The Chant of Savant

Wednesday 23 March 2011

Baada ya Dowanis, geshi la polishi

Ngoja niimbe wimbo wangu kipenzi wa kumfuata bwana kwa kuwaua kondoo wake.

Mbuye mkhale nawo

Mbuye mkhale nawo moyo wanga

Ndifunitsa, ndifunitsa

Ndifunitsa kuyenda naye

Ndifunitsa ndifunitsa kumtsata

Ndimukonda ndimtsata ndifunitsa

My desire is to follow lord

My desire is to punish cowards

My desire is to make more money

Make more money buy selling cowards

Cowards of Bongolalaland

Mwili moyo mwili zones

Hizi bangi nazo! Tangu lini mvuta bangi akamtukuza Mungu? Hata hivyo acha nijisifu kama bwana Paulo aliyejiita mwanafunzi wa Yesu ingawa ushahidi ni kwamba hakumuona Yesu. Heri mimi namsifu Mungu na mibangi yangu kuliko Njaa Kaya Kikwekwe na vikwekwe wenzake wanavyotukuza na kuwaabudia mafisadi ambao wamegeuka miungu wao.

Baada ya kuwabimiza mkenge walevi kwa habari na vituko vya Loriyondo, nahisi wameanza kuzoea na kustukia janja yangu. Lazima niandae mkakati wa kuendelea kuwatwisha mkenge ama kujiandaa kuwatia adabu kama watastuka na kuamua kufanya kweli.

Najua wengi waliokwenda kwa babu huenda walipata habari zangu kuwa nami nilikwenda kule kupata kikombe ili kuimarisha afya yangu ugogoro kama Lyatongolwa. Laiti waandishi wa uongo wangeandika habari za wote tuliokwenda kwa babu mbona waliotupa ulaji wangekufa kwa presha ya ugonjwa wa moyo! Ya Loriyondo tuyaache ingawa ukweli umedhihiri kuwa wabongolalalanders karibu wote ni wagonjwa isipokuwa mzee Mpayukaji Nabii wa kweli kwa walevi.

Kwa vile za mwizi ni arobaini na njia ya mwongo ni fupi, niko kwenye harakati ya kuimarisha geshi la polishi ili kuwakong’ota walevi baada ya kuisha ganzi ya Loriyondo. Muhimu, mie si serikali. Hivyo geshi langu ni vibaka wa mtaani ambao nitawatumia kuwachapa walevi wenye kidomodomo. Najua baada ya hapo watataka kujua hatima ya Duwanzi. Duwanzi ni mradi wa kijiwe wa kununua mkaa wa kuchemshia kahawa. Kwa ufupi ni kwamba mradi huu ulikula njuluku nyingi za kijiwe lakini mkaa hakuonekana kijiweni kiasi cha walevi kukosa kahawa na kashata.

Mimi kwa kushirikiana na Mbwamwitu aka Ewassa, Kibaka aka Rostitamu na washikaji wengine, tulichota njuluku kiduchu kwa ajili ya kununua kula za kura. Si unajua walevi, bila kuwatembezea kitu kidogo hawakupi kula wala kura. Bila kura ya kula utakulaje? Kwa vile mtindo ni kula na kulipa, wao wanasota na shida ya kukosa kahawa na kashata nasi tunatanua kwa kulipana vinono. Zamu yetu kulipa ikifika bila kuwa na geshi lenye la vibaka na vifaa vya kuwachapia yaani visu na nondo tunaweza kujikuta wanatu-mubarak Mungu pisha mbali.

Kutokana na utaalamu wangu wa kuepukana na majanga niliyotengeneza mwenyewe, juzi nilipata simu toka kwa Mkuu mwenyewe wa Kaya akiomba anukuu mbinu zangu ili kuwanyamazisha wanakaya ambao nao wataamka na kudai mambo ya kiza baada ya kustukia ulaji wa Loriyondo. Kwanza nionye. Wewe unayosema haya hakikisha unasoma kimya kimya na ukimaliza chana gazeti na usimwambie yeyote hata mshirika wako wa bedroom. This is top secret which is classified for national security. Najua wengi wanajua kuwa Njaa mwenyewe huwa ananigwaya. Lakini mara chache chache huniomba ushauri kishikaji. Juzi tulikutana mitaa ya Bwagamoyo akaomba nimpe mbinu ya kupambana na wapuuzi wanaotaka pesa ya Dowanis isilipwe.

