The Chant of Savant

Wednesday 16 April 2014

Wanyakuzi ardhi: Tibaijuka kama Mwakyembe?


          Kwa waliokwisha zoea rongo rongo na ahadi hewa za wakubwa wetu, wana wasi wasi. Wanaamini ahadi hii itakufa sawa na ile ya kubomoa ghorofa la Uhindini. Wanahoji: Kama ameshindwa ghorofa moja tena ambalo limethibitika kujengwa chini ya viwango ataweza maelfu ya majumba tena mengi yakiwa mahekalu ya wenye nazo yaliyotapakaa jijini ukiachia mbali miji mingine mikubwa? Je Tibaijuka anajua anapambana na kundi la watu wa aina gani? Je alisema hayo kwa kupitiwa, kujiridhisha au kutafuta umaarufu? Je akishindwa kama alivyoshindwa kwenye kashfa ya ghorofa la Uhindini tumchukulieje? Je ataanza kutekeleza kitisho chake lini ili tumbane sawa sawa?
          Tambo na siasa za Tibaijuka zinatukumbusha tambo nyingine za waziri mwenzake wa Uchukuzi, Dk Harrison Mwakyembe aliyejitapa hadharani kuwa anepambana na wauza unga akaishia kunywea. Wengi wanauliza: Mwakyembe ameishiwa wapi na vita yake dhidi ya wauza unga au naye amemezwa kama bosi wake aliyepewa orodha ya majina ya wauza unga akaishia kuigwaya akikaa nayo na kuiangalia tu? Je Tibaijuka naye ataishia kunywea huku akihofia hata kuongelea masuala yanayohusu uvamizi ardhi wazi na ujenzi holela? Je Tibaijuka ana ubavu wa kubomoa majumba ya watu kama Getrude Rwakatare ambaye hekalu lake ni moja ya mengi yalitambuliwa kujengwa sehemu zisizo ruhusiwa kisheria? je ataanza lini?
 Tibaijuka alikaririwa hivi karibuni akisema, “Tuliweka mabango ya kutoa notisi katika maeneo yote ya wazi yaliyovamiwa, lakini wahusika walikaidi, sasa tutavunja hayo majumba na wale waliosema kuwa nimekwisha kisiasa nataka niwahakikishie kwamba sijaisha.” Huu ni ushahidi kuwa kumbe mtu mwenyewe analalamika. Kama walikaidi hata baada ya kuwekewa mabango matangazo ya kubomoa ni ya nini zaidi ya kuanza ubomoaji?
Aliendelea kusema, “Hizo kuta nilizoziona maeneo ya Mbezi na maeneo mengine tutazivunja bila kumwangalia mtu usoni. Hao wenye hati pandikizi wala hatutabembelezana nao bali tutakutana mahakamani baada ya kuvunja.’’ Bahati nzuri Tibaijuka amejifunga mwenyewe. Maana mazoea ni kwenda kwenye maeneo ya wanyonge na kuyaruka ya vigogo. Je kati ya hizo nyumba za Mbezi na Tibaijuka nani atabomoka?  Hapa hana kisingizio. Maana maneno yake yanaonyesha anajua hayo mahekalu na nyumba nyingine zilipo.
          Wengi wanangoja kwa hamu kubwa kuona huu mpambano wa Daudi na Goliati hasa ikizingatiwa kuwa uzoefu unaonyesha kuwa mfumo wetu ni wa hovyo kiasi cha kuwakatisha na kuwakwaza baadhi ya watu waliothubutu. Tibaijuka anazidi kutupa moyo kwa kusema kuwa mambo ni tofauti kama alivyokaririwa akisema, “Nilisema kwamba mfumo uliopo sasa si mzuri kwani watendaji wa ardhi hawako chini ya wizara yetu bali wako chini ya halmashauri (Tamisemi) ambapo ilikuwa vigumu kuwabana. “Ili kuwasaidia watendaji hawa wasiingie kwenye mitego ya rushwa, tumeweka mfumo mzuri ambapo sasa kamishna wa ardhi hataweza kujifungia mwenyewe ofisini na kuandika hati peke yake bila wenzake kujua anafanya nini.” Swali kubwa linaloulizwa ni: Kama mfumo unaruhusu kuondokana na jinai ya wezi wachache kujitwalia ardhi ya umma huku wengine wakijenga holela kwenye maeneo yasiyoruhusiwa, waziri anangoja nini? Wengi wangetaka wamuone kazini. Maana maneno matupu hayavunji mfupa walisema wahenga. Wengi bado wanauliza: Ahadi ya kurejesha maeneo ya wazi aliyoitoa mwaka 2011 nayo imeishia wapi au ni yale yale ya kungewa kusema huku wahusika wakichukia kutenda?
          Tumalizie kwa kumshauri profesa Tibaijuka afanye kweli akijua wazi kuwa wananchi wanasikia na kuyachukulia kwa uzito asemayo hasa ahadi zake. Pia afahamu kuwa wananchi hawa hawa hata kama hawapigi kelele wana kumbukumbu na wanajua jinsi jinai hii ya kuwadhulumu inavyotumiwa kisiasa. Hivyo, kuepuka kupoteza heshima yake kwa wale anaowaongoza na kuwatumikia kama kweli anafanya hivyo Tibaijuka anapaswa kuingia kwenye viatu vyao na kujiuliza: Ningekuwa mimi ningetaka kifanyike nini? Hii itamsaidia kujiepusha na ahadi na matendo yanayoweza kumweka kwenye kundi la wanasiasa wababaishaji woga na wapayukaji. Profesa Tibaijuka, watanzania wanangoja kwa hamu sana kuona unatenda haki kwa kubomoa mahekalu na majumba yaliyojengwa kwenye maeneo haramu angalau kwa kuanzia na jiji la Dar Es Salaam. Wanyakuzi ardhi: Tibaijuka kama Mwakyembe? Kila la heri. Yetu macho na masikio.
Chanzo: Dira Aprili 2014.

3 comments:

Jaribu said...

Mimi nilizidi kumponda mama huyu nilivyosoma kuwa alikuwa anajikomba kwa Sasquatch Rugemalira, "Basi Mzee Rugemalira tunashukuru kwa kutusaidia na huu mchango......", kwenye halfa ya mchango wa shule gani huko Kagera. Labda hata bosi wake naye, "Mzee Ruge...."

Ndugu Nkwazi N Mhango said...

Hata mimi mimi niliiona. Ilikuwa ni kwenye hafla ya shule ya Kajumlo Sekondari mwezi jana kule kwao Muleba. Nadhani wote ni mafisadi wanaotumiana bila sisi kujua ingawa wachache tunastuka. She's as useless as prof Issa Shivji and other academics used by CCM to do it dirty laundry.

Anonymous said...

Njaa na uvivu wa kufikiri ndiyo chanzo cha kuwa-viongozi-wanafiki na kuidharau taaluma yao.