The Chant of Savant

Saturday 10 January 2015

Mlevi kuandaa mkesha wa kuliambia taifa

Baada ya kuona wasanii wenye `roho mtakakitu’ wakiukata kwa kula na kunywa na `wanene’, Mlevi `nimeskuti’ nikaona nisipofanya kitu, wengi watapotea na Bwana Mkubwa aliye juu ataniadhibu kwa kutotoa `unabii’ alionipa kwa walevi.
Hivyo wakati wengi wakiwaingiza walevi kwa kuandaa mikesha ya kuombea taifa, mimi najipanga kwa ajili ya mkesha wa kuliambia taifa.
Hebu tuwaze pamoja. Hivi kweli taifa linahitaji kuombewa au kuambiwa ukweli? Hata hivyo, nani mwenye Roho Mtakatifu awezaye kuliambia taifa kuwa liendavyo sivyo? Escrow zimezidi. Kama kuna nabii aliyebakia wa kuweza kuliambia taifa si mwingine zaidi yangu.
Maana mimi sijapokea mshiko kutoka kwa Rugemalayer wala sina kanisa zaidi ya kushinda na kukesha baa. Naona yule anacheka atadhani niongeacho ni uongo.
Je, maji hayakubadilishwa kuwa mvinyo? Kwanini Mwana wa Adam hakubadili karatasi kuwa fedha au mawe kuwa dhahabu? Vya kazi gani wakati hushabikiwa na vipofu na wapumbavu? Bado kuna anayehoji umuhimu wa ulabu usawa huu?
Sasa nasema. Heri matajiri wa kweli wawasaidiao maskini kuliko wenye madaraka na fedha wawaibiao maskini na kujiona matajiri wakati ni wezi watupu.
Heri aogopaye kula haramu maana ataishi kihalali kuliko afurahiye kula haramu asijue atajilaumu. Heri aitwaye maskini akauchapa usingizi kuliko asifiwaye utajiri akakesha macho kwa hofu na mawazo.
 Je maskini ni yupi kati ya maskini mwenye furaha na tajiri mwenye huzuni?
Tuache mambo ya ulabu. Hivi kweli taifa linahitaji maombi wakati wakubwa `wameishabomu’ huko ughaibuni hadi inatia aibu na kinyaa?
Kwanini tutegemee kuomba badala ya `kuchakarika’ na kuchapa kazi kwa bidii? Kwa nini tusipambane na `ufisi’ ambao wengine huuita ufisadi? Kwa nini tusirejee vitabu vya Mzee Mchonga, kuhusiana na maadili tuliyogeuza madili? Kwa nini tusisutane na kukamatana uchawi badala ya kupakana mafuta kwa mgongo wa chupa? Mimi si mnafiki ati!
Ni mlevi tena wa haki na si sifa wala kujilisha pepo kama hawa wanaodanganya kuwa wanaombea taifa wakati wanatafuta fursa ya kukaa na kula na wanene, lau wawape mabaki ya akina EPA, Richmonduli, escrew, bomba la gesi na uchafu mwingine.
Mie wala si fisi wa kula mabaki na mifupa tena vya ufisadi. Nasema nabii aliyesalia ni mimi. Sina `mijumba’ wala `migari’ ya bei mbaya.
Wala siogopi kupayukia wezi hata wawe na majeshi na silaha za kutisha. Simuogopi ngurumbili bali Mkuu mwenyewe aliyeniumba.
Sibabaikii upuuzi kama fedha na dhahabu au ofa wala akaunti kwenye mabenki ya wizi. Mimi ni mlevi jeuri asiyehongeka wala kutishwa.
Hata ikitokea mtu akanihonga ulabu na bangi, nakatua na nikishautwika namtwisha vipande vyake kama nifanyavyo siku zote.
Japo nafundisha walevi, mimi ni Profesa wa kweli tofauti na wale wanaoongea utadhani wanafunzi wa chekechea. Mimi ni mlima usioweza kuingia kwenye mifuko ya mafisadi. Mimi ni jiwe la pembeni lililokataliwa na waashi, likatambuliwa na walevi.
