The Chant of Savant

Friday 14 November 2014

Mlevi aazimia kuanzisha operesheni kuwasachi vigogo Airport

Baada ya vyombo vya umbea duniani kuhanikiza kuwa  Rais wa Chaina aliingia Bongolalaland na kuondoka na shehena ya vipusa, Mlevi amekuja na jibu la kukomesha unoko na umbea huu. Kwanza, pamoja na ulabu na mibangi kichwani, sitaki niamini kuwa mkuu wa Chaina na mkuu wa Bongolalaland walitenda jinai hii.
   Hata hivyo, nao ni ngurumbili who knows kama hawakufanya mandingo au la? Kama wapo waliokwapua za EPA na hivi karibuni wakaamuru zichotwe za Escrow, watashindwa nini kuwashughulikia hayawani wasio sema wala wasio na mwenye usawa huu? Walevi wanalaani hujuma hii iwe ni ya vyombo vya umbea au watuhumiwa. 
Baada ya kukaa na kusukuti, nimegundua kuwa kumbe tunaweza kukomesha umbea na mchezo mzima tena kabla haujazoeleka kiasi cha kuzaa vitegemezi au kurithishana baina ya ngwe na ngwe. Kufanya hivyo, napanga kuanzisha kampuni ya ukaguzi wa ndege, magari hata majumba ya vigogo iitwayo Very Important Person Protocol Inspection (VIPPI). Tafadhali msiichanganye kampuni yangu ya yule kidhabu Rwesingasinga wa IpTL, PaP na ViP Egineering. Hatuna uhusiano na ujambazi huo. 
Wazo la kuanzisha VIPPI si langu kusema ukweli. Ni wazo la walevi wanaoona kuwa sasa hali ni mbaya kiasi hiki. Hivyo kukomesha dili zima ni kuwa na kampuni isiyofungamana na yeyote awa mbongo au mchaina. Walevi walifikia hatua hii baada ya kugundua kuwa kuna watu wenye roho mbaya wanaoweza kutumia nafasi hii kuwachafua marais wetu wapendwa na waaminifu.  
Hata hivyo, walevi wana hoja hasa ikizingatiwa kuwa siku hizi dingi anapokwenda kwenye matanuzi yake huwa majina ya wanaokwenda kutanua naye hatangazwi. Hivyo, hii inajenga hisia kuwa tuhuma husika zinaweza kuwa na chembe za ukweli. 
Hivi nani hajui kuwa ujumbe wa wale wanaoandamana na dingi kwenye miruko yake yanafichwa? Kwanini kama hakuna so? Je kuna watu wasiotakiwa wanaochomekwa mle ili kufanya biashara chafu kama hii? Nani anajua katika dunia hii iliyogeuka gunia ambapo fweza hata kama ni za fedheha ni kila kitu? 
Walevi wana uhakika kuwa VIPPI itaungwa mkono hasa na wakubwa kama kweli hawafanyi mambo. Hivyo, uwepo wa VIPPI utawasafisha kama kweli hawashiriki. Ila kama wanafanya huu mchezo mchafu lazima wataipiga vitu nyenzo hii ya uwajibikaji na uwazi. Tungoje tuone watakavyoikaribisha au kuifurumsha VIPPI. 
Mlevi mmoja anayefanya kazi kwenye ‘wizara ya mambo mambo ya nje nje’ alitutonya kuwa hii ikitu ni kweli  sema wahusika wanashikwa kigugumizi kuja na ukweli. Kwa vile aliyetutonya ni mlevi na mvuta bangi anayefikia hata kusahau jina lake, tulipata shaka na ukweli wake. Hata hivyo, ukiangalia ukweli mwingine toka kwa Bwana Ben Maembe alipotoa utetezi wake, unazidi kupata kizungumkuti juu ya ukweli na uongo ni upi. 
 Bwana Maembe, badala ya kujibu tuhuma, alirusha vimondo na matusi kwa waliovujisha habari za dili zima akisema wanataka wafanya biashara peke yao. Kumbe hapa tatizo si ukweli wa madai bali wivu tena wa kike kwa wale wanaotaka wafaidi biashara hata kama ni ya haramu peke yao siyo? 
Kwa anayejua tabia za kibongobongo, anashindwa kukataa au kukubali kama kitu hii ilitokea. La kujiuliza hata kama wengine tunafanya hivyo kwa kusukumwa na mibangi, ni kwanini tembo wamepungua kiasi hiki? Mlevi mmoja aliyesomea mambo ya wanyama hasa tembo alisema kuwa wakati mkuu akitia timu Danganyika ilikuwa na tembo 142,000. Ndani ya miaka tisa wamebakia tembo 55,000! Wuuui! Yaani mnamaliza wanyama wetu kienyeji hivi? 
 Walevi wanadhani kuwa hata kama mkuu Jin Ping Xi hakubeba mzigo, watu wake wanaosifika kwa biashara haramu walifanya hivyo, wanafanya hivyo na watafanya hivyo kutokana na ufisadi na upogo tunaoshuhudia. 
Je ni kwanini tunasingiziwa kirahisi hivi kama hakuna namna? Hili ni swali ambalo mlevi amekuwa akijiuliza bila kupata jibu. Huwezi kuruhusu majambazi kama Kagodamn, Richmonduli, EPA, Esrew na wengine wakaiba uchache uliokwisha wekwa benki ukashindwa kuuza pembe za ndovu. Kama ndovu hawauawi na wakubwa kusafirisha, ilikuwaje wanyama kibao walisafirishwa wakiwa hai na hakuna aliyefungwa zaidi ya kumtoa sadaka brother Kagashaki alipotaka kukomesha ushenzi huu? 
 Walevi wanashangaa hata hao madingi wa mbuga za wanyama na utalii ambao mkubwa wao aliwahi kudaiwa kuwa kinara wa mtandao wa kuua na kuuza bidhaa za wanyama na asifanywe kitu. Huwezi, kwa mfano, ukawa na waziri anayefanya biashara ya utalii kuwa mkuu wa wizara hiyo hata akizuga kuwa ameacha biashara ya utalii. Atampa kampuni mkewe na biashara itaendelea kwa upendeleo.  
Kwani haya walevi hawayaoni wala kuyajua? Brother Lazzie Nyirandu upo hapo? Hivi ile kampani yako ya utalii iliishiwa wapi? Ulliifuta au ulimpasia bi mkubwa na kuendelea kutesa? Je hapa mnamhadaa nani yarabi? Walevi wanajua kila kitu sema hawasemi hadi siku muafaka itakapowadia. 
Walevi wanajua mambo mengi sema wanajinyamazia na kujifanya hawajui ili wale wanaojidanganya kuwa wataendelea kuwatumia waendelee kupumbaa kama Blaise Compaore ili siku ikifika wapigwa chini kama yeye. Hamkumbuki walivyoshupaa baada ya mtuhumiwa wa ujangili na usafirishaji vipusa alipoteuliwa kuwa dingi wa chama twawala? 
Nani anamgusa mkubwa huyu mwenye asili ya kaya fulani yenye vita kwa sasa anayejulikana kwa dili zake? Brother wangu wa Al Shabaab hupo hapa? 
By the way, mlisikia hii ya mkulu kwenda kupasulia tezi dume huko majuu huku walevi wakishangaa tiba ndogo  kama hiyo kwanini isifanyike kwenye zahanati zetu za pale Manzese? 
Jamaa hawa huwa hawaishi vituko, kama vyura ukizuia huyu kupiga kelele mwenzie anahanikiza!  Hili  nalo  nalitafutia dawa.
CHANZO: NIPASHE 

3 comments:

Anonymous said...

Sasa unatushauri nini mkuu

Anonymous said...

Sasa unatushauri nini mkuu

Ndugu Nkwazi N Mhango said...

Nawashauri muingie mitaani kama Burkina ili muweze kujikomboa.