The Chant of Savant

Sunday 30 November 2014

Mlevi kuwa-Compaore waliotu-escrow


                   Jambazi Blaise Compaore aka Ebola alipotaka kubadili katiba ili agombee mara nyingine kinyume cha sheria, walevi wa Burkina Faso hawakumkawiza zaidi ya kumdondosha. Hebu fikiria. Kama angekuwa amefanya madudu kama vile ku-escrow au ku-IpTL wangemfanyaje kama siyo kumchoma moto kama kibaka? Je hawa jamaa wangekuwa kayani mambo yangekuwaje? Kwa wasiojua maana ya escrow ni excessive stupidity committed repeatedly on Walevi. Na IpTL ni Interdependent political Thugs and Liars.
          Najaribu kufikiri kilevi na kibangi bangi ingawa nina hoja. Inashangaza kuona walevi wa njuluku wanavyotutendea kana kwamba sisi ni hamnazo. Jamani tuna akili hata kama tu walevi na wavuta bangi. Bila akili unadhani unaweza kuvuta bangi au kulewa na kusurvive usawa huu wa kila jambazi kujihomolea utadhani kaya yetu ni shamba la bibi? Yaani majizi inatu-screw nasi tunaendelea kufurahi utadhani hatuna hisia wala akili! Hapana. This is too much, inatosha. Lazima walevi tuwakomboe kondoo wa Mchonga wanaokubali kupelekwa majilini kirahisi na mafisi na machunaji ya kila aina kuanzia ya kisiasa na kidini.
          Walianza na HEPA, tukaminya. Waliona haitoshi wakaongeza Richmonduli. Tuliminya ingawa tulimbanjua mmoja. Waliona inafaa na wamefanya vyema. Sasa wanataka kufunga kazi na escrow. Kweli kuna haja ya kuwavumilia mchwa na mafisi kama hawa kweli?
          Najaribu kufikiri zaidi kilevi. Hivi kama tutatumia bongo vizuri, watuhumiwa wa escrew kweli ni hawa watano au wote? Huwezi kushughulikia escrow bila kugusa mama yake yaani IpTL ambayo ni alpha na omega mbele ya lisirikali letu linaloigwaya kama Ebola. Je kweli linaigwaya au wakubwa wake ni washirika wazuri wa IpTL? Ngoja nifundishe historia kilevi na kibangibangi. Je wajua kuwa IpTL iliingizwa na hawa hawa wanaojifanya hayawahusu huku wakitanua ughaibu wakisukuti jinsi ya kuwatoa kafara wenzao?
          Nakumbuka kila kitu utadhani kilitokea jana. Uzuri ni kwamba wakati wezi hawa wakiingiza balaa hili nilikuwa bado sijaanza kuvuta bangi wala kunywa kama sina akili nzuri. Nakumbuka mheshimiwa Njaa Kaya alikuwa waziri wa Nishati Mimaji na Midini by then.  Nakumbuka jinsi mzee Ruksa alivyotoa ruksa kwa wizi huu wa mchana simply because wapembe wake walikuwa wamepewa chao na kumwingiza mkenge wasijue wanazamisha kaya nzima.
          Turejee kule Burkina. Kwa vile hawa jamaa wanaonekana hawana uwezo wa kusoma alama za nyakati, basi mlevi napanga kuwaingiza walevi wote mitaani ili kieleweke. Sasa nitafanyaje iwapo wapingaji nao wanaonekana kuwa lezi lezi? Maana kwa wafwadhili walivyoshupalia hii kitu, kama atatokea mrume akaweka watu kwa mtaa dude lote litaporomoka kama Compaore. Mko wapi wapingaji au nanyi ni woga na washirika wa siri wa huu u-escrow na u-IpTL? Hivi mnashindwa nini kupiga la mgambo kuwaita walevi waende warejeshe heshima yao kwa kuwatimua hata kuwachoma moto mibaka?
          Sijui walevi wanachelea au kungoja nini wakati sababu ya kufanya kweli ipo na ni zaidi ya sababu? Wakati walevi wakilaza damu, utawasikia wakilalamika utadhani hawana akili wala sababu ya kufanya kweli. Acheni upuuzi. Amkeni tuwa-Compaore hawa waliotu-screw. Wamezidi kutugeuza mabunga na shamba la bibi.  Je mnangoja waishiwa wafanye kazi hiyo wakati uzoefu unaonyesha watachukua mbuzi wawili watatu wa shughuli na mchezo unaendelea?  Hata hivyo waishiwa wanabidi wawe makini kipindi hiki hasa ikizingatiwa kuwa mwakani wanakwenda kutafuta kura ya kula tena. Ili kuwaridhisha walevi wanapaswa wafanye kweli angalau wapate sababu za kuwaeleza walevi jinsi walivyowapigania na kuwaondoa kwenye makucha ya manyang’au mafisi na mafisadi.
          Je kuna haja ya kuwaachia waishiwa kila kitu wakati sisi tuna nguvu kuliko wao na hata ndata na ndutu na mitutu yao kama tutaamua? Mwenzenu nilikuwa Ouaga wiki mbili zilizopita. Nimeyaona na kuyashiriki yote na kugundua siri nyingi za kufanikisha kitu kitakatifu kama hiki hasa usawa huu ambapo ICC iko macho.
          Kwanini walevi tusiungane tukachoma shamba zima la ujambazi badala ya kuwaachia waishiwa wakate matawi huku wakiacha shina mbegu na mizizi kuzalisha matawi mengine? Hawa jamaa bila ku-Compaorewa hawawezi kupata somo. Wataendelea kujifanya kamchezo kama walivyozoea hasa wakijua kuwa walevi nao ni sawa na vibogoyo kiakili na kimsimamo. Kwa vile wote wanaonekana kujifanya haya mauzauza hayawahusu, basi Mlevi lazima niwape tafu wafwadhili kuhakikisha tunaangusha hili genge ambalo halina maana.
          Ifahamike kuwa kama nitafanikiwa kutimiza kuleta ukombozi wa walevi sifanya uzembe kama uliotokea Burkina ambapo ndutu walipoka ulaji na kujifanya ndiyo waliomuangusha Compaore wakati lao ni moja. Hata kayani kama nitafanikiwa nitahakikisha hakuna cha ndata wala ndutu kujifanya wao ndiyo wanajua kutawala wakati mambo yalipoharibika walichangia kuwalinda washenzi na mafisadi.

          Nimalizie kwa kuwaalika wote wenye uzalendo, visheni, usafi na usongo na kaya wajiunge nami kuingia mitaani kuwa-Compaore waliotu-screw chini ya ujambazi wa Escrow. Naomba kutoa hoja.
Chanzo:Nipashe

No comments: