The Chant of Savant

Sunday 15 March 2015

Rais ajaye awe na uchungu na nchi apende elimu


kp1.jpeg
Hatutaki tena rais kihiyo kama huyu hapa wa vibonzo. Laiti angekuwa mtu kweli angestahili kunyongwa au kutupwa kwenye dimbwi la tindikali ili imtafune ateketee na ujuha wake!
Ingawa kila mtu ana vigezo vyake vya rais anayemtaka, kuna haja ya sisi –kama taifa – kuwa na vigezo vya pamoja –hasa tukiangalia matatizo yanayolikabili taifa –vya kumpata rais ajaye ili asafishe uchafu unaonuka na kutamalaki nchini ambako jinai na ubabaishaji vimegeuka sera hivi hivi. Kwa upande wangu ningependa rais ajaye awe na uchungu na nchi kwanza kabla ya mambo mengine. Maana, ukiwa na rais asiye na uchungu na nchi matokeo yake ni   kuendeleza na kuzidi kushamiri kwa ufisadi na matumizi mabaya ya fedha na raslimali za umma ambayo sasa ni tatizo na janga la kitaifa.  Tumeendekeza kuombaomba na kukopa kopa huku hata kidogo kinachopatikana tunaruhusu wezi wakubwa wakiibe na kutuacha maskini zaidi.
          Kitu kingine ningependa rais ajaye athamini elimu sawa na anavyothamini uhai wake. Maana, taifa lisiloelimika litaangamia, hali ilivyo sasa inatisha na kukatisha tamaa. Lazima apatikane mtu wa kutukwamua na jinai hii itokanayo na matumizi mabaya ya ubongo ambapo mambo ya kijinga yamefanywa mambo ya maana na ya maana kufanywa ya kijinga kiasi cha kugeuka taifa la kigodoro. Nikiangalia hali ilivyo sasa –ambapo ubabaishaji umeingia karibu kila nyanja ikiwamo elimu – najikuta nikichanganyikiwa na kupatwa na hofu sana juu ya mstakabali wa taifa hasa vizazi vijavyo. Maana, kwa namna mambo yanavyofanyika, ni kama vile hakuna kesho wala maisha baada ya hawa walaji waliopo kuondoka wakiacha nyuma nchi iliyopaganyika karibu na kuwa taifa lililofeli yaani failed state. Kwa ufupi ni kwamba bila kuwa na rais anayeona mbele na mbali na badala yake tukawa na mtu anayeangalia tumbo lake na jamaa zake waliomzunguka, taifa letu litaingia kwenye machafuko kwa sababu kuu nne yaani ulafi, upofu, ujinga na ufisadi.
          Mwalimu Julius Nyerere – rais wa kwanza – alituachia urathi mkubwa hasa kwenye elimu. Licha ya kutoa elimu ya bure kwa watanzania wote toka mwaka 1967 hadi 1990, alisoma na kutunga vitabu. Alikuwa gwiji wa kutoa na kushiriki mihadhara chuoni (wakati ule tulikuwa na chuo kikuu kimoja tu cha Dar Es Salaam kikisifika kwa fikra za kimapinduzi). Alipenda wakati mwingine kuitisha mikutano na waandishi wa habari mara nyingi akijibu hoja mbali mbali za wananchi. Alikuwa akiongoza nchi kwa mfano na si kwa mdomo. Alisema alichotekeleza na kutekeleza alichosema. Alikuwa mtu wa vitendo zaidi ya maneno. Baada ya kung’atuka, taratibu nchi yetu ilikwenda kwa mbwa kam alivyowahi kusema, “I can let my country go to the dogs” asijue itakwenda baada ya yeye kutoweka hasa wale aliowakataa kupewa ukanda.
          Baada ya kuondoka Nyerere –ambaye kitaaluma alikuwa mwalimu – tulipata mwalimu mwingine, Ali HassanMwinyi ambaye –hata hivyo –hakuonyesha mapenzi kwa elimu wala umahiri wa kushiriki na kutoa mihadhara kama mtangulizi wake. Kwa upande fulani alionekana kupenda kuhudhuria shughuli za kidini kuliko mihadhara ya kitaaluma. Hii, huenda inatokana na ukweli kuwa alikuwa shehe na msomi mkubwa wa dini ya kiislamu.
          Baada ya Mwinyi aliingia Benjamin Mkapa, mwandishi wa habari ambaye alionyesha kupenda kuandika na kusoma hotuba ndefu. Alipenda sana kusafiri na kushiriki makongamano ya kimataifa hadi kufikia kusema kuwa huwa anajisikia raha akihojiwa na waandishi wa habari wa nje kuliko wa nyumbani. Alikuwa akiwakandia waandishi wa habari wa ndani si kwa sababu walikuwa mbumbumbu kama alivyotaka waonekane bali kutokana na kujua ufisadi kibao na kumusulubu kwa masuala ambayo wageni hawakujua.
          Baada ya Mkapa aliingia Jakaya Kikwete mwanajeshi ambaye alipenda sana michezo na kusafiri kuliko mihadhara na makongamano ya kitaaluma. Tofauti na wenzake, rais Kikwete ataingia kwenye vitabu vya historia kama rais aliyehudhuria misiba mingi kuliko matamasha vyuoni na mashuleni ukiachia mbali kuizunguka dunia hadi watani wake wakambatiza jina la Vasco da Gama yule habithi wa kireno aliyeizunguka dunia akitafuta makoloni na nchi za kupora. Ataingia vitabuni kama rais aliyepiga picha na wasanii wengi kuliko wasomi.  Pia ataingia kwenye vitabu vya historia kama rais ambaye chini yake elimu ilivurugika sana. Lawama nyingi bila shaka zitakwenda kwa rafiki na mshirika wake toka jimbo la rais, Dk Shukuru Kawamba ambaye utawala wake uliua kabisa elimu ya Tanzania.
          Kwa kuangalia mdudu yaliyopo kwa sasa, rais ajaye asipokuwa na uchungu na taifa na elimu basi tumekwisha. Maana kwa sasa elimu haina maana tena kiasi cha kusahaulika na kuhujumiwa na kila ajaye. Imefikia mahali watu wanaghushi vyeti na wanaendelea na nyadhifa tena za juu serikali kama vile uwaziri. Je kama tumeweza kuvumilia mawaziri walioghushi, tutapata wapi motisha na uhalali wa kuwashughulikia makatibu muhtasi, walimu, wakunga, polisi na wengine tutaweza kuwashughulikia?  Hakuna kitu kinachoendelea kuwachanganya wengi kama mzaha uliotolewa hivi karibuni kama kupendekeza kuwa kuwa Kiswahili kitumike kama lugha ya kufundishia kuanzia shule za vidudu hadi vyuo vikuu. Bila kubatilisha uamuzi huu nchi itaingia matatani kitaaluma hata kimkakati.
          Tumalizie kwa kusema wazi kuwa rais ajaye lazima awe ni mpenda elimu kweli kweli.  Awe na uchungu wa hali ya juu na taifa vinginevyo miaka si mingi, tutaambulia kilio hata vurugu tokana na madudu yanayofanywa kwa sasa. Angalia ufisadi, wizi wa fedha za umma, ujambazi, biashara haramu ya mihadarati na uzembe na matumizi mabaya ya fedha za umma.
Chanzo: Dira.

2 comments:

Anonymous said...

Hapo washaanza kumpigia debe Lowasa, hiyo elimu kaisomea wapi?
Hivyo vigezo vya kimataifa watavifikiria wapi na wote wachumia tumbo

Ndugu Nkwazi N Mhango said...

Anon usemacho ni kweli. Tunaendeshwa na matapeli na mafisadi tena wajinga wa kawaida wenye kupenda kuzua zua mambo na kujipa sifa wasizo kuwa nazo.