Kama mkuu wa kijiwe, ifuatayo ni mipango ya kuhakikisha tunaendelea kuwaibia walevi na kuwatawala niliyompa Njaa Kaya Kikwekwe mwana wa Khal.

Mosi, Kununua mitambo mipya ya kuwachapa wapingaji hasa wanafunzi wa vyoo vikuu wanaotishia ulaji wa wakubwa. Wanasahau kuwa sisi na wakubwa ni chama tawala au bullying, sorry, ruling party kwa kiingereza cha mitaani? Najua kuna wahuni wanatuita lulling, looting, goofing, gooning, luring, fucking, screwing, fisadi’s ass-kising-and-licking party na majina mengine mengi tu.

Eti yanadai tulisoma bure. Ndiyo tulisoma bure. Nanyi mnataka kusoma bure? Tuwasomeshe bure wezi waongozeke hadi kutuibia siyo? Kwani nyinyi ni sisi? Sisi wajanja na kusoma bure sahau. Hatuna njuluku ya kuchezea hata mkidhani kujilipa kupitia Dowanis ni makosa si mjinyotoe roho na si ya kutuletea fujo? Jamani hamkuona uchafuzi ulivyopukutisha njuluku zetu? Hamjui pesa tunayolipa ililiwa na wazazi wenu tuliowakirimu? Shauri yenu. Kama hamjui, jueni.

Inabidi muelewe. Mnapoingilia ulaji wetu mnavunja amani ya kaya ambayo kimsing ni sisi si nyinyi.

Hivyo, kwa kujua umuhimu wa geshi la Polishi, nilipendekeza jamaa awangeze mshahara kwa kutembeza kichapo kila watakiwapo. Nilipendekeza wale genge la Fanya Fyoko Ukome (FFU) walipwe sawa na wakuu wa wilaya. Pia waadikiwe barua na vyeti vya shukrani kwa kufanya kweli kule AR.

Mbinu nyingine niliyotoa ni kuhakikisha vigogo wanakwenda Loriyondo kwa zamu kila mara ili habari zao zizidi kuwalewesha wabongolalalanders washikilie kujadili afya za vigogo na kusahau mambo ya msingi hasa Dowanis.

Ingawa mkuu alishakwenda kwa babu, nilimshauri, akiona wabongolalalanders wanaanza kustuka, aende. Mara hii aende bila kificho na kuwambia wazi kuwa anakwenda kule kunywa kikombe kwa ajili ya watu wote ambao wana magonjwa ya kutisha hasa woga, kusahau, kuridhika, kudanganyika, kujisahau na kutokuwa na vipaumbele.

Hili likifanyika, litasaidia kujenga chuki baina ya babu na matapeli wengine waliokuwa wakiwahadaa wabongolalalanders kwa maombi ya uongo na kuwatoa njuluku. Hawa hawatanyamaza. Lazima wataanza kuzoza mbovu dhidi ya babu kiasi cha vyombo vya habari kupata udaku wa kuandika na kusahau habari za Dowanis. Upo hapa mshirika? Kutokana na ubingwa wangu wa intelijensia, juzi CIA walinitumia barua wakiomba sana niwe mkurugenzi wao nikachuna. Nilipenda sana niwe dingi wao lakini sikuona sababu ya kwenda kupunguza umaarufu wa ndugu yangu, rafiki yangu Baraka Obama. Ingekuwa wakati wa Joji Kichaka ningekwenda kumtibulia. Lakini kwa vile huyu bwana mdogo ni mtoto wa schoolmate wangu niliamua kuwatolea nje.

Kuhusu mikakati yote niliyompa jamaa, naona nisitaje yote mkastuka na kumbwaga kama Mubarak. Hivyo kwa wale watakaotaka kujua zaidi ili wajue jinsi ya kupambana naye, namba yangu ya simu ni 0700,000111999.

Najua watakuja niwape mbinu mbadala za kupambana na hili kama watakuwa tayari kulipia huduma yangu. Sina njuluku ya kulipia choo ngoja ninonihino hapa kabla mgambo wa jiji hawajanidaka.
Chanzo: Tanzania Daima Machi 22, 2011.

No comments: