The Chant of Savant

Saturday 21 April 2012

Wito kwa wabunge wa CCM



Image Detail


Waheshimiwa wabunge wa Chama Cha Mapinduzi hasa wale ambao si mafisadi wala makokoro,
Wakati wa kujua kuwa nchi ni bora kuliko chama umewadia. Miaka nenda miaka rudi, wabunge wa CCM mmekuwa mkitumiwa kama mfuko au hata kokoro kuweka kila uchafu. Lakini kwa vile dunia  imebadilika lazima mbadilike nayo. Mchango wa baadhi ya wabunge wa CCM wakishirikiana na wale wa upinzani hauwezi kupuuziwa. Ni bora kuwa mmetambua kuwa kumbe genge liitwalo baraza la mawaziri limekuwa likiwatumia kama mataahira kuibia nchi nanyi kuangushiwa lawama. Wakati wa kulaumiwa kutokana na uchafu wa wengine mwisho ni sasa. Kama mlivyosimama kuwafichua mawaziri mchwa na kutaka wawajibishwe mara moja, hakikisha hili linafanyika. Likishafanyika na kufanikiwa hili, uwe mwanzo wa ukombozi wa taifa letu kwa ajili ya vizazi vyenu vijavyo.
Blogu hii ilifurahishwa na tishio lenu kuwa atakayetaka kuwalinda au kuwabeba wenzake naye aondoke nao. Huu ni msimamo wa maana sana. Ila wakati mkichukua msimamo huu, msiangalia karibu kwa kuangalia watu kama waziri mkuu. Anzeni kujenga taswira kuwa kwa mfano rais akiamua, kama alivyozoea kuwabeba watu wake, naye mshikishe adabu.
Kimsingi Tanzania ni zaidi ya CCM kwani CCM itaondoka kama vilivyoondoka UNIP, KANU, MCP, UDF na vinginine vingi lakini Tanzania itakuwapo milele. Wakati umefika wa kuinusuru Tanzania kutoka kwenye mikono michafu iliyoigeuza kuwa shamba la bibi. Msimamo wenu kama hamtaugeuka ni heshima kwenu na taifa.
Alluta Continua haya shime tujenge na kukomboa Taifa letu.

No comments: