The Chant of Savant

Tuesday 30 May 2017

Kijiwe kwenda ikulu kumpongeza rais


            Baada ya kuvunja mwiko wa kugeuzwa kichwa cha mwendawazimu kulikofanywa na rais Joni Kanywaji Makufuli, kijiwe kinapanga, kwa dhati kabisa, kwenda ikulu kumpa tano kikimtaka akaze buti na kufumua sekta nyingine bila kusahau tanzanie, almas na madude mengine ya thamani bila kubakiza ardhi na mbuga zetu za wanyama.
            Akiwa anaonyesha wazi kufurahi na gazeti lake mkononi, Msomi  Mkatatamaa anaingia kwa staili tofauti. Maana, kawaida, huingia mpole na mkimya na mwenye mawazo kama dalili za usomi.
            Baada ya kuamkua, anamtupia gazeti Mchunguliaji na kusema “mwenzenu kwa mara ya kwanza leo nina furaha sina mfano. Nani aliamini kuwa profwedheha Sossie Muongo angetumbuliwa kavu kavu kama ilivyotokea? Bila shaka hata Bashite ajiandae kupambana na visu vya daktari mtumbuaji. Mijitu ilijisahau na kujiona miungu kwa vile inafahamiana na rahis. Sasa yako wapi?  Sitaki niwakawize, timua timua ya juzi ilimenikosha imenikosha. Nangoja kumuona mbele ya pilato na baadaye lupango akifanya vitu vyake kwenye mtondoo. Alikuwa anatutia aibu wasomi ukiachia mbali kuitia kaya hasara kwa kumsomesha akaishia kuitumia elimu yake kulihujumu. Yako wapi sasa? Tulionya tangu kashfa ya Escrow kuwa jamaa ni jipu tena linalotoa usaha wa damu tukapuuziwa. Yako wapi sasa? Mwanaharamu hata ukimficha kwenye chupa atatoea kidole nje.”
            Mpemba anadakia “wallahi kwa hili nakuunga nkono ami. Hata mie nfurahi sana; na naanza rejesha matumaini kuwa kweli hakuna mjanja mbele ya dokta Kanywaji. Kwa vile jamaa aonesha anza ona mwanga, nangoja kuona atavochukua hatua kwa wevi wengine ukiachia hatua nyingine dhidi ya huyu Muongo. Maana washatuliza. Lazima nasi tuwalize ati. Haiwezekani wendelee tugeuza bichwa la mwendawazimu kama so shamba la bibi ati. Mijitu inafanya vitu kana kwamba haikwenda shule yarabi! Sasa faida iko wapi kupoteza njuluku za umma kuisomesha tusijue ingejaza ujinga vichwani kiasi cha kutumia masaburi badala ya vichwa? Inauma; nyie achene tu.
            Mipawa anakula mic “yote tisa mie nangoja kuona kama kweli wote walioasisi ujambazi huu ulioingiza kaya kwenye umaskini watashughulikiwa. Hapa sijui kama rafiki yake Njaa Kaya ambaye aliingia mingi ya mikataba ya kijambazi atamnusuru na abaki na udhu kama mpiganaji wa kweli.”
            Mogshi Machungi anakwanyua mic “Waahi hii imefuaisha kiasi cha kutitaka sisi kama wana kijiwe tiende ikuu kumpongeza doktai Kanywaji ii kumtia moyo na hamasa. Nadhani hapa titamkuna kiasi cha kumuacha hoi.”
            Mijinga anampoka mic na kulonga “ni bahati mbaya sana walio karibu na daktari wa majibu hawamjui vizuri. Huyu jamaa ni wa nyumbani namfahamu sana. Hata akina Denjaman Makapi na Njaa Kaya usishangae siku moja arobaini yao ikafika. Bila shaka ndugu yangu Jimmy Rugemalayer na Singasinga hawalali usingizi. Kwani arobaini yao naiona inawasogelea bila wao kutarajia. Halo halo!”
            Kapende anakwanyua mic “pamoja na hili kuwa jaribu kubwa kwa Kanywaji, bado tusiache kumpongeza japo kwa kuthubutu kupambana na mfumo huu zandiki wa kikoloni na kinyonyaji. Walizoea kutugeuza vichwa vya wendawazimu machizi kujifunzia kunyoa. Acha sasa nao wanyolewe tena bila maji. Hawajui misheni ya dokta Kanywaji hawa. Hawajui kuwa alijiandaa kuwa mkuu na si kwa bahati mbaya kama Njaa Kaya na Makapi mzee wa uvivu wa kufikiri. Sasa itakula kwao.”
            Mheshimiwa Bwege anakamua mic “mie nitashangilia siku nikiona mimali waliyokwanyua inarejeshwa huku nao wakipelekwa lupango wakafanyiwe kitu mbaya na kufia huku wana hizaya hawa. Ni bahati mbaya kuwa dokta Kanywaji amezungukwa na vipofu na viziwi tena wanaojiachia wasijue mwenzao ana mipango mikubwa na kaya yetu. Laiti wachovu wote wangemwelewa hata nusu, kaya ingepaa kimaendeleo na kuheshimika kimataifa. Lazima tumpe tafu awatumbue mabwege wote wenye mizigo kama kughushi, kuibia umma na ufisadi.”
            Kanji anakula mic “duguni yangu, mimi iko na vazo. Kwanini jive siandae tuzo na kuchunuku hii dokta ya Jipu ili jipu yote hata kama nakaa kwake jumbani ijue mambo iko badilka sana?”
            Kabla ya kuendelea da Sofia Lion aka Kanungaembe anamchomekea kwa kumkosoa “Kanji siyo kuchunuku bali kutunuku au nawe ni sawa ni ile gabachori naita dokta Kanywaji Mapombe Makufuri? Iko unga kono vazo lako Kanji. Tukiacha utani, japo nilikuwa naye maya kwa kuvunja nyumba ya mjomba wangu pale Jangwani Bondeni, sasa namsamehe na nimekubali kinoma huyu mwamba wa maendeleo na uzalendo. Nitume fursa hii kupendekeza kuwa tukienda ikulu kumpongeza lazima tumkumbushe kuacha wanasiasa wafanya siasa ili wasimharibie. Maana nijuavyo haya manchi fadhili yanaweza kutumia hii kumhujumu.”
            Mzee Kidevu anakwanyua mic “mie nikienda nitamshauri awe macho na wale waliomzunguka hasa ikizingatiwa kuwa anagusa ulaji wa wengi. Maana hata Isa bin Mariam au Yesu alisalitiwa na mijitu kama Muongo. Hivyo, achunge wale wanaojifanya wanamhusudu na kumuabudia.”
            Kijiwe kikiwa kinanoga mara tukasikia kelele za machinga wakizomea shangingi la Muongo aliyekuwa akipita kuelekea Relini.
Chanzo: Tanzania Daima Jumatano kesho.

No comments: