The Chant of Savant

Wednesday 19 November 2014

Kijiwe chajadili IpTL

 
BAADA ya kushuhudia hila, ghilba, minyukano na mizengwe kuhusiana na sakata zima la wizi wa fedha ya wachovu chini ya kashfa ya Esrew uliofanywa na baadhi ya wanene wasiogusika, Kijiwe kimeamua kujadili kadhia hii ili kutoa mapendekezo ya nini kifanyike.  Leo wanakijiwe wote tumerauka kweli kweli kuhakikisha tunatongoa na kutoa mchango kwa kaya yetu inayozidi kuangamizwa na mchwawatu na fisifisadi watu.
  Mpemba analianzisha, “Yakhe mmesikia hii mizengweee na nyimboo za hawa matwahuti wa Boko Haram ya kule Idodomya wanioendelea zungusha hili zali la IpTL?” anachomekea Mbwamwitu.
  “Unashangaa mizengwe ya Boko Haram wa Idodomya badala ya hili la mkulu kwenda kupasuliwa ughaibuni wakati hili laweza kufanyika hapa? Ami uwe na adabu. Utawezaje kuongea bila kutoa lau salamu kwa mkuu kwa kufanyiwa upasuaji wa busha?” Kapende anamtania Ami.”
“Hayo ya kupasuana mabusha mie hayanihusu. Yatanihusuje iwapo yangu hayawahusu hadi wenda nje kutumbua njuluku zetu kwa vijigonjwa viwezavyotibiwa hata Manzese?” Anauliza Mpemba kwa kuhudhika kidogo.
  “Mie kana kuna kitu kinanisumbua si kingine bai wizi wa Eskoo ambapo njuuku zetu zinazidi kuibiwa huku tikiona wavujaji wakienda kuganguliwa huko majuu wakati sisi tikiangamia kwa magonjwa yanayoweza kuzuiika na kutibiwa.” Anazoza Mgosi Machungi ambaye alipewa uprofesa hivi karibuni.
“Jamani mshaambiwa mali ya umma haiumi lazima uime. Ana shida gani wakati punda wa kuzalisha na kutoa njuluku kupitia kodi mpo kibao? Huyu kumbuka ni mfalme sawa na wale wa Uarabuni ambao huenda kutumbua Ulaya nyakati za mifungofungo” Anachomekea Mijjinga aliyekuja na tabu kubwa utadhani anakwenda chuo cha Manzese kuanza uprofesa wake wa kupewa.
  Mpemba anarejea, “Mie ndhani leo tuongelee hili la ujambazi wa IpTL badala ya kuongelea upuuzi mdogo mdogo kama vile mabusha. Sioni kama kupasua au kutoyapasua kwatusaidia kitu sie akina yakhe.”
  “Ami umenena vyema. Mabusha na kaya wapi na wapi. Naona tukumbushane kuwa kuna janga liitwalo IpTL-Escrow limtafuna kila mmoja wetu,” Msomi Mkatatamaa anazoza.
  Kabla ya kuendelea kudema Mgosi anamchomekea, “Hebu msomi tieewane. Unasema eti haya mazimwi yanatitafuna ukimaanisha nini? Kama kutafunwa watafunwe wae walioyaleta na kuendeea kuyakingia kifua lakini si Mgosi.”
  “Lisirikali litoe maelezo na baada ya hapo kuwawajibisha watendaji wake kwa kuwafikisha mahakamani baada ya kuwafilisi.” Mipawa anazoza kwa uchungu na ngoa.
 “Rugesingasinga na Harbinger of theft wakamatwe na kufilisiwa na wafie lupango ili liwe somo kwa wengine,” Anaongeza Mheshimiwa Bwege.
“Hivi mna ushahidi wa mnayosema au chuki na wivu ndivyo vinawasukuma kupayuka mnayopayuka?” Bi Sofi Lion aka Kanungaembe anaamua kuchafua hewa.
“Kwani wewe unao ushahidi wa haya unayosema?” Mchunguliaji anamuuliza Sofi kwa utani.
Kanji hakawii, “Kweli iko vatu iba juuku ya kaya lakini hapana dai yote. Mimi jua iko vatu dani ya lisirikali iba hii bilioni. Hii hindi kama natumiwa tu au naonewa. Mizi iko ofisini ya sirkali.”
“Hebu mwagia yeye sana. Maana Kanji iko toa pwenti kuba sana. Zengwe zima liitwalo IpTL litokomezewe mbali kwa kutamka wazi kuwa halitaruhusiwa kufanya shughuli yoyote kayani.” Mijjinga anampa ofa Kanji tokana na pwenti zake mulua.
Msomi anarejea, “Sheria zitungwe kuhakikisha kuwa hawa matapeli na mabwana wao kwenye lisirikali hawabadilishi jina na kuendelea kuula kama walivyofanya Richmonduli chini ya koti la Dowanis.”
Anabwia kahawa na kuendelea, “Nadhani wote ni kambale. Hao wakubwa tunaowalilia watende haki ndiyo wahusika wakuu. Mmesahau walivyotuibia kupitia EPA? Hapa la kufanya ni kupiga chini lisilikali la Chama Cha Mafisi na Mafisadi (CCMM) bila cha msalie mtume.”
“Wakigoma twende zetu Burkina Faso na kuwaonyesha kilichomnyima Compaore aka Ebola jeuri ya kung’ang’ania ulaji,” anababatiza Kapende.
“Mie naona ni kama tunatwanga maji. Kwanza tunapaswa kujua IpTL ni nani hawa badala ya kuzungwa na hawa mafisadi kuwadi wawili wanaotumikishwa na wenye mradi walioko nyuma ya pazia,” anachomekea Mipawa.
“Umesema vyema kwa vile IPTL ni zaidi ya Rugemalira na Ponjoro Singh. Ni serikali ndani ya serikali au vipi?” Mzee Maneno anaramba mic.
“Kwa wanavyozungusha, kuna namna. Sioni tofauti ya ujambazi huu na ule wa EPA ambapo mkulu mwenyewe alikamatika akashindwa hata kurukuta zaidi ya kujifanya hasikii wala kujua tuhuma.
Kwa wenye akili tunajua nini jambazi wa EPA sawa na hawa wa Esrew. In fact we have been screwed. Samahani namwanga kikameruni na kikwini aka kimombo tokana na hasira,” Msomi anazidi kuchanja mbuga,” Msomi anachukia hadi anamwaga ukameruni utadhani yuko London.
Mgosi anachomekea kwa utani, “Uongee na kishambaa kwa vie Mombo ni Ushoto kwai? Kama mbwai mbwai mbwa ale mbwa hapa.”
Kijiwe kikiwa kinanoga si likapita shangingi likiwa limewapakiza Sossie Muongo, Saada Mkuyati, Filiinchi Mramba, Ben Ndururu, A liar Kim Maswi, Jimmy Nshomile Rugesingasinga na Singa singa Harbinger of hell. Acha tulitimue kwa mawe tukitaka kulikamata na kuwachoma moto baada ya kuwanzia kitu mbaya ili kuondoa huu ujinga na usanii. Bahati yao dereva wao aliongeza mwendo na kutuacha na mimawe yetu.
Chanzo: Tanzania Daima leo.

No comments: