Tujuacho ni kwamba kudumu au kuvunjika kwa ndoa ni matokeo ya mambo mengi hata majaliwa, hasa wawili wanafungapo ndoa bila kujua wanachofanya japo wanaweza kujihisi wanajua wasijue hawajui. Pia, yapo mambo mengine mengi ambayo ni matokeo ya matendo au tabia za wahusika. Hivyo, kudumu au kutodumu kwa ndoa ni mkusanyiko wa mambo mengi makubwa na madogo.
Tokana na uzoefu, kitu tunachoweza kusema ni kwamba wanaojenga ndoa ndiyo hao waidumishao au kuibomoa. Mfano, wawili wanapofunga ndoa, hufikia uamuzi huu wao peke yao tena bila shuruti. Hivyo, kila matokeo ya ndoa huwategemea wao. Hata hivyo, pamoja na kuamua wenyewe peke yao, wapo baadhi ya ndoa ambao huigeuza ndoa kama klabu au ushirika. Hii maana yake ni nini? Bahati mbaya, wahusika huwaruhusu wasiohusika kujihusisha na ndoa yao. Kimsingi, wawili husahau kuwa ndoa ikidumu au kuvunjika, wanufaika au waathirika ni wao na si hao waliowahusisha.
Katika suluhisha migogoro mingi ya ndoa au kushuhudia zikivunjika, tumejifunza mambo makuu manne.
Mosi, wote huumia hata kuumizana tokana na pigo au hasara wanayopata tofauti na walivyotegemea wala kupanga. Asikudanganye mtu kuwa anaweza kuacha au kuachika akasherehekea japo, siku hizi, kumezuka uongo wa walioachika au kuacha kujifanya wanasherehekea. Ndiyo, wanaweza kutuonyesha kuwa wanasherehekea usoni. Ila nyoyoni wanaumia. Hili, halina mjadala. Jiulize. Walipofunga ndoa walihuzunika au kufurahi? Jibu liko wazi. Sasa inakuwaje waathirika hawa washerehekee hasara na pigo kubwa kama hili?
Pili, wote uhisi hasara na hata mapungufu. Kwanini wengine waweze sisi tushindwe? Binadamu, kiasili, anapenda mafanikio na kuchukia maanguko. Hivyo, ndoa inapodumu, wanandoa huona fahari na furaha. Ikivunjika, hata wajikaze vipi, maumivu tena makubwa yapo. Kwanza, kuna wasi wasi wa namna jamii inavyowaangalia. Pili, kuna malengo na matarajio yaliyouawa. Na tatu, kuna aibu ya kushindwa tofauti na ridhiko la kufanikiwa. Mara nyingi, wengi walioacha au kuachwa hasa wenye watoto, hushindwa kuwashauri watoto wao juu ya ndoa kwa vile wao walishindwa.
Tatu, ipo jamii inayowazunguka. Hapa, ndipo kichwa cha makala hii kinapoingia na kugusa pabaya. Wengi hasa wasiojua uhalisia wa ndoa wanaweza kuwacheka na kuwaona wanandoa ambao ndoa yao imesambaratika na kuvunjika kama watu walioshindwa. Hapa ndipo tatizo la kuwacheka wahusika au kuchekwa linapoanza. Kama tulivosema, wanaovunja ndoa ni wanandoa wengine wakisaidiwa na wasio wanandoa kwa namna mbalimbali. Je, kuna haja ya kuwacheka au kuwaonea huruma?
Nani anajua kesho yake au nani ni mkamilifu kiasi cha kuwacheka wengine badala ya kuwaonea huruma na kuwasaidia? Kabla ya kuwacheka, vaeni viatu vya wahusika. Jiulize swali moja kuu japo dogo lakini lenye mafunzo makubwa na mengi “je, ingekuwa mimi, ningetaka wenzangu wanifanyie nini au kunichukuliaje?” Tuwe na huruma na utu. Badala ya kuwacheka wanandoa, tushukuru Mungu kuwa hatupitii wanayopitia. Tujifunze kitu toka kwao badala ya kuwabaghaza, kuwacheka, na kuwasimanga. Kwani, hujafa hujaumbika na kutenda makosa ni asili ya binadamu.
Wanandoa ambao ndoa yao imevunjika ni kama wagonjwa. Hakuna haja ya kuwalaumu wala kuwasimanga bali kuwaonea huruma au kuwasaidia. Hakuna anayependa ndoa yake ivunjike japo wahusika wanavunja ndoa yao tokana na ujinga juu ya mambo fulani fulani yawe ya kimalezi, kitabia, kimahusiano, kiuchumi, kitaaluma, ubinafsi, uchoyo, upumbavu, hata kutojali mambo fulani fulani kwa wakati fulani.
Tumalizie kwa kusisitiza kuwa kuwacheka wanandoa walioachana si kuwatendea haki. Maana, kitanda usicholalia hujui kunguni wake. Ni rahisi kuhukumu, kulaumu, hata kutweza. Je, ushawahi kujiuliza? Ningekuwa mimi, ningependa nichukuliweje hasa kipindi hiki kigumu na pigo kubwa katika maisha?
Kwani, si wote wanaoacha au kuachika huoa au kuolewa tena. Tuwaoneeni huruma watu hawa.