika kama simu za mkononi. Taratibu watu wetu wanaanza kuamka na kupata angalau taarifa.