Mimi ni sawa na `Nabii Mchonga’ aliyesalitiwa na wale aliowatengeneza, wasijue walevi watamuenzi na kumfanya marejeo yao katika kila hekima na unabii.
Japo ‘Nabii Mchonga’ hayupo nasi leo, ana nguvu na hekima kuliko hata walio hai. Mimi ni sawa na ‘Nabii Sokoine’ aliyeuawa na wanafiki na `mafisi’ wasijue naja mkombozi mwenyewe!
Naona yule anasoma na kutikisa kichwa akidhani hizi ni bangi na ulevi. Si hivyo, wewe kama hujui wapo wanaojua. Kama huchomwi na maneno yangu wapo yanaowachoma wakaniombea hata dua mbaya wasijue mimi ni nabii kwa walevi.
Kama unadhani niandikayo ni bangi na ulabu jaribu uyaandike lau siku moja uone kama yatapendwa au hutopata kichaa kama siyo kufa kwa shinikizo la damu.
Mwenzenu sina shinikizo la damu kwa vile mwilini natumia ulabu na bangi. Sioti ndoto wala kuwa na majinamizi ya kuota nakamatwa na wale niliowaibia kama wao. Wala sina walinzi wala mabaunsa.
Nimuogope nani wakati nisemayo ni kweli. Nikilala sana sana naota ndoto tamu za ushindi na siyo hizi za majinamizi kama wale.
Sisi manabii ndivyo tulivyo. Uliwahi kusikia kuwa Mtume (SAW) au Yesu walikuwa na walinzi? Wanini wakati hawakula haramu wala kusema uongo? Wanini wakati walikuwa na imani thabiti?
Ukitaka kujua kuwa mimi ni nabii hebu njoo kwenye ubavu mbwa wangu. Sina ukwasi wala shida nao. Sitembelei mashangingi wala kuhubiria kwenye mahekalu. Uliwahi kuoniona kwenye runinga nikitangaza biashara ya ulanguzi kwa jina la Mungu?
Yanini wakati najua hapa duniani tuko safarini? Nani aliwahi kuona gari la kubeba maiti likikokota utajiri zaidi ya maiti?
Wangapi waliwahi kuzikwa kwenye mahekalu yao? Sasa kama mnajua yote haya mnawaibia walevi ili mwende wapi zaidi ya kuchuma dhambi na maya?
Wanaoniona mzushi na mvuta bangi hata mlevi wakatembelee makaburi ya watu kama Sani Abacha, Mobutu Seseko, Jean-Bedel Bokassa, Saddam Hussein na wajivuni wengine waliodhani wataisha milele, wasijue walikuwa kwenye kituo cha basi wakingoja kupelekwa makaburini.
Kwa kuzingatia ukweli kuwa tuna watu miongoni mwetu wanaotugeuza majuha wakituibia na kujifanya wanatuombea, mlevi naandaa mkesha wa kuliambia taifa ili litoke kwenye ufisadi na uchafu vinavyoendelea kufanya maisha ya walevi magumu bila sababu.
Wale wote watakaojua kwenye mkesha wa kuliombea taifa wajiandae kusikia mambo makubwa ambayo hawajawahi kuyasikia. Pia wasije na fedha ya sadaka wala nini zaidi ya masikio yao.
Onyo: Watakaohudhuria wasiwe woga wa `ndata’ wala kuswekwa lupango. Huko wakati mwingine ndipo ulipo ukombozi.
Unadhani bila Mzee Madiba `kusota lupango’ kule  Sauzi wangekuwa huru na jeuri ya kutuminyia wakitufanyia mtima nyongo wakati tulichangia sana uhuru wao? Basi njoo tulikomboe taifa kwa kuliambia kuwa ufisadi umezidi. 
CHANZO: NIPASHE Januari 10, 2015.

No comments: